image

Historia ya kushuka kwa quran

Historia ya kushuka kwa quran

Historia ya Kushuka Qur-an:



Qur-an ilianza kumshukia Mtume Muhammad (s.a.w) mwaka 610 A.D. alipokuwa na umri wa miaka 40. Mtume Muhammad (s.a.w) alianza kushushiwa Qur-an akiwa pangoni katika mlima Hira (Jabal Hira) katika usiku wa mwezi wa Ramadhani kama Qur-an yenyewe inavyotufahamisha:


Ni mwezi wa Ramadhani ambamo imeteremshwa hii Qur-an (2:185)



"Hakika Tumeiteremsha (Qur-an) katika Laylatul-Qadr (usiku wenye hishima kubwa). Na jambo gani litakujulisha (hata ukajua) ni nini huo usiku wenye hishima kubwa? Huo usiku wa hishima ni bora kuliko miezi elfu. Huteremka Malaika na roho (Jibriil) katika usiku huo kwa idhini ya Mola wao kwa kila jambo. Ni amani (usiku) huo mpaka mapambazuko ya alfajiri." (9 7:1-5)



Tunajifunza kutokana na aya hizi kuwa mwezi wa Ramadhani umetukuzwa kutokana na Qur-an kuanza kushuka katika mwezi huu. Pamoja na funga kufaradhishwa kwa umma za Mitume wote wa Allah (s.w); kwa ummat Muhammad (s.a.w),funga imefaradhishwa iwe katika mwezi wa Ramadhani ili iwe ni pamoja na kusherehekea kushuka kwa Qur-an na kilele cha sherehe hii kinakuwa katika usiku wa hishima (Laylatul-Qadr) ambamo Qur-an ilianza kushuka. Mtume (s.a.w) alikuwa akizidisha kusoma Qur-an katika mwezi huu na alikuwa akikaa Itiqaf katika kumi la mwisho la Ramadhani ili aweze kudiriki kilele cha sherehe. Usiku wenye hishima (Laylatul-Qadr) ulifichwa kwa Mtume (s.a.w) lakini alifunuliwa na Mola wake kuwa unapatikana katika kumi la mwisho la Ramadhani. Ni sunnah kwa Waislamu kuzidisha kusoma Qur-an katika mwezi mzima wa Ramadhani na kukaa Itiqaf katika kumi la mwisho, ili kushiriki kikamilifu katika sherehe ya kumbu kumbu ya kuanza kushuka Qur-an.


Historia ya kuanza kushuka Qur-an kwa Mtume Muhammad (s.a.w) kupitia kwa Malaika Jibril (a.s) inasimuliwa vyema katika Hadith ya bibi 'Aisha (r.a) ifuatayo:
Bibi 'Aisha (r.a) amesema:" Kilichoanza katika Wahyi wa Mtume (s.a.w) ni ndoto za kweli. Alikuwa Mtume (s.a.w) haoti chochote isipokuwa kilitokea kama alivyoota. Kisha akaona ni bora kujitenga. Akawa anakwenda Jabal Hira kujilinda na maovu. Basi alikuwa anakwenda Jabal Hira akifanya ibada masiku mengi na alichukua masurufu kwa ajili hiyo. Masurufu haya kila yalipokwisha alirudi tena kwa Bibi Khadija, aliyemtayarishia masurufu kama yale (ya kwanza) mpaka ikambainikia haki akiwa pangoni Hira. Basi akamjia Malaika (Jibril) humo pangoni akamuamrisha kusoma, Mtume (s.a.w) alijibu: "Sijui kusoma". Alinibana kwa nguvu mpaka nikahisi taabu. Kisha akaniachia na kuniamrisha tena kusoma na nikajibu: Sijui kusoma: Kisha akanibana tena kwa nguvu kwa mara ya pili mpaka nikahisi taabu. Kisha akaniachia na kuniamrisha tena kusoma. Nilijibu tena, "sijui kusoma". Akanikumbatia tena kwa nguvu kwa mara ya tatu mpaka nikahisi mashaka, kisha akaniachia na akasema:


"Soma kwa jina la Mola wako aliyeumba. Amemuumba mwanaadamu kwa pande la damu. Soma na Mola wako ni Karimu sana.Ambaye amefundisha kwa msaada wa kalamu.Amemfundisha mwanaadamu mambo aliyokuwa hayajui." (96:1-5)



Mtume wa Mwenyezi Mungu alirejea na Wahy huu, huku akitetemeka kwa khofu aliyokuwa nayo. Alikwenda kwa mkewe Khadijah na akamhadithia yale yote yaliyomtokea kisha akasema;


"Nakhofia kuwa kitu kinaweza kunitokea ". Khadijah alijibu: "Hapana! Naapa kwa jina la Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu hatakufedhehesha. Unakaa vizuri na kuwafanyia wema ndugu na jamaa zako, unawasaidia masikini na fukara, unawakirimu wageni na unawasaidia waliokabiliwa na matatizo. "Kisha Bibi Khadijah alimchukua Mtume (s.a.w) mpaka kwa bin-ami yake, Waraqa bin Naufal bin Asad bin Abdul Uzza, ambaye alikuwa Mkristo. Waraqa wakati huo alikuwa mzee sana na alikuwa hawezi kuona tena. Khadijah alimuambia Waraqa "Sikiliza hadithi ya mpwa wako, Ewe Bin-ami yangu" Waraqa aliuliza, "Ewe Mpwa wangu umeona nini?" Mtume wa Mwenyezi Mungu alimuhadithia habari yote kama alivyoona. Waraqa akasema: "Huyu ni yule mtunza siri (Malaika Jibril) ambaye Mwenyezi Mungu alimtuma kwa Mussa. Natamani ningelikuwa kijana na kuishi mpaka wakati huo watu wako watakapokukataa na kukufukuza." Mtume wa Mwenyezi Mungu akauliza: "Watanifukuza?" Waraqa akajibu kuwa watafanya hivyo na akasema, "Yeyote aliyekuja na kitu kama hicho ulichokuja nacho alifanyiwa uadui na watu wake, na ningejaaliwa kubakia hai mpaka siku hiyo watu wako watakapokufukuza, ningelikusaidia kwa hali na mali." Lakini baada ya muda mfupi Waraqa alifariki na Wahyi mwingine ulikawia kuja kwa kipindi kirefu. (Sahihi Bukhari)
Tunajifunza kutokana na Hadith kuwa kabla Mtume (s.a.w) hajaanza kushushiwa Qur-an kupitia kwa Malaika Jibril (a.s) alikuwa akipata Wahy kwa njia ya ndoto.
Qur-an yote kwa ujumla imehifadhiwa katika ubao mtukufu wa Allah (s.w) ulio katika Arshi yake kama tunavyofahamishwa katika Qur-an:


"Bali hii ni Qur-an tukufu iliyotolewa katika Lawhi Mmahfuudh (huo ubao uliohifadhiwa)." (85:21-22)


Kisha kutoka Lawhi Mmahfuudh Qur-an ilishushwa mpaka wingu wa kwanza. Kisha kutoka humo ikashushwa kidogo kidogo kwa Mtume (s.a.w) kupitia kwa Malaika Jibril (a.s) kwa kipindi chote cha Utume cha miaka 23.


"Kwa hakika hii (Qur-an) ni kauli (aliyokuja nayo) Mjumbe Mtukufu (Jibril), Mwenye nguvu na cheo cha hishima kwa Mwenyezi Mungu. (81:19-20)
Kama tunavyojifunza katika Hadith,aya za mwanzo kumshukia Mtume (s.a.w) ni aya tano za mwanzo za suratul-’Alaq. Aya zilizofuatia katika sura hii (96:6-19) zilishuka siku za baadaye.



Aya ya mwisho kumshukia Mtume (s.a.w) alipokuwa katika Hija ya kuaga (Hijjatul Wadaai) ni aya ya tatu ya suratul Maida (5:3) ambayo imeashiria mwisho wa wahy wa Qur-an katika sehemu ifuatayo:


Leo waliokufuru wamekata tamaa katika dini yenu, basi msiwaogope, bali niogopeni mimi. Leo nimekukamilishieni dini yenu, na kukutimizieni neema yangu, na
nimekupendeleeni Uislamu uwe dini yenu (5:3)



Pia tunajifunza kutokana na historia ya kushuka Qur-an kuwa sura ya kwanza kushuka nzima (ikiwa na aya zote) ni Suratul-Fatiha (Al-hamdu) na imekuwa ndio sura ya kwanza katika msahafu. Katika mtiririko wa kushuka suratul-Fatiha ni Wahy wa tano. Sura ya mwisho kushuka ikiwa nzima ni Suratun-Nasr, sura ya 114 katika utaratibu wa kushuka (rejea Jedwali 2 na 3).




                   






           

Je! umeipenda hii post?
Ndio            Hapana            Save post

Rajabu Tarehe 2024-05-10 14:53:23 Download PDF     Share On Facebook or Whatsapp Imesomwa mara 1914


Sponsored links
πŸ‘‰1 kitabu cha Simulizi     πŸ‘‰2 Kitau cha Fiqh     πŸ‘‰3 Madrasa kiganjani     πŸ‘‰4 Kitabu cha Afya    

Post zifazofanana:-

Maana ya Quran na Majina ya quran n amaana zao
Soma Zaidi...

Uthibitisho kuwa quran ni maneno ya Allah kutokana na Historia (Hadith)
Soma Zaidi...

HUKUMU ZA IDGHAM
Jifunze namna ya kusoma quran, pata mafunzo ya tajwid hapa Soma Zaidi...

Sababu za Kushuka Surat Al-Masad (tabat yadaa) na fadhila zake
4. Soma Zaidi...

Hukumu za waqfu na Ibtida
waqfu ni misimamo ambapo msomaji wa Quran anaruhusiwa kusimama, kuhema au kumeza mate. Na ibtidai ni kuanza baada ya kutoka kwenye waqf Soma Zaidi...

HUKUMU ZA MADD
Jifunze namna ya kusoma quran, pata mafunzo ya tajwid hapa Soma Zaidi...

Adabu za kusikiliza quran
ADABU ZA KUSIKILIZA QURANI 1. Soma Zaidi...

Sababu za kushuka surat al-Fiyl
Al fiyl ni neno la Kiarabu lenye maana ya tembo. Sura hii inazungumziakisa cha jeshi lenye tembo. Jeshi hili lilikuwa na nia ya kuvunja al qaaba Soma Zaidi...

Hukumu ya Ikhfau katika tajwid
Ikh-fau ni moja ya hukumu za nun sakina na tanwin kwenye hukumu za Quran tajwid Soma Zaidi...

HUKUMU ZA TAFKHIIM NA TARQIQ
Jifunze namna ya kusoma quran, pata mafunzo ya tajwid hapa Soma Zaidi...

Kwa nini quran ilishuka kidogo kidogo?
Kuna sababu nyingi za kuonyesha umuhimu wa Quran kushuka kwa mfumo wa kidogo kidogo Soma Zaidi...

Sababu za kushuka kwa surat al-Fiil
SURAT AL-FIILSura hii imeteremshwa Makkah na ina Aya Sita pamoja na Basmallah. Soma Zaidi...