1. Nuun, ndio harufi ya N, iliyo anzia Sura hii ni kama kupinzana na hao wanao kadhibisha, na ili kuwazindua wenye kusadiki.

 

2. Naapa kwa kalamu wanayo andikia Malaika na wenginewe, na hayo mambo ya kheri na manufaa wanayo yaandika, hakika wewe, na Mwenyezi Mungu amekuneemesha kwa kukupa Unabii, si mchachefu wa akili, wala mpumbavu wa mawazo.

 

3. Na hakika unapata thawabu kubwa zisio katika kwa ajili ya kufikisha Ujumbe.

 

4. Na hakika wewe bila ya shaka umeshikamana na sifa nzuri kabisa na vitendo vizuri kabisa alivyo kuumba navyo Mwenyezi Mungu.

 

5,6. Karibuni hivi, ewe Muhammad, utaona, na makafiri wataona, ni nani kati yenu aliye mwenda wazimu.

 

7. Hakika Mola wako Mlezi, Yeye ndiye Mwenye kumjua zaidi aliye iacha Njia yake, na Yeye ndiye Mwenye kuwajua zaidi wenye akili walio ongoka kumwendea Yeye.

 

8,9. Basi usiyaache uliyo nayo ya kuwapinga wanao kanusha.  Wanatamani lau ungeli kuwa laini kwao katika baadhi ya mambo, ili na wao wawe laini kwako, kwa tamaa upate kurudishiana nao. (Neno lililo tumiwa hapo "Tud- hinu fayud-hinuun", maana yake khasa "Upake mafuta na wao wapake mafuta". Kiswahili husema: Kumpaka mtu mafuta kwa mgongo wa chupa. Yaani kumpa sifa za uwongo, kumfanyia unaafiki. Kwa Kiarabu ni "Mudaahana". Kupakana mafuta)

 

10,11,12,13. Wala usiache mwendo wako ulio nao kwenda kinyume na kila mwingi wa viapo, mtu wa kudharauliwa, mtapitapi mwenye kueneza aibu za watu, mwenye kuwasengenya watu, kuwasema kwa siri, mwenye kutwaa maneno baina ya watu kwa sababu ya kuwafisidi, mwingi wa kupinga kila la kheri, dhaalimu, mwingi wa madhambi, mgumu wa moyo, mwenye tabia ya ukavu, muovu maarufu kwa shari, juu ya sifa hizo mbovu alizo nazo.

 

14,15. Ati kwa kuwa anajiona yeye ana mali na watoto wengi!  Amezikadhibisha Aya zetu na amezipuuza. Akisomewa Qur'ani husema: Hivi ni visa vya uwongo vya watu wa kale!

 

16. Tutambandika alama juu ya pua yake ya kumganda, apate kufedheheka mbele za watu.

 

17,18. Sisi tumewafanyia mtihani watu wa Makka kwa kuwapa neema, nao wakazikufuru; kama tulivyo wafanyia mtihani hao watu wenye shamba, walipo chukua kiapo kuwa watakwenda vuna mazao ya shamba lao asubuhi mapema, wala wasimkumbuke Mwenyezi Mungu, wakafunganisha hilo jambo lao na kupenda kwake.

 

19,20. Basi ikaliteremkia shamba hilo balaa kubwa ilio toka kwa Mola wako Mlezi, na hali wao wamelala. Likawa hilo shamba kama usiku wa giza kwa masaibu yalio lifikia.

 

21,22. Asubuhi wakawa wanaitana: Amkeni mapema mwende kondeni kwenu kama mmeazimia kuvuna.

 

23,24. Wakatoka, nao wakinong'ona kuambizana: Msimwachie masikini yeyote kukuingilieni leo!

 

25. Wakenda hapo asubuhi mpaka kwenye shamba lao, na azma yao ovu hiyo, na wao ni wenye uwezo kaamili wa kutenda hayo kwa kujigamba kwao.

 

26,27. Walipo liona limekuwa jeusi limeungua, walisema nao wamebabaika: Hakika sisi bila ya shaka tumepotea. Hili silo shamba letu! Bali ndilo shamba letu! Na sisi tumenyimwa!

 

28. Alisema aliye kuwa muadilifu wao na mbora wao akiwalaumu: Sikukwambieni mlipo kuwa mnasemezana kuwanyima masikini, hebu hamumkumbuki Mwenyezi Mungu mkaiacha niya yenu?

 

29. Wakasema walipo rejea kwenye uwongozi wao: Tunamtakasa Mwenyezi Mungu kuwa katudhulumu kwa yaliyo tusibu. Hakika sisi wenyewe ndio tumejidhulumu kwa makusudio yetu maovu.

 

30,31. Wakawa wanaelekeana wao kwa wao wakilaumiana, wakisema: Huku ni kuhiliki kwetu! Hakika sisi tulikuwa tumepita mipaka katika dhulma zetu.

 

32. Asaa Mola wetu Mlezi akatupa badala lilio bora kuliko hili shamba letu. Hakika sisi tunamtaka Mola wetu Mlezi peke yake atupe msamaha na malipo.

 

33. Mfano wa kama hayo yaliyo yasibu hilo shamba ndio inakuwa adhabu yangu ninayo iteremsha duniani kwa anaye stahiki. Na bila ya shaka adhabu ya Akhera ni kubwa zaidi lau kuwa watu wanajua hayo.

 

34. Hakika wachamngu watapata kwa Mola wao Mlezi Bustani za neema safi.

 

35,36. Je! Sisi tudhulumu katika hukumu yetu, tuwafanye Waislamu sawa na makafiri? Nini lilio kusibuni nyinyi? Vipi mnahukumia mfano wa hukumu kama hii ya dhulma?

 

37,38.  Kwani mnacho kitabu kitokacho kwa Mwenyezi Mungu mnacho kisoma, na humo yamo hayo mnayo yapenda?

 

39. Au kwani mnazo ahadi juu yetu zenye kutiliwa mkazo kwa viapo, zenye kubaki mpaka Siku ya Kiyama, kwamba mnayo haki ya hayo mnayo jihukumia?

 

40. Ewe Muhammad! Waulize washirikina: Ni nani dhamini wa hukumu hiyo?

 

41. Kwani wanao wanao shirikiana nao, na wanao fuata mwendo wao katika kauli yao hii? Basi na wawalete hao washirika wao, ikiwa wao ni wasema kweli katika madai yao.

 

42,43. Siku mambo yatapo shitadi na yakawa magumu, na wakatakiwa makafiri wasujudu kwa kuwaemea na kuwakejeli, na wasiweze, macho yao yameinama chini, yamefunikwa na fedheha. Na duniani walikuwa wakitakiwa wasujudu walipo kuwa wakiweza na wakakataa kusujudu. (Kuwekwa wazi mundi, ni kinaya ya kudhihirishwa kweli yote Siku ya kwima kondo, Siku ya Kiyama. Chambilecho Sayyid Abdulla bin Ali bin Nassir katika Al Inkishaf:
              Tafakari siku ya kwima kondo
              Ya kuaridhiwa kila kitendo
              Pindi madhulumu atapo ondo
              Achamba Ya Rabi namua naye)

 

44. Ewe Muhammad! Nachilie na hao wanao ikadhibisha Qur'ani. Tutawajongeza kwenye adhabu kidogo kidogo kwa jiha wasio ijua kuwa adhabu itatokea huko.

 

45. Na nitawapa muhula kwa kuiakharisha adhabu. Hakika mipango yangu ni ya nguvu, na hawezi kuporonyoka yeyote akasalimika nayo.

 

46. Kwani wewe unawaomba ujira kwa kuufikisha Ujumbe wako, na kwa hivyo wao wanaona uzito kwa gharama hiyo unayo wakalifisha?

 

47. Au kwani wao wanajua yaliyo fichikana na wao wanayaandika na ndio wanahukumu kwa hayo?

 

48. Basi wewe subiri kwa tunavyo wapa muhula na kukuakhirisha kukuletea manusura yetu juu yao. Wala usiwe kama Yunus, aliye mezwa na samaki, akawa na haraka na kuwaghadhibikia watu wake, alipo mnadia Mola wake Mlezi, naye kajaa hasira na ghadhabu, akitaka waadhibiwe kwa haraka.

 

49. Lau kuwa neema ya Mola wake Mlezi haikumdiriki kwa kukubali toba yake, angeli tupwa kutokana na tumbo la samaki ufukweni, naye akiteseka kwa kuteleza kwake.

 

50. Lakini Mola wake Mlezi kamteuwa kwa kuikubali toba yake, na akamjaalia miongoni mwa watu wema.

 

51. Na makafiri wangeli karibia kukutelezesha na pahala pako, kwa jicho lao wanalo kuangalia kwa uadui na chuki wanapo isikia Qur'ani, wakisema: Hakika huyu ni mwendawazimu.

 

52. Na Qur'ani si chochote ila ni mawaidha, na hikima, na ukumbusho kwa walimwengu wote.