Vitimbi vya Makafiri Dhidi ya Nabii Salih(a.s) na Waumini na kuangamizwa kwao


Makafiri wa Kithamud hawakuishia tu kwenye kuukataa ujumbe wa Nabii Salih(a.s), bali walidhihirisha jeuri yao kwa kumuua ngamia wa muujiza ili waione hiyo adhabu waliyoahidiwa (Rejea Qur-an 7:77). Baada ya kumuua ngamia walipewa siku tatu kama fursa ya mwisho ya kuamini na kutubia makosa yao. Badala ya kutubia kama vile haitoshi kwa kosa walilolifanya, walikula njama za kumuua Nabii Salih na wale walioamini pamoja naye.




Na walikuwamo mjini watu tisa wakifanya matata (kabisa) katika ardhi (hiyo) wala hawakusuluhisha (jambo ila kuharibu tu). Wakasema: “Apianeni kwa Mwenyezi Mungu (ya kwamba) tutamshambulia usiku yeye (Salih) na watu wake, kisha tutamwambia mrithi wake; Sisi hatukuona maangamio (yake wala) ya watu wake na bila shaka sisi ni wa kweli kwao.(27:48-49)



Basi wakapanga vitimbi (vyao); na sisi tukapanga mipango yetu
(tukapangua vitimbi vyao)na hali ya kuwa hawana habari. (27:50)

Kuangamizwa Makafiri na Kunusuriwa Waumini Mwisho wa siku ya tatu makafiri waliangamizwa na wakanusurika Salih(a.s) na wale walioamini pamoja naye kama tunavyojifunza katika Qur-an:



Basi ilipofika amri yetu, tukamuokoa Salih na wale walioamini pamoja naye kwa rehema Yetu; na (pia tukawaokoa) katika hizaya ya siku hiyo. Hakika Mola wako ndiye Mwenye nguvu (na) Mwenye kushinda.(11:66)



Na wale waliodhulumu (nafsi zao) uliwaangamiza ukelele (uliopigwa na Malaika); wakapambazukiwa wametulia tu (wamekufa) katika majumba yao. Kama kwamba hawakuwamo humo. Sikilizeni. Hakika Thamud walimkufuru Mola wao; basi Thamud wamepotelea mbali. (11:67-68)




Mtetemeko wa ardhi ukawanyakuwa (roho zao) na wakawa wamekufa humo katika miji yao. Basi (Salih) akawaacha (akenda zake), na huku anasema: “Enyi kaumu yangu! Nilikufikishieni ujumbe wa Mola wangu na nikakunasihini, lakini nyinyi hamwapendi wenye nasaha.” (7:78-79)



Kutokana na aya hizi tunajifunza kuwa jeshi la Allah(s.w) lililotumika kuwaangamiza makafiri wa Kithamud ni tetemeko la ardhi lililosababishwa na ukelele wa Malaika. Kumbuka:





“Na majeshi ya mbingu na ardhini ya Mwenyezi Mungu; na Mwenyezi Mungu ni mwenye nguvu, mwenye hikima.” (48:7)