1.
Mwenyezi Mungu amekwisha sikia kauli ya huyo mwanamke anaye kurejea wewe kwa
shauri ya mumewe aliye jitenga naye kwa kudai ati anamwona kama mgongo wa mama
yake, na akamlalamikia Mwenyezi Mungu. Na Mwenyezi Mungu anayasikia hayo maneno
mnayo jibizana. Hakika Mwenyezi Mungu anayasikia vyema yote ya kusikiwa,
anayaona vyema yote ya kuonekana. Imepokelewa kuwa Sahaba mmoja, aitwaye Aus bin
Ass'amit, aliudhika na mkewe aitwaye, Khola bint Tha'labah, akamwambia: "Wewe
kwangu mimi kama mgongo wa mama yangu." Na katika siku za Ujahiliya ilikuwa ndio
mwanamke kesha harimika kwa mumewe. Mwanamke akenda kumpa khabari Nabii s.a.w.,
na Mtume akamwambia: "Sijaamrishwa kitu katika kesi yako. Na sioni ila ni kuwa
kweli umekwisha harimika kwake." Mwanamke akajadiliana na Mtume s.a.w. na
akamrejea tena, na akawa anamshitakia Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa kukhofu
kufarikiana na mume na kupotea mwanawe. Haukupita muda ila ikateremka Aya hii na
tatu zilizo baada yake.
2. Enyi Waumini! Hao
miongoni mwenu wanao jitenga na wake zao kwa kuwashabihisha katika kuharimikiana
nao kuwa ati ni kama mama zao, ni wakosa. Wake zao sio mama zao. Ukitaka haki
mama zao ni wale walio wazaa tu. Na hakika wanao watenga wake zao kwa kusema
hivyo wanasema kauli inayo chusha, inayo udhi katika murwa mwema, na ni uwongo
ulio tokana na haki. Na hakika Mwenyezi Mungu bila ya shaka ni Mkuu wa kusamehe
na kughufiria kwa yaliyo kwisha pita kwenu.
3. Na wale wanao watenga
wake zao na kisha wakarejeza kauli yao, wakayaona makosa yao, na wakataka kubaki
na wake zao, basi juu yao kumkomboa mtumwa kabla ya kugusana. Hayo aliyo
yawajibisha Mwenyezi Mungu, ya kukomboa mtumwa, ni mawaidha kwenu mnawaidhiwa
ili msirejee tena katika makosa hayo. Na Mwenyezi Mungu ni Mwenye kuyajua
vilivyo myatendayo.
4. Na asiye pata mtumwa wa
kumkomboa, basi yampasa afunge miezi miwili mfululizo kabla hawajagusana. Na
asiye weza kufunga hivyo basi itampasa awalishe masikini sitini. Tumeyalazimisha
hayo ili mpate kumuamini Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na mtende kwa mujibu wa
Imani hiyo. Na hiyo ndiyo mipaka ya Mwenyezi Mungu, basi msiikiuke. Na makafiri
watapata adhabu yenye machungu makali.
5. Hakika wanao mfanyia
inda Mwenyezi Mungu na Mtume wake kwa kupingana nao watatupiliwa mbali kama
walivyo tupiliwa mbali walio kuwa kabla yao. Na Sisi tumekwisha teremsha dalili
zilizo wazi za kuonyesha Haki. Na hao wapinzani watapata adhabu ya
kuwafedhehesha mno.
6. Siku Mwenyezi Mungu
atapo wafufua wote baada ya kwisha kufa kwao, na awape khabari za yale waliyo
yatenda. Mwenyezi Mungu amewawekea yote na ameyahifadhi, na wao wameyasahau. Na
Mwenyezi Mungu ni Shahidi wa yote na anayajua yote.
7. Kwani hujui kwamba
Mwenyezi Mungu anayajua yaliomo mbinguni na yaliomo katika ardhi, na wala hapana
siri ya watu watatu ila Yeye Mwenyezi Mungu ndiye wane wao kwa kuyajua kwake
wanayo fanyia siri, wala hawawi watano ila na Yeye ndiye wa sita wao. Wala duni
kuliko hivyo, wala kuzidi hivyo, ila Yeye yuko pamoja nao, anayajua hayo wanayo
yanong'ona, popote walipo. Kisha Siku ya Kiyama atawapa khabari kwa kila walilo
litenda. Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye kutimia ujuzi wake.
8. Ewe Mtume! Huwaoni hao
walio katazwa kufanya njama za siri wao kwa wao kwa mambo ya kutia shaka katika
nyoyo za Waumini, kisha wakayarejea yale yale waliyo katazwa? Na wanafanya njama
kwa madhambi wanayo yatenda, na uadui wanao uazimia, na uasi dhidi ya Mtume wa
Mwenyezi Mungu. Na wanapo kuja kwako wanakuamkia kwa kauli ya kupotoa, sivyo
anavyo kuamkia Mwenyezi Mungu. Na wao husema katika nafsi zao: Mbona Mwenyezi
Mungu hatuadhibu kwa haya tunayo yasema ikiwa huyu ni Mtume kweli? Inawatosha
hao Jahannamu. Wataingia humo waungue kwa moto wake. Na marejeo maovu yalioje
marejeo yao. Ilikuwako sulhu baina ya Waislamu na Mayahudi katika mji wa Madina.
Na ikawa akipita mtu katika Waislamu kwao Mayahudi hunong'ona wao kwa wao ili
adhani yule Muislamu kuwa wao wanapanga njama za kutaka kumuuwa, au lolote la
kumdhuru apate kugeuza njia asiwapitie tena. Mtume s.a.w. akawakataza hayo,
lakini hawakuacha mtindo wao, wakayarejea yale yale waliyo katazwa. Na wakawa
akija Mtume s.a.w. wakimwamkia kwa maamkio ya kumuapiza. Ndiyo ikashuka Aya hii.
9. Enyi mlio msadiki
Mwenyezi Mungu na Mtume wake! Mnapo sema siri, basi msiwe mkisema siri katika
mambo ya madhambi, na kufanya uadui, na kwenda kinyume na Mtume. Semeni siri
katika mambo ya kheri, na kuepukana na madhambi. Na mwogopeni Mwenyezi Mungu
ambaye kwake Yeye tu, si kwengineko, ndio mtakusanywa baada ya kufufuliwa.
10. Hakika kusema siri
kwa kuchochea shaka shaka ni katika kuzainishwa na Shetani, ili apate kuingiza
huzuni katika nyoyo za Waumini. Wala hayo hayawezi kuwaletea madhara yoyote wao
ila kwa kupenda Mwenyezi Mungu. Basi Waumini wamtegemee Mwenyezi Mungu peke
yake.
11. Enyi mlio msadiki
Mwenyezi Mungu na Mtume wake! Mkitakiwa baadhi yenu kuwafanyia nafasi wenzenu
mnapo kaa katika majlisi zenu, basi wafanyieni nafasi. Na Mwenyezi Mungu
atakufanyieni nyinyi nafasi. Na mkitakiwa kuondoka pale mlipo kaa basi ondokeni.
Mwenyezi Mungu hutukuza vyeo vya Waumini, na wale walio pewa ilimu kwa daraja
nyingi. Na Mwenyezi Mungu anazo khabari za mnayo yatenda.
12. Enyi mlio msadiki
Mwenyezi Mungu na Mtume wake! Mkitaka kusema siri na Mtume wa Mwenyezi Mungu,
basi kabla ya mazungumzo yenu hayo tangulizeni kutoa sadaka. Hivyo ndio kheri
yenu, na ni usafi zaidi kwa nyoyo zenu. Lakini ikiwa hamkupata cha kutoa sadaka,
basi hakika Mwenyezi Mungu ni Mkunjufu wa kusamehe, Mwenye kukusanya rehema
zote.
13. Mnachelea
kujilazimisha kutoa sadaka kabla ya mazungumzo yenu na Mtume wa Mwenyezi Mungu?
Na ikiwa hamkutoa, na Mwenyezi Mungu akakusameheni, basi hifadhini kushika Sala
na kutoa Zaka, na mt'iini Mwenyezi Mungu na Mtume wake. Na Mwenyezi Mungu anazo
khabari za vitendo vyenu, naye atakulipeni kwavyo.
14. Ewe Mtume! Huwaoni
wanaafiki walio wafanya marafiki watu ambao Mwenyezi Mungu ameghadhibika nao.
Hawa wanao fanya urafiki si katika nyinyi, na hao wanao fanywa ni marafiki pia
si katika nyinyi. Na wanaapa kwa uwongo, na huku wanajua kuwa wao ni waongo.
15. Mwenyezi Mungu
amewatengenezea hawa wanaafiki adhabu ya mwisho wa ukali. Hakika vitendo vyao
walivyo kuwa wakivitenda, vya unaafiki, na kuchukua viapo vya uwongo, ni viovu
mno.
16. Wamefanya viapo vyao
kuwa ndio viwe ni kinga ya kuwakinga wasiuliwe wenyewe, na watoto wao wasiwe
mateka, na mali yao yasiwe ngawira. Kwa hayo wakaizuilia Njia ya Mwenyezi Mungu.
Basi watapata adhabu ya fedheha.
17. Mali yao na watoto
wao hayatawalinda na adhabu ya Mwenyezi Mungu hata chembe. Hao ni watu wa
Motoni, wa kudumu humo milele.
18. Siku atapo wafufua
Mwenyezi Mungu wote watamwapia kuwa hakika wao walikuwa ni Waumini, kama wanavyo
kuapieni nyinyi hivi sasa. Na wanadhani kuwa kwa kuapa kwao huku ni ujanja
utakao wafaa. Ama kweli, hakika hawa wamefika ukomo wa uwongo!
19. Shetani amewatawala
na amewasahaulisha kumdhukuru Mwenyezi Mungu na kuukumbuka utukufu wake. Hao
ndio kundi la Shetani. Ama kweli, hakika kundi la Shetani ndilo lilio fikilia
mwisho wa kukhasiri.
20. Hao wanao mfanyia
inda Mwenyezi Mungu na Mtume wake, hao ndio katika hisabu ya walio fikilia ukomo
wa udhalili.
21. Mwenyezi Mungu
amekata hukumu: Bila ya shaka Mimi na Mtume wangu tutashinda. Hakika Mwenyezi
Mungu ni Mwenye nguvu zilizo timia, hashindwi na yeyote.
22. Huwakuti watu wanao
msadiki Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho wanapendana na wenye kumfanyia uadui
Mwenyezi Mungu na Mtume wake, hata wakiwa ni baba zao, au ni watoto wao, au ni
ndugu zao, au ni jamaa zao. Hao ambao hawafanyi urafiki na wanao mpinga Mwenyezi
Mungu, Mwenyezi Mungu ameithibitisha Imani katika nyoyo zao, na amewaunga mkono
kwa nguvu zinazo tokana naye Yeye Mwenyewe, na atawatia katika Mabustani
yapitayo mito kati yake wakikaa humo milele. Neema zake haziwakatikii. Mwenyezi
Mungu amewapenda hao, na wao wamempenda. Hao ndio wanao ambiwa kuwa ni katika
Hizbullahi, yaani Kundi la Mwenyezi Mungu. Hakika ni kweli Kundi la Mwenyezi
Mungu ndilo lenye kufuzu.
Copyright � 22 August 1997, Sheikh
Ali Muhsin Al Barwani