SIRA (HISTORIA YA ) MTUME MUHHAMAAD (S.A.W) KUZALIWA KWAKE, VITA ALIVYOPIGANA, SUNNAH ZAKE NA MAFUNDISHO YAKE

SIRA (HISTORIA YA ) MTUME MUHHAMAAD (S.A.W) KUZALIWA KWAKE, VITA ALIVYOPIGANA, SUNNAH ZAKE NA MAFUNDISHO YAKE

Darsa za Sira

Ustadh Rajabu

DARSA ZA SIRA

NASABA YA MTUME (S.A.W):
Wanazuoni katika fani ya historia wamegawanya nasaba ya Mtume katiak makundi matatu. Kundi la kwanza ndilo linakubaliwa na kuwa ni usahihi kwa makubaliano ya wanazuoni wote na hili ni kundi linaloiangalia nasaba ya Mtume kutoka tangu kwa baba yake mpaka kufika kwa Mzee 'Adnan. Kundi la pili lina shaka kwani hakuna makubaliano ya ujumla juu ya baadhi ya watu. Na kundi hili ni lile linaloangalia nasaba ya Mtume kutokea kwa mzee Adnan mpaka kufika kwa Mtume Ibrahimu (a.s). kundi la tatu lina shaka juu ya ukweli wake. Na hili ni lile kundi linaloangalia nasaba ya Mtume kutoka kwa Mtume Ibrahimu mpaka kufika kwa Mtume Adam (a.s).


Kundi la kwanza: Muhammad bin 'Abdullah bin 'Abdul-Muttalib (ambaye aliitwa Shaiba) bin Hashim, (aliitwa 'Amr) bin 'Abd Munaf (aliitwa Al-Mugheera) bin Qusai (pia aliitwa Zaid) bin Kilab bin Murra bin Ka'b bin Lo'i bin Ghalib bin Fahr (ambaye aliitwa Quraish na kutoka kwa huyo ndipo tunapata kabila la Quraysh) bin Malik bin An-Nadr (pia aliitwa Qais) bin Kinana bin Khuzaiman bin Mudrikah (pia aliitwa 'Amir) bin Elias bin Mudar bin Nizar bin Ma'ad bin 'Adnan.


Kundi la pili: 'Adnan bin Add bin Humaisi' bin Salaman bin Aws bin Buz bin Qamwal bin Obai bin 'Awwam bin Nashid bin Haza bin Bildas bin Yadlaf bin Tabikh bin Jahim bin Nahish bin Makhi bin Aid bin 'Abqar bin 'Ubaid bin Ad-Da'a bin Hamdan bin Sanbir bin Yathrabi bin Yahzin bin Yalhan bin Ar'awi bin Aid bin Deshan bin Aisar bin Afnad bin Aiham bin Muksar bin Nahith bin Zarih bin Sami bin Mazzi bin 'Awda bin Aram bin Qaidar bin Ishmael mtoto wa Abraham (amani iwe juu yao).


Kundi la tatu: kuanzia kwa Nabii Ibrahim (amani iwe juu yake) , Ibn Tarih (Azar) bin Nahur bin Saru' bin Ra'u bin Falikh bin Abir bin Shalikh bin Arfakhshad bin Sam bin Noah (amani iwe juu yake) , bin Lamik bin Mutwashlack bin Akhnukh [who was said to be Prophet Idris (Enoch) (amani iwe juu yake) bin Yarid bin Mahla'il bin Qabin Anusha bin Shith bin Adam (amani iwe juu yake)


FAMILIA YA MTUME (S.A.W)
Mtume ametokana katika ukoo wa Ibn Hashimu. Na ukoo huu umeitwa kwa jina hili kutokana na kurithi jina hili kutoka kwa mzee wao Hashim Ibn Abd Manaf. Hapa tutaona kwa ufupi.


Hashim:
Huyu alikuwa ni katika wazee wanaoheshimika sana katika kabila la kikuraishi Maka enzi hizo. Pia ndie ambaye alikuwa na jukumu la kuwapa chakula na maji mahujaji wote. Mzee huyu alitambulika pia kwa kuwa tajiri na mtu mkweli na muwazi. Pia alijulikana kuwa ndiye mzee wa kwanza kuwalisha mahujaji mkate uliochanganywa na mhuzi.


Jina lake halisi ni Amr na ameitwa Hashim kutokana na kitendo chake cha kutengeneza mikate kwa mahujaji. Pia ndie ambaye alianzisha safari mbili za makuraishi wakatika wa kipupwe na kiangazi jerea Quran suat Quraysh. Pia imeripotiwa kuwa aliwahi kwenda Syria kama mfanya biashara. Alipokuwa Madina alimuoa Salma mtoto wa Amr kutoka kabila la Bani 'Adi bin An-Najjar. Alikaa pamoja na mkewake Madina kwa muda kisha akaelekea tena Syria wakati ho alimwacha mkewe akiwa ana ujauzito.


Mzee Hashim alikfariki 497 B.K nchini Palestina katika mji uitwao Ghazza. Bada ya kifo cha mzee huyu mke wake alijifungua mtoto wa kiume aliyeitwa 'Abdul-Muttalib na lilijulikana kwa jina la utani kama Shaiba. Alipewa jina hili kwa sababu alizaliwa akiwa na nywele nyeupa yaani mvi kwenye kichwa chake. Mke wake alimchukuwa Mtoto 'Abdul-Muttalib na kumpeleka kwenye nyumba ya baba yake Madina. Kuzaliwa kwa kijana 'Abdu-Muttalib hakukujulikana na yeyote katika familia ya Hashim.


Hashim alikufa akiwa na watoto wanne; Asad, Abu Saifi, Nadla na 'Abdul-Muttalib. Pia alikuwa na watoto wakike watano ambao ni; Ash-Shifa, Khalida, Da'ifa, Ruqyah na Jannah.


AL-Muttalib:
Baada ya kifo cha Hashim, kazi ya kulisha mahujaji alipewa ndugu yake Al-Muttalib bin 'Abd MAnaf ambaye alifahamika kwa kuwa na sifa ya ukarim, uwazi na ukweli. Sasa wakati ambao 'Abdul-Muttalib alipofikia umri wa ujana mzee Al-Muttalib alizipata habari juu ya kuwepo kwa mtoto wa kaka yake Hashimu huko Madina. Hivyo akafunga safari ili akamchukuwe mtoto wa ndugu yake. Basi pindi alipomuona tu machozi yalimtoka na kudondoka kupitia kwenye mashavu yake. Alimkumbatia na kumpandisha kwenye ngamia wake. Lakini kijana alikataa kwenda madina mpaka apate ruhusa kutoka kwa mama yake.


Basi mzee Al-Mutalib akaenda kwa mama yake kijana na kuomba aruhusiwe aondoke nae kuelekea Makkah. Lakini mama nae akakataa kumruhusu kijana wake kuondoka. Lakini mzee Al-Muttalib akatumia maneno ya ushawishi kwa kumwambia kuwa 'mtoto wako anakwenda Makka kushika madaraka ya baba yake pia kwa ajili ya kuitumikia Al-kaba (nyumba tukufu ya Allah). Kwa maneno haya mama alikubali kumruhusu mwanae.


Zee al-Muttalib alipofika Makka na kijana wake watu wakadhani kuwa yule ni mtumwa wake, lakini akawaambia kuwa 'huyu ni mwanangu, ni mtoto wa kaka yangu Hashim' Kijana Abdul-Muttalib akapelekwa nyumbani kwa baba yake mzee Al-Muttalib, na aliishi pale mpaka mzee Al-Muttalib alipofariki katika sehemu iitwayo Bardman huko Yemen, basi hapo madaraka yote alipewa Abdul-Muttalib. Alifahamika kwa utawala wake ulio mzuri na upendo kwa watu wa Makkah. Alikuwa ndiye kiongozi katika mambo ya kusimamia Nyumba ya Allah yaani Al-ka'aba.


Wakati mzee Al-Muttalib alipofariki, Nawfal alichukuwa madaraka kimaguvu kutoka kwa Abdul-Muttalib. Hivyo Abdul-Muttalib akaomba msaada kwa maquraish wakakataa kumsaidia, akaamuwa aombe msaada kwa mjomba wake Abu Sa'd bin 'Adi kutoka katika kabila la Bani A-Najjar ambaye alikubali kumsaidia hivyo akaja maka akiwa na wanajeshi wapanda farasi 80. Alipofika akaenda kwa Nawfal na akawashuhudishia wazee wa kiqurayshi kuwa kama Nawfal hatarudisha madaraka kwa mpwa wake basi atamkata kwa upanga. Baada ya hapo akaenda nyumbani kwa mpwa wake na akakaa hapo kwa muda wa siu tatu. Alifanya ibada ya Umrah kisha akarudi Madinah.


Baadae Nawfal akaingia makubaliano ya kusaidiana kati ya ukoo wake na ukoo wa Bani 'Abd Shams bin 'Abd Munaf, makubaliano ya kusaidiana dhidi ya kuwapinga bani Hashim (yaani ukoo wa Abdul-Muttalib). Wakati kabila la Khuzaa lilipoona ukoo wa Bani An-Najjar wanawasaidia bani Hashim nao wakaingia makubaliano na ukoo wa Bani Hashim dhidi ya kumpinga Nawfal na Kundi lake. Kaika wakati wa utawala wa mzee Abdul-Muttalib alishuhudia matukio makuu mawili ambayo ni kuchimbwa kisima cha zamzam pamoja na kuangamizwa kwa jeshi la tembo.


KUCHIMBWA UPYA KISIMA CHA ZAMZAM
Kwa kifupi ni kuwa Abdul-Muttalib alipata agizo kutoka ndotoni kuwa achimbe kisima cha zamzam, na akaelekezwa sehemu ya kupachimba. Basi akachimba na ndipo akakuta chini ya kisima vitu ambavyo vilifukiwa pamoja na kisima. Walofukia vitu hivi ni watu kutoka kabila la Jurhum. Hawa pindi walipolazimika kuondoka Maka walikifukia kisima cha zamzam na kufukia baadhi ya vitu vya thamani kama mapanga, nguo za vita, na dhahabu. Baada ya hapo mlango wa alka'aba ukatengenezwa kwa hii dhahabu waloipata. Na unyweshwaji wa maji ya zamzam kwa mahujaji ukarudi upya.


Basi kisima cha zamzam kilipoanza kutoa maji, watu kutoka kabila la quraysh walitaka kufanya makubaliano juu ya maji yale lakini Abdul Al-Muttalib alikataa kwa kudai kuwa Allah amempa mamlaka yeye tu. Basi wakakubaliana wakamuulize kuhani kutoka ukoo wa Bani Sa'ad juu ya swala hili. Basi Allah akawaonesha alama za ukweli juu ya madai ya Abdul Al-Muttalib. Baada ya hapo mzee Abdul Al-Muttalib kwa shukran yake kwa Allah akaapa kumtoa kafara mtoto wake kwa Mwenyezi Mungu.


KUANGAMIZWA KWA JESHI LA TEMBO
Tukio la pili ni lile tukio la tembo, na ilikuwa hivi:- Kiongozi mmoja wa kiyemeni aliyetambulika kwa jina la Abrah aliona waarabu kutoka maeneo mbalimbali wanafunga misafara kuelekea Makkah kwa lengo la kwenda kuhiji. Hivyo akaamuwa kujenga kanisa kubwa sana ambalo alifikiri kuwafanya waarabu wasiende Makkah ila waende kuhiji kwenye kanisa lake. Kulikuwa na kijana mmoja kutoka katika kabila la Kinana alifahamu jambo hili la Abraha. Hivyo akaingia kwenye kanisa wakati wa usiku kisha akachafua ukuta wa kanisa kwa kuupaka vinyesi. Abraha alipolijuwa jambo hili akaandaa jeshi kubwa sana ili akaivunje Al-ka'aba. Jeshi la Abraha lilikuwa na washujaa elfu sitini (60,000). kisha akachaguwa tembo aliye mkubwa ndio akampanda yeye. Katika jeshi hili kulikuwa na tembo kati ya tisa mpaka kumi na tatu. (9-13)


Safari ya Abraha iliendelea mpaka akafika sehemu inayoitwa Magmas. Na hapo ndipo akaliweka sawa jeshi lake na akaliweka tayari kwa kuingia Makkah. Akaendelea mpaka akafika sehemu iitwayo Bonde la Muhassar bonde hili lipo kati ya Muzdalifah na Mina. Na hapo ndipo tembo wa abraha akakataa kuendelea na safari. Tembo alipiga magoti na kukaa chini, na kugoma kabisa kuelekea upande wa Makkah. Basi akimuelekeza upande mwingine anakubali lakini pindi akimuelekeza upande wa Makkah anagoma kabisa.


Na hapo ndipo Allah alipoleta jeshi la ndege waliobeba vijiwe vya moto na kuwapiga nvyo jeshi la Abraha. Ndege hawa kila mmoja alibeba vijiwe vitatu, kijiwe kimoja kwenye mdomo na viwili kwenye miguu yao. Kila kijiwe kiliuwa mtu katika jeshi la Abraha. Kuna wengine walikufa palepale na wengine walikimbia na kufia mbele ya safari. Abraha alibahatika kukimbia kwani alijeruhiwa vibaya, alipofika sehemu iitwayo San'a hali yake ikawa mbaya zaidi na akafariki.


Kwa upande mwingine wakazi wa Makkah walikimbia mji na kujificha kwenye majabali. Na huu ni ushauri walopewa na kiongozo wao Abdul Al-Muttalib. Baada ya maombi waloyaomba kwa Allaha na hatimaye wakamuachia Allah ailinde Nymba yake na wao wanusuru maisha yao. Basi jeshi la Abraha baada ya kuangamizwa wakazi wa Makkah wakarudi majumbani kwao wakiwa salama.


Tukio hili lilitokea mwezi wa Muharram siku hamsini aua hamsini na tano kabla ya kuzaliwa kwa Mtume Muhammad (s.a.w) ambapo ni sawa nan Mwezi wa Pili au mwanzoni mwa Mwezi wa Tatu mwaka 571 B.K. na hii ilikuwa ni zawadi kutoka kwa Allah kwenda kwa mtume wake na watu wa familia yake. Na hapo ndipo Nyumba ya Allah yaani Al-ka'aba ilipata maarufu kwa utukufu wake. Na mwaka huu waarabu wakauita mwaka wa Tembo.


Mzee Abdul Al-Muttalib alikuwa na watoto wa kiume kumi ambao ni Al-Harith, Az-Zubair, Abu Talib, 'Abdullah, Hamzah, Abu Lahab, Ghidaq, Maqwam, Safar na Al-'Abbas. Pia alikuwa na watoto wa kike sita ambao ni Umm Al-Hakim, Barrah, 'Atikah, Safiya, Arwa and Omaima.


Abdallah: huyu ndiye baba wa Mtume Muhammad (s.a.w). mama yake aliitwa Fatimah mtoto wa 'Amr bin 'A'idh bin Imran bin Makhzum bin Yaqdha bin Murra. Abdallah alikuwa ndiye mtoto mtanashati zaidi kuliko watoto wote wa mzee Abdul-Muttalib alikuwa mcheshi zaidi na alipendwa zaidi kuliko watoto wote wa Mzee Abdul-Al-Muttalib.na huyu ndiye mtoto ambaye mishale ya kafara ya ahadi aloiweka mzee Abdul al-Muttalib ilimuangukia.


Pindi watoto wake mzee Abdul al-Muttalib walipofikia balehe aliwaita na kuwaambia kiapo cha siri alichokiweka juu wa kutoa kafara ya mtoto wake kwa mungu wao Hubal. Basi majina ya watoto yakaandikwa kwenye mishale ya kuangalizia utabiri na jina la Abdallah ndilo likatokelezea kuwa ndie aliyechagulia kutolewa kafara. Kwa kuwa huyu ndiye Mtoto anayependwa zaidi na mzee Abdul al-Muttalib hivyo akashauriwa kubadilisha na ngamia. Baada ya kuangalizi ni ngamia wangapi wanafaa ngamia miamoja ndio wakaonekana wanafaha badala ya kuchinjwa kwa Abdallah. Mtume (s.a.w) alikuwa akisema 'mimi ni mtoto wa wachinjwa wawili' yaani ismail mtoto wa Mtume Ibrahimu na Abdallah mtoto wa Abdul al-Muttalib.


Addallah alifariki baada ya mke wake kupata uja uzito kwa muda wa miezi miwili. Wanazuoni wa historia wanatueleza kuwa alifariki akiwa na umri wa miaka 18 na hakuacha chochote katika urithi. Abdallah alifariki Madina alipokuwa anarudi kutoka kwenye safari za kibiashara kutokea Sham baada ya kupatwa na ugonjwa wa ghafla na alizikwa Madina upande wa ujombani kwake.


KUZALIWA KWA MTUME (S.A.W) NA MAISHA YAKE KABLA YA UTUME.
Mtume (s.a.w) alizaliwa siku ya juma tatu katika mweze rabil-awali (mfunguo sita) mwezi tisa (9) kwa mujibu wa wanahistoria katika mwaka wa tembo 571 B.K. baada ya kuzaliwa mama yake alituma mtu aende akatoe habari kwa mzee Abdul al-Muttalib juu ya kuzaliwa kwa mtoto. Kwa furaha kabisa alikuja mzee na akamchukuwa mtoto akambeba na kuelekea nae mbele za al-ka'aba (nymba tukufu ya Allah) kwa kutoa shukrani zake za dhati kwa Mwenyezi Mungu. Kisha akampa jina la Muhammad, jina ambalo halikuwa likijulikana na waarabu.


Kama ilivyo kawaida ya waarabu na jamii zingine wakati ule, Muhammad alinyonya kwa mama yake na kwa baadhi ya wanawake. Mtu wa kwanza kumnyonyesha Mtume baada ya mama yake ni Thuwaibah huyu alikuwa na mtumwa wa baba yake mdogo Abuu Lahab. Alivyonya Mtume Kwa Thuwaibah pamoja na mtoto wake Thuwaybah aitwaye Mosrouh. Pia Thuwaybah aliwahi kumvyonyesha Hamzah bin 'Abdul-Muttalib na baadaye alimnyonyesha Abu Salamah bin 'Abd Al-Asad Al-Makhzumi.


MAISHA YA UTOTONI YA MTUME S.A.W
Ilikuwa ni tamaduni kwa waarabu waishio mjini kuwapeleka watoto wao wachanga vijijini wakalelewe ili wapate ukakamavu, wajifunze lugha vyema na pia kuwaepusha na magonjwa ya miripuko yanayotokea mijini. Hivyo Mtume s.a.w alichukuliwa na Halima bint Dhuaib kutoka katika kabila la bani Sa'ad bin Bakar. Mume wake aliitwa Al-Harith bin 'Abdul'Uzza pia alitambulia kwa jina la Abi Kabshah.


Halima anasimulia kuwa ulikuwa ni wakati wa ukame sana hususana sehemu ambay alikuwa akiishi yeye na watu wao. Mvua zilikata, wanyama hawakuweza kutoa maziwa kwa ukame uliopo. Wanyama hawakuweza kushiba. Shakula pia kilikuwa ni taabu, lakini tumaini lao lilikuwa ni kusubiria mvua inyeshe. Wakati huo walitoka watu waende mjini kwenda kutafuta watoto wa kuwalea ili waweze kupata kipato kama ujira wa kulea na kunyonyesha watoti hao kama ilivyokuwa ni kawaida yao. Alikuwepo kwenye msafara huu Halima na mume wake.


Bi Halima akiwa amepata punda wake aliyeonekana ni dhaifu sana na mumewe alikuwa amepanda ngamia ameye hakuwa ni mwenye kutoa maziwa. Walifika Maka na wakaanza kutafuta watoto wa kuwanyonyesha. Anaeleza bi halima kuwa katika msafara ule walotoka watu wote walifika kwa mama yake Mtume na kuelezwa kuwa mtoto huyu ni yatima, basi wote wakakataa kumchukuwa Muhammad kwenda kumlea kwa kuhofia wazazi wake hawataweza kulipa gharama kwani mtoto ni yatima.


Msafara huu uliendelea kuzungua Makkah kutafuta watoto wa kuwalea, halimaye bi Halima hakibahatika kupata mtoto, hivyo akashauriana na mumewe kuwa arudi kule kwa mtoto yatima kwani anaona vibaya kurudi mtupu pila ya kuwa na mtoto. Basi mumewe akakubali, na hapo bi Halia akarudi na kumchukuwa mtoto muhammad (s.a.w). na maajabu ndo yakaanza hapa kama vile bi Halima anavyotueleza, Nitataja kwa ufupi zaidi mambo haya yalotokea.


Anaeleza bi Halima kuwa alipombeba mtoto badi alipofika kwenye hema lao aloshangaa kuona maziwa yamejaa, kwa hakika hii ni ajabu kwake kwani hata mtoto wake alikuwa akikosa usingizi usiku kwa uchache wa maziwa. Lakini leo anakuwa na maziwa na kumtosha mtot muhammad pamoja na mtoto wake. Kwa hakika walinyonya watoto hawa wawili mpaka wakashiba na kulala.


Bi halima anasimulia kuwa mume wake alipotoka kwenda kumuangalia ngamia wake alishangaa kuona ngamia ana maziwa ya kutosha, alikamua maziwa kutoka kwenye ngamia wake wakanywa na kushiba. Hii pia ni ajabu aloishuhudia Bi halima baada ya kumchukuwa kijana Mhammad kwa ni hapo mwanzo ngamia wao hakuweza kutoa hata tone la maziwa ya kuweza kunywa, lakini leo ngamia huyu anatoa maziwa ya kuweza kushiba watu wa familia hii na kuyabakisha. Bi Halima anasimula kuwa asubuhi ya siku ilofata mume wangu aliniambia ' hakikahalima umechukuwa mtoto mwenye kubarikiwa' nikamjibu 'nami natarajia iwe hivyo'.


Siku ilofata safari ya kurudi kutoka maka kwenda kwao ilianza. Katika msafara huu walishangaa kumuona punda wa halima amebadilika kwani amekuwa na nguvu na ameongeza uwezo wa kukimbia. Ilifikia wakati wnzie wakawa wanamwmbia nenda kipolepole ewe Halima kwa hakika huyu si yule pinda ulokuja ne. Ukweli ni kuwa punda ni yuleyule lakini Allah ameta miujiza yake hapa.


Walipofika nyumbani walishangaa kuona mifugo yao inarudi kutoka malishoni ikiwa imeshiba sana, wakati kulikuwa na ukame mkubwa sana. Mifugo yao iliweza kutoa maziwa mengi. Ilifikia wakati wamiliki wa mifugo wakawa wanawaambia wachungaji wao kuwa wachunge pale anapochungia mchungaji wa bi Halima. Ukweli ni kuwa majani ni yale yale isipokuwa Allah anaweza miujiza yake kwa bi Halima.


Kwa hakika bi Halima aliona miujiza mingi sana, na maisha yake yalibadilika na kuwa na raha na amani to ka amchukuwe mtoto Muhammad (s.a.w). bi Halima anasimulia kuwa mtoto Muhammad alikuwa anakuwa kwa haraka zaidi tofauti na alivyozoea. Bi Halima alimlea mtoto huyu kwa muda wa miaka miwili hata muda wa kumuachisha ziwa ukawadia. Ilikuwa anatakiwa ampeleke mtoto kwa mama yake.


Basi mtoto alipotimia miaka miwili kwa shingo upande bi Halima alimrudisha mtoto kwa mama yake. Huku akiwa haridhiki kwani ameona neema nyingi toka amchukuwe mtto huyu. Alipofika Makkah alimshawishi mamayake amruhusu aweze kurudi nae aendelee kumlea kwa kuhofia mtoto atpata maradhi ya mjini maradhi ya milipuko. Kwa sababu hii mama yake Mtume bi Amina alikubali hivyo bi Halima akaendelea kumlea mtoto huyu. Hvyo Mtume aliendelea kuishi kule na kuendelea kuimarika kimwili na kuwa na afya njema pamoja na kupata ufasaha katika lugha ya kiarabu.


KUPASULIWA KWA KIFUA MTUMEWAKATI AKIWA MTOTO.
Mtume alipokuwa mtoto tukio hili la kupasuliwa kwa kifua chako na kutolewa moyo wake na kusafishwa. Yote haya yalitokea kipindi akiwa analelewa na bi Halima katika kabila la bani Sa'ad. Wanazuoni wa sirah wameeleza kwa urefu tukio hili jinsi lilivyotokea. Na hapa tutaangalia kwa ufupi tu.


Ni kuwa siku moja mtume (s.a.w) alikuwa anacheza na watoto wenzie. Ghafla akatokea mtu mmoja naye ni Jibrib akamshika Muhammad na kumlaza chini kisha akamtoa moyo wake na kuuosha kwa maji ya zamzam na aliondoa uchafu wa shetani kisha akaurudisha kwenye kifua na kukifunika.


Watoto walokuwa wakicheza na Mtume (s.a.w) wakakimbia na kwenda kumueleza bi Halima kuwa Muhammad kauliwa. Bi Halima akatoka kwa haraka kufika akamkuta Muhammad akiwa amebadilika rangi. Muhammad alikuwa ni mzima wa afya, hapa bi Halima alipata mashaka makubwa mpaka akawa na hofu juu ya kuendelea kumlea kijana Muhammad.


Katika maelezo mengine waandishi wa sirah wameeleza tukio hili kama kupasuliwa kwa tumbo. Kwani zimekuja nukuu kuwa sikumoja waroto walipokuwa wakisheza pamoja nao alikuwepo Muhammad (s.a.w) basi ghafla wakaja wanaume wawili walovaa nguo nyeupe (Malaika) wakaulizana ni hyu? Basi yule mwingine akajibu ndio ni huyu, wakamlaza kisha wakampasua tumbo lake na kutoa uchafu wa shetani kisha wakafunika kama lilivyo. Basi watoto walokuwa wakicheza nae wakaenda mbio kusema wa bi halima na alipokuja kuulizwa Muhammad (s.a.w) akasema kuwa watu wawili wamekuja na kunipasua tumbo langu. Utapata maelezo zaidi ya kisa hiki kwenye kitabu kiitwacho Nurul- Yaqin.


Bi Halima aliendelea kumlea Mtume (s.a.w) kwa muda wa miaka miwili mingine hata alipotimiza miaka minne aliamuwa kumrudisha mtoto kwa mama yake. Alihofia kuendelea kumlea mtoto huyu huenda akapatwa na jambo. Miaka minne alikuwa imemtosha mtoto huyu kuwa na mwili imara na kuweza kuzungumza lugha ya kiarabu wa ufasaha tofauti na watoto walolelewa maeneo mengine.


KULELEWA NA MAMA YAKE ALIPOFIKA MIAKA MINNE
Mtume (s.a.w) alirudishwa kwa mama yake alipokuwa na umri wa miaka minne, na aliendelea kuishi na mama yake mpaka alipotimia miaka sita, na hapo ndipo wakati ambao mama yake kipenzi alifariki dunia. Wanazuoni wanaeleza juu ya kufariki kwa mama yake kama ifuatavyo:-


Mama yake Mtume (s.a.w) alifunga msafara kwenda kuzuu kaburi la mume wake huko madina. Katika msafara huu alikuwepo Mtume (s.a.w), mjakazi wa kike aitwaye Ummu Ayman, Mtume (s.a.w) pamoja na baba mkwe wake bi Amina aitwaye 'Abdul Al-Muttalib. Walikaa huko kwa muda wa mwezi mmoja, na walipokuwa wanarejea mama yake Mtume (s.a.w) alipatwa na maradhi ya ghafla na akafariki wakiwa njiani sehemu iitwayo Abwai ni kijiji kilichopo kati ya Makkah na madinah.


KULELEWA NA BABU YAKE:
Mzee 'Abdul Al-Muttalib alimchukuwa mjukuu wake na wakarejea Makkah na aliendelea kuishinae na kumlea kwa mapenzi makubwa sana. Mzee huyu alimpenda sana mjukuu wake kuliko ambavyo alivyokuwa anawapenda watoto wake. Alikuwa katu hamuachi mjukuu wake akiwa peke yake. Mzee Abdul Al-Muttalib alikuwa akiwekewa godoro kwenye kivuli cha Al-kabah na watoto wake wanakaa pembeni ya godoro kwa heshima ya baba yao, basi alikuwa Mtume (s.a.w) anakaa kwenye godoro lile. Baba zake wadogo wanapomtoa mzee Abdul al-Muttalib alikuwa akiwakataza na kuwaambia kuwa kijana huyu atakujakuwa na nafasi nzuri.


Mzee Abdul al-Muttalib alikuwa sikuzote akipendezwa na vitendo vya mjukuu wake. Mzee huyu aliendelea kumlea yatima huyu mpaka alipofikia umri wa miaka nane, na hapa ndipo mzee huyu alipofariki dunia na kuongeza majonzi zaidi kwa kijana huyu. Mzee Abdul al-Muttalib alifariki wakati Mtume (s.a.w) alipokuwa na umri wa miaka nane na miezi miwili na siku kumi (10).


KULELEWA NA BABA YAKE MDOGO
Baada ya kufariki kwa mzee huyu, kiongozi mkubwa wa maquraysh na makkah, kiongozi ambaye jeshi la Abrah liliangamizwa ndani ya utawala wake. Kiongozi ambaye alikabidhiwa mamlaka ya kukichimba upya kisima cha zamzam baada ya kufukiwa na watu kutoka kabila la Jurhum pindi walipoondoka Makkah. Alisimama Abu Talib kumlea mtoto wa ndugu yake. Kwani huyu ndiye aliyekuwa mtoto mkybwa wa Abdul al-Muttalib.


Abu Talib alimpenda sana kijana wake zaidi ya anavyowapenda watoto wake. Mtume (s.a.w) alikuwa ni mwenyekuridhika kwa kile ambacho alikuwa akikipata. Allah alimuongezea rizk mzee Abu Talib. Mzee huyu alimlea kijana wake Mpaka alipofika umri wa miaka arobaini. Watu walimpenda kijana Muhammad jinsi alivyokuwa na tabia njema na uaminifu.


Watu wa Makkah walikuwa wakiomba mvua kupitia utukufu wake. Imesimuliwa kutoka kwa Ibn 'Asakir kuwa Jalhamah bin Arfuta kuwa amesema nilifika Makkah wakati ambao kulikuwa hakuna mvua, Maquraish wakatoka kumueleza mzee Abu Talib kuwa awaombee mvua. Basi akatoka akiwa na kijana chake na akamsimamisha pembeni ya ukuta wa al-kabah kisha akaomba dua. Kwa hakika kulikuwa hakuna mawingu lakini ghafla mawingu yakajikusanya kutoka huku na kule na hatimaye mvua ikanyesha.


KUKUTANA NA BAHIRA (MTAWA) WA KIYAHUDI
Mzee Abu talib alikuwa ni mfanya biashara, hivyoslikuwa akimchukuwa kijana wake kwenda kwenye biashara. Sikumoja wakati Mtume alipokuwa na umri wa miaka kumna mbili (12) alitoka yeye na kijana wake kuelekea Sham (Syria) kwa ajili ya kufanya biashra. Basi walipofika sehemu inayoitwa Busra walikutana na kuhani mmoja wa kiyahudi aliyeitwa Bahira na inasemekana jina lake halisi ni George (Joji kwa matamshi ya kiswahili). Mtu huyu aliwaonesha ukaribu mkubwa sana, a katu hajawahi kuonesha ukarimu huu kwao watu hawa kwani walikuwa ni wageni kwake.


Bahira aliushika mkono wa Mtume na akasema 'huyu ndiye kiongozi wa watu wote, Allah atamtuma kwa kumpa ujumbe ambao utakuwa ni rehma kwa viumbe wote' hapa mzee Abu Talib akamuuliza 'umejuaje jambo hili' Mzee huyu akajibu kwa kumwambia 'mlipokuwa mnakuja alipotokea upade wa Aqabah niliona miti na majabali vyote vinamsujudia (yaani vinampa heshima) na huwa vitu hivi havifanyi hivi ila kwa mitume tu. Pia naweza kumjuwa kwa kuwa ana mhuri wa mitume chini ya bega lake kama tunda la tofaha (epo) yote haya tumeyasoma kwenye vitabu vya dini yetu'


Baada ya mazungumzo Bahira akamwambia mzee Abu Talib amrudishe kijana Makkah kwani Bahira alihofia kuwa watu wa huko wendako huenda wakamgunduwa kuwa huyu atakujakuwa mtume wa mwisho hivyo wakamfanyia hasadi na kumuua. Kwani Mayahudi walikuwa wakihubiri kuhusu Mtume wa Mwisho lakini walitarajia kuwa atatokea miongoni mwa kabila lao hivyo wakitambua kuwa Mtume wa Mwisho ni Muarabu wanaweza kumuuwa kama walivyowauwa mitume wao huko nyuma. Basi mzee Abu talib alitii na kumrudisha kijana wake Makkah.


Wanazuoni wa sirah wanazungumza maelezo mengi kuhusu habari hii ya Bahirah na Kijana Muhammad. Wapo wanaoeleza kuwa Bahira baada ya kutamka maneno ya kuwa huyu kijana atakujakuwa ni mtume alitaka kujiridhisha zaidi hivyo akaanza mazungumzo na kijana ili aweze kubaini mengi zaidi. Basi katika mazungumzo yake Bahira alisema 'Nakuapia kwa Mungu Lata na Uzza' bahira alitambuwa kuwa Lata na Uzza ni miungu wa washirikina wa Makkah hivyo Mtume hatavumilia maneno haya. Basi kijana Muhammad aliposikia maneno yake akamwambia 'Usitaje Lata na Uza mbele yangu, ninawachukia' Kufika hapa Bahira akawa amejiridhisha kabisa kuwa huyu ndiye Mtume wa Mwisho.


Katika masimulizi mengine ni kuwa Bahira alikaribisha msafara mmoja wa kibiashara kwenye tafrija yake. Msafara huu ndio ulikuwa msafara wa Abu Talib na wenzie. Basi bahira akawaambia watu wote waingie ndani kwenye tafrija isipokuwa hyuy mtoto (Muhammad) abakie nje ili kulinda mizigo. Basi wakati tafrija inaendelea bahira akaanza kuona miujiza kama Kusujudi kwa mitu (kutoa heshima) na kufunikwa na mawingu wakati kwa ajili ya kivuli. Hapo ndipo Bahira akatambua kuwa huyu ni Mtume.


Na hapo ndipo alipomsahuri mzee Abu talib kuwa kijana huyu asiendenae huko Syria kwani mayahudi wakimjuwa watamuua. Mzee abu Talib alitii ushauri huu hivyo akauza bidhaa zake paleple kwa bei iliyo nafuu ili aweze kurudi zake Makkah. Abu Talib safari yake ya biashara ikaishia palepale bila ya kufika Syria.


MAPIGANO YA AL-FIJAR (MAPIGANO YA UOVU).
Vita hivi ni vita vilivyotokea kati ya kabila la kiquraysh wakisaidiwa na Kinana kutokea makkah na kabila la Qays 'Aylan kutokea taif. Na vita hivi vilitokea ndani ya miezi mitukufu na vilidumi kwa muda wa miaka mktano. Na mapigano halisi yalidumu kwa muda wa siku tano tu. Vita hivi vimeitwa vita vya uovu kwani vilifanyika ndani ya miezi mitukufu. Vilitokea vita hivi wakati Mtume alipokuwa na miaka kumi na tano. Na alishiriki katika vita hivi. Ijapokuwa Mtume hakupenda kushiriki vita hivi alifanikiwa kutokushiriki ndani ya siku 2 za kwanza lakini siku tatu zilizofata ilibidi ashiriki. Hakuwahi kunyanyua upanga kwa ajili ya kupigana ila alishiriki katika kuokota misahare na kuwapatia wapiganaji.


Inasemekana katika mwezi wa dhul-qada (mfunguo ilikuwa ni ada ya waarabu enzi hizo kufanya sherehe katika sehemu iitwayo Ukaz. Katika sehemu hii ndani ya masiku haya michezo mbalimbali ilifanyika kama kamari, mashindano ya kuchezea panga, kushindana kuimba mashairi, wanawake kucheza na mengineyo mengi. Pia biashara zilikuwa zikifanyika katika eneo hili. Sasa vita hivi vilitokea kwasababu ya sintofahamu iliyotokea kati ya watu wawili wafanyabiashara. Mmoja kutoka kwenye kabila la Quraysh (Makkah) na mwengine kutokea kabila la Qays 'Aylan kutoke taif.


Sababu ni kuwa mtu mmoja kutoka katika kabila la Quraysh alikuwa na mteja, na ikatokea kuwa mfanyabiashara mwingine kutoka kabila la Qays 'Aylan akawa anamfatilia mteja yuleyule. Basi ahapa ndipo pakazuka mgogoro na hatimaye Mtu kutoka kabira la quraysh akamuua yule wa kabila la Qays 'Aylan. Watu kutoka Taif wakaandaa jeshi kuja kulipa kisasi cha ndugu yao alouliwa bila ya sababu. Watu kutoka kabila la Quraysh wakaandaa jeshi nao kwa kulinda heshima ya kabila lao. Bila ya kujali mwezi mtukufu ambao ni haramu kumwaga damu au kupigana, na bila ya kujali sheria zao juu ya mtu aliuliwa kwa makusudi sheria inasemaje. Wakaamuwa kupigana vita kali sana.


Vita vilianza mwanzoni mwa siku na toka vinaanza ushindi ulikuwa ni kwa kabila la Qaysh 'Aylan lakini ilipofika mida ya jioni meza ikabadilika na ushindi ukawa ni wa Quraysh. Harb bin Umayyah (Mjomba wake mdogo Mtume (s.a.w)) ndiye alokuwa kiongozi wa vita kwa upande wa Mqauraysh na wasaidizi wake. Mwishoni mwa siku ya tano viongozi wa pande zote walikubali kuacha kupigana na wakaamuwa kufanya majadiliano ya amani kumaliza vita na hapa wakawekeana mkabata (maakubaliano) ulofahamika kwa jina la Al-Fudhul.


MKATABA WA AL-FUDHUL
Baada ya vita hivi viongozi wa pande mbili hizi waliamuwa wakae chini na wakubaliane kuweka kanun i na utaratibu utakaozuia kutotokea uonevu kama huuu tena. Na hii ni kuwa maeneo mengi ya waarabu enzi hizo yalikuwa na utaratibu kama huu wa kuweza kusaidiana na kuzuia uonezu na unyanganyi wa haki. Makataba huu ulikuwa na lengo la kuwasaidia watu wanyonge ambao hawana urafiki na mahusiano na watu wenyenguvu, madaraka ama uwezo wa kipesa.


Hivyo lengo kuu la kiapo au mkataba huu ilikuwa kulinda haki za wanyonge, kuzuia dhulma na uonevu. Kuwapa haki watu wanaostahiki kupewa haki bila ya kujali wapi wametoka, ni nani ndugu zao au wanauwezo gani. Makataba huu ulifanyika kwenye nyumba ya mzee mwenye heshima,na mwenye umri aliyefahamika kwa jina la Abdallah bin Jad'an. Walohudhuria kwenye mkutano huu ni wawakilishi kutoka kabila la Banu hashim, Banu Al-Muttalib, Asad bin Abdul 'Uzza, Zahran bin Kilab pamoja na Taim bin Murra.


Baada ya makubaliano yao ya kujenga amani kati yao wenyewe na wageni wao wanaokuja Makkah walikwenda kwenye Al-Ka'abah na kufanya kiapo. Kiapo chao ni kuyatekeleza walokubaliana kuwa watampa kila mtu haki yake na watapigana na yeyote ambaye atadhulumu na kumsaidia atakaye dhulumiwa. Watapigana na yeyote atakayevunja makubaliano haya mpaka haki ipatuikane. Walifanya kiapo ndani ya al-ka'aba mbele ya kiwe jeusi.


Miongoni mwa walohudhuria mkutano huu kutoka upande wa maquraysh ni Mtume s.a.w. na baada ya kupewa utume Mtume (a.s.w) alisema: 'nilishuhudia (mkutano, makubaliano mkataba) kwenye nyumba ya Abdallah bin Jad'an, mkutano ninaoupenda kuliko ngamia mwekundu, na lau ningeliitwa tena kwenye mkutano kama huu hakika ningehudhuri'. Maneno haya yanathibitisha kuwa mkutano huu uliridhiwa na Allah. Hizi pia zilikuwa ni katika vitangulizi vya kuja kwa mtume wa mwisho.


Na inasemekana kuwa Chimbuko na wao kukutana ni kuwa alitokea mfanyabiashara mmoja kutoka katika kabila la Zubaid alikuja Makkah kufanya biashara. Hivyo akamuuzia Al-'As bin Wa'il As-Sahmy baadhi ya bidhaa zake. Baadaye Al-As akakataa kumlipa mtu huyu. Hivyo mfanyabiashara akawa anaomba msaada kwa Maquraysh waweze kumsaidia ili apate haki yake, lakini hakuna ambaye alimjali.


Azubair bin 'Abdul Al-Muttalib alisikia malalamiko ya Mtu huyu hivyo akamfata na kumuuliza nini hasa chanzo cha haya. Yule mfanya biashara akamueleza kilicho tokea. Basi katika kuitafuta haki ya huyu mfanya biahara ndio mkutano huu ukatokea na yakakubaliwa hayo tuloyataja hao juu.

kuendelea kusoma kitabu hiki bofya hapo chini.



Pata kitabu Chetu Bofya hapa



Je! umeipenda hii post?
Ndio            Hapana            Save post

Kama unahitaji kuuliza maswali Bofya hapa

Mwandhishi Tarehe 2018-08-01     Share On Facebook or Whatsapp Imesomwa mara 378


Download our Apps
👉1 Kitau cha Fiqh     👉2 Kitabu cha Afya     👉3 kitabu cha Simulizi     👉4 Madrasa kiganjani    

Post zifazofanana:-

quran na sayansi
Soma Zaidi...

MTAZAMO WA UISLAMU JUU YA ELIMU
Maana ya elimuElimu ni ujuzi ulioambatanishwa na utendaji. Soma Zaidi...

MAANA YA HADITHI SUNNAH
Maana ya SunnahKilugha: Neno sunnah katika lugha ya Kiarabu lina maana ya mwenendo au mila. Soma Zaidi...

swala ya idi na nmna ya kuiswali swala ya idi
6. Soma Zaidi...

HISTORIA YA KUUMBWA KWA NABII ADAMU (A.S)NA HADHI YAKE NA HADHI YA WANAADAMU DUNIANI
Adam(a. Soma Zaidi...

quran na sayansi
Soma Zaidi...

Quran si njozi za mvurugano alizoota Mtume Muhammad
(ii)Dai kuwa Qur-an ni zao la njozi za Mtume (s. Soma Zaidi...

haki na hadhi za mwanamke katika jamii inayoishi kiislamu
Soma Zaidi...

Kushuka na kuhifadhiwa kwa quran, hatua kwa hatua: mafunzo ya baadhi ya sura za quran
QUR'AN 5. Soma Zaidi...

Kuanzishwa kwa Polisi na magereza kati uislamu wakati wa Makhalifa
Kuanzishwa kwa Polisi. Soma Zaidi...

Shufaa
Soma Zaidi...

UMBILE LA MBINGU NA ARDHI
'Katika kuumbwa mbingu na ardhi na mfuatano wa usiku na mchana,ziko alama (hoja) za kuonyesha kuwepo Allah (s. Soma Zaidi...