Zaka ya mapambo ya dhababu na fedha, mali ya bishara na mali iliyofukuliwa ardhini
(iv)Vito (mapambo )vya Dhahabu na Fedha
Mapambo ya dhahabu na fedha yameharamishwa kwa Waislamu Wanaume. Wanawake wenye mapambo ambayo kiasi cha dhahabu au fedha kilichopo kwenye mapambo hayo kinafikia Nissab,wanalazimika kutoa Zakat kila mwaka unapopindukia.
Zainab mke wa Abdullah(r.a) ameeleza: Mtume wa Allah alituhutubia na akasema: “Enyi jumuia (mkusanyiko wa) wa wanawake! Toeni Zakat hata kutoka kwenye mapambo yenu, kwa sababu katika wakazi wa motoni mtakuwa w engi zaidi katika siku ya Kiyama ” (Tirmidh).
Amr bin Shuaib(r.a) amesimulia kutoka kwa baba yake na baba yake alisema kuwa wanawake wawili walikuja kwa Mtume (s.a.w) na bangili mbili za dhahabu wamevaa mikononi mwao Mtume aliwauliza “mmelipa Zakat yake” ‘Hapana’, walijibu. Kisha Mtume (s.a.w) akawauliza: ‘Mngetaka kwamba Allah awavalishe bangili za moto?’ ‘Hapana ’ walijibu. Alisema (Mtume): “Basi lipeni Zakat yake ” (Tirmidh).
(v)Mali yakuchimbuliwa chini ya ardhi au mali ya kuokota
Mali iliyofukuliwa chini au madini hutolewa ushur au Zakat kiasi cha moja ya tano (1/5 au 20%) ya thamani ya mali hiyo kama tunavyofahamishwa katika Hadith.
Abu Hurairah ameeleza kuwa Mtume wa Allah amesema: “... Na kuna moja ya tano (1/5) inayolazimu kutolewa Zakat kutokana na mali iliyo chini ya ardhi”. (Bukhari na Muslim).
Hadith hii inatufahamisha kuwa mali yoyote iliyochimbuliwa chini ya ardhi ambayo haikuwa na mmiliki yoyote kabla ya hapo, itakuwa ni halali kwa aliyeigundua na kuichimbua lakini atalazimika kutoa ushuru au kiwango cha Zakat kiasi cha 1/ 5 au 20% ya mali hiyo. Hali kadhalika mali yoyote ya kuokota iliyokosa mwenyewe baada ya kutangazwa kwa muda mrefu wa kutosha unaokubalika katika sharia ya kiislamu inakuwa ni mali ya mwenye kuokota, na atalazimika kuitolea Zakat kiasi cha 1/5 au 20% ya mali hiyo. Mali ya kuchimbuliwa chini au mali ya kuokota haina Nisaab wala haina muda bali Zakat yake hutolewa pale pale inapopatikana.
(vi)Mali ya Biashara
Bidhaa za biashara pamoja na fedha taslimu zinatakiwa zihesabiwe na kutolewa Zakat baada ya mwaka kupindukia.
Samura bin Jundab (r.a) ameeleza: Mtume wa Allah alikuwa akituelekeza tukusanye Zakat kutoka kwenye vile tulivyovihesabu kama bidhaa (za biashara). (Abu Daud).
Bidhaa za biashara zitatolewa Zakat kwa kuthamanishwa na fedha taslim kwa kiasi cha 1/40 au 2.5% ya mali yote ya bidhaa zote za biashara. Kwa hiyo mali ya biashara nisaab yake itakuwa sawa na nisaab ya fedha au dhahabu. Tofauti na dhahabu, fedha na fedha taslim ambazo hutolea Zakat baada ya kukaa kwa kipindi cha mwaka mmoja, bidhaa za biashara si lazima zikae kwa kipindi cha mwaka mmoja ndio ijuzu Zakat juu yake bali kila mwisho wa mwaka, mfanyabiashara atahesabu bidhaa zake zote anazozifanyia biashara na kuzitolea Zakat kwa kiwango cha 2.5%. Hapana Zakat juu ya vifaa vinavyotumika kwa matumizi ya nyumbani au vitendea kazi. Kwa mfano, nyumba za kufanyia kazi kama vile maduka, ofisi, na hoteli, mashine za kufanyia kazi, samani za nyumbani, ofisini dukani, hotelini, n.k. magari ya kusafiria na kusafirishia bidhaa, vyote hivi havistahiki kutolewa Zakat.
Kwa msisitizo zaidi Zakat inajuzu tu kwa mali inayotengenezwa kwa ajili ya kuuzwa au mali inayonunuliwa kwa ajili ya kuuzwa; kwa mfano magari yaliyonunuliwa au nyumba zilizotengenezwa kwa ajili ya kuuzwa zitatolewa Zakat kila mwisho wa mwaka.Jambo muhimu linalotakiwa lizingatiwe kabla ya kutoa Zakat ni madeni. Ni sharti madeni na haki nyingine zote za watu zitolewe ndio mali ihesabiwe kwa ajili ya Zakat.