"Ewe mwanangu! Kwa hakika jambo lolote lijapokuwa na uzito wa chembe ya hardali, likawa ndani ya jabali au mbinguni au katika ardhi, Mwenyezi Mungu Atalileta (amlipe aliyefanya); bila shaka Mwenyezi Mungu ni Mjuzi wa mambo yaliyofichikana, (na) Mjuzi wa mambo yaliyo dhahiri"(31:16).
Aya hii inatuhakikishia kuwa kila mtu amekadiriwa jambo lake na hapana yeyote na hila yoyote itakayomzuia mtu asipate kile alichokadiriwa kukipata au kumuwezesha mtu kupata kile ambacho hakukadiriwa. Pia aya ifuatayo inatuweka wazi zaidi:
“Na hakuna mnyama yoyote (kiumbe chochote) katika ardhi ila riziki yake iko juu ya Mwenyezi Mungu….. " (11:6)
Kutokana na aya hii tunajifunza kuwa lengo la maisha yetu si kutafuta rizki na maslahi ya dunia bali vitu hivi ni vitendea kazi tu vyakutuwezesha kulifikia lengo kuu. Lengo letu kuu ni kuusimamisha Uislamu katika jamii ili tuweze kumuabudu Allah (s.w) ipasavyo katika kila kipengele cha maisha yetu ya kibinafsi na ya kijamii ambalo ndilo lengo la kuumbwa kwetu.
Hivyo katika mchakato wa kuliendea lengo hili la kusimamisha Uislamu katika jamii, tusimchelee yeyote wala
tusichelee kupoteza chochote kwani hamna mwenye uwezo wa kutupokonya au kutuzidishia chochote kile kinyume na alivyotukadiria Allah (s.w). Katika hili ni vyema tukazingatia pia aya ifuatayo:
Hautokei msiba katika ardhi wala katika nafsi zenu ila umekwishaandikwa katika Kitabu (cha Mwenyezi Mungu) kabla Hatujaumba. Kwa yakini hili ni sahali kwa Mwenyezi Mungu." (57:22).