1. Naapa kwa jua na mwangaza wake na kuchomoza kwake na kwa joto lake!

 

2. Na kwa mwezi unapo lifuata na likawa nyuma yake kwa kutoa mwangaza baada ya kuchwa jua,

 

3. Na kwa mchana unapo lidhihirisha jua, likaonekana wazi halikufichikana.

 

4. Na kwa usiku unapo lifunika jua, ukawa mwangaza wake hauonekani.

 

5. Na kwa mbingu na kwa Mweza Mtukufu aliye inyanyua na akaijenga kwa hikima yake.

 

6. Na kwa ardhi na kwa Mweza Mtukufu aliye ikunjua kwa kila upande, na akaitengeneza kwa ajili ya utulivu, na akaifanya kama tandiko.

 

7. Na kwa nafsi, na aliye iumba na akaiweka sawa, kwa kuipa nguvu,

 

8. Akaifunza jema na baya, na akaipa uweza wa kutenda itakayo katika hayo,

 

9. Hakika amefuzu mwenye kuisafisha nafsi yake kwa ut'iifu na vitendo vya kheri.

 

10. Na hakika amekhasiri mwenye kuzificha fadhila zake, na akayaua matayarisho aliyo umbwa nayo ya kutenda kheri.

 

11,12. Kina Thamudi walimkanusha Nabii wao kwa upotovu wao na jeuri zao, alipo gutuka mwovu wao mkubwa kabisa kutaka kumchinja ngamia.

 

13. Saleh, Mtume wa Mwenyezi Mungu, akawaambia: Mwachilieni huyu ngamia wa Mwenyezi Mungu ale maridhawa katika ardhi ya Mwenyezi Mungu, na tahadharini msimzuie maji katika siku yake aliyo wekewa.

 

14. Wakamkadhibisha Mtume wao katika hilo onyo lake, wakamchinja. Mola wao Mlezi akazibomoa nyumba zao kwa sababu ya dhambi zao; akazisawazisha na ardhi!

 

15. Wala Yeye Mwenyezi Mungu hakhofu matokeo ya adhabu hiyo, kwani hiyo ni malipo ya haki kwa yale waliyo yatenda.