Nabii Lut(a.s), kama Mitume wengine walivyofanya aliwanasihi watu wake wamuamini Allah(s.w) na wamche ipasavyo na waogope adhabu yake ambayo ikimfika mtu hapana awezaye kuizuia au kuiondosha.
(Wakumbushe) alipowaambia ndugu yao, (Nabii) Lut: “Je, hamuogopi?” “Bila shaka mimi kwenu ni Mtume muaminifu.” “Basi Mcheni Mwenyezi Mungu na nitiini.(26:161-163)
“Wala sikutakini ujira juu yake; ujira wangu hauko ila kwa (Mwenyezi Mungu) Mola wa walimwengu wote.” “Je, mnawaingilia wanaume katika viumbe (vyake Mwenyezi Mungu)!” “Na mnawacha alichokuumbieni Mola wenu katika wake zenu? Kweli nyinyi ni watu mnaoruka mipaka (mliyowekewa).”(26:164-166)
Na (wakumbushe) Lut alipowambia watu wake: “Je, mnaufanya uchafu, na hali mnaona?” Mnawaingilia wanaume kwa matamanio mabaya badala ya wanawake? Hakika nyinyi ni watu mfanyao ya ujinga kabisa. (27:54-55)
Pamoja na nasaha hizi nzuri zilizoambatana na hoja madhubuti, hawakumuamini Lut(a.s) ila watu wachache tu. Lakini hatukupata humo ila nyumba moja tu yenye Waislamu. (51:36)
Pamoja na Nabii Lut(a.s) kuwanasihi kwa maneno ya hekima na hoja zilizo wazi, watu wake hawakuwa tayari kabisa kuacha maovu yale.
Naapa kwa umri wako! Hakika wao walikuwa katika ulevi wao (wa maovu); wanahangaika ovyo. (15:72)
Walishakuwa walevi wa machafu hayo na walipania kumfukuza Nabii Lut na wale walioamini pamoja naye ambao huchukia ubaladhuli huo.
“Basi haikuwa jawabu ya watu wake ila kusema: Wafukuzeni wafuasi wa Lut katika mji wenu, hao ni watu wanaojitakasa, (basi wasikae na sisi wachafu)” (27:56)
“Wakasema: Kama usipoacha, ee Lut (kutukataza haya), bila shaka utakuwa miongoni mwa wanaofukuzwa (katika nchi hii).” (26:167)