image

Uandishi wa hadithi wakati wa Matabii tabiina (tabiitabiina)

Hii ni historia ya uandishi wa hadithi wakati wa tabii tabiina. Yaani wafuasi wa wale wafuasi wa Masahaba

Wakati wa Wafuasi wa Masahaba (Tabi'i Tabi'ina)201-300 A.H


Hatua ya nne ya ukusanyaji na uandishi wa Hadith ni ile iliyopitiwa katika karne ya Tatu Hirjiriyah (201-300 A.H.). Kazi ya karne ya pili au hata ya tatu ya uandishi wa Hadith tuliyoiona, Hadith zake hazikutosheleza yote yanayohitajika katika utekelezaji wa Uislamu katika kila kipengele cha maisha ya kila siku.

Kwa mfano kitabu cha Imamu Malik kilichokuwa mashuhuri sana kilitumiwa au kupatikana sana huko Hijaz na kiligusia baadhi ya mambo tu yakiwemo ya Ibada kama kufunga, kuhiji, Sala na Zakat. Hivyo kulikuwa na haja kubwa ya kueleza mambo mengine yaliyohusu Uislamu katika nyanja zote za maisha. Kwa hiyo kipindi hiki kilikuwa cha kazi nzito ya kukusanya na kuhifadhi Hadith na kuziweka katika hali zilivyo hivi sasa. 

Katika kipindi hiki walitokea wanazuoni mashuhuri sita waliojitahidi na kutumia sehemu kubwa ya maisha yao katika kukusanya Hadith. Walisafiri masafa marefu kwa ajili ya kazi hii ya ukusanyaji wa Hadith na ilibidi wajifunze tabia za watu kadhaa kabla ya kuandika Hadith moja. Sio kila Hadith waliyoambiwa waliiandika bali kulikuwa na utaratibu wa kuchambua Hadith iliyo sahihi na isiyo sahihi. Ndio maana vitabu sita vya Hadith walivyoandika vilijulikana kwa jina la "Sahihu-Sitta." Vitabu hivi sita ni vile vya:

(a)Sahihi ya al-Bukhari
Kitabu cha Muhammad bin Isma'il Abu 'Abdallah al'Ju'fi anayejulikana kwa jina la "Imamu al-Bukhari." Alizaliwa 13 Shawwal, 194 A.H./21 Julai, 810 A.D. katika mji wa Bukhara huko Urusi, na alifariki 30 Ramadhan, 256 A.H./31 Agosti 870 .D. Hamu yake ya kuhifadhi Hadith aliipata bado akiwa mtoto wa umri wa miaka kumi na moja. 

Alipofikia umri wa miaka kumi na sita alikwenda kuhiji Makka na kubakia humo humo kujifunza Hadith kwa wanazuoni mbali mbali. Baada ya kutoka Makka alikwenda Misr kisha Basra na sehemu nyingine za Asia ambapo alitembea huku na huku katika kujifunza na kukusanya Hadith kwa muda wa miaka kumi na sita.

Kazi yake ya miaka kumi na sita inaonekana katika kitabu chake mashuhuri kijulikanacho kwa jina la "Al-Jami'u al-Sahihi au Sahihi al-Bukhari".Kitabu hiki ndio kitabu cha kwanza cha Hadith kinachotemgemewa na Umma wa Waislamu baada ya Qur-an, kwa sababu ya uangalifu mkubwa uliochukuliwa na Imamu Bukhari katika ukusanyaji na uchambuaji wa Hadith zake. 



Jumla ya Hadith alizokusanya ni 600,000 na katika hizo alihifadhi Hadith 200,000. Lakini kutokana na uangalifu na tahadhari kubwa aliyoichukua katika kuhakiki usahihi wa Hadith alizozipokea, ni Hadith 7,275 tu zilizotokea katika kitabu cha sahihi al-Bukhari. Kabla hajaikubali Hadith kuwa ni sahihi, ilibidi kwanza achunguze historia ya maisha ya kila mpokeaji wa Hadith hiyo kutokea kwa Mtume (s.a.w) mpaka kumfikia.



Imamu Bukhari amezipanga Hadith katika kitabu chake kufuatana na mada za fiq-h. Ameigawanya kazi yake katika juzuu tisini na saba na katika milango (sura) 3,450.



(b)Sahihi ya Muslim
Ni kitabu cha Hadith sahihi kinachofuatia sahihi al-Bukhari kilichokusanywa na Abul Husain Muslim bin al-Hajjaj anayejulikana kwa jina la Imamu Muslim. Imamu Muslim alizaliwa katika mji wa Misabur, 202 A.H./817 A.D. na alifariki 261 A.H./875 A.D. katika mji huo huo. Kama alivyokuwa Imamu Bukhari, naye alisafiri sana huku na huko katika nchi za Uarabuni, Misr, Syria (Sham) na Iraq ambapo alipata fursa ya kusoma kwa wanazuoni wengi waliokuwa mashuhuri. Miongoni mwa wanazuoni mashuhuri ambao alisoma kwao ni Ahmad bin Hambal, mwanafunzi wa Imam Shafii.



Imam Muslim alikusanya Hadith 300,000 na katika hizo ni Hadith 9,200 alizoziandika katika kitabu chake kinachojulikana kwa jina mashuhuri "Sahihi Muslim". Alimpenda sana Imam Bukhari na kazi yake. Kama imam Bukhari, Muslim naye amekifuma kitabu chake kulingana na mada za fiq-h. Naye alichukua uangalifu mkubwa mno katika kuchagua Hadith zilizo sahihi kwa kiasi amba c h o H a d i t h z a k e n y i n g i z i m e k u b a l i a n a n a z i l e z a A l - B u k h a r i . Alikuwa mwangalifu sana katika kuchambua sehemu ya upokezi (isnad) kwa kiasi ambacho Hadith moja ilikuwa na isnad nyingi (misururu mingi ya wapokeaji). Kwa msomaji, Sahihi Muslim imekuwa katika mpango mzuri zaidi kuliko ule wa Sahihi al- Bukhari. 



(c)Sunnan ya Abu Dawud
Ni kitabu cha Hadith cha Abu Dawud. Alizaliwa 203 A.H. na akafiriki 275 A.H. Elimu yake ya mwanzo aliipata Khurasan. Alisafiri sehemu mbali mbali ambazo zilikuwa mashuhuri kwa kuwa na wanazuoni wa Hadith. Ni miongoni mwa wanafunzi wa Imam Ahmad bin Hambali. Alikusanya Hadith 500,000 na alizoziandika katika kitabu chake cha Hadith kinachojulikana kwa jina la "Sunnah" ni Hadith 48,000 tu.



Japo hakuwa mkali sana katika uchambuzi na uhakiki wa Hadith zake kama walivyokuwa Bukhari na Muslim, Sunan yake imekuwa ni kitabu cha Hadith mashuhuri sana kwa Umma wa Kiislamu na imeshika daraja la 2 kwa usahihi baada ya sahihi mbili. Hapana shaka kitabu hiki kimejaza mapengo ya mambo yale ambayo hayakugusiwa na Imam Bukhari na Imamu Muslim. Pia Abu Dawud naye alipanga Hadith zake kulingana na vichwa vya habari vya mada mbali mbali.



(d)Jami'u ya at-Tirmidh
Abu Isa Muhammad bin 'Issa bin Sarwa bin Shaddad anayejulikana kwa jina la at-Tirmidh alisoma kwa Imamu Bukhari, Ahmad bin Hambali na Abu Dawud al-Sijistani. Alizaliwa katika mji wa Tirmidh mnamo 209 A.H. na akafariki mwaka wa 279 A.H. Imamu Tirmidh alikuwa mwanazuoni mkubwa. Pamoja na kitabu chake cha Hadith aliandika vitabu vingine vya Sharia na Tarekh. Alisafiri sana katika kukusanya Hadith katika nchi za Khurasan, Iraq na Hijaz.



Kitabu chake cha Hadith kinachojulikana kwa jina la Jamiu kimemfanya kuwa maarufu sana. Alikuwa mwanazuoni wa kwanza kuchambua Hadith kutokana na majina ya wasimulizi. Alizingatia majina yao, majina yao ya ukoo, majina ya utani, n.k. Jami'u ina Hadith chache zaidi ukilinganisha na Sahihi Bukhari na Sahihi Muslim. 


(e) Sunan ya Ibn Majah
Hiki ni miongoni mwa vitabu sita vya Hadith sahihi kilichoandikwa na Muhammad bin Yazid anayejulikana kwa jina la Ibn Majah aliyezaliwa 209 A.H. na akafariki 295 A.H. Katika kukusanya Hadith alisafiri nchi mbali mbali palimokuwa na vituo vya elimu kama Basra, Kufa, Baghdad, Makka, Syria (Sham) na Misr.



Kitabu chake cha Hadith kinachojulikana kwa jina la "Sunan" kimejishughulisha na Hadith zinazohusu sharia zinazoonyesha halali na haramu. Katika uchambuzi wa Hadith sahihi hakuwa makini sana kama walivyokuwa Maimam wawili wa mwanzo. Hivyo Hadith zake zimewekwa kwenye daraja la pili la usahihi. Hadith za daraja la kwanza ni Hadith za Bukhari na Muslim.



(f)Sunan ya an-Nasai
An-Nasai ambaye jina lake kamili ni Abu 'Abdur-Rahman Ahmad bin an-Nasai alizaliwa katika mwaka 214 A.H na kufariki 303 A.H./315 A.D. An-Nasai alikuwa mwanafunzi wa Abu Dawud na Hadith za kitabu chake kinachojulikana kwa jina la "Sunan" amezipanga katika muundo alioutumia mwalimu wake. Kazi ya an- Nasai katika ukusanyaji Hadith imekuwa ni kazi muhimu sana kwa Uma wa Kiislamu lakini kwa kuwa hakuwa mwangalifu sana katika uchujaji wa Hadith sahihi, kazi yake imeangukia katika kundi la Hadith za daraja la pili. Baadhi ya Hadith za kitabu hiki ni dhaifu na zenye kutiliwa mashaka zilizo simuliwa na watu wanaotiliwa mashaka.



Hivi ndivyo vitabu sita mashuhuri vilivyodhibiti Hadith katika maandishi katika kipindi hiki cha nne cha hsitoria ya uandishi wa Hadith. Vitabu hivi vimeitwa Sahihi kutokana na uangalifu uliochukuliwa na waandishi katika kuzikusanya Hadith na kuzidhibiti katika maandishi. Kila waandishi walivyochukua tahadhari ya hali ya juu katika kuzichuja Hadith ndivyo Hadith zao zilivyopanda daraja la usahihi.


Ni kwa msingi huu Hadith za Imam Bukhari na Muslim zimekuwa daraja la kwanza na zinajulikana kwa jina la "Sahihain"(Sahihi mbili), na Hadith za Maimamu wanne waliofuatia zimekuwa katika daraja la pili la Usahihi. Vipimo au vigezo vya Hadith sahihi tutaviona katika kipengele kinachofuatia. Hata hivyo, pamoja na vitabu hivi sita mashuhuri, pana vitabu vingine vya Hadith vilivyoandikwa katika karne hii ya tatu Hijiriyyah ambavyo pia hutegemewa na Waislamu na ambavyo imetubidi tuvitaje hapa ili kuonyesha jinsi kazi ya uandishi wa Hadith ilivyopamba moto katika karne ya tatu Hijiriyyah. Kwa hiyo, pamoja na "Sahihi Sita" tulizozitaja, vifuatavyo pia viliandikwa na vilikuwa mashuhuri kwa kiasi chake.

(g) Kitabu cha al-Waqidi
- Wa Baghdad aliyefariki 207 A.H.

(h)Masnad ya Imam Ahmad - Kitabu cha Hadith cha Imam Ahmad bin Hambali aliyezaliwa 164 A.H. na kufariki 241 A.H. kilikuwa kitabu mashuhuri sana kwa wakati wake.

(i)Kitabu cha 'Abdullah bin Hakam - Aliyezaliwa 221 A.H. na alifanyia kazi yake Basra.

(j)Kitabu cha Yahya bin Mayum - aliyezaliwa 233 A.H. na kufanyia kazi yake Madina.

(k)Sunan ya Darimi: - Ni kitabu cha Abu Muhammad 'Abdulah bin Ad-Darimi aliyezaliwa 181 A.H. na kufariki 255 A.H. Baada ya kitabu hiki ndipo vikafuata vitabu vya "Sahihi Sita".

(l)Kitabu cha Bayhaqi: - Kilichoandikwa na Imamu Abu bakr Ahmad al-Bayhaqi aliyelizaliwa 348 A.H. na akafariki 456 A.H. Kitabu hiki ni miongoni mwa kazi za mwanzo za karne ya nne Hijiriyyah.

 





           

Je! umeipenda hii post?
Ndio            Hapana            Save post

Rajabu Tarehe 2024-05-10 14:53:23 Download PDF     Share On Facebook or Whatsapp Imesomwa mara 714


Sponsored links
👉1 Kitabu cha Afya     👉2 Kitau cha Fiqh     👉3 Madrasa kiganjani     👉4 kitabu cha Simulizi    

Post zifazofanana:-

Dua za wakati wa shida na taabu
Hizi ni Dua ambazo unatakiwa uziombe wakati wa shida na taabu Soma Zaidi...

sunnah
Soma Zaidi...

Historia ya uandishi wa Hadithi, na ni kwa nini wakati wa Mtunme hakukuwa na uandishibmkubwa wa hadithi
Hapa utakwendabkuijuwabhistoria ya uandishi wa hadithi. Pia utaijuwa sababu iliyopelekea uandishi wa hadithi kuwa mdogo . Soma Zaidi...

Dua za kuomba wakati unapokuwa na maumivu kwenye mwili
Posti hii inakwenda kukufundisha dua za kuomba wakati wa kuwa na maumivu kwenye mwili wako. Soma Zaidi...

SWALA YA MTUME (s.a.w)
SWALA YA MTUME Kumswalia Mtume (s. Soma Zaidi...

HALI AMBAZO MTU AKIOMBA DUA HUJIBIWA
HALI AMBAZO MTU AKIOMBA DUA ITAJIBIWA. Soma Zaidi...

DUA YA MUUMINI NA DUA YA KAFIRI
DUA YA KAFIRI NA DUA YA MUUMINI. Soma Zaidi...

Jinsi ya kutoa salamu katika uislamu
MAkala hii itakwenda kukufundisha jinsi ya kutoa salamu kwenye uislamu Soma Zaidi...

Dua sehemu ya 04
Soma dua mbalimbali za kila siku ambazo unatakiwa uzijuwe. Dua 120 ambazo muislamu anatakiwa kuzijua Soma Zaidi...

Hadithi Ya 35: Msioneane Choyo, Msizidishiane Bei, Msichukiane
Soma Zaidi...

Adabu za kuomba dua kuifanya dua yako ikubaliwe kwa haraka
Post hii inakwenda kukugundisha adabu zinazotakikana kwa mwenye kuomba dua. Soma Zaidi...

NAFASI YA SUNNAH KATIKA UISLAMU
Nafasi ya Sunnah katika UislamuMtume Muhammad (s. Soma Zaidi...