1. Mbingu itapo chanika, ikaamrishwa iondoke,
2. Na ikamsikiliza Mola wake Mlezi na ikamt'ii, na ndio
maelekeo yake isikie na kut'ii,
3. Na ardhi ikazidi upana wake kwa kulazwa milima na kuondolewa
kifusi chake,
4. Na ardhi ikatoa nje maiti na khazina ziliyo kuwamo ndani
yake, na ikaachana navyo vyote hivyo,
5. Na ikamwelekea Mola wake Mlezi kwa kuzidi kutanuka kwake na
kutoa vilio kuwemo ndani yake na kuachana navyo, na hayo ni haki yake kuwa.
Yakitokea yote hayo yaliyo tangulia kusimuliwa basi kila mtu atapata malipo ya
vitendo vyake.
6. Ewe mtu! Hakika wewe unafanya juhudi katika vitendo vyako
vikufikishie lengo lako. Basi utakuja kukutana na Mola wako Mlezi kwa a'mali
yako, naye atakulipa kwayo.
7,8,9. Ama mwenye kupewa daftari la vitendo
vyake kwa mkono wake wa kulia basi atahisabiwa kwa hisabu nyepesi, na atarejea
kwa jamaa zake Waumini naye furahani.
10,11,12. Ama mwenye kupewa daftari lake
kwa mkono wa kushoto wake nyuma ya mgongo wake kwa kudharauliwa shani yake, huyo
atatamani ajiue, na ataingia Motoni aungulie mbali!
13. Kwani huyo hakika duniani alikuwa furahani kati ya jamaa
zake akitanaamu na pumbao alilo kuwa nalo hata akapuuza a'mali ya kuitenda kwa
mustakabali wake.
14. Hakika huyo alidhani kuwa kabisa hatorejea kwa Mwenyezi
Mungu akamhisabu.
15. Bali atarejea, na atahisabiwa! Kwani Mola wake Mlezi
alikuwa anamwona vyema yeye na vitendo vyake.
16. Basi naapa kiapo cha mkazo kwa wekundu wa mbingu baada ya
kuchwa jua!
17. Na kwa usiku na unavyo vikusanya vyote katika giza lake,
wanaadamu, wanyama na vyenginevyo!
18,19. Na mwezi unapo kamilika kupevuka na kutimia
nuru yake, hapana shaka yoyote mtakutana na hali baada ya hali, baadhi yake zina
shida zaidi kuliko nyenginezo, za kufa na kufufuliwa na vitisho vya Kiyama.
20. Wana nini hawa makafiri yanayo wazuia wasimuamini Mwenyezi
Mungu na kufufuliwa baada ya kuwekwa wazi dalili zake zote za kuwajibika kwake?
21. Na pindi wakizisikia Aya za Qur'ani hawasujudu
wakanyenyekea?
22. Bali watu hawa, kwa ukafiri wao, wanakanusha kwa inadi na
kutakabari kuikataa Haki!
23. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kujua kabisa hayo wanayo
yadhamiria katika nyoyo zao.
24. Basi wabashirie, kwa kejeli, kuwa watapata adhabu ya
kutia uchungu.
25. Lakini walio amini na wakatenda mema watapata, kutoka kwa Mwenyezi Mungu, ujira usio wakatikia na wala usio kuwa na hisabu juu yao.