Tarjuma ya Quran Tukufu kwa kiswahili

KWA JINA LA MWENYEEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU
0

1. Ya-Sin 1

2. Kwa Haki ya Qur'ani yenye
hikima! 2

3. Hakika wewe ni miongoni mwa
walio tumwa, 3

4. Juu ya Njia Iliyo Nyooka. 4

5. Uteremsho wa Mwenye nguvu,
Mwenye kurehemu. 5

6. Ili uwaonye watu ambao baba
zao hawakuonywa , basi wao wamekuwa wenye kughafilika.6

7. Bila ya shaka kauli imekwisha
thibiti juu ya wengi katika wao, kwa hivyo hawaamini.7

8. Tumeweka makongwa shingoni
mwao, yakawafika videvuni. Kwa hivyo vichwa vyao viko juu tu. 8

9. Tumeweka kizuizi mbele yao, na
kizuizi nyuma yao, na tumewafunika macho yao; kwa hivyo hawaoni. 9

10. Ni sawa sawa kwao ukiwaonya au usiwaonye,
hawataamini. 10

11. Hakika wewe unamwonya mwenye kufuata ukumbusho, na
akamcha Arrahman, Mwingi wa Rehema, kwa ghaibu. Basi mbashirie huyo msamaha na
ujira mwema. 11

12. Hakika Sisi tunawafufua wafu, na tunayaandika wanayo
yatanguliza, na wanayo yaacha nyuma. Na kila kitu tumekihifadhi katika daftari
asli lenye kubainisha.12

13. Na wapigie mfano wa wakaazi wa mji walipo wafikia
walio tumwa. 13

14. Tulipo watumia wawili, wakawakanusha. Basi
tukawazidishia nguvu kwa mwingine wa tatu. Wakasema: Hakika sisi tumetumwa
kwenu. 14

15. Wakasema: Nyinyi si chochote ila ni watu kama sisi.
Na Mwingi wa Rehema hakuteremsha kitu. Nyinyi mnasema uwongo tu. 15

16. Wakasema: Mola wetu Mlezi anajua kwamba hakika sisi
tumetumwa kwenu.16

17. Wala si juu yetu ila kufikisha ujumbe ulio wazi. 17

18. Wakasema: Sisi tumeagua kuwa nyinyi ni wakorofi.
Ikiwa hamtaacha basi kwa yakini tutakupigeni mawe, na mtapata adhabu chungu
kutoka kwetu. 18

19. Wakasema: Ukorofi wenu mnao wenyewe! Je! Ni kwa kuwa
mnakumbushwa? Ama nyinyi ni watu walio pindukia mipaka. 19

20. Na akaja mtu mbio kutokea upande wa mbali wa mjini,
akasema: Enyi watu wangu! Wafuateni hawa walio tumwa. 20

21. Wafuateni ambao hawakutakini ujira, hali ya kuwa
wenyewe wameongoka. 21

22. NA KWA NINI nisimuabudu yule aliye niumba na kwake
mtarejeshwa? 22

23. Je! Niishike miungu mingine badala yake? Arrahmani,
Mwingi wa Rehema, akinitakia madhara uombezi wa hao hautanifaa kitu, wala
hawataniokoa. 23

24. Basi hakika mimi hapo nitakuwa katika upotovu ulio
dhaahiri. 24

25. Hakika mimi nimemuamini Mola wenu Mlezi, basi
nisikilizeni! 25

26. Akaambiwa: Ingia Peponi! Akasema: Laiti kuwa watu
wangu wangeli jua 26

27. Jinsi Mola wangu Mlezi alivyo nisamehe, na
akanifanya miongoni mwa walio hishimiwa. 27

28. Na hatukuwateremshia kaumu yake baada yake jeshi
kutoka mbinguni, wala si wenye kuteremsha. 28

29. Hakukuwa ila ukelele mmoja tu; na mara walizimwa! 29

30.
Nawasikitikia waja wangu. Hawajii Mtume ila wao
humkejeli.30

31. Je! Hawaoni umma ngapi tulizo ziangamiza kabla yao?
Hakika hao hawarejei tena kwao.31

32. Na hapana mmoja ila wote watakusanywa waletwe mbele
yetu. 32

33. Na Ishara hiyo kwao - ardhi iliyo kufa, nasi
tukaifufua, na tukatoa ndani yake nafaka, wakawa wanazila! 33

34. Na tukafanya ndani yake mabustani ya mitende na
mizabibu, na tukatimbua chemchem ndani yake, 34

35. Ili wale matunda yake, na hayo hayakufanywa na
mikono yao! Basi je, hawashukuru?35

36. Subhana, Ametakasika, aliye umba dume na jike vyote
katika vinavyo mea katika ardhi na katika nafsi zao, na katika wasivyo vijua. 36

37. Na usiku ni Ishara kwao. Tunauvua humo mchana, mara
wao wanakuwa gizani. 37

38. Na jua linakwenda kwa kiwango chake. Hayo ni
makadirio ya Mwenye nguvu, Mwenye kujua. 38

39. Na mwezi tumeupimia vituo, mpaka unakuwa kama karara
kongwe. 39

40. Haliwi jua kuufikia mwezi, wala usiku kuupita
mchana. Na vyote vinaogelea katika njia zao.40

41. Na ni Ishara kwao kwamba Sisi tuliwapakia dhuriya
zao katika jahazi ilio sheheni. 41

42. Na tukawaumbia kutoka mfano wake wanavyo vipanda. 42

43. Na tukitaka tunawazamisha, wala hapana wa
kuwasaidia, wala hawaokolewi, 43

44. Isipo kuwa kwa rehema zitokazo kwetu na starehe kwa
muda. 44

45. Na wanapo ambiwa: Jilindeni na yalioko mbele yenu na
yalioko nyuma yenu, ili mpate kurehemewa...45

46. Na haiwafikii Ishara yoyote katika Ishara za Mola
wao Mlezi ila wao huwa ni wenye kuipuuza. 46

47. Na wanapo ambiwa: Toeni katika aliyo kupeni Mwenyezi
Mungu, walio kufuru huwaambia walio amini: Je! Tuwalishe ambao Mwenyezi Mungu
angependa angeli walisha mwenyewe? Nyinyi hammo ila katika upotofu ulio
dhaahiri. 47

48. Na wanasema: Ahadi hii itatokea lini, ikiwa nyinyi
ni wakweli? 48

49. Hawangojei ila ukelele mmoja tu utakao wachukua nao
wamo kuzozana. 49

50. Basi hawataweza kuusia, wala kwa watu wao hawarejei.
50

51. Na litapulizwa barugumu, mara watatoka makaburini
wakikimbilia kwa Mola wao Mlezi. 51

52. Watasema: Ole wetu! Nani aliye tufufua kwenye malazi
yetu? Haya ndiyo aliyo yaahidi Mwingi wa Rehema na wakasema kweli Mitume. 52

53. Haitakuwa ila ukelele mmoja tu, mara wote
watahudhuruishwa mbele yetu. 53

54. Basi leo nafsi yoyote haitadhulumiwa kitu, wala
hamtalipwa ila yale mliyo kuwa mkiyatenda. 54

55. Hakika watu wa Peponi leo wamo shughulini,
wamefurahi. 55

56. Wao na wake zao wamo katika vivuli wameegemea juu ya
viti vya fakhari.56

57. Watapata humo kila namna ya matunda na watapata kila
watakacho kitaka.57

58. "Salama!" Hiyo ndiyo kauli itokayo kwa Mola Mlezi
Mwenye kurehemu. 58

59. Na enyi wakosefu! Jitengeni leo! 59

50. Je! Sikuagana nanyi, enyi wanaadamu, kuwa msimuabudu
Shet'ani? Hakika yeye ni adui dhaahiri kwenu.50

61. Na ya kwamba mniabudu Mimi? Hii ndiyo Njia Iliyo
Nyooka. 61

62. Na bila ya shaka yeye amekwisha lipoteza kundi kubwa
miongoni mwenu. Je, hamkuwa mkifikiri? 62

63. Hii basi ndiyo Jahannamu mliyo kuwa mkiahidiwa. 63

64. Ingieni leo kwa vile mlivyo kuwa mkikufuru. 64

65. Leo tunaviziba vinywa vyao, na iseme nasi mikono
yao, na itoe ushahidi miguu yao kwa waliyo kuwa wakiyachuma. 65

66. Na tungeli penda tungeli yafutilia mbali macho yao,
wakawa wanaiwania njia. Lakini wange ionaje? 66

67. Na tungeli taka tunge wageuza sura hapo hapo walipo,
basi wasinge weza kwenda wala kurudi. 67

68. Na tunaye mzeesha tunamrudisha nyuma katika umbo.
Basi je! hawazingatii? 68

69. Wala hatukumfundisha (Muhammad) mashairi, wala
hayatakikani kwake hayo. Haukuwa huu ila ni ukumbusho na Qur'ani inayo bainisha.
69

70. Ili imwonye aliye hai, na neno litimie juu ya
makafiri. 70

71. Je! Hawaoni kwamba tumewaumbia kutokana na iliyo
fanya mikono yetu wanyama wa mifugo, na wao wakawa wenye kuwamiliki. 71

72. Na Sisi tukawadhalilishia. Basi baadhi yao wako
wanao wapanda, na baadhi yao wanawala. 72

73. Na wao wanapata kwao manufaa na vinywaji. Basi je,
hawashukuru? 73

74. Na wameishika miungu mingine badala ya Mwenyezi
Mungu ili ati wapate kusaidiwa! 74

75. Hawataweza kuwasaidia. Bali hao ndio watakuwa askari
wao watakao hudhurishwa. 75

76. Basi maneno yao yasikuhuzunishe. Hakika Sisi
tunayajua wanayo yaweka siri na wanayo yatangaza. 76

77. Kwani mwanaadamu haoni ya kwamba Sisi tumemuumba
yeye kutokana na tone la manii? Kisha sasa yeye ndio amekuwa ndiye mgomvi wa
dhaahiri! 77

78. Na akatupigia mfano, na akasahau kuumbwa kwake,
akasema: Ni nani huyo atakaye ihuisha mifupa nayo imekwisha mung'unyika? 78

79. Sema: Ataihuisha huyo huyo aliye iumba hapo mara ya
mwanzo. Na Yeye ni Mjuzi wa kila kuumba. 79

80. Aliye kujaalieni kupata moto kutokana na mti wa
kijani nanyi mkawa kwa huo mnawasha. 80

81. Kwani aliye ziumba mbingu na ardhi hawezi kuwaumba
mfano wao? Kwani! Naye ndiye Muumbaji Mkuu, Mjuzi. 81

82. Hakika amri yake anapo taka kitu ni kukiambia tu:
Kuwa! Na kikawa. 82

73. Basi Ametakasika yule ambaye mkononi mwake umo
Ufalme wa kila kitu; na kwake Yeye mtarejeshwa. 83
Imetarjumiwa na Sheikh Ali Muhsin
Al-Barwani
Ikiwa una ushauri au maoni juu ya tarjuma
hii, andika kwa anwani hii qurani-tukufu@geocities.com
Copyright � 22 August 1997, Sheikh Ali Muhsin Al
Barwani