Mtume Ilyasa ni mmoja wa Mitume waliotumwa kupitia kizazi cha Bani Israil. Alitumwa kwa watu ambao walitupa mafundisho ya Mitume waliotangulia na badala yake wakawa wanaabudu Mungu- jua waliyemuita - Baal. Mtume Ilyasa(a.s) aliwaita watu wake wamwabudu Mungu Mmoja, Allah(s.w); lakini walimkadhibisha. Kwa ajili hiyo ya kukataa mafundisho ya Mtume wao, wakawa katika kundi la watakaoingia katika adhabu ya Allah(s.w). Isipokuwa kwa wale waliorejea kwa Mola wao wakajitakasa. Kwa muhtasari ujumbe wa Mtume Ilyasa(a.s) unapatikana katika aya zifuatazo:
"Na hakika Ilyas alikuwa miongoni mwa Mitume. (Wakumbushe) Alipowaambia watu wake: "Oh! Hamuogopi?" "Mnamuomba (na kumuabudu) Baal na mnamuacha aliye Mbora wa waumbaji (na ndiye Muumbaji peke yake)." "Mwenyezi Mungu, Mola wenu na Mola wa wazee wenu wa mwanzo!" Wakamkadhibisha. Basi bila shaka watarudishwa (adhabuni). Isipokuwa waja wa
Mwenyezi Mungu waliosafishwa (na Mwenyezi Mungu). Na tumemuachia (sifa nzuri) kwa (watu wote) Amani kwa Ilyas" (37:123-130).