Wanaoongozwa na Qur-an:



Lengo la kushushwa Qur-an kama ilivyobainishwa katika Qur-an yenyewe ni kuwaongoza binaadamu wote katika njia iliyonyooka. Njia iliyonyooka ni njia sahihi ya maisha itakayomuwezesha binaadamu kufikia lengo la kuumbwa kwake. Pamoja na Qur-an kuwa muongozo kwa watu wote, haiwaburuzi kwa nguvu kwenye uongofu bila ya wao wenyewe kudhamiria kuongoka.Qur-an huongoza wacha-Mungu tu kama tunavyojifunza katika aya zifuatazo:


"Hiki ni kitabu kisichokuwa na shaka ndani yake, ni uwongozi kwa wamchao Mwenyezi Mungu.Ambao huyaamini yasiyoonekana (maadam yamesemwa na Mwenyezi Mungu na Mtume wake) na husimamisha Swala na hutoa katika yale Tuliyowapa.Na ambao wanaamini yaliyoteremshwa kwako na yaliyoteremshwa kabla yako na wanaamini (kuwa iko) Akhera. Hao wako juu ya uongozi utokao kwa Mola wao, na hao ndio wenye kufaulu." (2:2-5)



Kwa mujibu wa aya hizi wanaongozwa na Qur-an ni wacha-Mungu wenye sifa zifuatazo:
- Waumini wa kweli wa vipengele vyote vya nguzo za Imani. - Wasimamishaji Swala. (Rejea juzuu ya pili).
- Wanaotoa yale aliyowaruzuku Allah (s.w) kwa ajili ya kuwahurumia wanaadamu wenye kuhitajia msaada na katika kusimamisha Dini ya Allah(s.w). Aliyoturuzuku Allah (s.w)ni kila tulichonacho ikiwa ni pamoja na mali, elimu, afya, nguvu,vipaji na kadhalika.


Wasioongozwa na Qur-an:
Tunajifunza katika Qur-an kuwa makundi mawili ya watu Makafiri (na washirikina) na Wanafiki hawataongozwa na Qur-an. Kuhusu makafiri na washirikina tunafahamishwa:


Hakika wale waliokufuru ni sawa kwao ukiwaonya (kwa hii Qur-an) au usiwaonye; hawataamini. (Kama kwamba) Mwenyezi Mungu amepiga muhuri juu ya nyoyo zao na juu ya masikio yao; na juu ya macho yao pana vifuniko; basi watakuwa na adhabu kubwa. (2:6-7)



Pamoja na Qur-an kuwa na sifa ya ukweli na uwazi kama majina yake yanavyodhihirisha, haiwezi kuwaongoza wapinzani (makafiri) wa wazi wa Mwenyezi Mungu(sw) na ujumbe wake. Haiwezi kwa sababu binaadamu amepewa uhuru na Mola wake wa kuamua na kufanya atakavyo. Akiamua kutii anaweza na akiamua kuasi anaweza. Hivyo mtu aliyeamua kuukataa mwongozo huu kwa makusudi huna namna ya kumuongoza.



Kuhusu wanafiki tunafahamishwa:


"Na katika watu, wako (wanafiki) wasemao "Tumemuamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho" na hali ya kuwa si wenye kuamini. Wanataka kumdanganya Mwenyezi Mungu na wale walioamini, lakini hawadanganyi ila nafsi zao, nao hawatambui. Nyoyoni mwao mna maradhi, na Mwenyezi Mungu amewazidishia maradhi. Basi watakuwa na adhabu iumizayo kwa sababu ya kule kusema kwao uongo.(2:8-10)


Na wanapoambiwa msifanye uharibifu ulimwenguni Husema "Sisi ni watengenezaji." Hakika wao ndio waharibuji, lakini hawatambui. Na wanapoambiwa: "Aminini kama walivyoamini watu, "husema "Oh! Tuamini kama walivyoamini wapumbavu?" Hakika wao ndio wapumbavu lakini hawajui. (2:11-13)


Na wanapokutana na walioamini husema, "Tumeamini," na wanapokuwa peke yao kwa mashetani wao husema: "Hakika sisi tu pamoja nanyi, tunawacheza shere tu." Na Mwenyezi Mungu atalipa shere yao na kuwawacha katika upotofu wao wakitangatanga ovyo. Hao ndio waliokhiari upotofu kuliko uongofu, lakini biashara yao haikupata faida wala hawakuwa wenye kuongoka." (2:14-16)



Wanafiki pamoja na kujiita Waislamu na pengine wakawa ni wanachuoni wa Qur-an walio mahiri katika kuifasiri Qur-an kwa kutumia balagha, mantiq, sarfu, n.k; hawataongozwa na Qur-an maadamu wamekhiari maslahi ya dunia kinyume na mwongozo wa Mwenyezi Mungu(sw). Si tu hawa wasomi wa Qur-an wenye sifa hizo zilizoainishwa katika aya hizi hawataongozwa na Qur-an bali pia Allah (s.w) amewafananisha na mbwa katika aya zifuatazo:


"Na wasomee (Ewe Muhammad) habari za wale tuliowapa Aya zetu (kuzijua), kisha wakajivua nazo (wasizifuate). Na shetani akawaandama na, wakawa miongoni mwa waliopotea.Na kama tungelitaka tungeliwanyanyua kwazo, lakini wao waligandamana na ardhi (kutaka maslahi ya kidunia wakayapuuza ya Akhera) na wakayafuata matamanio yao. Basi hali yao ni kama hali ya mbwa; ukimpigia kelele (hukimbia na huku) anahema, na ukimwacha pia huhema.Hiyo ndio hali ya watu waliokadhibisha Aya zetu. Basi simulia hadithi, huenda wakatafakari. "(7:1 75-176)



Hivyo, kwa mujibu wa Aya hizi, mnafiki hata akiwa ni A’alim (Sheikh) wa Qur-an na Hadith, kamwe hawezi kuongozwa na Qur-an.