image

Sifa za waumini zilizotajwa katika surat ash-Shuura

“Basi vyote hivi mlivyopewa ni starehe ya maisha ya dunia tu, lakini kilicho kwa Mwenyezi Mungu ni bora na cha kudumu (milele).

Sifa za waumini zilizotajwa katika surat ash-Shuura

Sifa za waumini zilizotajwa katika surat ash-Shuura


“Basi vyote hivi mlivyopewa ni starehe ya maisha ya dunia tu, lakini kilicho kwa Mwenyezi Mungu ni bora na cha kudumu (milele). Watastahiki wale walioamini na wakawa wanamtegemea Mola wao." (42:36)


"Na wale wanaojiepusha na madhambi makubwa na mambo mabaya na ambao wanapokasirika husamehe ". (42:37)



Na wale waliomuitikia Mola wao (kwa kila amri zake) na wakasimamisha swala na wanashauriana katika mambo yao na wanatoa katika yale tuliyowaruzuku." (42:38)


"Na wale ambao jeuri inapowafikia huzitetea nafsi zao." (42:39)


"Na malipo ya ubaya ni ubaya uliosawa na (ubaya) huo; lakini anayesamehe na kusuluhisha ugomvi; ujira wake uko kwa Mwenyezi Mungu; bila shaka yeye hawapendi madhalimu. Na wanaolipiza kisasi baada ya kudhulumiwa, hao hakuna njia ya kulaumiwa. Bali lawama iko juu ya wale waliodhulumu na wakawafanyia jeuri katika ardhi pasipo haki; hao ndio watakaopata adhabu iumizayo. Na anayesubiri na kusameme (atalipwa wema wake). Bila shaka hilo ni katika mambo makubwa ya kuazimiwa kufanywa (na kila Muislamu) "(42:40-43)



Mafunzo:
Kutokana na aya hizi (42:36-43) tunajifunza kuwa,
Kwanza, neema zote tulizopewa hapa duniani ikiwa ni pamoja na vitu mbali mbali vya thamani tunavyovipenda na


vinavyotushughulisha sana katika kuvisaka, tunafahamishwa na Mola wetu Muumba kuwa ni kwa ajili tu ya matumizi ya maisha ya hapa duniani. Vitu hivi havina thamani yoyote katika maisha maisha ya akhera. Historia ya mwanaadamu, ni ushahidi tosha kuwa hapana mtu yeyote, hata wale waliokuwa wafalme na matajiri wa kupindukia, aliyeondoka na chochote katika safari yake ya akhera. Katika kushajihisha kipengele hiki, Allah (s.w) anatukumbusha tena na tena juu ya starehe za maisha ya dunia ukilinganisha na maisha ya akhera katika aya zifuatazo:


"Watu wametiwa huba ya kupenda wanawake na watoto na mirundi ya dhahabu na fedha, na farasi wanaotunzwa vizuri, na wanyama na mashamba. Na hayo ni matumizi katika maisha ya dunia, na kwa Mwenyezi Mungu ndiko kwenye marejeo mazuri. Sema: "Nikwambieni yaliyo bora kuliko hivyo?" Kwa ajili ya wamchao Mungu ziko bustani kwa Mola wao, zip itazo mito mbele yake. Watakaa humo milele na wake (zao) waliotakaswa (na kila uchafu na kila ubaya). Na wana radhi ya Mwenyezi Mungu; na Mwenyezi Mungu anawaona (wote) waja (wake). (3:14-1 5)



Kila nafsi itaonja mauti. Na bila shaka mtapewa ujira wenu kamili siku ya Kiyama. na aliyewekwa mbali na moto na akaingizwa Peponi, basi amefuzu (amefaulu kweli kweli). Na maisha ya dunia (hii) si kitu ila ni starehe idanganyayo (watu). (3:185)


Enyi mlioamini! Mna nini mnapoambiwa "Nendeni (kupigana) kwa ajili ya dini ya Mwenyezi Mungu", mnajitia uzito katika ardhi? Je, mumekuwa radhi na maisha ya dunia kuliko ya Akhera? Lakini starehe za maisha ya dunia kwa (mkabala wa maisha ya) akhera ni kidogo tu. (9:38)


"Mwenyezi Mungu hukunjua riziki kwa amtakaye na huidhikisha (kwa amtakaye). Na wamefurahia maisha ya dunia (kuliko ya Akhera). Na uhai wa dunia kwa mkabala wa Akhera si kitu ila ni starehe ndogo tu. (13:26)


Na wapigie mfano wa maisha ya dunia: (Maisha ya dunia) ni kama maji tunayoyateremsha kutoka mawinguni; kisha huchanganyika nayo (maji hayo) mimea ya ardhi (ikastawi), kisha (baadaye) ikawa (mimea hiyo) majani makavu yaliyokatikakatika ambayo upepo huyarusha huku na huko. Na Mwenyezi Mungu Ana uweza juu ya kila kitu. (18:45)



Jueni ya kwamba maisha ya dunia ni mchezo na upuuzi na pambo na kufaharishana baina yenu (kwa nasaba), na kufaharishana kwa mali na watoto. (Na hali ya kuwa vyote hivi hamdumu navyo. Mfano wake) ni kama mvua ambayo huwafurahisha (wakulima) mazao yake, kisha yanakauka ukayaona yamepiga umanjano (badala ya kupiga uchanikiwiti), kisha yanakuwa mabuwa (hayana chochote). Na Akhera kuna adhabu kali (kwa wabaya); na (pia) msamaha wa Mwenyezi Mungu na radhi (Yake kwa wema). Na hayakuwa maisha ya dunia ila ni starehe idanganyayo; (mara huondoka). (5 7:20)


"Bali nyinyi mna penda zaidi maisha ya dunia, hali ya kuwa ya akhera ni bora (zaidi kabisa) na yenye kudumu ". (87:16-17)
Kutokana na aya hizi tunajifunza kuwa hapa duniani si uwanja wa kustarehe bali ni uwanja wa kutafutia starehe za kudumu milele za maisha ya akhera. Hivyo wale watakao kanusha maelekezo haya ya Mola wao, badala yake wakaifanya dunia kuwa ni sehemu ya kustarehe na wakatumia vipaji vyao na umri wao wote katika harakati za kutafuta starehe hizo, watakuwa wamekhasirika kweli kweli.
Kwanza starehe hawataiona kwa vile umbile la binaadamu la hapa duniani si lenye kuhimili starehe halisi. Kwa mfano mtu mwenye wasaa wa kula na kunywa vizuri mara hunenepa na


kuandamwa na magonjwa chungu nzima - ugonjwa wa moyo, presha, kisukari, n.k. Pili, hata wale watakaojidhania na kujidanganya kuwa wanastarehe, starehe hizo ni za muda mchache mno. Hata kama tukijaalia kuwa kuna mtu aliyepata starehe kwa saa 24 za kila siku katika umri wake wote, bado ukilinganisha umri wa maisha ya dunia na umri wa milele wa maisha ya akhera, ni starehe isiyokuwepo. Ndiyo maana Allah (s.w) anatufahamisha kuwa starehe ya maisha ya dunia ni starehe idanganyayo na ni mchezo na upuuzi.



Pili, starehe hasa ni starehe ya maisha ya akhera ambamo mtu atakuwa katika starehe katika kila pumzi ya maisha yake ya milele. Watakaostahiki starehe hizi ni waumini wenye sifa zifuatazo:



(i)Wanaomtegemea Mola wao, ambao hawamchelei yoyote katika kutekeleza wajibu wao kama walivyoamrishwa na Mola wao, wakijua kuwa hapana hila wala uwezo ila kutoka kwa Allah (s.w). Wanayakini kuwa aliyenusuriwa na Allah (s.w) hapana mwenye uwezo wa kumdharau na aliyeandikiwa kudhurika hapana wa kumnusuru.



(ii)Wanaojiepusha na madhambi makubwa na mambo mabaya, yaani wanajitahidi kwa kadiri ya uwezo wao kujiepusha na mambo maovu yaliyobayana. Pia mara kwa mara huleta stighfari (kuomba msamaha wa Allah) kwa pale walipomkosea bila ya kujitambua kutokana na udhaifu wa kibinaadamu
.
(iii)Ambao wanaopokasirika husamehe. Yaani pamoja na kukasirika baada ya kukasirishwa, huwa tayari kusamehe baada ya kuombwa msamaha au hata bila ya kuombwa msamaha. Kwa ufupi ni wale wanaojitahidi kuzuia hasira na kuwasamehe binaadamu wenzao.


(iv) Wanaomuitikia Mola wao, yaani wanaomtii Mola wao ipasavyo kwa kutekeleza kila alilowaamrisha na kuacha kila alilowakataza kwa unyenyekevu. Kwa maana nyingine, wale wanaomuabudu Allah (s.w) ipasavyo katika kukiendea kila kipengele cha maisha yao.



(v)Wanaosimamisha Swala, yaani wanaodumu na ibada ya swala katika maisha yao yote kama alivyoitekeleza Mtume (s.a.w). kwa kuchunga masharti na nguzo za swala na kuswali kwa khushui.



(vi)Wanaoshauriana katika mambo yao. Yaani wale ambao wanapokuwa na jambo juu ya kuupeleka Uislamu mbele na kuusimamisha katika jamii, hulijadili na kila mtu akatoa ushauri na maoni yake na hatimaye hufikia muafaka na kuazimia kulitekeleza kwa kutegemea msaada wa Allah (s.w)



(vii)Wanaotoa katika yale waliyoruzukiwa na Allah (s.w). Yaani hutoa mali zao, nguvu zao, elimu zao, muda wao, na kila walichoruzukiwa na Allah (s.w) kwa ajili ya kuwahudumia na kuwasaidia binaadamu wenzie wanaohitajia msaada na kwa ajili ya kuusimamisha Uislamu, kuuendeleza na kuulinda.



(viii)Wale wanaotetea nafsi zao baada ya kufanyiwa jeuri. Yaani wale ambao hawakubali kudhulumiwa haki zao kirahisi, bali hufanya juhudi za makusudi za kupambana na dhalimu mpaka wapate haki zao.




                   






           

Je! umeipenda hii post?
Ndio            Hapana            Save post

Rajabu Tarehe 2024-05-10 14:53:23 Download PDF     Share On Facebook or Whatsapp Imesomwa mara 595


Sponsored links
👉1 kitabu cha Simulizi     👉2 Kitabu cha Afya     👉3 Kitau cha Fiqh     👉4 Madrasa kiganjani    

Post zifazofanana:-

Kumuamini malaika wa mwenyezi Mungu
Nguzo za Imani (EDK form 2: dhana ya elimu ya uislamu) Soma Zaidi...

Kujiepusha na kukaribia zinaa
Si zinaa tu iliyoharamishwa bali hata yale yote yanayotengeneza mazingira na kuchochea kufanyika kwa zinaa nayo pia yameharamishwa. Soma Zaidi...

Kuamini vitabu vya mwenyezi Mungu (s.w)
Nguzo za Imani (EDK form 2: Dhana ya elimu ya uislamu) Soma Zaidi...

KUAMINI VITABU VYA ALLAH (S.W)
Mtu hawi Muumini wa kweli mpaka awe na yakini juu ya vitabu vya Allah (s. Soma Zaidi...

Maana ya Elimu katika uislamu na nani aliye elimika?
Hili ni swali kutoka katika maarifa ya elimu ya dini ya kiislamu kidato cha kwanza (EDK FORM 1) Soma Zaidi...

DUA YA 1 - 10
1. Soma Zaidi...

Kuamini mitume wa mwenyezi Mungu
Nguzo za Imani (EDK form 2:. Dhana ya elimu ya uislamu Soma Zaidi...

mgawanyiko wa elimu
Soma Zaidi...

Kujiepusha na Shirk
Shirki ni kitendo chochote cha kukipa kiumbe nafasi ya Allah (s. Soma Zaidi...

Kwanini Uislamu Ndio Dini Pekee Inayostahiki Kufuatwa na Watu?
Soma Zaidi...

Makemeo juu ya Zinaa na Hukumu kwa Wazinifu.
Tendo la zinaa ni tendo chafu kimaadili na Allah (s. Soma Zaidi...

Kuongea na Allah (s.w) nyuma ya Pazia
Hii ni njia ambayo mwanaadamu huongeleshwa moja kwa moja na Allah (s. Soma Zaidi...