image

Kwanza yanipasa nimshukuru Mwenyezi Mungu Jalali, asiye kuwa na mithali, kwa neema zake za kila hali na kila mahali, hata nikaweza, mimi mja mpungufu, kutimiza kazi hii tukufu, ya kuutarjimu Msahafu pamoja na Tafsiri inayo itwa, "AL-MUNTAKHAB FI TAFSIRI 'L-QUR'AN" kwa lugha ya Kiswahili. Kwa kazi hii nawashukuru wote walio simama nami kutekeleza waajibu, ambao mimi ungeli nishinda peke yangu. Mtaalamu mmoja wa Kizungu alisema: "Haidhurishi kitu mwaandishi akiwa hana ufundi, maadamu anao masahibu wa dhati ambao anawasiliana nao vizuri." Mimi, Alhamdulillahi, nilipata wenzangu wa dhati wa kunisaidia katika kazi yangu hii tangu mwanzo wake mpaka kuishia kwake kwa kunisahihishia makosa katika muswadda.


Lakini nasikitika katika watatu wa kunisahihishia makosa, mmoja wao, Dk. Ahmed Murshid, ambaye ni Rais wa Idara ya Lugha katika Chuo Kikuu cha Ummul Quraa (Makka-T'aif) haikumkinika kutimiza kazi yake kwa umbali wa mawasiliano baina ya nilipo mimi na alipo yeye. Juu ya hivyo msaada niliyo upata kwake na nasaha zake si haba. Nuksani ni yangu.


Wa pili aliye nisaidia kusahihisha makosa ni Dk. Jaafar Tijani aliye kuwa ustaadhi wa lugha katika Vyuo Vikuu vya Dar es salaam na Nairobi na sasa anasomesha Kiingereza katika Maahad al Islami ya Maskati. Yeye ameupitia Msahafu mzima, na maoni yake yamenifaa sana.


Mtaalamu wa tatu aliye nichungulia na kunisahishishia muswadda wangu kwa utulivu mno ni Mwanachuoni Sheikh Hamoud bin Ali Al Harthy. Yeye si kama amesahihisha lugha tu, bali, kwa kutumia ilimu ya Tafsiri aliyo jaaliwa kuwa nayo kwa vizuri, ameyapa uzani mwingine masahihisho yake. Kwa hakika kusahihisha kwake kumekuwa kwangu ni darsa kaamili, hata mwishoe sikuweza ila kumwambia:
"Lau kuwa si Hamoud angeliteketea Ali", kama alivyo sema Sayyidna Omar R.A. kwa mnasaba wa Sayyidna Ali R.A.


Sehemu kubwa kabisa ya upungufu wa juhudi zangu imeondolewa na kazi waliyo ifanya Sheikh Hamoud na Dr. Jaafar. Kama dosari iliyo bakia, na najua imebakia nyingi, inatokana ama na ujinga wangu, au ukaidi wangu kutojali mashauri ya watu wanao jua zaidi kuliko mimi.


Wa mwisho kumtaja, wala si wa mwisho wa kunifadhili, siwachi kumshukuru Sheikh Said Abdalla Seif Al-Hatimy aliye upitia muswadda mara ya mwisho naye hali ni mgonjwa. Kaweza kunizindua mwahala kadhaa wa kadhaa.. Namshukuru yeye na namshukuru Mufti wa Oman, Sheikh Ahmed Al-Khalili, aliye chukua taklifu kumtafuta mchunguzi wa kutosha kwa kazi hii muhimu.


Ijapo kuwa umuhimu wa kazi yangu ni kutarjimu yaliyo andikwa katika hii Tafsiri inayo itwa Al-Muntakhab, ilinipasa kuzipitia Tafsiri kadhaa wa kadhaa nyenginezo ili nipate kufahamu vilivyo makusudio ya hayo niliyo kuwa ninayatarjimu. Miongoni mwa hizo ni Tafsiri za Kiarabu ya Jalalein, ya Ibn Kathir, ya Zamakhshari, ya Baidhawi, ya Shaltout (Juzuu kumi), ya Qurt'uby, "Attafsir Alkabir" ya Imam Arrazi, "Haymayanu Zzaad" ya Muhammad bin Yusuf, na mwanzo wa "Jawaahiru Ttafsir" ya Sheikh Ahmed Al-Khalili, Mufti wa Oman, na "Fi Dhilali Al-Qur'an" ya Sayyid Qut'b. Ama za Kiswahili  ni za marehemu Sheikh Al-Amin bin Aly Mazrui (baadhi ya Juzuu), na Sheikh Abdulla Saleh Al-Farsy. Tena  ya Sheikh Abdulla Yusuf Ali, na ya Muhammad Asad, na ya Muhammad Pickthall (za Kiingereza).


Sheikh Hamoud bin Ali Al Harthy ameongezea katika upungufu  wangu kwa Tafsiri nyengine ambazo sinazo. Miongoni mwa hizo ni Tafsiri ya Almaraghy na Tafsiri ya Manara ambazo yeye amezirejea mara nyingi katika kusahihisha muswadda wa maandishi haya. Kadhaalika yamenifaa makamusi kadhaa wa kadhaa, na katika hayo ni khasa makamusi yaliyo khusika na maneno ya Qur'ani kama ya Sheikh Makhluf aliye kuwa Mufti wa Misri, na "Mu'jamu Alfaadhi Al-Qur'ani Alkarim" ya Majmau' Al lughati Al A'rabiya.


Mbali ya hao wanazuoni walio upitia muswadda wangu, wapo wengi walio nisaidia kwa njia mbali mbali. Wanangu mara kadhaa wa kadhaa nilikuwa nikiwauliza kila ninapo kwama katika kutarjimu.  Na wapo walio nisaidia kwa upande wa kifundi, kama mwanangu Muhammad Ali, aliye nipatia  Computer; na yeye pamoja na wenziwe, Suleiman Shahbal na Walid Muhammad Badr wakanifundisha kutumia hiyo Computer ambayo ndiyo iliyo niwezesha kufanya kazi hii kwa wepesi. Na pia namshukuru kijana mwema wa Kisham, Basim Ist'wany, ambaye alipo jua nini ninalo lifanya, alijitolea kunisaidia bure juu ya kuwa kutengeneza Computer ndiyo kazi yake ya kumpatia maisha. Pia siwezi ila nimshukuru Bw. Abdulrahman Salim Basadiq, aliye nitunukia "Printer" mpya ghali kwa ajili ya kazi zangu.  Mwenyezi Mungu awajaze kheri wote nilio wataja na nisio wataja.


Katika walio nishajiisha kikweli katika kazi hii ni Dr Ezzeddin Ibrahim, Mshauri wa Mtukufu Rais Sheikh Zayid bin Sultan Al Nahyan, Rais wa U.A.E.  Yeye anastahiki shukrani zangu za dhati.
Ama hima ya Dr Mustafa Momen, sahibu yangu wa miaka mingi, haiwezi kusahaulika kabisa kwa kuchukua kwake hima ya kunihimiza mimi kuendelea nayo kazi hii, na khatimaye yeye akaifikisha kwenye nadhari ya Al Imam Al Akbar Sheikh Jaad al Haq Ali Jaad Al Haq, Sheikh wa Al Azhar. Mwenyezi Mungu ndiye Mlipaji. Atawalipa Mashekhe hawa watukufu kwa juhudi yao kulifikisha neno la Mwenyezi Mungu kwa wasemao Kiswahili kwa kuwaletea Tafsiri ya mwanzo iliyo kamilika katika lugha ya Kiswahili kwa njia iliyo nyepesi, na isiyo na mapendeleo ya kimadhehebu, na yenye kuelezwa kwa kuambatana na ilimu za sayansi za kisasa kila inapo hitajika.


Kwa wazazi wangu, na mashekhe zangu, na walimu wangu, sina ila shukra za daima, kwani wao ndio walio nilea na kunifunza, hata nikajua nilicho jua. Wao hao na mwenzangu wa maisha, marehemu mke wangu, nawaombea maghfira na rehema kwa Mwenyezi Mungu. Ilikuwa hamu yangu walau mke wangu marehemu awahi kushirikiana nami katika furaha nilipo maliza kuandika Tarjuma hii, na awahi kuuona Msahafu huu ulio tarjumiwa kwa njia hii umepigwa chapa. Lakini yote ni ya Mwenyezi Mungu.


Katika Utangulizi wa wenye kuifasiri hii Qur'ani imefahamika kuwa katika Kiarabu "Tafsiri" ni "maelezo ya maana ya Qur'ani". Kazi hiyo siyo niliyo ifanya mimi, wala mimi sina uwezo wa kufanya hayo. Nililo lifanya ni kugeuza lugha ya Kiarabu kwa Kiswahili, kwa kufuata uwongozi wa wataalamu walio kwisha ifasiri Qur'ani kwa kuieleza kwa hicho hicho Kiarabu. Kazi yangu ni "Kutarjimu tafsiri", yaani kugeuza maana ya maneno kutokana na Kiarabu nikayaingiza katika Kiswahili, kama afanyavyo mkalimani katika mahkama.


Basi hii ni Tarjuma ya Kiswahili ya Tafsiri ya Qur'ani iliyo fasiriwa na wanazuoni wakubwa wa Misri walio jikusanya katika kikundi kinacho itwa  Halmashauri ya Qur'ani na Sunna chini ya uangalizi wa Baraza Kuu la Mambo ya Kiislamu. Tafsiri hiyo inaitwa: AL-MUNTAKHAB FI TAFSIRI 'L-QUR'AN. Maana yake ni "YALIYO PEMBULIWA KATIKA TAFSIRI YA QUR'ANI". Qur'ani Tukufu imefasiriwa, au imeelezwa, na watu wengi sana. Tafsiri zake ni kwa mamia na mamia. Lakini zote hizo ni za watu binafsi. Kila mojapo ni maoni ya mwanachuoni fulani. Hii Al-Muntakhab, kwa mara ya kwanza ni juhudi ya kikundi cha wanazuoni walio pembua kutoka Tafsiri mbali mbali, na wakakhiari walio yaona ni muwafaka ndio wakayakubali. Kwa hivyo kama ilivyo mkinika Tafsiri hii ya AL-MUNTAKHAB imejaribu kuepuka khitilafu za kimadhehebu katika mambo ya Fiqhi na Itikadi. Kwa sababu hii na kwa kuwa imejaribu kueleza mambo ambayo yamekwisha hakikishwa na ilimu za sayansi, ndio nikavutika nayo mimi na nikataka kuiandika kwa lugha ya Kiswahili,  ili Waswahili wenzangu wasio jua Kiarabu wapate nao kuifahamu na iwaongoze kama ilivyo niongoza mimi. Kwa kuwa urefu wake ni wa wasitani, wa kutosha kufahamisha, na si wa kuchosha, basi nimeona ni mnasaba sana kwa wasomaji wa Kiswahili ambao wamekwisha onjeshwa utamu wa Qur'ani kwa tafsiri za Sheikh Al-amin bin Aly Mazrui na Sheikh Abdulla Saleh Al-Farsy au walio isikia ikisomwa tafsiri ya Jalaleini misikitini.

LUGHA:

Mtaona kuwa mimi humu sikutumia kuendeleza maandishi yangu kwa mujibu wa mtindo unao juulikana kuwa ni wa "Standard Swahili". Mimi nimejitahidi kuandika kama ninavyo sema mwenyewe, na khasa kama nilivyo kuwa nawasikia wazazi wangu wakisema nami. Wao na wenzao wao nawachukulia kuwa ni mfano mwema kwa kusema Kiswahili kwa kuwa hawakuharibiwa lugha yao kwa maskuli tuliko pelekwa sisi.
Kiswahili kabla hajaja mkoloni kutulazimisha tutumie maandishi yake kilikuwa kinaandikwa kwa harufi za Kiarabu, kama kinavyo andikwa Kiurdu, na Kifursi, na Kimalay, na Kiturki kabla Kamal Ataturki hajaingiwa na shauku ya kutaka kuiga Uzungu katika kila kitu.


Katika kitabu "The Swahili: Idiom and Identity" Mabwana Alamin M. Mazrui na Ibrahim Noor Shariff wametaja vipi katika 1931 marehemu Sheikh Al-Amin bin Aly Mazrui alivyo hadharisha khatari ya kuacha kutumia maandishi ya Kiarabu katika lugha ya Kiswahili, na akaonya kuwa haya lazima yatakuja kuathiri vibaya matamshi ya vizazi vijavyo. Akitumia gazeti lake la Al-Islah, aliwahimu umma wake wakipige pande hicho alicho kiita "Kiswahili cha skuli".

Kazi tuliyo nayo sisi hii leo ina ncha mbili:
(1) Kufundisha watu kutumia harufi za Kiarabu kuandikia Kiswahili kama walivyo kuwa wakiandika wote hapo zamani kabla ya kuja wakoloni. Hapana jambo jepesi kama hilo. Kwa majaribio yangu nimeweza  kuwafundisha vijana kadhaa wa kadhaa wa Kitanzania kusoma na kuandika kwa harufi za Kiarabu  kwa muda wa siku chache tu na wakaweza kuisoma Qur'ani popote nilipo wafungulia. Nimetunga kijitabu juu ya hayo nilicho kiita: "Jifunze Kusoma na Kuandika Kiarabu kwa Wiki Tatu", ambacho kimepigwa chapa. Yeyote anaweza kujifunza mwenyewe kwa kufuata uwongozi uliomo katika kijitabu hicho, badala ya mtu kupitisha mwaka au miaka chuoni, na pengine aondokee patupu kwa kufunzwa kwa namna ya kizamani.
(2) Ncha ya pili ni kuzitumia hizi hizi harufi za Kizungu, lakini iwafikiwe baadhi yake zitengenezwe kwa kufuata matamshi fas'ihi ya Kiswahili. Kiswahili si lugha ya pekee inayo tumia hizi harufi za Kizungu, zinazo itwa za Kirumi. Lugha ya Kiingereza ni mfano mzuri kabisa wa lugha inayo tamkwa kwa namna isiyo kuwa ile inavyo andikwa.
Kusema kuwa Kiswahili kilegezwe, na kikamuliwe utamu wake wote, kwa sababu wageni wa lugha wanaona dhiki kutamka baadhi ya maneno yake, ni hadi ya kutudharau. Imekuwa kama lugha hii haina mwenyewe wa kuitetea. Mbona hapana aliye thubutu kukidharau Kiarabu, au Kiingereza, au Kifaransa, au hata Kizulu, Kixhosa au Kitsandawi au Kinyamwezi? Kila lugha ina hishimiwa usemi wake, na mbinu zake, na matamshi yake, wageni wakipenda wasipende.

Mimi, basi, katika maandishi haya nimejaribu kuipa sura fikra yangu ya kufanya niwezavyo kwa wepesi bila ya matatizo, sana kwa kutumia ' kuonyesha kuwa harufi fulani itamkwe kama inavyo stahiki kutamkwa.
Kadhaalika katika uendelezi wa maneno ambayo kwa hicho Kiswahili cha Skuli hufanywa maneno mbali mbali yakaungwa pamoja, na ilhali ni maneno mbali, mimi nimeyafanya ni maneno mbali. Kwa mfano "aliyekuja". Sifahamu kwa nini haya maneno mawili, ambayo ukiyaandika kwa harufi za Kiarabu ni mawili, na ukiyafasiri kwa Kiarabu au kwa Kiingereza pia ni zaidi ya neno moja, tuyaandike hivyo, na tusiandike hivi: "aliye kuja"?
Mtaona katika maandishi haya nimejaribu nisiongeze langu ila katika maelezo nilipo ona inahitaji kwa ajili ya kuzidi kuwafahamisha wasomaji wa Kiswahili. Na hapo yale yangu nimeyatia baina ya mipinde miwili, kama hivi: (...).
Nitashukuru sana kupata maoni ya wasomaji, khasa ya kunionyesha nilipo kosa, ili katika nakla zijazo baadaye tupate kusahihisha makosa yetu.
Wassalamu Alaykum.

        Ali Muhsin Barwani
        S.L.P. 10679
        Dubai
        U.A.E.
        26 Mfungo Tano 1413
        25 Agosti 1992