1. Umewakaribia washirikina wakati
wao wa kuhisabiwa Siku ya Kiyama, nao hali wameghafilika na kitisho chake,
wanapuuza kuiamini.
2. Haiwajii Qur'ani kutokana na
Mola wao Mlezi pale inapoteremka kuwakumbusha ya kuwanufaisha, ila wao
huisikiliza na hali wao wameshughulika na mengine yasiyo na faida nao, wakicheza
kama wachezavyo watoto wadogo.
3. Nyoyo zao zimo katika pumbao,
hazizingatii, wameshikilia kuficha njama zao za kumpinga Nabii na Qur'ani,
wakiambizana wenyewe kwa wenyewe: Huyu Muhammad si chochote ila ni mtu tu kama
nyinyi. Na Mtume hawi ila Malaika. Basi, je! Mnamsadiki Muhammad na mnahudhuria
baraza za uchawi na hali nyinyi mnaona kuwa hakika huo ni uchawi?
4. Mtume, kwa kuwa Mwenyezi Mungu
kamjuulisha waliyo kuwa wakiyasema kwa siri, aliwaambia: Mola wangu Mlezi
anayajua yote yanayo semwa katika mbingu na katika ardhi, na Yeye ndiye anaye
sikia kila linalo sikiwa; na anajua kila linalo tokea..
5. Bali wao wakasema: Hizi ni
mchanganyiko wa ndoto alizo ziota (Muhammad); bali kazua tu na akamsingizia
Mwenyezi Mungu kwa uwongo. Kisha wakaacha hayo na wakasema: Bali huyu ni mtunga
mashairi anaziteka nafsi za wenye kumsikiliza. Kama kweli, basi na atuletee
muujiza khasa wa kuonyesha ukweli wake, kama walivyo tumwa Manabii wa zamani
wakitiwa nguvu kwa miujiza mbali mbali.
6. Hizo kaumu tulizo ziangamiza
baada ya kukadhibisha hiyo miujiza hazikuamini. Basi, je! Watakuja amini hawa
yatapo wajia hayo wayatakayo?
7. Ewe Nabii! Kabla yako wewe
hatukuwatumia watu ila watu wa kibinaadamu vile vile, ambao tuliwafunulia Dini
waifikishe kwa watu. Basi, enyi mnao kataa! Waulizeni wanazuoni wajuao ilimu za
Vitabu vilivyo teremka, ikiwa nyinyi hamyajui hayo.
8. Wala Sisi hatukuwajaalia Mitume
kuwa na miili inayo khitalifiana na miili ya wanaadamu wengine, wakawa wanaishi
bila ya chakula, na wakabaki siku zote, na wala hawakuwa wanaishi daima milele.
9. Kisha tukawatimizia na
tukawahakikishia ahadi, na tukawaokoa wao na pamoja nao tukawaokoa tulio taka
kuwaokoa miongoni mwa Waumini. Na makafiri walio vuka mipaka tuliwaangamiza kwa
kukadhibisha kwao na kuukataa Ujumbe wa Manabii wao.
10. Sisi hakika
tumekuteremshieni Kitabu. Ndani yake yamo mawaidha ya kuwakumbusheni ikiwa
mtakisoma na mtayatenda yaliyomo ndani yake. Basi huwaje mkakipuuza na
mkakikataa? Je, inda na upumbavu umefika hadi ya kukufikisheni hali hii mlio
nayo, mkawa hamuelewi lipi lenye manufaa nanyi mkalikimbilia?
11. Na wengi katika watu
wa miji tuliyo iteketeza kwa sababu ya ukafiri wao na kuwakadhibisha Manabii, na
baada yao tukasimamisha kaumu nyengine zenye hali bora na mwisho mwema kuliko
hao.
12. Na tulipo taka
kuwateketeza, na wakahisi ukali wa adhabu yetu na uwezo wetu wa kuwateremshia
hayo yatakayo wapata, wakafanya haraka kukimbia, kama wanyama hayawani, ati
kutafuta kuokoka!
13. Enyi wapinzani!
Msikimbie! Hapana kitu chochote kitacho kulindeni na adhabu ya Mwenyezi Mungu.
Rudini kwenye zile zile neema na majumba mliyo kuwa nayo, huenda watumishi wenu
na wenzenu watakutakeni msaada na rai kama ilivyo kuwa ada yenu. Wapi!
Hamtoweza!
14. Kwa kuwa hao makafiri
wamekwisha sikia wanavyo kejeliwa na wanavyo itwa kwenda teketezwa na wana
yakini nako, basi watasema: Hakika kweli sisi tulikuwa ni wenye kudhulumu tulipo
yaacha yanayo tunafiisha, na tusiziamini Ishara za Mola wetu Mlezi.
15. Maneno hayo hawaachi
kuyakariri na kuyapigia makelele mpaka kwa adhabu yetu tukawafanya kama mimea
iliyo fyekwa, na moto ulio zimika, hawana tena uhai.
16. Wala hatukuziumba
mbingu na ardhi na viliomo baina yao kwa mpango huu wa hikima, na muundo huu wa
namna peke yake, kwa mchezo. Bali tumefanya yote haya kwa hikima ya juu ambayo
wanaifahamu wenye kuzingatia.
17. Lau kuwa tunataka
kufanya mchezo na pumbao isingeli mkinika kuchukua ila yaliyo katika ufalme
wetu, kwani hapana ufalme ila wetu - ingeli kuwa Sisi ni wa kufanya hayo. Wala
nasi si wenye kufanya hayo, kwa kuwa si laiki ya haki yetu.
18. Lakini jambo linalo
tuelekea Sisi kulifanya ni kuipambanisha kweli juu ya uwongo ipate kuuondoa. Na
nyinyi makafiri mtahiliki kwa sababu ya kumzulia Mwenyezi Mungu na Mtume wake.
19. Na ni vya Mwenyezi
Mungu peke yake vyote viliomo mbinguni na katika ardhi, kwa kuviumba na
kuvimiliki. Basi ni haki Yeye peke yake kuabudiwa. Na Malaika walio karibishwa
kwake hawana kiburi cha kuwazuia kumuabudu na kumnyenyekea, wala hawaoni machofu
na kunyong'onyea kwa ibada ya mchana na usiku.
20. Wanamtakasa aliye
tukuka shani yake na kila lisio muelekea. Kumtakasa huku hakusiti, bali huo ni
mtakaso wa daima, hawana shughuli nyengine ya kuwashughulisha.
21. Washirikina hawafanyi
wafanyavyo walio karibishwa katika kumsafishia ibada Mwenyezi Mungu, bali wao
wamewaabudu wenginewe, na wakafanya miungu duniani isiyo stahiki kuabudiwa. Na
huwaje kwenda kuabudu kitu kisicho kuwa Mwenyezi Mungu, ambacho hakiwezi
kufufua?
22. Lau kuwa mbinguni na
duniani kuna miungu isipo kuwa Mwenyezi Mungu wanao endesha mambo yao, basi
ingeli haribika nidhamu iliyo simamishiwa hizo mbingu na ardhi kwa kuumbwa, na
ikafikilia mwisho wa mpango na hikima. Basi na atakasike Mwenyezi Mungu, Mwenye
Ufalme wote, na yote wanayo msingizia washirikina.
23. Yeye Subhanahu
hahojiwi kwa anayo yatenda, kwani ni Yeye pekee mwenye utukufu na madaraka,
Mwenye hikima na ujuzi. Hakosei katika kutenda chochote. Ni wao ndio
watahisabiwa na kuhojiwa kwa wanayo yatenda, kwa kuwa wao hukosea kwa udhaifu
wao na ujinga wao na kughilibiwa na matamanio.
24. Hawaujui waajibu wa
Mwenyezi Mungu uliyo juu yao, ndio maana wakawa na miungu mingine isiyo kuwa
Yeye wakaiabudu bila ya kuwa na ushahidi wowote wa kuingia akilini, wala
uthibitisho wa kweli. Ewe Nabii! Waambie: Leteni uthibitisho wenu kama kweli
Mwenyezi Mungu ana mshirika katika utawala hata akafaa kushirikishwa katika
kuabudiwa. Hii Qur'ani iliyo kuja kuukumbusha umati wangu kwa linalo wajibikia,
na hivi Vitabu vya Manabii wengine vilivyo kuja kukumbusha kaumu za kabla yangu,
vyote hivyo vimesimama juu ya Tawhid, Upweke wa Mwenyezi Mungu. Lakini wengi wao
hawajui yaliyo kuja ndani ya Vitabu hivyo, kwa sababu hawajishughulishi
kuyazingatia yaliomo humo. Basi wao wamekuwa wenye kuipuuza Imani ya Mwenyezi
Mungu.
25. Ewe Nabii! Sisi
hatukumtuma Mtume yeyote kabla yako ila tulimpa wahyi (ufunuo) awafikishie watu
wake kuwa hastahiki kuabudiwa isipo kuwa Mimi. Basi nisafieni ibada, iwe kwangu
tu.
26. Na baadhi ya makafiri
wa Kiarabu walisema: Arrahman, Mwenyezi Mungu Mwingi wa Rehema, ana mwana, kwa
yale madai yao kuwa Malaika ni binti za Mwenyezi Mungu. Ametakasika na kuwa na
mwana! Kwani hao Malaika ni waja wake walio tukuzwa tu kwa kuwakaribisha, na kwa
wanavyo muabudu Yeye.
27. Hawamtangulii Mwenyezi
Mungu kwa kauli yao wainenayo kabla ya Yeye kuwapa ruhusa. Na wao hawatendi
lolote ila kwa amri yake tu, wala hawapindukii mipaka ya amri anayo waamrisha.
28. Mwenyezi Mungu
anazijua hali zao zote na vitendo vyao vyote, walivyo vitanguliza na walivyo
viakhirisha. Wala hawamwombei mtu kwake ila kwa aliye ridhia Mwenyezi Mungu. Na
wao jinsi ya wingi wa khofu yao kumwogopa Mwenyezi Mungu Mtukufu, na kumtukuza
Yeye, daima wana hadhari naye..
29. Na miongoni mwa
Malaika atakaye sema: Mimi ni mungu wa kuabudiwa badala ya Mwenyezi Mungu, huyo
tutamlipa kwa kumtia Jahannamu. Mfano wa malipo hayo tunamlipa kila mwenye
kupindukia mipaka ya haki, na wakajidhulumu nafsi zao kwa kudai Ungu na kuingia
katika ushirikina.
30. Wenye kukufuru
wamepofuka, na hawaoni kuwa mbingu na ardhi hapo mwanzo zilikuwa zimeshikamana.
Kwa uwezo wetu tukazibambandua mbali mbali. Na tukajaalia kutokana na maji,
ambayo hayo si kitu hai, kila chenye uhai kutokana na hayo hayo. Basi je! Baada
ya yote haya wangali kupuuza tu, na hawaamini kuwa bila ya shaka yoyote hapana
mungu isipo kuwa Sisi? "Je! Hao walio kufuru hawakuona kwamba mbingu na ardhi
zilikuwa zimeambatana, kisha Sisi tukazibabandua? Na tukajaalia kwa maji kila
kilicho hai? Basi je, hawaamini?" Aya hii ina maana ya kisayansi yenye kutilia
nguvu nadhariya ya ilimu za kisasa katika kuumbwa sayari na ardhi. Nayo ni kuwa
mbingu na ardhi asili yao zilikuwa zimeshikamana. Na ukweli wa sayansi zinazo
kubaliwa ni kuwa hakika ziliambatana, na sayansi mbali mbali zinathibitisha
hayo. Na zipo nadhariya nyengine kadhaa wa kadhaa ambazo kwazo zaweza kuelezea
dhaahiri ya mambo haya. Lakini bado kuthibiti nadhariya mojapo kwa njia ya mkato
kwa wanazuoni kwa kuwafikiana wote. Kwa kuonyesha mfano tutaja nadhariya mbili:
Nadhariya ya Kwanza: Imekhusu kuumbwa kwa mfumo wa jua (Solar System). Kwa mfano
imethibiti kuwa mawingu au umande ulio zunguka jua ulianza kuenea kwenye anga
lilio baridi, na chembechembe za gasi zinazo fanya hayo mawingu au moshi
zikakusanyika kwenye chembechembe za vumbi linalo kwenda kwa kasi kubwa. Kisha
chembechembe hizo zikawa zinagongana na zinarindika, na huku ndani yake zikawamo
gasi nzito, na kukazidi kurindika na kujumuika kwa kupita mamilioni na mamilioni
ya makarne mpaka zikafanyika sayari na mwezi na ardhi kwa umbali unao stahiki.
Na yajuulikana kuwa huko kukusanyika na kurindika huzidisha mbinyo (Pressure),
na huo huzidisha joto. Na gamba la ardhi lilipo ingia kupoa, na wakati zilipo
ripuka volkano ardhi ikapata mvuke wa maji na gasi ya Carbon dioxide ilio tokana
na miripuko ya volkano...na katika iliyo saidia kupatikana Oxygen katika hewa
baada ya hapo ni nishati na nguvu za miyale ya jua kwa njia ya mwanga juu ya
mimea na majani ya mwanzo. Ama Nadhariya ya Pili: Imekhusiana na uumbaji wa
ulimwengu kwa jumla, ambao kwa mukhtasari unaelezwa na kauli yake Mtukufu:
"Zilikuwa zimeambatana", yaani zimeshikamana na kuwa kitu kimoja. Na hayo ndiyo
yaliyo fikilia mwishoni ilimu za sayansi katika uumbaji wa ulimwengu. Nayo ni
kwamba kabla ya kufikilia sura yake hii ya sasa ulikuwa kama donge lilio
kusanyika lenye kutisha, la mkusanyiko wa chembechembe zenye kuambatana chini ya
mbinyo pressure, hata akili haiwezi kuifikiria. Na hizi sayari zote na nyota
zilioko mbinguni hivi leo tunazo ziita mfumo wa jua solar system zilikuwa ni
mkusanyiko wa donge moja lisilo zidi 1/2 diameter yake maili milioni tatu. Na
neno lake Mwenyezi Mungu: "Tukazibambandua" linafahamisha ule mripuko mkubwa wa
mwanzo wa ki-nuclear ukazalisha uumbaji wa anga na sayari za namna mbali mbali
tunazo ziita kwa pamoja "Mfumo wa Jua" au Solar System. "Na tukajaalia kwa maji
kila kilicho hai": Aya hii imethibitisha uhakika wa kisayansi ulio thibitishwa
na ncha mbali mbali za ilimu. Imethibitisha Cytology, sayansi ya "cells",
(khalaya), kwamba maji ni muhimu kabisa katika ujengaji wa "cells" zote za vitu
vilivyo hai, ikiwa mimea au wanyama. Na ilimu ya "Kimyaa", Chemistry kwamba maji
ni lazima yapatikane katika vitendo na mageuko yoyote katika viumbe vilivyo hai.
Basi hayo maji ama yawe ni kiungo, kitu cha kusaidia, au cha kuwamo ndani ya
kitendo, au ni matokeo yake. Na imethibitisha ilimu ya viungo physiology kwamba
maji ni dharura kwa viungo kufanya kazi yao. Bila ya hayo maji hautodhihiri uhai
katika viungo.
31. Na katika dalili za
uweza wetu ni kuwa tumeifanya milima imesimama imara kwenye ardhi ili
isiyumbeyumbe nao watu, na tumefanya humo njia pana, za kupitia kwa wasaa, ili
waweze kuongoza njia humo kwa makusudio yao. Maoni ya wataalamu juu ya Aya ya
31: "Na tukaweka katika ardhi milima iliyo thibiti ili isiwayumbishe, na
tukaweka humo njia pana ili wapate kuongoka." Ilivyo kuwa ndani ya ardhi kila
kitu kimeyayuka, na lau kuwa milima imewekwa tu katika baadhi ya sehemu za huu
mpira wa dunia kama majabali yaliyo nyanyuka juu tu, uzito wao ungeli sabibisha
gamba la dunia liyumbe, au lipindane na kupasuka. Kwa hivyo Mwenyezi Mungu kwa
utukufu wa shani yake ameifanya milima isimame imara kwa kuwa na mizizi iliyo
zama kwenye gamba la ardhi mpaka chini kwenye kina kirefu kulingana na urefu
wake kwendea juu. Kwa hivyo imekuwa hiyo milima kama vigingi, kama alivyo jaalia
eneo la minyanyuka hii na mizizi ni duni kuliko maeneo ya gamba lilio zunguka.
Yote haya ni kwa ajili ya kueneza sawa uzito wa juu ya gamba kwa pande zote ili
pasiwepo kuyumbayumba na kupasuka. Kwani hakika kuenezwa kwa uzito juu ya uso wa
dunia yakaribia kuwa hakuleti athari kubwa ya kutajika. Na ilimu za kisasa
zimethibitisha kuwa kuenezwa kwa nchi kavu na maji juu ya ardhi, na kuwepo
mfululizo wa milima juu yake ni katika yanayo hakikisha hali ilivyo ardhi, na
imethibitika kuwa chini ya milima mizito kuna vitu vyepesi kubungunyika, na
chini ya maji ya bahari kuu vipo vitu vizito. Kwa kuenezwa uzani wa namna hiyo
mbali mbali katika dunia, na mgawanyo huu wa milima, makusudio yake ni
kusawizisha uzani wa mpira huu wa ardhi. Na ilivyo nyanyuka milima zikatokea
nyanda na mabonde na njia baina ya milima na mwambao na bahari na minyanyuko, na
zikawa njia.
32. Na tumeifanya mbingu
kama dari iliyo nyanyuliwa, na tukailinda isianguke, au visianguke viliomo humo.
Na juu ya hayo, wao hawazioni wala hawaziingatii Ishara zetu zenye kuonyesha
uweza wetu na hikima yetu na rehema yetu. Maoni ya wataalamu juu ya Aya 32: "Na
tukaifanya mbingu kuwa dari iliyo hifadhiwa lakini wanazipuuza Ishara zake. ":
Aya hii tukufu imethibitisha kuwa mbingu na vyote viliomo ndani yake
vimehifadhiwa visiwe na ila yoyote, na vimehifadhiwa visidondoke juu ya ardhi.
Na mbingu ni kila kilicho juu yetu, kuanzia kifuniko hichi cha hewa inayo
walinda walioko juu ya ardhi na khatari nyingi za angani ambazo zinazuia maisha,
mfano wa vimondo vya nyota za mkia, na miyale. Na juu ya ardhi pana kifuniko cha
hewa kinacho linda ardhi kwa nguvu za mvutano, na haifai kukosekana hivyo bila
ya maangamizo kabisa. Na juu ya kifuniko cha hewa ndio kuna hizo sayari za
mbinguni, na zipo kwa umbali mbali mbali kufuatana na nyendo zao tangu mwanzo.
"Na tukaifanya mbingu kuwa dari iliyo hifadhiwa" yaani hizo sayari na vyote
vilio mbinguni vyaonekana kwa nadhari yetu kama kwamba ni dari, na tunaona vilio
juu ya vichwa vyetu kama ni vidogo kuliko vilioko upeo wa macho. Na hayo ni
kiini macho tu, kama tunapo liona jua kubwa wakati wa kuchomoza na kuchwa kuliko
adhuhuri. Na hili qubba la mbingu lina sifa zake, zinazo khitalifiana kila
ukizidi mnyanyuko wa ardhi, kama hizo sayari za mbinguni kwa mujibu wa jicho
linavyo ona katika qubba la mbingu.
33. Na Mwenyezi Mungu
ndiye aliye umba usiku na mchana, na jua na mwezi. Vyote hivyo vinakwenda katika
njia zake kama alivyo zijaalia Mwenyezi Mungu, na zinamtakasa bila ya kupotea.
Maoni ya wataalamu juu ya Aya 33: "Na Yeye ndiye aliye umba usiku na mchana na
jua na mwezi, vyote katika anga vinaogelea." Kila sayari ya mbinguni ina
mzunguko wake makhsusi inayo ogelea kuufuata. Na zote hizo hazisiti, na
zinakwenda kwa mwendo wao maalumu katika anga. Na sisi tunaona hayo kwa hakika
kwa kutazama mwendo wa jua na mwezi. Kama kadhaalika mzunguko wa ardhi wake
wenyewe ndio unao leta usiku na mchana kwa zamu, kama kwamba unaogelea.
34. Ewe Nabii!
Hatukumjaalia mwanaadamu yeyote kabla yako wewe aishi milele, hata ikawa hao
makafiri wakawa wanakutamania ufe wewe. Vipi wanakutamania mauti wewe na hali na
wao vile vile watakufa kama wewe? Ukifa wewe, je, ndio wao watabakia kushinda
wanaadamu wote?
35. Kila nafsi haina budi
kuonja mauti. Na Sisi tunakufanyieni hapa duniani kama wenye kukupeni mtihani,
kwa kukupeni yenye manufaa yenu na yenye madhara pia, ili abagulike mwenye
kushukuru kwa kupewa kheri na kuvumilia balaa, na yule asiye na fadhila kwa
neema aipatayo na anapapatika akipata misiba. Nanyi mtarejeshwa kwetu, na hapo
tutakuhisabieni vitendo vyenu.
36. Na wakikuona, ewe
Nabii, wale walio mkataa Mwenyezi Mungu na ulio kuja nayo wewe, hawakufanyii
wewe ila maskhara na kejeli. Huambiana wao kwa wao: Ndiye huyu anaye watia aibu
miungu yenu? Na hali wao hawasadiki kumdhukuru Mwenyezi Mungu ambaye ndiye aliye
waeneza rehema yake!
37. Na ikiwa wao wanataka
waletewe adhabu kwa upesi, basi ndio tabia ya binaadamu kutaka kila jambo kwa
haraka. Basi enyi wenye haraka! Nitakuonesheni neema yangu duniani, na adhabu
yangu Akhera. Msijishughulishe kuhimiza kitu ambacho hakina budi kuwa. Maoni ya
wataalamu juu ya Aya 37: "Mwanaadamu ameumbwa na haraka. Nitakuonyesheni Ishara
zangu. Basi msinihimize." Makusudio ya kauli ya "Ishara" ni ishara za maumbile
zenye kuonyesha kuwepo kwa Mwenyezi Mungu na uweza wake. Na ujuzi wa ilimu za
sayansi utavumbua kwa mujibu wa itavyo nyanyuka akili ya binaadamu. Na hayo ni
kwa mujibu wa miadi ilio wekwa kwa wakati wake. Kila ukifika wakati maalumu
Mwenyezi Mungu hudhihirisha Ishara yake, au huwasahilishia wanaadamu njia za
kuzifikilia Ishara hizo.
39. Lau kuwa hao walio mkufuru
Mwenyezi Mungu wangeli ijua hali yao wakati watapo kuwa hawawezi kuuondoa Moto
kwenye nyuso zao na migongo yao, na wala hawampati wa kuwasaidia kuuondoa,
wasingeli sema wayasemayo.
40. Kiyama hakiwajii kwa
kukitarajia kutokea kwake, bali kitawazukia kwa ghafla tu kiwababaishe, wasiweze
kukirudisha, wala wao hawatapewa muhula wa kutubia na kutafuta udhuru kwa waliyo
kwisha yatenda..
41. Na Mitume wa kabla
yako yaliwapata vile vile ya kufanyiwa kejeli na makafiri katika kaumu zao.
Ikawateremkia hao walio wakataa Mitume na kuwafanyia maskhara adhabu hiyo hiyo
ambayo wao waliifanyia maskhara na kejeli.
42. Ewe Nabii! Waambie: Ni
nani anaye kuhifadhini na nakama zake wakati wa usiku na mchana, na
akakurehemuni na kukuneemesheni? Hapana awezae hayo. Lakini wao wanaipuuza
Qur'ani ambayo ndiyo inawakumbusha ya kuwafaa na kuwalinda na adhabu.
43. Kwani wao wanao miungu
wa kuwalinda na adhabu itokayo kwetu? Hasha! Hiyo miungu yao haiwezi kujilinda
wenyewe, licha kumlinda mwenginewe. Wala hapana yeyote awezae kumlinda yeyote
kati yao karibu yake au pamoja naye pindi tukitaka kumuadhibu na kumteketeza.
44. Sisi hatufanyi haraka
kuwaadhibu hawa kwa ukafiri wao, lakini tunawapururia na kuwastarehesha katika
uhai wa dunia, kama tulivyo wastarehesha baba zao kabla yao, mpaka umri ukawa
mrefu kwao. Je! Wanajitia upofu hawaoni yanao wazunguka wakaona kuwa Sisi
tunaiendea nchi na tukaipunguza ncha zake kwa ushindi wa Waumini? Ni wao ndio
wenye kushinda au Waumini ambao Mwenyezi Mungu amewaahidi kuwasaidia na kuwaunga
mkono? Maoni ya wataalamu juu ya Aya 44: "Je, hawaoni ya kwamba Sisi tunaifikia
ardhi tukiipunguza mipaka yake? Basi je! Hao ni wenye kushinda?": Aya hii ni
katika Aya za miujiza ya kisayansi katika Qur'ani Tukufu. Hii inaonyesha kuwa
dunia si mduwara kaamili. Na wataalamu wa sayansi hawakutamakani kupima masafa
ya dunia baraabara mpaka kiasi ya miaka 250 tu takriban, walipo ingia kikundi
cha mabingwa walio khusika na ilimu ya kupima marefu baina ya daraja mbili za
urefu longitudes. Na hayo kwa pahala mbali mbali duniani. Katika kupima huku
ikadhihiri kuwa nusu ya kati ya dunia kwenye equator inazidi kuliko nusu ya
poles kwa takriban kilomita 21.5. Yaani dunia imepungua katika ncha zake, yaani
katika poles. Na inajuulikana maalumu kuwa sura ya dunia na masafa yake ndio
msingi katika kuchorwa kwa ramani.
45. Ewe Nabii! Sema:
Sikuhadharisheni kwa maneno yanayo tokana nami. Lakini nakuhadharisheni kwa
Wahyi (Ufunuo) unao tokana na Mwenyezi Mungu Mtukufu ulio nijia mimi. Na huo ni
wa Haki na kweli. Lakini hao kwa sababu ya kupuuza kwao kurefu kuipuuza Sauti ya
Haki, Mwenyezi Mungu ameyaziba masikio yao mpaka wakawa kama viziwi. Na kiziwi
hasikii Wito anapo hadharishwa na adhabu!
46. Na kuwa na yakini kuwa
nao wakisibiwa hata na chembe ya adhabu ndogo wanayo ifanyia maskhara, hupiga
kelele kwa khofu wakisema: Ole wetu! Hakika sisi tulikuwa tunajidhulumu nafsi
zetu, na tukiwadhulumu wenginewe, tulipo yakataa tuliyo ambiwa.
47. Na Sisi tunaweka
mizani ya kupimiwa kwa uadilifu Siku ya Kiyama. Basi hadhulumiwi mtu kwa
kupunguziwa wema wake au kuongezewa maovu yake. Hata ikiwa ni kiasi ya uzani wa
chembe ndogo hii tutaileta na tutaihisabu. Na yatosha kuwa ni Sisi ndio wa
kuhisabu. Basi hapana atakaye dhulumiwa kitu. Maoni ya wataalamu juu ya Aya ya
47: "Nasi tutaweka mizani za uadilifu kwa Siku ya Kiyama. Basi nafsi
haitadhulumiwa kitu chochote. Hata ikiwa ni uzito wa chembe ya khardali
tutaileta. Nasi tunatosha kuwa washika hisabu.": Aya hii tukufu inaonyesha kuwa
chembe ya khardali ni hadi ya udogo katika mizani. Imethibitika kwa majaribio ya
sayansi kuwa Kilogram ya chembe za khardali ni chembe 913,000. Kwa hivyo chembe
moja ya khardali ni takriban sehemu moja katika elfu ya gram, yaani ni takriban
sawa na Miligram moja. Na huu ni uzito mdogo kabisa unao juulikana katika mbegu
za mimea mpaka sasa. Kwa hivyo hutumiwa katika kupimiwa vitu vidogo vidogo
kabisa.
48. Na Musa na Haaruni
tuliwapa Taurati ya kupambanua baina ya kweli na uwongo, na halali na haramu. Na
juu ya hivyo hiyo ni nuru ya kuwaongoa watu wafuate njia ya kheri na uwongozi
mwema, na ni kumbusho la kuwafaa wachamngu...
49. Ambao wanamkhofu
Muumba wao Mwenye kumiliki mambo yao yote, juu ya kuwa wako mbali na watu, na
wala hawamwoni mtu. Nao wamo katika khofu ya daima kuikhofu Siku ya Kiyama.
50. Na hii Qur'ani ni
kumbusho, lenye kheri nyingi. Tumekuteremshieni kama tulivyo mteremshia Musa.
Basi yawaje nyinyi muikatae, na hali nyinyi ndio mnao stahiki zaidi kuiamini
kuliko watu wote!
51. Na hakika Sisi
tulikwisha mpa Ibrahim uwongofu na fikra ya kutafuta Haki kwa usafi wa niya
kabla ya Musa na Haaruni. Na Sisi ni Wenye kujua vyema hali yake na fadhila zake
zilizo mfanya astahiki kuchukua Utume.
52. Ewe Nabii! Kumbuka
pale Ibrahim alipo mwambia baba yake na watu wake kuwaonya juu ya masanamu
waliyo kuwa wakishughulikia kuyaabudu: Ni nini haya masanamu ambayo nyinyi
mmeshika kuyaabudu?
53. Wakasema: Tumewakuta
baba zetu wakiyatukuza na wameshika kuyaabudu. Nasi tukawafuata.
54. Yeye akasema: Nyinyi
na baba zenu kabla yenu, ni wazi kuwa nyote mko mbali na Haki.
55. Wakasema: Je! Umetujia
kwa haya uyasemayo na hakika ya kweli unayo iamini, au kwa maneno haya wewe ni
katika wanao fanya pumbao na mchezo tu bila ya kuwa na maana yoyote?
56. Akasema: Hapana
maskhara katika niyasemayo. Bali Mola wenu Mlezi anaye stahiki peke yake
kutukuzwa na kuogopwa na kuabudiwa ndiye aliye ziumba mbingu na ardhi, na
akazileta bila ya kuwapo mfano wake wa kuigiza. Basi ni haki yake Yeye tu peke
yake kuabudiwa. Na mimi kwa haya niyasemayo ni katika wenye hakika ambao hunena
wanayo yashuhudia na wanayajua.
57. Na akasema moyoni
mwake: Naapa kwa Mwenyezi Mungu, nitayafanyia vitimbi haya masanamu yenu
niyavunje pale mtapo ondoka, ili mpate kuona upotovu wenu.
59. Baada ya kwisha ona yaliyo
wapata miungu yao wakasema: Nani aliye itendea haya miungu yetu? Hakika mtu huyu
hapana shaka ni katika walio jidhulumu wenyewe kwa adhabu itayo mpata..
60. Wakasema baadhi yao:
Tumemsikia kijana mmoja akiitaja kwa kuisubu; naye anaitwa Ibrahim.
61. Wakasema wakubwa wao:
Nendeni mkamlete, ahukumiwe mbele ya macho ya watu, na washuhudie aliyo yatenda!
62. Baada ya kwisha
mhudhurisha, wakasema: Ni wewe ulio itenda haya miungu yetu, ewe Ibrahim?
63. Kuwanabihisha upotovu
wao, alisema kwa kuwakejeli: Hili kubwa lao ndilo lililo tenda hayo! Iulizeni
hiyo miungu aliyo yatenda huyu, kama kweli inaweza kujibu suala yenu!
64. Wakazirejea nafsi zao
wakiifikiria ile ibada yao kuabudu vitu visivyo mnufaisha yeyote wala haviwezi
kujitetea wenyewe. Wakayaona makosa yao. Baadhi yao wakasema: Ibrahim si katika
walio dhulumu, bali nyinyi ndio madhaalimu kwa kuabudu vitu visio stahiki
kuabudiwa.
65. Kisha wakarejea tena,
wakaacha uwongofu, wakarudia upotovu. Wakamwambia Ibrahim: Hakika wewe umekwisha
jua kuwa haya masanamu tunayo yaabudu hayasemi kitu. Basi vipi unatutaka
tuyaulize?
66. Ibrahim akasema: Ikiwa
hali yao haya masanamu ni hii, hayawezi kitu, na nyinyi ndio makhusiano yenu nao
ni hivi, basi nyinyi mmekuwa mnaacha kumuabudu Mwenyezi Mungu, na badala yake
mnaabudu vitu visivyo kupeni faida hata chembe mkiviabudu, wala havikudhuruni
kwa lolote mkiviachilia mbali?
67. Aibu yenu! Nyinyi na
miungu yenu mmelaanika! Mnaacha fikra zenu zipotee, na mnapuuza kuzingatia? Bila
ya shaka haya masanamu hayafai kuabudiwa!
68. Wakaambiana wenyewe
kwa wenyewe: Mchomeni moto mpate kuinusuru miungu yenu kwa mateso haya, ikiwa
nyinyi mnataka kufanya kitu cha kuiunusuru miungu yenu.
69. Sisi tukaufanya moto
ule uwe baridi na salama, hauna madhara yoyote, kwa Ibrahim.
70. Wao walitaka
kumuangamiza, lakini Sisi tukamwokoa, na tukawafanya wao ndio watu walio khasiri
mno.
71. Na tukamwokoa yeye na
Luut'i na njama zilizo pangwa, wakaelekea kwenye nchi tuliyo ijaalia kheri
nyingi kwa watu wote, na tukawapeleka huko Manabii wengi.
72. Na tukampa Ibrahim
mtoto Is-haq, na kutokana na Is-haq tukampa Yaaqubu, zaidi kuliko aliyo taka. Na
wote wawili, Is-haq na Yaaqubu tuliwajaalia kuwa ni watu wema.
73. Na tukawafanya ni
Manabii wakiwaendea watu, wakiwaongoa kwenye kheri kwa mujibu wa tulivyo
waamrisha. Na tukawaonyesha vitendo vyema, na kudumisha Sala kama inavyo faa, na
kutoa Zaka. Na wakawa wanatunyenyekea na kutusafia ibada Sisi tu.
74. Luut'i tukampa kauli
ya kukata na madhubuti katika hukumu na ilimu yenye manufaa. Na tukamwokoa
kutokana na mji ambao watu wake wanafanya kitendo cha namna ya peke yake katika
uovu. Hakika hao walikuwa watu walio shikilia kufanya maovu, walio toka kwenye
ut'iifu wa Mwenyezi Mungu na tabia iliyo zowewa.
75. Tukampeleka njia ya
watu wa rehema yetu. Hakika huyo alikuwa miongoni mwa watu wema alio wakusanya
Mwenyezi Mungu katika rehema yake na akawakunjulia msaada wake.
77. Tukamlinda kwa nusura yetu na
vitimbi vya kaumu yake walio zikanusha Ishara zetu zenye kuthibitisha Utume
wake. Hakika hao walikuwa watu wa shari. Basi tukawagharikisha wote!
78. Ewe Nabii! Wataje Daud
na Suleiman walipo toa hukumu katika kesi ya konde, ilio ingiliwa na mbuzi wa
watu mbali usiku na wakala mazao yake. Na Sisi tulikuwa tunaijua hukumu iliyo
khusiana na kesi hiyo. Kisa cha hiyo hukumu: Mbuzi waliingia usiku mmoja katika
konde ya mtu, wasibakishe kitu. Daud akahukumu kuwa wale mbuzi wawe wa mwenye
konde kulipia khasara yake. Suleiman akatoa hukumu nyengine, akasema: Mbuzi wale
wabakie mkononi mwa mwenye konde mpaka itapo mea tena mazao yake, na avumilie
kwa yaliyo mpata. Na baada yake warejesheane.
79. Basi tulimfahamisha
Suleiman hiyo fatwa. Na wote wawili tuliwapa hikima na ilimu ya maisha na mambo
yake. Na tulimfanyia Daud pamoja na milima it'ii na imtakase Mwenyezi Mungu kama
alivyo kuwa anamtakasa yeye Daud na kila lisio kuwa linamwelekea Mwenyezi Mungu.
Na kadhaalika tuliwafanya ndege hivyo hivyo wamsabihi Mwenyezi Mungu pamoja
naye. Na tulifanya hayo kwa uweza wetu usio shindika.
80. Tukamfundisha Daud
kufuma nguo za chuma, ili zikulindeni katika vita vyenu. Basi mshukuruni
Mwenyezi Mungu kwa neema hii aliyo kuneemesheni.
81. Na tulimsahilishia
Suleiman upepo unao vuma kwa nguvu umtumikie, nao huo ulikuwa unakwenda kwa
kufuata amri yake mpaka kwenye nchi tuliyo izidishia kheri yake. Nasi ni wenye
kuyajua yote hayo. Halitupotei kubwa wala dogo.
82. Na tukawafanya
mashetani wamtumikie kwa kuzamia chini baharini kumletea lulu na marijani; na
wakifanya kazi nyenginezo, kama kujenga ngome na majumba ya kifalme. Na Sisi
tulikuwa tukiwaangalia katika kazi zao hizo, basi hapana hata mmoja wao aliye
pata shida, wala hawakuvunja amri ya Suleiman.
83. Ewe Nabii! Mtaje
Ayyubu, pale alipo mwita Mola wake Mlezi, na maradhi yalikwisha mdhoofisha, na
akasema: Ewe Mola wangu Mlezi! Hakika nimesibiwa na madhara na yananiuma! Na
Wewe ni Mbora wa wanao rehemu..
84. Tukamwitikia kwa aliyo
yaomba, tukamwondolea madhara, na tukampa watoto kwa kadri ya waliyo kwisha
kufa. Na tukamwongezea mfano wa wale, kuwa ni rehema iliyo tokana na fadhila
yetu, na pia ni kuwa ni kumbusho kwa wenginewe wanao tuabudu ili wapate nao
kusubiri kama alivyo subiri yeye, na watumai kupata rehema ya Mwenyezi Mungu
kama alivyo tumai yeye.
85. Ewe Nabii! Watajie
watu wako khabari za Ismail, na Idris, na Dhulkifli. Wote hao ni miongoni wanao
subiri wakahimili taklifa na shida.
86. Na tukawajaalia
miongoni mwa watu wa kupata rehema yetu. Hakika hao ni katika waja wetu wema.
87. Ewe Nabii! Taja kisa
cha Yunus, aliye mezwa na samaki..Pale alipoona dhiki kwa vile watu wake walipo
puuza wito wake, naye akawahama akenda mbali nao na huku amewakasirikia.
Akadhani ya kuwa Mwenyezi Mungu amemruhusu kuwahama, na kwamba haitopita hukumu
juu yake. Samaki akammeza, na akaishi katika kiza cha bahari. Akamwita Mola wake
Mlezi kwa kumnyenyekea, na kuungama aliyo kuwa nayo, akasema: Ewe Mola wangu
Mlezi! Hapana wa kuabudiwa kwa haki ila Wewe. Ninakutakasa na kila lisio
kuelekea Wewe. Ninaungama kuwa hakika mimi nilikuwa miongoni mwa walio dhulumu
nafsi zao kwa kutenda yasio kupendeza.
88. Tukamwitikia kwa aliyo
kuwa akiyaomba, na tukamvua na dhiki aliyo kuwa nayo. Na mfano wa hivi ndivyo
tunavyo waokoa Waumini wanao ungama makosa yao, na wakatuomba kwa usafi wa moyo.
89. Na kitaje kisa cha
Zakariya alipo mwita Mola wake Mlezi baada ya kwisha ona uweza wake Subhanahu
kwa alivyo mtia katika nafsi yake matarajio ya rehema yake. Alisema: Ewe Mola
wangu Mlezi! Usiniache mpweke bila ya kuwa na mrithi, na Wewe ndiye Mbora wa
wanao rithi. Kwani Wewe ndiye utakaye baki baada ya kumalizika viumbe vyote.
90. Tukamtimizia matumaini
yake, na tukamwitikia dua yake, na tukamtunukia juu ya ukongwe mwanawe, Yahya,
tukamfanya mkewe tasa aweze kuzaa. Hakika wasafi hao Manabii walikuwa wepesi wa
kutenda kheri tunayo waitaka waitende, na wanatuomba kwa kutumai rehema yetu, na
kuikhofu adhabu yetu. Na walikuwa hawamtukuzi mtu wala hawamwogopi mtu isipo
kuwa Sisi tu.
91. Pamoja na hawa simulia
kisa cha Maryamu aliye ulinda uke wake, nasi tukamfikishia siri katika siri
zetu. Tukamjaalia achukue mimba bila ya mume, na tukamjaalia mwanawe azaliwe
bila ya baba. Akawa yeye na mwanawe dalili iliyo wazi ya uweza wetu kugeuza
sababu na vinavyo sabibishwa. Na hakika Sisi ni waweza wa kila kitu.
92. Hakika mila hii, nayo
ndiyo Uislamu, ndiyo mila iliyo sahihi inayo kupasini kuilinda, kwa kuwa ni mila
moja iliyo shikamana wala haikukhitalifiana baina ya hukumu zake. Basi nanyi
msifarikiene katika mila hii kwa makundi na vyama. Na Mimi ndiye Muumba wenu, na
Mwenye kumiliki mambo yenu yote. Basi niabuduni Mimi tu, wala msinishirikishe na
mwengine.
93. Na juu ya kuwepo
uwongozi huu aghlabu ya watu wamegawanyika kwa mujibu wa matamanio yao,
wakafanya mambo yao ya Dini mapande mapande, wakawa makundi mbali mbali. Na kila
kundi litaturejea Sisi tulihisabie vitendo vyake.
94. Basi mwenye kutenda
vitendo vyake vyema, naye ni mwenye kumuamini Mwenyezi Mungu na Dini yake aliyo
iridhia, hatopunguziwa kitu katika juhudi yake. Bali atalipwa malipo kaamili. Na
Sisi ni wenye kuiandika hiyo juhudi yake. Basi hakitopotea kitu.
95. Na haitakuwa kwa watu
wa mji tulio uteketeza kwa sababu ya dhulma yao kwamba hawatarejea kwetu Siku ya
Kiyama, bali hapana budi kuwa watarejea na tutawahisabia vitendo vyao viovu.
96. Mpaka itapo funguliwa
milango ya shari na ufisadi, wakaingia wana wa Juju na Maajuju wakikimbizana
kuteremka milimani na majiani kwa kufanya vitendo vya fujo na rabsha.
97. Na ikakaribia miadi
iliyo haina budi kutimizwa, nayo ni Siku ya Kiyama, wakawa wale walio kufuru
wanakutikana wakikodoa macho yao kwa wingi wa kitisho, wakipiga makelele kusema:
Kitisho gani hichi cha kutuangamiza! Hakika sisi tulighafilika na Siku hii. Bali
tulikuwa ni wenye kujidhulumu nafsi zetu kwa ukafiri na inda.
98. Wataambiwa makafiri
hawa: Nyinyi na hiyo miungu mliyo kuwa mkiiabudu badala ya Mwenyezi Mungu ni
kuni za Moto wa Jahannamu. Nyinyi mtaingia humo muadhibiwe!
99. Lau kama hawa mlio
waabudu badala ya Mwenyezi Mungu ni miungu inayo stahiki kuabudiwa, wasingeli
ingia nanyi humo. Na nyote, wenye kuabudu na kuabudiwa, mtabaki Motoni, wala
hamtatoka.
100. Humo watatoa pumzi
zitokazo vifuani kwa sauti kama ya mwenye kukabwa, kwa dhiki watayo pata, na
hawatasikia la kuwafurahisha.
101. Hakika wale tulio
wakubalia kwa kufuata kwao Haki na vitendo vya kheri, na tukawaahidi malipo
mema, hao watawekwa mbali kabisa na Jahannamu na adhabu yake.
102. Hawatasikia sauti ya
Moto wake unavyo vuma. Nao huko watapata kila ambacho nafsi inatamani, daima
milele.
103. Hawato huzunishwa na
Kitisho Kikubwa kinacho wafazaisha makafiri. Na Malaika watawapokea kwa
kuwapongeza kwa kusema: Hii ndiyo Siku yenu ya neema aliyo kuahidini Mola wenu
Mlezi!
104. Siku tutapo zikunja
mbingu kama zinavyo kunjwa karatasi katika kitabu. Na tutawarejeza viumbe kwa
ajili ya hisabu na malipo. Wala hatushindwi kuwarejeza, kwani tuliwaumba mara ya
kwanza. Na kama tulivyo waanza tutawarejeza. Ahadi yetu kwa hayo ni ahadi ya
kweli. Daima Sisi tunatenda tunayo yaahidi.
105. Na tulikwisha andika
katika Zaburi - nacho ni Kitabu cha Daud baada ya Taurati - kwamba nchi
watairithi waja wangu walio wema wapate kuitengeza, na kusahilisha njia za
maisha bora humo. ("Bali wenye upole watairithi nchi"..Zaburi 37.11 "Wenye haki
watairithi nchi, nao watakaa humo milele".. Zaburi 37.29)
106. Hakika katika haya
tuliyo yataja, khabari za Manabii pamoja na kaumu zao, na khabari za Pepo na
Moto, yanatosha kuwakumbusha na kuwafanya wazingatie watu walio tayari kumuabudu
Mwenyezi Mungu pekee na hawasalitiki na mapambo ya dunia.
107. Na hatukukutuma, ewe
Nabii, ila uwe ni Rehema kwa walimwengu wote.
108. Ewe Nabii! Sema:
Hakika kiini cha Wahyi aliyo nipa Mwenyezi Mungu ni kwamba hakika nyinyi hamna
Mungu isipo kuwa Yeye. Na yote yaliyo bakia niliyo funuliwa yanafuata asili hii.
Ikiwa mambo ni hivyo, basi inakuwajibikieni mjisalimishe na mnyenyekee kwa
Mwenyezi Mungu peke yake.
109. Wakito ujali wito
wako, basi waambie: Nimekufunzeni yote aliyo niamrisha Mola wangu Mlezi; na kwa
hivyo tumekuwa sawa kwa kuyajua hayo. Wala mimi sijui hayo ya kufufuliwa na
kuhisabiwa mliyo ahidiwa, yatakuwa karibu au mbali.
110. Hakika Mwenyezi
Mungu anayajua yote yasemwayo, mnayo yadhihirisha na mnayo yaficha.
111. Na sijui pengine
huko kupewa muhula na kuakhirishiwa adhabu nyinyi ndio Mwenyezi Mungu
anakufanyieni mtihani tu, na kukustarehesheni kwa ladha za maisha mpaka alipo
kadiria Mwenyezi Mungu kukuhisabieni kwa hikima yake.
112. Ewe Nabii! Sema: Ewe
Mola Mlezi! Tuhukumu baina yangu na hawa nilio wafikishia Wahyi kwa uadilifu ili
wasiwe sawa Waumini na makafiri. Na Mola wetu Mlezi Mwenye kuneemesha kwa neema
kubwa, Mwenye kustahiki kuhimidiwa na kushukuriwa, ndiye wa kutakiwa msaada
kuvunja uzushi mnao zua, enyi makafiri.
Copyright � 22 August 1997, Sheikh
Ali Muhsin Al Barwani