1. Mwenyezi Mungu Mtukufu ameanza Sura hii kwa harufi, nazo ni T'a na Ha, ili kupingana na makafiri wanao kanya, na kuwa kama ishara ya kwamba hii Qur'ani imeundwa kwa hizi hizi harufi mnazo zitumia katika kusema kwenu. Na juu ya hivyo nyinyi mmeajizika (yaani mmeshindwa, ndio likatokea hilo neno "Muujiza") kuleta Sura walau ndogo, au baadhi ya Aya zilizo mfano wa Qur'ani.
 

2. Ewe Mtume! Sisi hatukukufunulia wewe Qur'ani hii iwe ni sababu ya kukupa dhiki ya nafsi yako kwa kuwasikitikia hao wapuuzi kukupuuza wewe.
 

3. Lakini tumekuteremshia iwe ni kumbusho kwa mwenye kumkhofu Mwenyezi Mungu apate kumt'ii.
 

4. Hii Qur'ani umeteremshiwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, Mwenye uwezo, Muumba ardhi na mbingu zilio nyanyuka juu.
 

5. Mtukufu wa rehema, ametawala sawa sawa juu ya Ufalme wake.
 

6. Ni wake Yeye tu, Subhanahu, ufalme wa mbinguni na viliomo humo, na wa ardhi na viliomo juu yake, na ufalme wa vilio baina ya hivyo, na maadeni na kheri nyenginezo zilizo fichikana chini ya ardhi.
 

7. Na kama uwezo wa Mwenyezi Mungu ulivyo kusanya kila kitu, kadhaalika ujuzi wake pia umekusanya kila kitu. Na ewe mtu, ukinyanyua sauti kwa kusema, basi  Mwenyezi Mungu anajua. Kwani Yeye anajua unapo sema na mtu, na anajua unapo zungumza na nafsi yako.
 

8. Yeye ndiye Mwenyezi Mungu, Mungu wa Pekee, Mwenye kustahiki kuabudiwa peke yake. Kwani Yeye amesifika kwa sifa za ukamilifu, naye ndiye Mwenye bora ya sifa.
 

9. Ewe Nabii! Unajua khabari za Musa na Firauni?
 

10. Pale Musa alipo uona moto katika safari yake ya usiku kutoka Madyana kwendea Misri, akamwambia mkewe na walio kuwa naye: Ngojeni hapa! Mimi nimeuona moto ule; natumai nitakupatieni kijinga  cha moto kutoka kule mpate kuashia moto, au huko nitapata mtu wa kuniongoza njia.
 

11. Alipo fika huko, akasikia sauti yenye kutoka juu inamwita: Ewe Musa!
 

12. Hakika Mimi ni Mwenyezi Mungu, Mola wako Mlezi! Basi vua viatu vyako  kwa hishima ya pahala hapa; kwani wewe upo katika bonde safi lenye baraka, nalo ni T'uwa.
 

13. Na Mimi Mwenyezi Mungu nimekuteuwa wewe kwa kukupa Utume. Basi sikiliza haya ninayo kufunulia uyajue na ukawafikishie watu wako.
 

14. Hakika Mimi ni Mwenyezi Mungu, Mungu wa Pekee, hapana wa kuabudiwa kwa haki isipo kuwa Mimi. Basi niamini Mimi, na niabudu Mimi, na dumu daima katika kuishika Sala ili uwe daima unanikumbuka.
 

15. Hakika Saa ndiyo miadi ya kukutana nami; nami miadi hiyo nimeificha kwa waja wangu, na nimewaonyesha ishara zake. Hiyo Saa itakuja bila ya shaka yoyote, na kila nafsi itahisabiwa kwa iliyo tenda.
 

16. Ewe Musa! Asikuachishe kuiamini Saa na kujitayarisha kwa ajili yake yule ambaye haisaidiki, na akafuata pumbao lake akahiliki.
 

17. Na nini hicho ulicho kamata kwa mkono wako wa kulia?
 

18. Musa akajibu: Hii ni fimbo yangu, najikongojea ninapo kwenda, na ninachungia kondoo na mbuzi wangu, na inanifaa kwa manufaa mengine, kama kuwatetea hayawani wangu.
 

19. Mwenyezi Mungu Subhanahu  akamwambia Musa: Itupe hiyo fimbo chini kwenye ardhi.
 

20. Musa akaitupa; akashtuka kuiona imegeuka nyoka anakwenda!
 

21. Akamwogopa. Mwenyezi Mungu akamtuza kwa kumwambia: Mwokote wala usikhofu, kwani tutamrejesha hali yake kama ya kwanza.
 

22. Na ingiza mkono wako ndani ya mfuko wa nguo ukiambatisha na ubavu wako, utatoka mweupe safi bila ya maradhi. Na huo tumekufanyia ni muujiza wa pili wa Utume wako...
 

23. Ili tukuonyeshe baadhi ya miujiza yetu mikubwa iwe ni dalili ya ukweli wa Utume.
 

24. Nenda kwa Firauni umtake amuamini Mwenyezi Mungu Mmoja wa Pekee. Kwani yeye Firauni amepindukia mipaka kwa ukafiri wake na ujeuri wake.
 

25. Musa akamnyenyekea Mola wake Mlezi kwa kumwomba: Nikunjulie kifua changu, iniondoke ghadhabu, nitimize ujumbe wa Mola wangu Mlezi.
 

26. Na unisahilishie kazi yangu ili nipate kutimiza waajibu wangu.
 

27. Na likate fundo la ulimi wangu, nibainishe maneno,
 

28. Ili watu wafahamu vyema niyasemayo.
 

29. Na nijaalie mtu wa kuniunga mkono katika watu wangu,
 

30. Naye ni ndugu yangu Harun.
 

31. Anizidishe nguvu zangu.
 

32. Na umshirikishe nami katika kubeba mizigo ya ujumbe na kuifikisha.
 

33. Ili tukithirishe kukutakasa na yasiyo kuwa laiki yako,
 

34. Na tuyakariri majina yako mazuri kwa wingi.
 

35.   Ewe  Mola  wetu  Mlezi!  Hakika  Wewe  daima  unatuangalia  sisi, na unayashughulikia mambo yetu...
 

36. Mwenyezi Mungu akamwita Mtume wake, Musa, kwa kusema: Nimekwisha kukubalia uliyo yaomba, na hii ni zawadi tulio kutunukia wewe kwa hisani.
 

37. Na Sisi tumewahi zamani kukufadhili wewe kwa hisani bila ya kuomba.
 

38. Tulipo mwongoza mama yako kwa uwongozi wenye nafuu katika maisha yako.
 

39. Tulimuamrisha akuweke, na hali wewe ni mtoto mchanga wa kunyonya, katika kisanduku, na kisha hicho kisanduku akitie katika mto, ili usije kuuliwa na Firauni, pale alipo kuwa anawauwa watoto wote wanaume wa  Banu Israili. Tukayafanya maji ya mto yachukue kisanduku kile mpaka ufukweni. Kwa mujibu wa mipango yetu Firauni, adui yangu na wako, akakichukua kile kisanduku. Nami nikakupa mapenzi ya rehema na ulinzi, ukapendwa na kila aliye kuona. Ukapata malezi mazuri yaliyo bora chini ya ulinzi wangu.
 

40. Ewe Musa! Jua ya kwamba zamani Sisi tulikwisha kukufanyia hisani pale dada yako alipo kuwa anakwenda akiangalia hali yako ulipo kuwa katika jumba la Firauni, na akawaona wanakutafutia mtu wa kukunyonyesha. Ni yeye aliye waongoza kwa mama yako, nasi tukakurejesha kwake apate kufurahi kukuona uhai na umerejea kwake, na asite huzuni na kilio. Na ulipo kua, na ukamuuwa mtu katika kaumu ya Firauni bila ya kukusudia, tukakuvua kutokana na dhiki iliyo kupata, na tukakusalimisha na shari yao. Ukenda mpaka Madyana na huko ukakaa miaka kadhaa wa kadhaa, kisha ukatoka Madyana ukarejea kwa muda tulio kukadiria kwa ujumbe wako..
 

41. Na nikakuteua kukupa Wahyi (Ufunuo) na kubeba Utume wangu.
 

42. Nenda, wewe na nduguyo, nanyi mkisaidiwa na miujiza yangu yenye kuashiria Unabii na Utume, wala msidhoofike katika kutimiza Ujumbe wangu, wala msighafilike kunikumbuka na kuniomba msaada.
 

43. Nenda pamoja na duguyo Harun kwa Firauni. Hakika huyo amepindukia mipaka katika ukafiri wake na jeuri zake.
 

44. Mtakeni kwa upole na ulaini aniamini Mimi  kwa kutaraji asaa akakumbuka Imani aliyo isahau, na akaogopa matokeo ya ukafiri wake na ujeuri wake.
 

45. Musa na Harun wakanyenyekea kwa Mwenyezi Mungu, wakasema: Ewe Mola wetu Mlezi! Hakika sisi tunaogopa huyu Firauni asituvamie kwa madhara, na akapindukia mpaka katika uovu.
 

46. Mwenyezi Mungu akawapoza kwa kusema: Msimkhofu Firauni; kwani Mimi ni pamoja nanyi kukuangalieni na kukulindeni, nayasikia ayasemayo, na nayaona ayatendayo. Sitomwachia kukudhuruni.
 

47. Nendeni kwa Firauni, na mwambieni: Hakika sisi ni Mitume tulio tumwa kwako na Mola wako Mlezi. Tumekuja kukutaka umuamini Yeye, na uwaache Wana wa Israili watoke utumwani na adhabuni. Na sisi tumekuletea muujiza kutokana na Mwenyezi Mungu kuwa ni ushahidi wa ukweli wa haya tunayo kuitia, na mwenye kuufuata uwongofu atasalimika na adhabu  ya Mwenyezi Mungu na kughadhibika kwake.
 

48. Na hakika Mwenyezi Mungu ametufunulia sisi kuwa adhabu yake kali itamshukia anaye tukadhibisha, na akapuuza wito wetu.
 

49. Firauni kwa ujeuri wake na ujabari wake akasema: Ewe Musa! Ni nani huyo Mola wenu Mlezi?
 

50. Musa akamjibu: Mola wetu Mlezi ni yule aliye kipa neema ya umbo kila kilicho umbwa, akakiumba kwa sura aliyo ipenda Yeye Subhanahu, na akakielekeza kwa alivyo kiumbia.
 "Akasema: Mola wetu Mlezi ni yule aliye kipa kila kitu umbo lake, kisha akakiongoa." Mwenyezi Mungu Subhanahu amekijaalia kila kiumbe kina sifa zake makhsusi za kutekeleza kazi yake kilicho umbiwa nacho katika maisha, kama alivyo pewa hidaya mwanaadamu.
 

51. Firauni akasema: Je, nini hali ya karne za zamani, na yaliyo pitikana huko?
 

52. Musa akasema: Ujuzi wa karne hizo uko kwa Mola wangu Mlezi peke yake. Hayo yamedhibitiwa katika madaftari ya vitendo vyao. Hapana kitendo kinacho mpotea asikijue, wala Yeye hasahau.
 

53. Yeye huyo ndiye Mungu Mwenye kuwafadhili waja wake kwa kuwaumba na kuwalinda. Amekutengenezeeni ardhi, akaikunjua kwa uwezo wake, na akakupasulieni njia mnazo pitia, na akakuteremshieni mvua zinazo leta mito, na Yeye Subhanahu akatoa namna mbali mbali za mimea, inayo khitalifiana kwa rangi, na utamu, na manufaa. Mingine myeupe, mingine myeusi, myengine mitamu na mingine michungu..
 

54. Naye Subhanahu amewaelekeza waja wake wanufaike kwa mimea aliyo watolea, kwa kula na kulishia mifugo yao na kama hayo. Na akataja kuwa katika kuumba huku, na kuanzisha huku, na kutumia huku, ni dalili zilizo wazi za kumwongoa mwenye akili afikie Imani ya kumuamini Mwenyezi Mungu na kuamini Mitume wake.
 

55. Na kutokana na udongo wa ardhi hii ndio Mwenyezi Mungu amemuumba Adam na dhuriya zake. Na humo ndio anawarudisha baada ya kufa kwa ajili ya kusitiri miili yao. Na kutoka humo atawatoa tena  kuwafufua na kuwalipa kwa waliyo yatenda.
 

56. Na hakika Sisi kwa kupitia kwa Musa tulimwonyesha Firauni miujiza ya dhahiri ya kuunga mkono Ujumbe wa Musa na ukweli wake kwa yote aliyo simulia kutokana na Mwenyezi Mungu na athari ya uwezo wake. Juu ya hayo Firauni alishikilia ukafiri wake, akayakadhibisha yote hayo, na akakataa kuyaamini.
 

57. Firauni akamwambia Musa: Je, umetujia upate kututoa katika nchi yetu ipate kuwa mikononi mwa watu wako kwa uchawi wako ulio ulia watu?
 

58. Basi sisi tutauvunja huo uchawi wako. Weka miadi baina yetu na wewe, tukutane, wala tusikhitalifiane.
 

59. Musa akawajibu: Miadi yetu ni siku ya Idi yenu mnapo jipamba, na watu wakusanyike kabla ya adhuhuri siku hiyo, waone yatayo kuwa baina yetu na nyinyi.
 

60. Firauni akaondoka na akayashughulikia mambo mwenyewe. Akakusanya mipango yake, na wakuu wa wachawi, na zana za uchawi. Kisha akahudhuria na yote hayo kwa mujibu wa miadi.
 

61. Musa akawaambia kuwahadharisha maangamizo ya Mwenyezi Mungu na adhabu yake, na akawakataza wasizue uwongo, kwa kumdaia ungu Firauni, na kuwakadhibisha Mitume wa Mwenyezi Mungu, na kuikataa miujiza. Na akawatisha kwamba Mwenyezi Mungu atawapatiliza kwa adhabu wakiendelea na hayo, na akatilia mkazo sana khasara ya mwenye kumzulia uwongo Mwenyezi Mungu.
 

62. Wakatishika na maonyo ya Musa, wakaingia kusemezana wao kwa kwao wakivutana, na kila mmoja akitoa maoni yake juu ya aliyo yasema Musa.
 

63. Wakawafikiana kwamba Musa na Harun ni wachawi ambao wanafanya hila kutaka kuwatoa katika nchi yao, kwa kuwapokonya madaraka, yatoke mikononi mwao. Na hayo ni kwa uchawi, ili Wana wa Israili wapate ushindi. Na wawaharibie watu wa Firauni imani yao wanayo iona kuwa ni nzuri!
 

64. Basi fanyeni njama zenu muwafikiane kitu kimoja cha kumfanyia Musa, kisha mkusanye wateuliwa, ili watazamaji waingiwe na kitisho kwa heba yao. Atakaye fuzu leo basi ndio kashinda kweli.
 

65. Wachawi walimkabili Musa kwa rai moja, na wakamkhiarisha kwa majivuno na kiburi, waanze wao au aanze yeye kuonyesha ubingwa wake.
 

66. Musa akasema: Bali anzeni nyinyi! Basi wakazitupa kamba zao na fimbo zao. Zikamdhihirikia Musa, kwa uchawi, kuwa zimegeuka nyoka zinakwenda.
 

67. Musa akaingiwa na khofu kwa aliyo yaona kwa kuzugwa na uchawi, na kuona huenda watu wakadanganyika kwa uchawi wakadhani ni muujiza.
 

68. Mwenyezi Mungu akamdiriki kwa upole, akamwambia: Usiogope kitu. Wewe utaushinda tu leo huu upotovu wao.
 

69. Itupe hiyo fimbo uliyo nayo mkononi mwako wa kulia ivimeze hivyo walivyo vizua kwa uchawi. Kwani hayo waliyo yaunda ni mazonge tu ya uchawi, na hakika mchawi popote alipo hawezi kufuzu.
 

70. Musa akaitupa fimbo yake, na hapo hakika ikageuka kwa uwezo wa Mwenyezi Mungu ikawa joka kubwa la kutisha. Likavimeza vyote walivyo unda wao. Wachawi walipo uona muujiza huu mbio mbio wakasujudu kwa kuyakinika na ukweli wa Musa, huku wakisema: Tumemuamini Mwenyezi Mungu Mmoja wa Pekee, Mola Mlezi wa Harun na Musa, Mola Mlezi wa kila kitu.
 

71. Firauni akasema: Vipi mnamuamini huyu bila ya ruhusa yangu? Hakika huyu ndiye mkubwa wenu aliye kufunzeni uchawi, wala kitendo chake hichi si muujiza kama mnavyo dhani! Akawatishia kwa kusema: Kwa yakini nitaikata mikono yenu na miguu yenu mbali mbali, mkono wa kulia kwa mguu wa kushoto n.k. Na hakika nitakubandikeni misalabani kwenye vigogo vya mitende. Na hapo mtajua ni mungu gani kati yetu aliye mkali zaidi na kudumu zaidi katika mateso - mimi au mungu wa Musa?
 

72. Wachawi wakasimama imara juu ya Imani yao, na wakajibu vitisho vya Firauni kwa kauli yao: Sisi hatuendelei na kubakia nawe katika ukafiri baada ya kwisha tubainikia yaliyo ya kweli katika muujiza wa Musa. Wala sisi hatutakukhiari wewe kuliko Mungu wa Musa ambaye ndiye aliye tuumba. Basi wewe tenda utakayo yatenda! Madaraka yako hayapindukii maisha haya mafupi.
 

73. Kwani hakika sisi ni wenye kusimama juu ya Imani kumuamini Mola wetu Mlezi wa Haki, ili atufutie madhambi yetu yaliyo pita, na atusamehe huku kushughulikia uchawi ulio tulazimisha tujifunze na tuufanye! Na Mola wetu Mlezi ni Mbora wa malipo kuliko wewe, akit'iiwa; na ufalme wake na uwezo wake kulipa unadumu zaidi kuliko wako.
 

74. Hakika anaye kufa katika ukafiri akakutana na Mwenyezi Mungu hali naye ni mkhalifu basi malipo yake ni Jahannamu. Humo hafi, akapumzika na adhabu; wala hawi hai wa maisha ya kustarehe na neema.
 

75. Na mwenye kukutana na Mola wake Mlezi naye yumo katika Imani na a'mali njema, basi huyo atakuwa na vyeo vya juu.
 

76. Vyeo hivyo ni Bustani za Peponi za kudumu katika neema. Baina ya miti yake inapita mito, na humo watadumu milele. Hayo ni malipo ya mwenye kuitakasa nafsi yake na ukafiri kwa kuijaza Imani, na ut'iifu baada ya ukafiri na maasi.
 

77. Tena vikapishana vituko baina ya Firauni na Musa. Mwenyezi Mungu akampa Wahyi (ufunuo) Mtume wake, Musa, atoke Misri na Wana wa Israil, wakati wa usiku. Na aipige bahari kwa fimbo yake, utatokea muujiza mwingine, nao ni kufunguka njia kavu baharini. Naye akamtuliza asiingiwe na khofu kuwa atakamatwa na Firauni, au kuwa atazama katika maji!
 

78. Musa akafanya kama alivyo muamrisha Mwenyezi Mungu. Akatoka Firauni na askari wake nyuma yake, akawakuta kwenye bahari. Akenda nyuma yao kwenye njia iliyo funguka baharini kwa ajili ya Musa na kaumu yake. Na hapo ukatokea muujiza; nao ni maji kumfudikiza Firauni na kaumu yake, wakazama wote!
 

79. Hivi ndivyo Firauni alivyo potea yeye na watu wake wakaacha Haki, wakateketea wote!
 

80. Enyi Wana wa Israili! Sisi tulikuokoeni na adui yenu, Firauni, na tukakuahidini kuokoka kwa ulimi wa Musa kuwa mtafika salama mpaka kwenye kando ya mlima. Na tulikuteremshieni Manna na Salwa, chakula kizuri, cha tam-tam na nyama ya ndege nono.
 

81. Kuleni vitu hivi vizuri tulivyo kuruzukuni bila ya taabu yoyote kwenu. Wala msidhulumu, wala msiingie kumuasi Mwenyezi Mungu katika maisha haya ya starehe, isije kukuteremkieni ghadhabu yangu. Kwani anaye teremkiwa na ghadhabu yangu huporomoka katika matabaka ya chini kabisa ya mateso ya Mwenyezi Mungu.
 

82. Na hakika Mimi ni Mtukufu wa Kusamehe kwa anaye acha ukafiri wake, na akatengeneza Imani, na akatenda yaliyo mema, na akadumu juu ya hayo mpaka akakutana na Mwenyezi Mungu.
 

83. Musa aliwatangulia watu wake kwenda mlimani, apate kuzungumza na Mola wake Mlezi. Mwenyezi Mungu akamuuliza sababu ya kufanya kwake haraka kufika mbele kabla ya kaumu yake.
 

84. Musa akasema: Hakika watu wangu wapo karibu nami, watanikuta. Ewe Mola wangu Mlezi! Mimi nimewatangulia ili kutaka kukuridhisha Wewe.
 

85. Mwenyezi Mungu akamwambia: Sisi tumewafanyia mtihani watu wako baada ya wewe kuwawacha. Wakaingia katika fitna; Msamaria amewapotoa!
 

86. Musa akawarejea watu wake naye kaghadhibika sana, na huzuni ya uchungu. Akawasemeza watu wake kwa hamaki: Mola wenu Mlezi alikuahidini kuwa atakuokoeni na atakuongoeni, kwa kuiteremsha Taurati na kupata ushindi kwa kuingia nchi takatifu. Haujapita muda mrefu wa ahadi ila nyinyi mmekwisha sahau ahadi ya Mwenyezi Mungu aliyo kupeni. Kwa kitendo chenu kiovu hichi mnataka ghadhabu ya Mwenyezi Mungu ikuteremkieni kwa maasi yenu aliyo kuhadharisheni nayo? Mmesahau ahadi yenu mliyo nipa kuwa mtafuata mwendo wangu, na mtafuata nyayo zangu?
 

87. Watu wa Musa wakasema kwa kutafuta udhuru: Hatukwenda kinyume na ahadi yako kwa khiari yetu. Lakini tulipo toka Misri tulibebeshwa mizigo ya mapambo ya watu. Kisha tukaona - kwa uzito wake kwetu - tuepukane nayo. Msamaria akawasha moto katika shimo, tukaitupa hiyo mizigo. Na kadhaalika Msamaria naye katupa vyombo alivyo kuwa navyo.
 

88. Basi Msamaria akawaundia ndama aliye na mwili wa dhahabu, ukipita upepo ndani yake, hutoa sauti, husikilizana kama mlio wa ng'ombe, ili udanganyifu utimie. Akawaita wamuabudu na wao wakamwitikia. Akasema yeye na wafwasi wake: Huyu ndiye mungu wenu, na ndiye mungu wa Musa. Akasahau Msamaria kuwa ni wepesi mtu, akizingatia na kutafuta dalili, kufahamu kuwa ndama  hawezi kuwa mungu.
 

89. Macho yaliingia upofu yalipo zingatia kuwa huyu ndama ni mungu! Hawaoni kwani hawarejezei kauli yao? Wala hawezi kuwaondolea madhara yoyote? Wala kuwaletea manufaa yoyote?
 

90. Na Harun alikuwa pamoja nao ilipo tokea fitna hii. Naye kabla ya kurejea Musa a.s. alikwisha waambia: Enyi watu wangu! Nyinyi mmeingia katika fitna ya Msamaria kwa upotovu huu! Hakika Mungu wenu wa Haki ni Mwenyezi Mungu,  Arrahman, Mwingi wa Rehema, wala hana mwenginewe. Nifuateni mimi kwa haya ninayo kunasihini, na ishikeni rai yangu kwa kuachilia mbali upotovu huu.
 

91. Wakasema: Sisi tutaendelea kumuabudu huyu ndama mpaka atakapo rejea Musa kwetu!
 

92. Musa kwa kuathirika na aliyo yajua na kuyaona ya watu wake, alisema: Ewe Harun! Sababu gani iliyo kukataza hata usiwazuie na upotovu ulipo kwisha waona wameuingia?
 

93. Na usisimame msimamo wangu kwa kuwanasihi kama nilivyo chukua ahadi kwako? Hukunifuata katika ahadi niliyo ahidiana nawe, au umevunja amri yangu?
 

94. Harun akamwambia Musa: Ewe mwana wa mama yangu! Usinichukulie papara kwa hasira zako, wala usizishike ndevu zangu na kichwa changu. Hakika mimi nilikhofu lau ningeli wafanyia ukali, wakafarikiana makundi na mapande usije ukaniambia: Umewagawanya Wana wa Israil, wala hukuyafuata niliyo chukua ahadi kwako.
 

95. Musa a.s. akamwambia Msamaria: Jambo hili jambo gani la khatari ambalo laonekana ni balaa ulilo lizua?
 

96. Msamaria akamwambia Musa: Nimejua ustadi wa ufundi na mbinu zake wasizo zijua Wana wa Israil; nikawaundia sanamu la ndama lenye kutoa sauti, na nikachukua sehemu ya Taurati nikaitia ndani ya ndama, kuwazuga watu. Basi ndio hivyo, nafsi yangu imenizaini nifanye hayo niliyo yafanya.
 

97. Musa akamwambia Msamaria: Tokana nasi, na uwe mbali nasi. Na jaza yako duniani uwe unatanga tanga ovyo, na watu wakikukimbia, mpaka usiwe na makhusiano na yeyote, na asiwepo ndudu ya mtu kukukaribia, wala wewe usimkaribie mtu. Na hakika adhabu yako kesho Akhera umewekewa kwa ahadi huwezi kuikimbia!     Musa tena akimbeua huyo mungu wake kwa kusema: Tazama sasa nini tunalo mfanyia huyu mungu wako ulio kaa wewe ukimuabudu, na kwa sababu yake ukawafitini watu! Tutamuunguza, na kisha tutamtawanya baharini apotelee mbali!
 

98. Musa akaingia kutimiza aliyo yasema, na kisha baada ya mazingatio hayo aliwaelekea Wana wa Israili kuwaambia: Hakika Mungu wenu ni Mmoja. Yeye ndiye ambaye hapana anaye abudiwa kwa haki isipo kuwa Yeye. Na ujuzi wake umeenea kila kitu kilicho kuwa na kitakacho kuwa.
 

99. Ewe Mtume! Kama tulivyo kusimulia khabari za Musa, tunakupa khabari za kweli za kaumu zilizo tangulia. Na Sisi tumekuteremshia wewe Kitabu kutoka kwetu, ndani yake yamo mawaidha kwako na kwa umma wako, ya kukufaeni katika Dini yenu na dunia yenu.
 

100. Mwenye kuacha kukiamini Kitabu hicho na kufuata uwongofu wake, basi amepotea katika maisha yake, na Siku ya Kiyama atakuja naye amebeba madhambi ya aliyo yatenda, na atalipwa kwa adhabu kali.
 

101. Na atadumu katika adhabu hii, na ni mzigo muovu kweli huo Siku ya Kiyama.
 

102. Ewe Mtume! Watajie umma wako Siku ambayo tutawaamrisha Malaika walipulize baragumu la kuwafufua watu kutoka makaburini, na kuwaita hapo pa mkutano, na tutapo wachunga wakhalifu kwendea ufundoni na nyuso zao rangi ya buluu kwa khofu na kitisho.
 

103. Wakinong'onezana wao kwa wao katika udhalili na kubabaika jinsi walivyo ona maisha ya dunia ni mafupi, hata waone kama kwamba hawajapata kustarehe nayo, na wala hawakukaa humo duniani ila siku kumi tu!
 

104. Wala si kama hiyo minong'ono yao ndiyo haisikilizani, kwani Sisi tunajua vyema wao wananong'onezana nini, na tunayajua vyema wanayo yasema wale walio kuwa mahodari zaidi kulinganisha hisiya zao kwa dunia, kuwa hayo maisha ya duniani ni kama kwamba hayakutimia hata siku moja.
 

105. Ewe Mtume! Wanakuuliza hao wanao kanya kufufuliwa, nini hali ya milima Siku ya Kiyama hiyo unayo itaja? Wajibu: Mwenyezi Mungu ataivuruga kama mchanga, kisha ataipeperusha kwa upepo kama vumbi!
 

106. Na pahala pao baada ya kwisha vurugika milima patakuwa sawa sawa laini.
 

107. Hutoona kwenye ardhi kudidimia wala kunyanyuka, kama kwamba haikupata kukaliwa kabla yake.
 

108. Siku ya Kiyama watu wakisha toka makaburini, watamfuata mwenye kuwaita mpaka pahala pa mkutano nao wamesalimu amri. Hawezi yeyote kati yao kuelekea kulia wala kushoto. Sauti zote zimenyenyekea kwa utulivu na kitisho kwa utukufu wake Arrahmani, Mwingi wa Rehema. Basi husikii ila sauti ya chini kabisa ya mnong'ono.
 

109. Siku hiyo hapana uombezi unao faa kitu, ila wa aliye pata hishima ya Mwenyezi Mungu kwa kuruhusiwa naye na kuridhiwa aseme. Na hapana uombezi wa yeyote utao faa ila wa aliye pata ruhusa ya Mwenyezi Mungu kuombea, na akawa ni Muumini, na Mwenyezi Mungu akaridhia kauli yake kwa Tawhidi na Imani.
 

110. Na Mwenyezi Mungu, aliye tukuka shani yake, anayajua mambo yao waliyo yakadimisha katika dunia yao na waliyo yaakhirisha. Yeye Subhanahu anawapangia mambo yao kwa mujibu wa ujuzi wake. Na wao hawaijui mipango yake na hikima zake.
 

111. Nyuso zitadhalilika Siku hii, na zitamnyenyekea Mwenyezi Mungu Aliye Hai asiye kufa, Mwenye kusimamia kupanga mambo yote ya viumbe vyake. Na amepoteza uwokofu na thawabu Siku ya Akhera mwenye kuidhulumu nafsi yake duniani, na akamshirikisha Mola wake Mlezi.
 

112. Na mwenye kutenda mambo ya ut'iifu, naye akawa anayasaidiki aliyo yaleta Muhammad, s.a.w. huyo hana khofu ya kuzidishiwa makosa yake au kupunguziwa mema yake.
 

113. Na mfano wa maelezo haya ya haki yaliyo kwisha tangulia katika Sura hii, ya kumtukuza Mwenyezi Mungu, na hadithi ya Musa na khabari za Kiyama, Mwenyezi Mungu ameyateremsha katika Kitabu hichi  cha Qur'ani kwa lugha ya Kiarabu, na ameeleza mara kwa mara  kwa njia za kuonya ili watu waweze kutanabahi waache maasi, na Qur'ani iwazindue upya kwa kuwapa mawaidha na mazingatio.
 

114. Basi ametukuka na dhana dhana, na amejitenga na kushabihiana na viumbe, huyo Mfalme ambaye anahitajiwa na watawala na wanao tawaliwa, Mwenye haki katika Uungu wake na Utukufu wake. Na wewe, ewe Muhammad, usiifanyie haraka Qur'ani kabla Malaika hajakusomea. Na sema: Ewe Mola wangu Mlezi, nizidishe ilimu kwa Qur'ani na maana zake.
 

115. Ewe Mtume! Sisi tulimuusia Adam tangu mwanzo, asende kinyume na amri yetu, akasahau ahadi yetu akenda kinyume. Na hatukumwona tangu mwanzo wake kuwa ana azma baraabara, na ukakamavu wa kutosha asiingiliwe na Shetani akamtia wasiwasi katika nafsi yake.
 

116. Ewe Mtume! Na kumbuka pale Mwenyezi Mungu alipo waamrisha Malaika wamtukuze Adam kwa njia aliyo itaka Yeye Subhanahu, na wakafuata. Lakini Iblisi, naye alikuwa pamoja nao, alikuwa jini, akenda kinyume akakataa, akatolewa akafukuzwa!
 

117. Mwenyezi Mungu akamsemeza Adam kwa kumwambia: Hakika huyu Shetani aliye kwenda kinyume na amri yetu ya kukuadhimisha wewe ni adui yako wewe na Hawa, mkeo. Basi tahadhari na uchochezi wake kukuingizeni katika maasi, isije kuwa ndio sababu ya kutoka kwenu kwenye Bustani hii, ukaja pata taabu, ewe Adam, katika maisha baada ya kutoka kwenye Bustani.
 

118. Sisi tunakudhaminia mahitaji ya maisha yako katika Bustani. Humo hutopata njaa wala hutakuwa uchi.
 

119. Na wala hutopata kiu, wala hutopata joto la jua, kama wanavyo pata wanao sumbuka nje ya Bustani.
 

120. Shetani akamfanyia hila akimnong'oneza katika roho yake, kumraghibisha yeye na mkewe, waule ule mti walio katazwa, akiwaambia: Ewe Adam! Mimi nitakuonyesha mti huo, ataye kula basi ataishi milele, na atapata ufalme usio na mwisho.
 

121. Akamwonyesha mti ulio katazwa. Adam na mkewe wakakhadaika kwa kudanganywa na Iblisi, na wakasahau makatazo ya Mwenyezi Mungu, na wakaula. Utupu wao ukadhihiri, kuwa ni malipo ya tamaa yao, mpaka wakasahau wakaingia katika ukhalifu. Wakawa wakikata majani ya miti ya Bustani ile ili wajisitiri utupu wao.  Ikawa Adam  kamkhaalifu Mola wake Mlezi. Hayo yalikuwa kabla hajapewa Unabii. Akayakosa maisha ya milele aliyo kuwa anayatamani, na yakaharibika maisha yake.
 

122. Kisha Mwenyezi Mungu alimteuwa ampe Utume, na akaipokea toba yake, na akamwongoa atake udhuru na aombe msamaha.
 

123. Mwenyezi Mungu aliwaamrisha Adam na mkewe watoke kwenye Bustani, wateremke kwenye ardhi, naye Subhanahu akawaambia kwamba utakuwapo uadui baina ya vizazi vyao, na kwamba Yeye Subhanahu atawaongoa kwa uwongofu na uwongozi. Mwenye kufuata uwongofu wa Mwenyezi Mungu hatoingia katika maasi duniani, wala hatoteseka kwa adhabu.
 

124. Na mwenye kujiepusha na uwongofu wa Mwenyezi Mungu na ut'iifu wake, basi ataishi maisha yasiyo na starehe, hatokinai na chochote anacho pewa na Mwenyezi Mungu, wala hatokuwa radhi na hukumu ya Mwenyezi Mungu na kudra yake. Mpaka ikija Siku ya Kiyama atakuja kwenye mkutano wa hisabu atashikwa kwa madhambi yake, naye hana hoja ya kutoa, kama alivyo kuwa duniani ni kipofu hazioni ishara zote za Mwenyezi Mungu.
 

125. Na kwenye mkutano huo atamuuliza Mola wake Mlezi kwa fazaa: Ewe Mola wangu Mlezi! Vipi umenisahaulisha hoja, hata nisiweze kujitolea udhuru, na umenisimamisha kama kipofu, na hali mimi duniani nilikuwa naona kila kitu, nikishindana na kutetea?
 

126. (Naye atajibiwa:) Mambo kwako ndivyo kama yalivyo. Zimekujilia dalili zetu, na Mitume wetu duniani;  yote hayo ukayasahau, na ukajitia upofu, na hukuamini. Na leo basi kadhaalika unaachwa umesahauliwa umo katika adhabu na fedheha.
 

127. Na mfano wa malipo haya mabaya tunamlipa duniani mwenye kutenda maasi, na akamkadhibisha Mwenyezi Mungu na ishara zake. Na hakika adhabu za Akhera zina uchungu mkali zaidi, na zinadumu zaidi kuliko za dunia.
 

128. Vipi wanajitia upofu na ishara za Mwenyezi Mungu, na wanajua kuwa tumezihiliki kaumu nyingi zilizo tangulia kwa sababu ya ukafiri wao, nao hawakuwaidhika  kwao juu ya kuwa wao wanapita wanatembea kwenye majumba yao na maskani zao, na wanayaona magofu yao na athari ya adhabu zilizo wapata? Hakika mambo kama hayo peke yake ni mawaidha kwa watu wenye akili za kufahamu.
 

129. Na lau kuwa haikutangulia hukumu ya Mola wako Mlezi ya kuwaakhirishia adhabu mpaka siku ya miadi maalumu, nayo ni Siku ya Kiyama, basi adhabu lazima ingeli wapata hapa hapa duniani kama ilivyo kwisha wapata makafiri wa karne zilizo pita.
 

130. Ewe Mtume! Vumilia hayo wayasemayo ya kukukadhibisha na kuukejeli Utume wako, na mtakase Mola wako Mlezi na yote yasiyo mfalia kwa kumsifu, na kumuabudu Yeye pekee daima, na khasa kabla ya jua kuchomoza, na kabla halijachwa. Na mtakase, umuabudu katika saa za usiku, na katika ncha za mchana kwa kusali, ili yadumu mawasiliano yako na Mwenyezi Mungu, upate kutua kwa hayo uliyo nayo, na uridhike kwa uliyo kadiriwa.
 

131. Wala usivuke mipaka kwa kuangalia yale mambo ya starehe ya namna mbali mbali tuliyo waonjesha makafiri. Kwani starehe hizi ni uzuri na pambo la duniani tu analo wafanyia mtihani kwayo Mwenyezi Mungu waja wake. Na Mwenyezi Mungu anakuwekea wewe Akhera yaliyo bora zaidi na yenye kudumu zaidi kuliko starehe hizi.
 

132. Na waelekeze ahli zako washike Sala kwa nyakati zake. Kwani Sala ni kiungo chenye nguvu kabisa cha kuwaunganisha na Mwenyezi Mungu, na kudumu kuishika Sala kwa nyakati zake ndio ukamilifu. Sisi hatukulazimishi ujiruzuku nafsi yako, bali ni Sisi ndio kazi yetu kukuruzuku. Na hakika mwisho wa kusifiwa duniani na Akhera ni wa watu wema na wenye kumcha Mungu.
 

133. Na makafiri katika inadi yao wanasema: Kwa nini Muhammad hatuletei dalili inayo toka kwa Mola wake Mlezi inayo tulazimisha sisi kumuamini? Na vipi wao wanaipinga Qur'ani, nayo imewajia hali imekusanya yaliyomo katika Vitabu vilivyo tangulia katika khabari za watu walio pita, na maangamizo yao kwa sababu ya kuwakadhibisha Mitume? Na Muhammad si wa kwanza katika hayo!
 

134. Na lau kuwa Mwenyezi Mungu ange wafanyia haraka kuwahiliki makafiri hawa, kabla ya kumtuma Muhammad kwao, wange toa udhuru Siku ya Kiyama kwa kusema: Ewe Mola wetu Mlezi! Kwa nini hukutuletea Mtume duniani mwenye ishara tumfuate, kabla hujatuteremshia adhabu na hizaya Akhera? Lakini sasa hawana udhuru wowote baada ya kutumiwa Mtume.
 

135. Ewe Mtume! Waambie hawa wenye inda: Hakika sisi sote tunangojea yatavyo kwenda mambo yetu na yenu. Na mtajua kwa hakika nani katika makundi mawili walio watu wa Dini ya Haki, na wenye kuongoka kwa uwongofu wa Mwenyezi Mungu.