NAMNA AMBAVYO MALARIA HUTOKEA

Kama tulivyokwisha kuona kuwa malaria inaweza kuambukizwa kwa kung'atwa na mbu aina ya anophelesi. basi tambua kuwa ni mbu jike tu ndiye huweza kuambukiza malaria.  basi hapa nitakueleza namna ambavyo malaria huweza kutokea.

 

kwanza kabisa lazima kuwepo kwa vimelea vya malaria aidha kwa mtu ama kwenye mwili wa mbu jike aina ya anophelesi. vimelea hivi vya malaria vinaanza kuzaliana kwenye mwili wa mbu jike. baada ya siku 10 mpaka 18 vimelea hivi vinakomaa na kuwa kimelea kipya kinachojulikana kama sporozoite. Kisha hivi vimelea vingi vinahamia kwenye tezi za mate za mbu na hatimaye kuingia kwenye mate ya mbu.

 

Mdomo wa mbu una mirija mikuu miwiliu. Mmoja ni wa kunyonyea damu na mwingine ni wa kutolea mate. Wakati anapong'ata mtu mate yake huingia kwenye mwili wa mtu. Mate haya yakiwa yana vimelea vya malaria (sporozoite) vijidudu hivi huingia kwenye mwili wa mtu. Na hapa hatua nyingine ya vimelea hivi inaanza.

 

Vimelea hivi (sporozoite) vinapoingia kwenye mwili wa mtu moja kwa moja vinaelekea kwenye ini. na huko huanza kukuwa na kuwa schizonts baadaye hupasuka na kutoa merozoites hivi ni vimelea vipya vilivyokomaa. vimelea hivi kama havitapatiwa dawa ya kuondolewa vitaendelea kwenye mfumo wa damu na kuanza kushambulia seli nyekundu za damu.

 

Baada ya merozoite kupatikana huelekea kwenye mfumo wa damu na kuanza kushambulia seli hai nyekundu za damu na kuanza kuzaliana humo kwa mara nyingine na kuleta vimelea vipya vitambulikavyo kama schizont na baadaye kupasuka na kutoa vimlea waitwao merozoites.

 

Na hapa sasa vimelea hawa wapya wanaanza kushambulia seli hai nyekundi na kuzaliana humo kisha seli hupasuka na kuleta vimelea wengi zaidi. Na kuanzia hapa ndipo mgonjwa sasa ataanza kuona dalili za malaria kama homa, maumivu ya kichwa, tumbo, misuli na viungo, kichefuchefu, kutapika na kuharisha.

 

Kama vimelea hivi havitatibiwa athari zaidi itatokea na kuanza kushambulia maeneo mengine ya mwili kama ini, figo, mapafu na moyo. hapa mgonjwa ataweza kuchanganyikiwa, matatizo ya ini na figo, kupumua kwa shida ama kuhohoa. Kama mgonjwa hatatibiwa athari zaidi inaweza kutokea kama kupoteza fahamu na hatimaye kifo.