Yanayoharibu au Kupunguza Thamani ya Funga


Yanayoharibu funga ya mtu au kupunguza thamani yake ni kujiingiza katika mazungumzo yaliyokatazwa kama vile kusengenya, kusema uwongo, kupiga porojo, n.k., na kujiingiza katika matendo maovu. Japo mtu mwenye kufanya matendo haya atajiona amefunga kwa vile atakuwa hajala, au hajanywa au hajafanya kitendo chochote katika vile vinavyobadtilisha funga atakuwa hana funga au hakupata malipo ya funga kwa ushahidi wa Hadith ifuatayo:


Abu Hurairah(r.a) ameeleza kuwa Mtume wa Allah amesema: “Yoyote yule ambaye hataacha mazungumzo mabaya na vitendo viovu, Allah (s.w) hana haja na kuacha kwake chakula chake na kinywaji chake (Allah (s.w) hatapokea funga yake). (Bukhari).


Wakati mmoja Mtume (s.a.w) aliwaamuru watu wawili wafuturu (wavunje funga) kwa sababu walikuwa wanasengenya.
Wanachuoni wameshindwa kutoa uamuzi kuwa mtu akizungumza maneno maovu na machafu au akijiingiza katika matendo maovu, atakuwa amefungua kwa sababu ni vigumu kujua matendo ya ndani ya mtu. Hivyo, japo hapatakuwa na mtu yeyote atakayekuambia umefungua kwa kufanya vitendo viovu, wewe mwenyewe ujihesabu kuwa hukupata kitu kutokana na funga yako kama Mtume (s.a.w) anavyotufahamisha katika hadith ifuatayo:


“Abu Hurairah (r.a) ameeleza kuwa Mtume wa Allah amesema: Ni watu wangapi wanaofunga, lakini hawana funga ila huambulia kiutu ...” (Darimi).
Mfungaji anatakiwa, ili funga yake iweze kutimia na kufikia lengo, ajiepushe na mambo yote maovu na machafu. hata akichokozwa na mtu, ajiepushe kugombana naye kwa kumwambia, “Nimefunga, nimefunga” kama anavyotushauri Mtume (s.a.w):


Abu Hurairah (r.a) ameeleza kuwa Mtume (s.a.w) amesema: Wakati mmoja wenu atakapoamka akiwa amefunga, asitumie au asitoe lugha chafu na asifanye matendo maovu. Na kama yeyote yule anamchokoza au anagombana naye, hana budi kusema: “Nimefunga, nimefunga.”