Namna ya kuhiji, hatua kwa hatua

Namna ya kuhiji, hatua kwa hatua

KUTEKELEZA IBADA YA HIJA HATUA KWA HATUA


Ihram:



Tumejifunza kuwa Ihram ni vazi rasmi kwa ajili ya Hija na Umra na pia Ihram ni hali anayokuwa nayo mwenye kuhiji au kufanya Umra ambapo analazimika kuchunga mambo mbali mbali. Ihram kama vazi ni zoezi kubwa sana la kuwakumbusha waumini kwa vitendo juu ya usawa wa binaadamu. Bila shaka ubaguzi wowote, hali ya tajiri na maskini, mfalme na raia, afisa na mtumishi, mweusi na mweupe nakadhalika, wanaume wote huvalia vazi la aina moja ambalo ni shuka ya kufunga kiunoni na nyingine ya kuteremsha lubega, kuacha wazi kichwa na kuvalia makubazi (malapa) au viatu vya wazi (sandles) bila ya soksi. Wakati wote Mahujaji wanapokuwa katika vazi hili wanathibitisha kwa matendo ujumbe wa Mwenyezi Mungu (s.w) ufuatao:



Enyi watu! Kwa hakika tumekuumbeni (nyote) kwa (yule) mwanamume (mmoja, Adam) na yule mwanamke (mmoja Hawwa). Na tumekufanyeni mataifa na makabila (mbali mbali) ili mjuane (tu basi, sio kubaguana). Hakika aheshimiw aye sana miongoni mw enu mbele ya Mw enyezi Mungu ni yule amchaye Mwenyezi Mungu zaidi katika nyinyi. Kwa yakini Mw enyezi Mungu ni Mjuzi, Mw enye habari (za mambo yote). (49:13)



Katika kuchunga masharti mbali mbali anapokuwa katika hali ya Ihram Haji hupata mazoezi ya hali ya juu ya utii kwa Mwenyezi Mungu (s.w). Tumejifunza kuwa Hajj anapokuwa katika hali ya Ihram, Haji hukatazwa kufanya matendo ya kuchana nywele na kunyoa. Je, mtu aliyejizatiti katika kuchunga masharti haya madogo madogo kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (s.w) kwa muda wote anapokuwa katika ihram, itakuwa vigumu kwake kujiepusha na makatazo yote ya Mwenyezi Mungu (s.w) katika kuendesha maisha yake ya kila siku baada ya Hija? Isitoshe Hajj, aweza kuvunja mojawapo ya masharti haya bila ya yoyote kumbaini lakini bado hafanyi hivyo. Ikitokea kwa bahati mbaya kavunja sharti mojawapo, bila ya kushitakiwa na mtu yoyote yeye mwenyewe hujihukumu na kujiadhibu kwa kutoa fidia (faini) kwa kuchinja mnyama na kutoa sadaqa au kwa kutoa chakula kuwalisha maskini au kufunga. Je, huoni kuwa kuchunga masharti ya ihram pia humzoesha Hajj kuwa muadilifu na mcha-Mungu mwenye kuchunga mipaka ya Mwenyezi Mungu (s.w) pasi na usimamizi wowote katika kuendesha maisha yake ya kila siku?



Kwa hiyo, tunajifunza kuwa, ambapo vazi la Ihram linampa Haji mazoezi ya kudumisha usawa kati ya wanaadamu na kukata mzizi wa ubaguzi wa aina yoyote na majivuno, uchungaji wa masharti ya ihram, unampa Haji zoezi la kumtii Mwenyezi Mungu (s.w) kwa uadilifu katika kuacha makatazo yake na kufuata maamrisho yake katika kuendesha maisha yake ya kila siku.



Talbiya



Talbiya ni kuitikia wito wa Mwenyezi Mungu (s.w) kwa maneno yafu atayo:


Labbayka Allaahumma Labbayka. Labbayka laashariika laka labbayka. Innal-hamda wanni-imata laka wal-mulku; laashariika
laka.
'Naitika w ito w ako Ee Mw enyezi Mungu, Naitika. Naitika, ewe us iye na Mshirika, Naitika. Hakika sifa zote njema na neema zote ni Zako na Ufalme ni wako, Ewe Usiye na mshirika.' (Bukhari na Muslim).



Kutekeleza nguzo ya Haji ni kuitika wito wa Mwenyezi Mungu (s.w) ambaye alimuamrisha Nabii Ibrahim (a.s), mwanzilishi wa Ibada ya Hija, kuwaita watu wote ulimwenguni waje kuhiji Makka katika nyumba takatifu, Al-Ka'aba. Mwito huu umedhihirishwa katika aya ifuatayo:



'Na (Tukamwambia Ibrahim), utangaze kwa watu habari za Hijja, watakujia (wengine) kwa miguu na (wengine) juu ya kila mnyama aliyekonda, wakija kutoka katika kila njia ya mbali. (22:27)


Talbiya, inampa haji zoezi la kumuitika Mwenyezi Mungu (s.w) katika maamrisho yake yote. Je, mtu anayejitoa muhanga kwa kumuitikia Mwenyezi Mungu (s.w) kwa kufunga safari nzito ya Hija, atashindwa baada ya kurejea nyumbani, kumuitikia Mwenyezi Mungu (s.w) katika miito mingine iliyo miepesi zaidi kama vile mwito wa kusimamisha swala tano, kutoa Zaka, kufunga Ramadhani na miito ya kiutekelezaji katika maisha ya kila siku.



Talbiya ambayo makundi kwa makundi ya Waislamu huitamka pamoja wakiwa na vazi la sare (Ihram) wakati wakiwa katika msafara wa kutekeleza Ibada ya Hija, huwahamasisha Waislamu na kuwakumbusha kuwa wao ni askari wa Mwenyezi Mungu (s.w) ambao ni tishio la maadui wa Mwenyezi Mungu ulimwenguni kote kutokana na umoja na mshikamano wao uliojengwa katika msingi thabiti ya kumuamini na kumwitikia Mwenyezi Mungu (s.w) pekee. Historia inatuthibitishia jin si Waislamu walivyokuwa tishio kwa washirikina wakati Waislamu walipofunga safari ya Umra, mwaka wa 6 A.H. na kuzuiliwa kuingia Makka na Makuraysh waliojizatiti kwa vita. Bila ya silaha, Waislamu kwa umoja wao na uthabiti wao katika kumuitikia Mwenyezi Mungu (s.w) na Mtume wake walichukuwa ahadi mbele ya Mtume (s.a.w) kupambana na washirikina hawa kama tunavyojifunza katika aya ifuatayo:



Hakika Mw enyezi Mungu am ekuw a radhi na Waislam u w alipofungam ana nawe chini ya mti; na anajua yaliyomo nyoyoni mw ao. Basi akateremsha utulivu juu yao, na akawapa kushinda kwa zama za karibu. (48:18).



Washirikina wa Makka, pamoja na silaha zao, waliogopa kupigana na Waislamu ambao hawakuwa na silaha na badala yake wakawekeana mkataba wa amani - mkataba wa Hudaybiyyah. Miaka miwili baada ya Hudaybiyyah, mwaka wa 8 Hijiria. Waislamu elfu kumi waliiteka Makka kwa Tahalili na Takbir bila ya kutumia silaha. Umoja wa jeshi hili la Waislamu, uliodumishwa na kalima ya 'Laailaaha illallahu allaahu Akbar' ulikuwa ni tishio kwa washirikina wa Makka ambao walijifungia ndani kwa khofu na kuwawezesha Waislamu kuikomboa Makka na Ka'aba kwa amani bila ya kumwaga hata tone la damu katika mji Mtakatifu.



Tawaf



Haji anapoingia Makka huendelea na Talbiya mpaka atakapofika kwenye Jiwe Jeusi na kulibusu au kuliashiria tayari kuanza tawaf. Tawaf ni ibada ya kuizunguka Ka'aba mara saba. Kila mzunguko huanza kwenye Jiwe Jeusi kwa kulibusu, au kuligusa kwa fimbo au kuliashiria. Jiwe Jeusi ndio jiwe la msingi la nyumba takatifu ya Al-Ka'aba.Kuna mafunzo mengi yanayopatikana katika tawaf.



Kwanza, kule kuishuhudia Ka'aba na mazingira yake, hasa sehemu ile iitwayo 'Maqamu Ibrahim', mahali aliposimama Nabii Ibrahim wakati wa kuinua kuta za Ka'aba, humpelekea Haji kuwa na yakini zaidi juu ya kuwepo Mwenyezi Mungu (s.w). Kwa maana nyingine Muislamu aliyeitikia wito wa Hija kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (s.w), kuwemo katika mazingira ya Ka'aba huzikurubisha fikra zake kwa Mwenyezi Mungu (s.w) kuliko anapokuwa katika sehemu nyingine yoyote katika ardhi. Mwenyezi Mungu (s.w) anabainisha hili katika Qur-an:



Kwa yakini Nyumba ya kwanza iliyowekwa kwa ajili ya watu (kufanya ibada) ni ile iliyoko Makka, yenye baraka na uwongozi kwa ajili ya walimwengu wote. Humo mna ishara zilizo wazi (za kuonyesha utukufu wake na ukongwe wake. Miongoni mwa hizi ni) mahali alipokuwa akisimama Ibrahim, na anayekuwa katika sehemu hiyo huwa katika amani' (3:96-97)


Pili, kitendo cha kutufu, endapo kitafanywa kwa kumzingatia Mwenyezi Mungu (s.w) kwa undani kama mazingira yenyewe yanavyoruhusu, humpa Haji zoezi kubwa la kumdhukuru na kumtukuza Mwenyezi Mungu (s.w) katika kiwango cha juu kabisa kama kile cha Malaika. Tunafahamishwa katika Hadithi kuwa Ka'aba ni nakala halisi ya Baitil-Ma'amuur, nyumba tukufu ya Mwenyezi Mungu (s.w) iliyopo Mbinguni ambayo daima kuna makundi ya Malaika yanayomdhukuru Mwenyezi Mungu (s.w) mpaka siku ya Kiyama. Hivyo Mahujaji wakitufu kwa kumzingatia Mwenyezi Mungu (s.w) na wakasimama kwa swala katika Maqamu Ibrahim baada ya Tawaf, hufanya kitendo kile kile wanachokifanya Malaika katika mbingu ya saba.



Tatu, kitendo cha kubusu Jiwe Jeusi kila mutawaf anapoanza mzunguko, ni kitendo cha kuchukua ahadi upya kwa Mwenyezi Mungu (s.w) kuwa atamuabudu ipasavyo na hatamshirikisha na yeyote au chochote katika maisha yake yote. Kuhusu ahadi hii, imebainishwa katika hadithi iliyosimuliwa na ibn Abbas kuwa Mtume wa Mwenyezi Mungu amesema: 'Jiwe Jeusi ni mkono wa kuume wa Mwenyezi Mungu hapa ardhini, kwa mkono huo anapeana mkono waja wake, kama ambavyo mtu anavyopeana mkono ndugu yake.



Nne, Ibada ya Tawaf, ambayo Waislamu kutoka sehemu mbali mbali za dunia, wenye rangi na lugha tofauti huifanya kwa pamoja bega kwa bega, wanaume na wanawake, matajiri na masikini, wafalme na raia, weusi na weupe, wenye nguvu na dhaifu, bila ya ubaguzi wa aina yoyote, inatoa zoezi kubwa la kuwawezesha Waislamu kudumisha udugu na umoja wa Waislamu na usawa wa binaadamu.



Funzo hili la udugu, umoja na usawa linalopatikana katika ibada ya Tawaf, linadhihiri katika matendo mengine ya Hija ambapo Waislamu huyafanya kwa pamoja kama vile tendo la Sai, Kusimama Arafa na Kutupwa mawe katika Minara mitatu. Tunajifunza kutokana na matendo haya ya Hija kuwa, udugu, umoja na usawa halisi na wa kweli kati ya wanaadamu haupatikani mahali popote au kwa njia yoyote ila chini ya bendera ya 'Laailaaha illaallaahu Muhammaadar-rasuulullaah' kwa kumuabudu Mwenyezi Mungu (s.w) ipasavyo kwa pamoja na kushirikiana bega kwa bega kusimamisha ufalme wake hapa ulimwenguni.



Sa'i
Sai ni ibada ya kutembea mara saba kati ya vilima viwili - Safa na Marwa, vilivyo karibu na Ka'aba - ambapo kuna kukimbia matiti kwa wanaume katika sehemu ya bondeni.


Kitendo hiki cha Sai kinawawezesha Waislamu, Kumtii Mwenyezi Mungu (s.w) kwa kuwa tayari kutekeleza kila wanaloamrishwa.



Pili, kukimbia matiti (jogging) kunawapa Waislamu wanaume mazoezi na kuwakumbusha kuwa kupigana kwa uhodari na ushujaa kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (s.w) kumelazimishwa juu yao, kama kulivyolazimishwa juu yao kusimamisha swala, kutoa Zaka, kufunga Ramadhani na Kuhiji. Rejea Qur-an


Mmelazimishwa kupigana vita (kwa ajili ya dini ya Mwenyezi Mungu). Nalo ni jambo zito kwenu. Lakini huenda mkachukia kitu, nacho ni kheri
kwenu. Na huenda mkapenda kitu nacho ni shari kwenu. Mungu ndiye anayejua (lakini) nyinyi hamjui. (2:216)


Tatu, ibada ya Sai inawazoesha Waislamu kuwa tayari kuhangaika kwa namna yeyote ile kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (s.w). Ili tulipate funzo hili vizuri, ni vyema tujikumbushe historia ya nabii Ibrahim (a.s), mwanzilishi wa Hija. Nabii Ibrahim (a.s) kama historia yake inavyosimuliwa katika Qur-an (Rejea juzuu ya tatu), alipewa na Mola wake amri nyingi na nzito, ambazo, kutokana na utiifu wake wa hali ya juu kwa Mola wake, alizitekeleza zote kwa moyo mkunjufu. Miongoni mwa amri hii ni ile ya kumwacha mkewe Hajrah na mtoto wake mchanga (Ismail) ambaye alikuwa ni mtoto pekee aliyekuwa naye, katika bonde kavu la Makka lisilokaliwa na mkazi yeyote na bila ya kuwaachia chochote, isipokuwa ulinzi wa Mwenyezi Mungu (s.w). Tukio hili la Nabii Ibrahim (a.s) kuwaacha ahli zake Makka pasi na msaada wowote limerejewa katika Qur-an:



'Mola wetu! Hakika mimi nimewaweka (nimewakalisha) baadhi ya kizazi changu (mwanangu Ismail na mama yake Hajrah) katika bonde (hili la Makka) lisilokuwa na mimea yoyote; katika nyumba yako takatifu (Al-Ka 'aba). Mola wetu! Wajaalie wasimamishe swala. Na ujaalie nyoyo za watu zielekee kwao (wapende kuja kukaa hapa ili pawe mji) na uw aruzuku matunda ili w apate kukushukuru '. (14;3 7)



Bibi Hajra aliyakinisha kuwa Nabii Ibrahim (a.s) hakuwaacha pale kwa kuwatupa tu ila ni katika kutekeleza amri ya Mwenyezi Mungu (s.w) alibakia pale na mtoto wake kwa ridhaa au kwa kauli ya Muumini: 'Nimesikia na Nimetii'. Baada ya Nabii Ibrahim (a.s) kutoweka, bibi Hajra na mtoto wake, pamoja na upweke waliokuwa nao, walishikwa na kiu kali, lakini hapakuwa na dalili yoyote ya kupata maji katika eneo lile. Alimwacha mtoto wake karibu na Ka'aba na akakimbilia kwenye kilima cha Safa kuwa pengine atapata mpita njia (msafiri) amsaidie maji kwa ajili ya mtoto wake na yeye mwenyewe. Alipoona katika kilima cha Safa hakufanikiwa kumuona mpita njia yoyote, alikimbilia kwa shauku kilima cha pili cha Marwa, ambapo pia hakufanikiwa kumuona mtu yoyote. Aliendelea kukimbia huku na huko katikati ya vilima hivi viwili mara saba bila ya mafanikio yoyote. Katika kilele cha mahangaiko na mwisho wa jitihada za kibinaadamu Mwenyezi Mungu (s.w) alijaalia chem.-chem hii pamoja na kukidhi haja ya bibi Hajra na mtoto wake, aliwavutia watu kufanya makazi katika sehemu ile na ikawa ndio jibu la Dua aliyoiomba nabii Ibrahim (a.s) wakati alipowaacha pale. (Rejea Qur-an 14:37). Chem chem, hiyo ambayo inajulikana kwa jina la Zam-zam, haijakauka tangia wakati huo na mpaka siku ya mwisho.
Haji, endapo ataiweka mbele yake historia hii wakati wa kusai, atapata zoezi kubwa litakalomuwezesha kuwa tayari kujitoa muhanga kwa nafsi yake na kwa nafsi ya wapenzi wake kwa ajili ya Mwenyezi Mungu (s.w).



Funzo analolipata Haji, wakati wa kunywa maji ya Zam-zam, endapo atakumbuka historia ya chanzo chake, ni kwamba Mwenyezi Mungu (s.w) hawatupi waja wake wema wala hakusudii kuwatesa kwa kuwapa maamrisho mengi na magumu, bali anawapa mazoezi yatakayowawezesha kuwa wacha-Mungu na kubakia katika hadhi yao ya ukhalifa wa Mwenyezi Mungu (s.w) hapa ulimwenguni.


Kupiga kambi Mina, Mwezi 8 Dhul-Hija



Mwezi 8 Dhul-Hajj, ya Tarwiya, Mahujaji wanapiga kambi Mina, ambapo wanashinda na kulala humo. Kitendo hiki huwazoesha Waislamu kuwa askari wa Mwenyezi Mungu (s.w) ambao daima watakuwa tayari kuacha majumba yao na starehe za kimji na kutoka kupigania dini ya Mwenyezi Mungu (s.w).
Kuzidisha kuleta talbiya humo kambini, kunatukumbusha kuwa mwanajeshi wa Kiislamu tofauti na wanajeshi wengine, anapokuwa vitani hafanyi ufisadi na ufasiqi, bali hubakia katika kumkumbuka Mwenyezi Mungu (s.w) na kuchunga mipaka yake ipasavyo.



Kusimama Arafa, Mwezi 9 Dhul-Hajj



Haji wote wanalazimika kukusanyika pamoja katika uwanja wa Arafa siku ya mwezi 9 Dhul-Hajj wakiwa wamevalia ihram. Shughuli kubwa zinazofanywa katika uwanja huu, pamoja na kumdhukuru Mwenyezi Mungu kwa wingi, ni kusikiliza khutba inayotolewa na kiongozi wa Hija wakati wa Adhuhuri na kuomba dua na maghfira baada ya swala ya Adhuhuri (ambayo huchanganywa na Asr) mpaka kutua kwa jua.



Zoezi hili la kusimama Arafa linawakumbusha Waislamu mkutano mkuu wa siku ya Kiyama ambapo atayeonekana bora na muheshimiwa mbele ya Mwenyezi Mungu (s.w) ni yule amchaye Allah (s.w) ipasavyo na akasimamisha au kujitahidi kusimamisha ufalme wa Mwenyezi Mungu (s.w) hapa ulimwenguni. Kwa maana nyingine siku hiyo, tofauti kati ya wanaadamu katika misingi ya taifa, lugha, rangi, hali na hadhi, haitakuwa na maana yoyote. Khutuba inayotolewa na Kiongozi wa Hija, ni katika kuwakumbusha Waislamu kukumbuka mkutano huo wa Siku ya Malipo ambamo walimwengu wote wa mwanzo na wa mwisho watahudhurishwa mbele ya Mola wao wakiongozwa na Mitume wao ili wakalipwe kulingana na walivyowajibika kwa Mola wao hapa ulimwenguni.



Kupiga Kambi Muzdalifa



Kitendo cha kulala Muzdalifa na kuamka asubuhi kuelekea Mina kwenye Mnara mkubwa na mawe saba mkononi, kinafanana sana na zoezi la askari wapiganaji waliojiandaa usiku kuwashambulia maadui asubuhi na mapema. Kwa hiyo Haji anapokuwa Muzdalifa na hasa wakati wa kuokota mawe kwa ajili ya kazi ya kesho yake - hana budi kukumbuka kuwa yeye ni askari wa Mwenyezi Mungu (s.w) anayetakiwa daima awe tayari kupambana na maadui wa dini Yake.


Kitendo cha kuomba dua au Kumuomba Mwenyezi Mungu (s.w) na kumtukuza kwa utukufu wake katika mash-arul-haram, kinamkumbusha kila mpiganaji katika jeshi la Mwenyezi Mungu (s.w) kuwa ushindi katika vita vya kupigania Dini ya Mwenyezi Mungu (s.w) haupatikani kwa kutegemea ubora wa silaha na uhodari wa wapiganaji tu, bali ni lazima pawe na kumtegemea Mwenyezi Mungu (s.w) na kumtii ipasavyo.



Kutupa Mawe Mina



Ibada ya kutupa mawe Mina, Minara Mitatu ambayo inamuwakilisha Shetani, hufanyika mwezi 10 Dhul-Hajj na siku tatu za tashriq zinazofuatia.
Zoezi hili la kutupa mawe, humkumbusha Muislamu wajibu wake wa kupambana na maadui wote wa Mwenyezi Mungu (s.w) watakaosimama kumzuilia kusimamisha Dini ya Mwenyezi Mungu (s.w) katika maisha ya kila siku. Aidha, zoezi hili ni kumbukumbu ya kitendo alichokifanya Nabii Ibrahim (a.s) alipokuwa akimfukuza Shetani alipokuwa akimfuata na kumlaghai ili amuasi Mola wake katika kutekeleza amri ya kumchinja mwanawe Ismail (a.s).



Waislamu hatuna budi kufahamu kuwa Dini ya Mwenyezi Mungu (s.w) ina maadui wengi sana na wa aina mbali mbali wanaotumia mbinu mbali mbali za kuihujumu na kuifanya isiwemo au iwe chini ya dini zao. Ni jukumu la Waislamu kuwafahamu maadui wa Dini yao, kufahamu mbinu na silaha wanazotumia maadui hao katika kuuhujumu Uislamu na kuwa tayari kupambana nao vikali kwa mali na nafsi.



Kuchinja Mnyama
Zoezi la kuchinja mnyama siku ya mwezi 10 Dhul-Hajj ni zoezi la utii kwa Mwenyezi Mungu (s.w) kama inavyobainishwa katika aya ifu atayo:


' Nyama zao (wanyama hao wanaochinjwa) hazimfikii Mwenyezi Mungu (wala damu zao, lakini unamfikia Mwenyezi Mungu utii wenu (Kwake). Namna hivi tumewatiisha kwenu, ili mumtukuze Mwenyezi Mungu kwa sababu ya huku kukuongozeni. Na wape habari njema wafanyao mema'. (22:37)


Wote wawili, Ibrahim (a.s) na mtoto wa Ismail (a.s) aliwatangazia ushindi na kumfanya Ibrahim (a.s) kuwa kiongozi wa wacha-Mungu ulimwenguni kote na mila yake kuifanya mila ya walimwengu wote.



Kutokana na kisa hiki, tunajifunza kuwa Muislamu wa kweli anatakiwa amfanye Mwenyezi Mungu mpenzi wa moyo wake kuliko kipenzi kingine chochote kile. Na katika kufaulu na kustahiki malipo mema pamoja na nusra ya Mwenyezi Mungu (s.w) kurehemu kutokana na magumu mbali mbali kama alivyomnusuru Ismail kutokana na kisu kikali kilichokuwa tayari kukata juu ya koo lake. Mafanikio haya kwa Nabii Ibrahim (a.s) na mwanawe yanadhihirishwa katika aya zifuatazo:


'Basi wote waw ili walipojisalimisha (kwa Mwenyezi Mungu) na akamlaza kifudi fudi (amchinje), pale pale tulimuita: 'Ewe Ibrahim, umesadikisha ndoto!' Kwa yakini hivi ndivyo tunavyowalipa watendao mema. Bila shaka (jambo) hili ni jaribio lililodhahiri. Basi tukamkom boa kwa mnyama wa kuchinjwa mtukufu. Na tukamwachia (sifa nzuri) kwa watu wote w aliokuja baadaye. Amani kw a Ibrahim. Hivi ndivyo tuw alipavyo w atenda wema. Bila shaka yeye alikuwa miongoni mwa waja wetu walioamini (kweli kweli)' (37:103-111)



Endapo Muislamu ataitekeleza ibada hii ya kuchinja mnyama, huku kumbukumbu ya kisa hiki cha Nabii Ibrahim cha kumchinja mwanawe amekiweka mbele yake, bila shaka zoezi hili litamuandaa kuwa tayari kujitoa muhanga nafsi yake na nafsi ya kila kipenzi chake kwa ajili ya kusimamisha Dini ya Mwenyezi Mungu hapa ulimwenguni.


Kupiga kambi Mina mwezi 11 - 13 Dhul-Hijja



Siku za Tashriq ndio kilele cha ibada ya Hijja ambapo askari wa Mwenyezi Mungu (s.w) hupumzika kambini kwao baada ya mazoezi makali ya kijeshi waliyoyaanza tangu mwezi 8, Dhul-Hajj, ambayo endapo watakuwa wameyafanya kwa mazingatio makubwa yanayostahili yatawawezesha kuwa wapiganaji hodari wa Mwenyezi Mungu katika kusimamisha dini yake na ufalme wake hapa ulimwenguni. Pamoja na mapumziko haya, askari hawa wa Mwenyezi Mungu (s.w) hawawi kama askari wa majeshi ya kilimwengu ambao katika sherehe zao hujizamisha katika ufasiqi kama vile ulevi, uzinifu, uporaji wa mali za raia, n.k., bali wao wanaendelea kumkumbuka na kumtukuza Mwenyezi Mungu (s.w) kwa Takbira, Swala, Dua na Stighfari na kila baada ya jua kupindukia hujitokeza kwa mazoezi ya shabaha katika kuilenga kwa mawe ile minara mitatu ambayo imesimamishwa pale kuwakilisha maadui wote wa Dini ya Mwenyezi Mungu (s.w).
Kuaga Ka'aba



Baada ya siku tatu (siku za Tashriq) za sherehe za kufunga ibada ya Hijja Mahujaji hujiandaa kurejea makwao. Baada ya kuwa tayari kuondoka, huenda kwenye Ka'aba na kufanya Tawaf ya kuaga.



Katika kufanya zoezi hili la Tawaf ya kuaga, Haji akiwa anazingatia mafunzo aliyoyapata katika zoezi zima la ibada ya Hija, ambayo yamelengwa kuwaandaa Waislamu kuwa Makhalifa wa Mwenyezi Mungu (s.w) hapa ulimwenguni kwa ufalme wa Mwenyezi Mungu (s.w) hapa ardhini na kuporomosha falme nyingine zote kwa silaha ya udugu na umoja na kujitoa muhanga kwa mali na nafsi, ataaga kwa kutoa ahadi tena kwa Mwenyezi Mungu (s.w) kuwa kuanzia pale atayaingiza mafunzo aliyoyapata katika matendo na atahakikisha kuwa hafi isipokuwa ametekeleza wajibu wake katika kusimamisha Dini ya Mwenyezi Mungu. Si katika kumaliza ibada maalum kwa kutoa ahadi kwa Mwenyezi Mungu (s.w) kuwa atayaingiza mafunzo aliyoyapata katika ibada hiyo katika matendo kwa kutumia juhudi zake zote kwa ushirikiano wa kidugu na Waislamu wenzake. Kila Muislamu anapomaliza swala ya faradhi, anapokamilisha ibada ya Zaka na ibada ya funga, anatakiwa atoe ahadi hii ya kuaga kwa Mwenyezi Mungu (s.w) kwani hana uhakika kuwa ataweza kufikia ibada nyingine kama hiyo kabla hajarejea kwa Mola wake. Ni katika mtazamo huu Mwenyezi Mungu (s.w) anatutanabahisha:



'Enyi mlioamini! Mcheni Mwenyezi Mungu kama ipasavyo kumcha; w ala msife isipokuwa mmekwisha kuwa Waislamu kamili'. (3:102)




                   




Je! umeipenda hii post?
Ndio            Hapana            Save post

Kama unahitaji kuuliza maswali Bofya hapa

Mwandhishi Tarehe 2018-08-01     Share On Facebook or Whatsapp Imesomwa mara 214


Download our Apps
👉1 Madrasa kiganjani     👉2 Kitabu cha Afya     👉3 Kitau cha Fiqh     👉4 kitabu cha Simulizi    

Post zifazofanana:-

KUMUAMINI MWENYEZIMUNGU
Soma Zaidi...

KUMUAMINI MWENYEZI MUNGU
Jifunze tawhid yaani kumpwekesha Allah subhaanah wata'aala Soma Zaidi...

Hadhi na haki za Mwanamke Ulaya Wakati wa mapinduzi ya viwnda
Soma Zaidi...

UGONJWA WA MALARIA NA TAKWIMU ZA ATHARI YAKE KIDUNIA
Malaria ni katika maradhi ambayo husambazwa na na mbu jike aina ya anopheles. Soma Zaidi...

Wanaadamu kushindwa Kuandika Kitabu Mithili ya Qur-an:
Soma Zaidi...

DUA ZA KUSWALIA, KUAMKA, WACHAWI, MAJINI, ASUBUHI, NA JIONI NA NYINGINEZO
Soma Zaidi...

Historia ya kujengwa kwa Alkabah (Maka)
Kama tulivyoona katika maisha ya Mtume Ibrahim(a. Soma Zaidi...

Kujielimisha kwa Ajili ya Allah (s.w).
Elimu ndiyo zana'aliyotunukiwa'mwanadamu'ili aitumie'kutekeleza'majukumu'yake kama Khalifa wa Allah (s. Soma Zaidi...

HISTORIA NA MAISHA YA NABII ISMAIL(A.S)
Ismail(a. Soma Zaidi...

UTARATIBU WA KULEA MIMBA
Soma Zaidi...

Sifa za wanafiki zilizotajwa katika surat al-Baqarah
Na katika watu, wako (wanafiki) wasemao: "Tumemwamini Mwenyezi Mungu na siku ya mwisho"; na hali ya kuwa wao si wenye kuamini. Soma Zaidi...

Madai ya Makafiri dhidi ya kuwepo kwa Allah (s.w) na Udhaifu wa Madai hayo.
2. Soma Zaidi...