1. Alif Lam Mym 'Saad. (A.L.M.S'.)
Hizi ni harufi za kutamkwa ambazo zinaanzia baadhi ya Sura za Makka, kwa ajili
ya kuwazindua Washirikina kuwa hakika hii Qur'ani Tukufu imeundwa kwa harufi
zile zile wanazo zitamka wao. Na juu ya hivyo wao wanaemewa hawawezi kuleta
mfano wake. Kadhaalika harufi hizi zinapo somwa huwazindua wao wasikilize,
kwa kuwa walikuwa wananasihiwa na wakubwa zao kuwa wasiisikilize Qur'ani.
2. (Ewe Nabii!) Umeteremshiwa wewe
Qur'ani ili uwaonye hao wanao kanya wapate kuamini, na uwakumbushe Waumini
wapate kuzidi Imani yao. Basi usiingie dhiki katika kifua chako unapo ifikilisha
kwa kukhofu kuwa utakanushwa.
3. (Enyi Watu!) Fuateni aliyo
kufunulieni Mola wenu Mlezi, wala msiwafuate marafiki au walinzi wengineo badala
yake Yeye, mkawa mnawaitikia wao na mkiwaomba msaada! Itakuwa kama hamkuwaidhika
ikiwa mtaiacha Dini ya Mwenyezi Mungu na muifuate nyengineyo, hali ya kuwa yapo
mengi ya kuzingatia katika haya mliyo funuliwa.
4. Kwani Sisi tumekwisha iteketeza
miji kadhaa wa kadhaa, kwa sababu watu wao walikuwa wakiwaabudu wasio kuwa
Mwenyezi Mungu, na kwa kuwa katika mwendo wao hawakufuata Njia yake. Ikawajia
adhabu yetu wakati wao wameghafilika na wametuwa usiku nao wamelala, kama
yalivyo wapata kaumu ya Lut'; au wakatekezwa mchana nao wamepumzika wakati wa
kujinyoosha, kama yalivyo wapata kaumu ya Shua'ib.
5. Basi wakaungama kwa madhambi
yao yaliyo waletea msiba wao. Hakuwa hata mmoja katika wao walipo ona adhabu ila
alisema, na wakati huo kusema huko hakufai kitu: Hakika sisi tulikuwa
tumejidhulumu nafsi zetu kwa maasiya, wala Mwenyezi Mungu hakutudhulumu kwa
kutupa adhabu.
6. Na Siku ya Kiyama hisabu ya
Mwenyezi Mungu itachungua kila kitu kwa uadilifu. Tutawauliza watu tulio watumia
Mitume: Je, Ujumbe umewafikilia? Na wamewajibu nini hao Wajumbe tulio watuma? Na
tutawauliza Mitume pia: Je, mmefikisha yaliyo teremshwa kwenu kutoka kwa Mola
wenu Mlezi? Na hao kaumu zenu wamekujibuni nini?
7. Na tutawapa wote khabari ya
kweli yote yaliyo kuwa kwao, kwa sababu hakika Sisi tumewadhibitia kila kitu
chao, kwani Sisi hatukuwa mbali nao, wala hatukuwa hatujui waliyo kuwa
wakiyafanya.
8. Na Siku tutapo wauliza na
kuwaeleza, vipimo vya vitendo vyao kwa ajili ya kulipwa vitakuwa vipimo vya
uadilifu. Wale ambao mema yao yatazidi kuliko maovu yao watakuwa ndio wenye
kufuzu, tutakao walinda na Moto na tutawatia Peponi.
9. Na wale ambao maovu yao
yatakithiri kuliko mema yao, hao ndio watakuwa khasarani, kwa kuwa wameziuza
nafsi zao kwa Shetani, wakaacha kuzingatia Ishara zetu kwa ukafiri na inda.
10. Nasi tumekuwekeni
katika ardhi, na tukakupeni nguvu za kuiamirisha mkajipatia manufaa ndani yake,
na tukakusahilishieni njia za kupatia maisha. Juu ya neema hizi zote, kumekuwa
kuchache mno kumshukuru kwenu Mwenyezi Mungu. Nanyi mtakuja pata malipo ya hayo
myatendayo!
11. Na katika khabari za
wale wa mwanzo pana mazingatio na mawaidha, yanayo dhihirisha kuwa Shetani
anajaribu akuondoleeni neema kwa kusahau kwenu amri za Mwenyezi Mungu. Sisi
tumemuumba baba yenu Adam, na tukampa Sura. Kisha tukawaambia Malaika:
Mtukuzeni! Wakamtukuza kwa kut'ii amri ya Mola wao Mlezi, ila Iblisi hakut'ii.
12. Mwenyezi Mungu kwa
kuudhika naye kwa uasi wake alimwambia: Nini kilicho kuzuia usimtukuze Adam, na
hali Mimi nimekuamrisha ufanye hivyo? Iblisi akajibu kwa inda na kiburi: Mimi
bora kuliko Adam. Umeniumba kwa moto, na yeye umemuumba kwa udongo. Na moto ni
mtukufu zaidi kuliko udongo.
13. Mwenyezi Mungu
alimlipa kwa inda yake na kiburi chake kwa kumfukuza katika makao ya utukufu
wake, na akamwambia: Teremka kutoka hapo baada ya kuwa katika pahala pa juu.
Haikufalii ukapandwa kichwa na ukaasi humo! Toka huko, nawe umehukumiwa hizaya
na udhalili!
14. Iblisi akamwambia
Mwenyezi Mungu: Nipe muhula, unibakishe mpaka Siku ya Kiyama.
15. Mwenyezi Mungu
akamjibu: Wewe utakuwa katika walio bakishwa wa mwisho.
16. Kwa kumchukia Adam na
kumhusudu alisema: Kwa sababu ya kunihukumia kupotoka na kupotea, nakuapia
nitawapoteza wana wa Adam wasiifuate Njia yako Iliyo Nyooka, kwa kutumia kila
hila zinazo mkinika.
17. Na ninaapa,
nitawatokelea mbele yao, na nyuma yao, na kuliani kwao, na kushotoni kwao, na
kila upande ninao weza, nikitafuta kila kipengee cha kughafilika kwao au udhaifu
wao, nipate kuwapotosha, hata wasiwe wengi wao wanao kuamini Wewe, kwa kuto
shukuru neema yako.
18. Mwenyezi Mungu akazidi
kuudhika, akamwambia: Toka kwenye makao ya ukarimu wangu, wewe ulio hizika kwa
kiburi chako na uasi wako, na khatima yako ni kuhiliki tu! Na ninaapa nitaijaza
Jahannamu kwa wewe na hao wana wa Adam watao kufuata nyote pamoja!
19. Na ewe Adam! Kaa wewe
na mkeo katika makao ya ukarimu wangu, nayo ndiyo hiyo Bustani, mneemeke humo,
mkila kila chakula mpendacho, isipo kuwa mti huu. Msiukaribie! Msije mkawa wenye
kujidhulumu nafsi zenu kwa adhabu itayo kupateni kwa kuvunja amri.
20. Shetani akawazaini
waivunje amri ya Mwenyezi Mungu, ziwavuke nguo zilizo wasitiri zikashifike tupu
zao. Akawaambia: Mola wenu Mlezi hakukukatazeni mti huu ila ni kwa kuwa hataki
muwe Malaika, au msije mkawa mnaishi milele, na neema yenu haikatiki daima
katika makao haya!
21. Naye akawaapia kuwa
ati yeye ni katika wanao wapa nasaha njema, na akakariri kiapo chake.
22. Basi akawachochea kwa
udanganyifu mpaka wakenda kula ule mti. Walipo uonja tupu zao zikafichuka,
wakaingia wanakusanya majani ya miti kujisitiri tupu zao. Mola wao Mlezi
akawakaripia, na akawatanabahisha makosa yao kwa kuwambia: Mimi sikukukatazeni
mti ule, na nikakwambieni kuwa Shetani ni adui yenu wa dhaahiri, hakutakieni
kheri?
23. Adam na mkewe wakasema
nao wamejuta wananyenyekea: Ewe Mola wetu Mlezi! Tumejidhulumu nafsi zetu kwa
kuvunja amri yako, kuliko pelekea kuondoka kwa neema. Na ikiwa hutusamehe
ukhalifu wetu, ukaturehemu kwa fadhila yako, hapana shaka tutakuwa katika wenye
kukhasiri.
24. Mwenyezi Mungu
akawaambia wao na pia na Shetani: Teremkeni nyote nyinyi, mtakuwa maadui nyinyi
kwa nyinyi. Makao yenu na starehe yenu kwa muda mpaka ifike ajali yenu, yatakuwa
katika ardhi.
25. Katika ardhi
mnazaliwa, na mnaishi, na humo mnakufa na kuzikwa. Na kutoka huko mtatolewa
wakati wa kufufuliwa.
26. Enyi Binaadamu! Sisi
tumekuneemesheni. Tumekuumbieni nguo kusitiri tupu zenu, na vitu vya pambo.
Lakini ut'iifu ndio nguo bora ya kukukingeni na adhabu. Neema hizo ni katika
Ishara zenye kuonyesha uwezo wa Mwenyezi Mungu, na rehema yake, ili watu
waukumbuke utukufu wake. Yeye tu ndiye anaye stahiki Ungu. Na kisa hichi ni
katika nyendo za Mwenyezi Mungu za uumbaji wake, zinazo bainisha nini
malipo ya kuvunja amri ya Mwenyezi Mungu, ili watu wakumbuke, na wafanye pupa
kumt'ii Allah na kumshukuru.
27. Enyi wanaadamu!
Msimuitikie Shetani na upotovu wake, mkatoka kwenye neema hizi, ambazo hazidumu
ila kwa kushukuru na kut'ii, kama walivyo muitikia wazazi wenu, Adam na mkewe,
akawatoa Shetani kwenye neema na ukarimu, na akawavua nguo zao zikaonekana tupu
zao. Basi yeye Shetani na wasaidizi wake wanakujieni kwa namna msio watambua,
wala hamuhisi mipango yao na vitimbi vyao! Lakini Shetani hana madaraka juu ya
Waumini. Sisi tumemfanya yeye na wasaidizi wake kuwa ni marafiki wa wale wasio
amini Imani ya kweli yenye kulazimikana na ut'iifu ulio timia.
28. Na wakanushao
wakitenda jambo ovu la mwisho, kama shirki, na kut'ufu kwenye Al Ka'aba nao wako
uchi, na mengineyo, basi wao hutoa udhuru kwa kusema: Sisi tumewakuta baba zetu
wakenda mwendo huu huu, na sisi tunawafuata wao; na Mwenyezi Mungu ametuamrisha
hivi na ameturidhia kwa kuwa ametukiria! Waambie ewe Nabii kuwapinga kwa uzushi
wao: Hakika Mwenyezi Mungu hakuamrisha mambo haya maovu! Je, mnamnasibishia
Mwenyezi Mungu mambo msiyo kuwa nayo tegemeo lolote mnalo jua lina dalili ya
ukweli wa kumnasibisha nalo Subhanahu?
29. Wabainishie aliyo
yaamrisha Mwenyezi Mungu, useme: Mola Mlezi wangu ameamrisha uadilifu usio
ingiliwa na uchafu. Na amekuamrisheni mumkhusishe Yeye tu kwa ibada kila wakati
na kila pahala, na muwe wenye kumsafia niya katika hayo. Na nyote nyinyi
baada ya kufa ni wenye kurejea kwake. Na kama alivyo anza kukuumbeni kwa wepesi,
na mlikuwa hammiliki kitu chochote, basi kadhaalika mtarejea kwake kwa wepesi na
hali mmeziacha nyuma ya migongo yenu neema zote mlizo nazo.
30. Siku ya Kiyama watu
watakuwa makundi mawili:- Kundi moja lilio pata tawfiqi ya Mwenyezi Mungu kwa
kuwa lilichagua Njia ya Haki, likaamini na likatenda vitendo vyema. Na kundi
jengine limehukumiwa upotovu, kwa sababu lilikhiari njia ya baat'ili, nayo ni
ukafiri na uasi! Na hao walio potea waliwafanya mashetani ndio rafiki zao badala
ya Mwenyezi Mungu, wakawafuata, nao wanadhani kuwa wao wamewafikiwa kwa
kudanganyika kwao na khadaa za mashetani!
31. Enyi wanaadamu!
Chukueni pambo lenu, nalo ni nguo hizi "maaddiy" za kuonekana, za kusitiri
utupu, na nguo za "adabiy" zisizo onekana, bali ni za maana, nazo ni Taqwa,
Uchamngu, katika kila pahala pa Sala, na kila wakati mnapo fanya ibada. Na
jistarehesheni kwa kula na kunywa bila ya kufanya israfu au ubadhirifu, yaani
kutumia kwa fujo, katika hayo. Basi msitumie vitu vilivyo harimishwa, wala
msipite kiasi cha kiakili katika huko kujistarehesha. Hakika Mwenyezi Mungu hana
radhi na wanao tumia kwa fujo.
32. Ewe Muhammad! Waambie
kwa kuupinga ule uzushi wao kumzulia Mwenyezi Mungu juu ya kuhalalisha na
kuharimisha: Nani aliye harimisha pambo la Mwenyezi Mungu alilo waumbia waja
wake? Na nani aliye harimisha riziki iliyo halali na nzuri? Waambie: Hivi vitu
vizuri ni neema inayo toka kwa Mwenyezi Mungu. Isingeli faa wastarehe navyo
duniani ila wale walio amini, kwa sababu wao wanatimiza haki yao kwa shukrani na
ut'iifu. Lakini rehema ya Mwenyezi Mungu ni kunjufu, imewakusanya pia makafiri
na wakhalifu katika dunia. Na Siku ya Kiama neema hizi zitakuwa za Waumini peke
yao, wala hapana mwenginewe ataye shirikiana nao katika hayo. Na Sisi
tunazieleza Aya, Ishara, zinazo onyesha hukumu kwa mpango huu ulio wazi kwa
ajili ya watu wanao fahamu kwamba hakika Mwenyezi Mungu peke yake, Mwenye
kumiliki kila kitu, ndiye Mwenye uwezo wa kuhalalisha na kuharimisha.
33. Ewe Muhammad! Sema:
Hakika Mola wangu Mlezi ameharimisha mambo yaliyo zidi kwa ubaya, kama uzinzi;
sawa sawa ukifanywa kwa siri au kwa dhaahiri. Pia ameharimisha kila maasi ya
namna yoyote, na dhulma isiyo na njia ya haki. Na ameharimisha kumshirikisha na
chochote kisicho kuwa na hoja madhubuti, au dalili ya kweli. Na pia kumzulia
uwongo Subhanahu, Aliye takasika, katika kuhalalisha na kuharimisha, na
mengineyo.
34. Na kila umma una ukomo
wake maalumu. Na hapana uwezo wowote wa kuupeleka mbele mwisho huo au
kuuakhirisha muda wake hata ukiwa mdogo vipi.
35. Enyi wanaadamu!
Wakikujieni Mitume kutokana na hiyo jinsi yenu ya kibinaadamu kukufikishieni
Ishara zangu zilizo funuliwa nyinyi mnakuwa makundi mawili. Kwa wale wenye
kuamini na wakatenda mema kwa usafi wa niya, hapana khofu, wala wao
hawatahuzunika katika dunia yao na Akhera yao.
36. Na wale wanao
zikanusha hizo Ishara na wakapandwa na kiburi wasizifuate wala wasiongoke kwazo,
basi hao ni watu wa Motoni. Humo wataadhibiwa daima milele katika adhabu.
37. Hapana wakubwa wa
dhulma kuliko hao wanao mzulia Mwenyezi Mungu uwongo, kwa kumnasibisha na
mshirika na mwana, na kuzua kuhalalisha na kuharimisha na mengineyo, pasina
hoja. Au wanao kanusha Aya, Ishara, za Mwenyezi Mungu zilizo funuliwa katika
Vitabu vyake na zinazo onekana katika ulimwengu wake. Hao wanapata hapa duniani
sehemu ya aliyo waandikia Mwenyezi Mungu katika riziki, au uhai, au adhabu.
Mpaka akiwajia Malaika wa Mauti kuzipokea roho zao, hapo huwaambia kwa kuwasuta:
Iko wapi hiyo miungu yenu mliyo kuwa mkiiabudu badala ya Mwenyezi Mungu ije
kukukingeni na mauti? Nao wajibu: Wametukataa, wametuacha na wametukimbia. Na
wajishuhudie wenyewe wakikiri kuwa hakika walikuwa makafiri.
38. Siku ya Kiyama
Mwenyezi Mungu atawaambia hawa makafiri: Ingieni Motoni pamoja na kaumu nyengine
za kikafiri miongoni mwa watu na majini, walio kwisha kutangulieni. Kila umma
ukiingia Motoni huwalaani umma mwingine ulio kufuru mfano wao, na ambao
waliwafanya ndio wa kuwafuata. Mpaka wakisha ingia kwa kufuatana wote
wakakusanyika, wale walio fuata watawashutumu wale walio kuwa waongozi kwa
kusema: Ewe Mola wetu Mlezi! Hao walitupoteza tulipo wafuata, kwa kuwa
walitutangulia au kwa kuwa walikuwa ndio wakitutawala. Basi wakatugeuza kwenye
Njia ya Haki tusiifuate. Basi wao wape adhabu mara mbili, wabebe malipo ya uasi
wao na uasi wetu! Mwenyezi Mungu atawajibu: Kila mmoja wenu atapata adhabu mara
mbili ambayo hapana ataye iepuka katika makundi yenu mawili. Wanao fuata
watapata adhabu marudufu kwa ukafiri wao na upotovu wao, na kufuata kwao bila ya
kuzingatia na kufikiri. Na wale walio fuatwa watapata adhabu marudufu kwa
ukafiri wao na upotovu, na pia kwa kuwakufurisha na kuwapotoa wengineo. Lakini
nyinyi hamjui kiasi gani itakuwa adhabu ya kila mmoja wenu.
39. Na hapa tena watasema
wale walio fuatwa kuwaambia walio fuata: Kutuiga kwenu sisi katika ukafiri na
uasi hakukufanyeni nyinyi muwe bora kuliko sisi hata mstahiki kupunguziwa
adhabu! Basi Mwenyezi Mungu atawaambia wote: Onjeni adhabu mlio jiletea wenyewe
kwa kuwa mlikuwa mkizua ukafiri na uasi!
40. Hakika wale walio
kanusha Ishara zetu zilizo teremshwa katika Vitabu, na ziliopo katika ulimwengu,
na wakapanda kiburi kukataa kuhidika kwa Ishara hizo, na wala wasitubu, nawakate
tamaa kupokelewa a'mali zao na kupata rehema ya Mwenyezi Mungu, na kuingia
Peponi, kama alivyo kata tamaa ngamia kupita katika tundu ya sindano. Na kwa
mfano huu ndio tutawaadhibu hao wenye kiburi katika kila umma.
41. Huko katika Jahannamu
kitanda chao ni moto, na shuka ya kujifunika ni moto. Na kwa mfano huu
tutawaadhibu wanao zidhulumu nafsi zao kwa ukafiri na upotovu.
42. Na wenye kuamini na
wakatenda vitendo vyema ambavyo hatumlazimishi ila kwa kiasi anavyo weza mtu,
hao ndio watu wa Peponi. Watastarehe humo daima dawamu!
43. Na tutazitoa chuki
zote ziliomo katika nyoyo zao. Basi watakuwa katika Janna, Pepo, ndugu wenye
kupendana, ikipita mito ya maji matamu mbele yao. Watasema kufurahia neema
watayo ipata: Alhamdulillahi, yaani Kuhimidiwa ni kwa Mwenyezi Mungu, ambaye
aliye tuonyesha Njia ya kufikia neema hizi, na akatuwezesha kuifuata. Na ingeli
kuwa hakutuhidi, kutuongoa, Mwenyezi Mungu kwa kutupelekea Mitume na akatupa
tawfiq, tusingeweza sisi wenyewe kufikia uwongofu. Hakika Mitume wa Mola wetu
Mlezi wametujia na wahyi wa Haki! Hapo tena Mwenyezi Mungu atawaambia: Hakika
hii Pepo ni zawadi mmepewa kutoka kwa Mwenyezi Mungu. Mmepewa kwa fadhila yangu
bila ya kuwa nyinyi kutoa kitu, kama urithi. Na takrima hii mlio pata ni sababu
ya vitendo vyenu vyema duniani.
44. Watu wa Peponi
watawanadia watu wa Motoni kwa kuwaambia: Sisi tumekwisha ona thawabu alizo
tuahidi Mola Mlezi wetu kuwa ni kweli. Je, nyinyi hiyo adhabu aliyo kuahidini
Mola Mlezi wenu mmeiona kuwa ni kweli? Nao watajibu: Naam, Ndiyo! Basi
mtangazaji atawatangazia watu wa Peponi na watu wa Motoni: Laana, yaani kunyimwa
na kufukuzwa kwenye rehema ya Mwenyezi Mungu, ndio malipo ya wenye kuzidhulumu
nafsi zao kwa ukafiri na upotovu.
45. Hawa madhaalimu ndio
wanao wazuia watu wasende kwenye Njia ya Mwenyezi Mungu wa Haki, nayo ndiyo
Imani na kutenda mema; na wanaweka vikwazo, na shakashaka, ili hiyo Njia yende
upogo iwapoteze watu wasiweze kuifuata. Na hao wanaikanusha Akhera hawaiogopi
adhabu ya Mwenyezi Mungu.
46. Na baina ya watu wa
Peponi na watu wa Motoni patakuwa na pazia kuzuia kufikia kwenye Mnyanyuko - na
hapo ni pahala palipo nyanyuka palipo juu. Watu katika bora ya Waumini na
watukufu wao, watakuwa wanawaangalia khalaiki wote hao, na wanawajua wema na
waovu kwa alama zinazo onyesha ut'iifu wao na uasi wao. Wataitwa watu wema kabla
ya kuingia Peponi, na hali wao wanataraji kuingia humo, watawabashiria kwa Imani
na utulivu na kuingia Peponi.
47. Macho ya hao Waumini
yakigeukia upande wa watu wa Motoni baada ya wito huo, watasema kwa kitisho
watacho kioni cha Moto: Ewe Mola wetu Mlezi! Usitutie pamoja na hawa madhaalimu
walio dhulumu nafsi zao, wakadhulumu Haki, na wakawadhulumu watu!
48. Na wale watu wa daraja
za juu katika Pepo, nao ni Manabii, na Mas'iddiqina, watawaita walio kuwa
wakiwajua kwa sifa zao katika watu wa Motoni, wakisema kwa kuwalaumu: Huko
kujumuika kwenu kwa wingi, hakukufaini chochote, wala huko kupanda kiburi
kuikataa Haki kwa kutegemea ujamaa wenu na utajiri wenu. Na hivi sasa mnawaona
hawa, nini hali yao na nini hali yenu.
49. Hao wanyonge mlio kuwa
mkiwadharau, na mkaapa kuwa hayumkini Mwenyezi Mungu awateremshie rehema, kama
kwamba nyinyi ndio mnao ishika rehema yake, wao wamekwisha ingia Peponi! Na Mola
wao Mlezi atawaambia: Ingieni humo kwa amani. Hapana khofu juu yenu kwa jambo
lolote litalo kupateni, wala hamtahuzunika kwa jambo mlilo likosa.
50. Na watu wa Motoni
watawanadia watu wa Peponi kwa kuwaambia: Hebu twachilieni maji kidogo
yatumiminikie sisi, au tugaieni kitu katika vyakula na mavazi na starehe
nyengine alizo kupeni Mwenyezi Mungu Mtukufu! Nao watu wa Peponi
watawajibu: Sisi hatuwezi kufanya hayo, kwa sababu Mwenyezi Mungu amezuia vyote
hivyo wasipate watu wapinzani, walio mkanusha Yeye na neema zake katika dunia.
51. Hawa makafiri ndio
ambao hawakufanya juhudi kutafuta Dini ya Haki, lakini ikawa dini yao ni kufuata
pumbao na matamanio, ndio pumbao la kujipumbazia na upuuzi wa kuchezea, na
maisha ya dunia na anasa zake zikawakhadaa, wakadhania hayo tu ndiyo maisha, na
wakasahau kukutana nasi! Basi Siku ya Kiyama Sisi tutawasahau. Na wao hawato
istarehea Pepo, na watauonja Moto, kwa sababu ya sahau yao kuisahau Siku ya
Kiyama, na kuzikanusha Ishara zenye kubainika wazi, zinazo thibitisha
Haki.
52. Na hakika kwa ajili ya
kubainisha Haki tuliwapa Kitabu, na tukakipambanua. Kitabu hicho kimekusanya
ilimu nyingi, na ndani yake zimo hoja za Tawhid, Upweke wa Mwenyezi Mungu, na
Ishara za Mwenyezi Mungu katika ulimwengu; na pia zimo sharia zake, maelezo ya
Njia Iliyo Nyooka, na uwongofu wa kuifikilia. Na pia yamo ndani ya Kitabu hichi
mambo ambayo, lau watu wakiyafuata watapata rehema. Na wala hawanufaiki kwacho
ila wale ambao ni shani yao kuinyenyekea Haki na kuiamini.
53. Hakika wao hawaiamini
hii Qur'ani, na wala hawangojei ila matokeo ambayo Mwenyezi Mungu
ameyabainisha kuwa yatawapata wanayo ikataa! Na Siku yatapofika hayo
matokeo, nayo ni Siku ya Kiyama, walio ziacha amri zake na maelezo yake, na
wakaghafilika kuwa ni waajibu kuiamini, na hali wakiungama madhambi yao,
watasema: Hakika walikuja Mitume kutoka kwa Muumba wetu na Mlezi wetu,
wakituitia Haki waliyo tumwa kuileta, nasi tukaikataa! Nao wataulizwa: Je, mnao
waombezi wakakuombeeni? Nao hawatowapata! Au, je, watarudishwa tena duniani
watende mema? Hawatajibiwa! Wamepoteza vitendo vyao kwa kukhadaika na dunia, na
umewapotea ule uzushi wa uwongo wa kudai kuna mungu asiye kuwa Allah, Mwenyezi
Mungu.
54. Hakika Mola Mlezi wenu
ambaye Mitume wake wanakuiteni mwende kwenye Haki, na kuiamini Siku ya Mwisho na
Malipo, ndiye Muumba ulimwengu, naye ndiye aliye uanza. Kaumba mbingu na ardhi
kwa viwango sita, vinavyo shabihiana na siku sita, katika siku za dunia. Kisha
akatawala juu ya Ufalme ulio kamilika. Naye ndiye anaye ufanya usiku uufunike
mchana kwa kiza chake, na usiku unafuatia mchana kwa upesi na mpango na
kufuatana kusikosita, kama anavyo taka Yeye. Naye Mwenyezi Mungu Subhana
ameliumba jua, na mwezi, na nyota. Na vyote hivyo vinamnyenyekea Mwenyezi Mungu
Mtukufu, vinakwenda kwa amri yake. Na Yeye peke yake ndiye Mwenye kuumba na
Mwenye amri ya kuitikiwa. Baraka za Mwenye kuanzisha ulimwengu na viliomo ndani
yake zimetukuka.
Aya hii tukufu
imekusanya maana tatu:
* Ya
kwanza ni kuwa mbingu na ardhi ameziumba Mwenyezi Mungu Mtukufu mnamo siku sita.
Na hizi siku sio muradi wake hizi tuzionazo sasa, na tunazo zihisabu. Bali
muradi wake ni kubadilika hali, baina ya giza totoro, na giza-giza la alfajiri,
na mpambazuko wa asubuhi, na mchana, na adhuhuri, na jioni. Na haya yamekusanya
hali sita zinazo badilika. Na giza-giza la magharibi linakitangulia kiza cha
usiku.
Na hizo hali
sita au vipindi sita, ambavyo vimeitwa "siku" ndivyo wanavyo vitaja wanachuoni
wa sayansi, navyo ni: Kipindi cha "Ether", kilicho elezwa katika Surat Ad-dukhan
ya 44 ya kuwa ni moshi. Kisha kutokana na hiyo "Ether" yakatokea majua, ambayo
moja lake ni hili jua letu. Kisha kutokana na jua zikawa sayari, na miongoni mwa
sayari hizo ni hii dunia yetu. Tena katika ardhi zikawamo maadini mbali mbali.
Tena ndio kikawa kipindi cha Ardhi, na baadae ukatokea uhai juu yake.
* Maana ya pili ya Aya hii ni kuwa
kila kiliomo ulimwenguni kimo chini ya ufalme wa Mwenyezi Mungu peke yake, wala
hapana ufalme usipo kuwa wake Yeye. Na nguvu zozote anazo pewa mtu hatoweza
kuuendesha ulimwengu atakavyo. Ukomo wa uwezo wake ni kunufaika na vilivyo umbwa
na akajua baadhi ya siri ziliomo ulimwenguni ambazo zilikuwa zimefichika. Kwa
hivyo Mwenyezi Mungu pekee ndiye aliye tuwa na kutawala juu ya A'rshi iliyo juu
ya vyote vilivyo umbwa, na kwamba nyota na vitu vyote haviendi ila kwa amri yake
peke yake.
* Maana ya tatu ni
kuwa kupishana usiku na mchana kumetokea baada ya kwisha umbwa ardhi na mbingu.
Basi hizo ni hali zenye kukhusika na asli ya uumbaji wa dunia, na makhusiano ya
baina mbingu na ardhi na kuzunguka kwao na Mwenyewe Subhana Mwenye kuumiliki
ufalme na utukufu na ukarimu.
55. Ilivyo kuwa Mwenyezi
Mungu, Mola Mlezi wenu, ndiye aliye umba kila kitu peke yake, basi muombeni Yeye
tu kwa kumuabudu na kwa mengineyo, mkimtangazia hayo maombi, kwa udhalilifu na
kunyenyekea, kwa dhaahiri au bila ya kudhihirisha. Wala msipite mipaka kwa
kumshirikisha na wenginewe, au kwa kumdhulumu yeyote. Kwani hakika Mwenyezi
Mungu, hawapendi wanao ruka mipaka, na wafanyao uadui.
56. Wala msifanye fisadi
katika nchi njema kwa kueneza maasi na dhulma na uvamizi. Na muombeni Yeye
Subhanahu, Aliye takasika, kwa kuiogopa adhabu yake, na kwa kutumai thawabu
zake. Na hakika rehema yake ipo karibu kwa kila mwenye kufanya mema. Na hayo ni
hakika.
57. Na Mwenyezi Mungu,
Aliye takasika, Aliye tukuka, peke yake, ndiye anaye zipeleka pepo kubashiria
rehema yake, kwa mvua ambazo kwa sababu yake ndio makulima humea, na konde
humwagiwa maji. Hizo pepo hubeba mawingu ambayo nayo yamebeba maji. Tunayachunga
mpaka yafike kwenye nchi isiyo kuwa na mimea, ambayo ni kama maiti asiye na
uhai, yakamiminika maji, na tena Mwenyezi Mungu husabibisha kumea namna kwa
namna ya mazao na matunda. Na mfano kama huu wa kuihuisha ardhi kwa mimea,
ndivyo tunawafanya maiti wakawa wahai. Haya ni kwa ajili mpate kuikumbuka kudra
ya Mwenyezi Mungu, na mpate kuamini kuwa kupo kufufuliwa.
58. Na ardhi njema
yenye rutba nzuri huzalisha mimea inayo kua kwa nguvu, kwa idhini ya Mola Mlezi.
Na ardhi mbaya haitoi ila mimea michache, isiyo na faida, ambayo huwa ndio
sababu ya dhiki ya huyo mkulima.
59. Washirikina wakafanya
inda, na wakaikanusha Haki ilipo wajia kwa hoja za kukata zisio pingika. Lakini
huo ndio mtindo wa makafiri kwa Manabii wao tangu zamani. Sisi tulimtuma Nuhu
kwa watu wake alio tokana nao. Naye akawakumbusha kuwa yeye ni mmoja wao: Enyi
watu wangu! Muabuduni Mwenyezi Mungu Mtukufu peke yake. Kwani nyinyi hamna Mungu
asiye kuwa huyu. Na mjue kuwa kutakuwapo kufufuliwa na kuhisabiwa Siku ya
Kiyama. Na hiyo ni Siku adhimu. Mimi nakukhofieni Siku hiyo msije mkapata adhabu
kali kweli.
60. Wakasema wale
wahishimiwa wao, watu wa mbele mbele na uwongozi katika wao, wakiujibu ule
wito wake wa Tawhidi na Siku ya Akhera: Hakika sisi tunakuona wewe uko mbali
kabisa na hiyo haki.
61. Nuhu akawaambia
kukataa yale waliyo msingizia: Mimi sina upotofu kama mnavyo dai. Lakini mimi ni
Mtume niliye toka kwa Muumba wa viumbe vyote, basi hayumkini awe mbali na haki.
62. Na mimi katika huu
wito wa Haki mshike Tawhidi na kuamini Siku ya Mwisho, nafikisha Ujumbe aliyo
nituma Mwenyezi Mungu, nao mfuate hukumu za Mwenyezi Mungu ambazo ndizo zinazo
msilihi mwanaadamu. Na mimi nakupeni nasaha ya kweli itokayo kwenye moyo wangu
ulio safi. Na Mwenyezi Mungu amenifunza mambo ambayo nyinyi hamyajui.
63. Mnanizulia kuwa
nimepotea na kuwa nipo mbali na Haki? Na mnastaajabu kukujieni kumbusho kutokana
na Mwenyezi Mungu aliye kuumbeni kwa ulimi wa mtu aliye kuja kwenu kukuonyeni
adhabu pindi mkikanusha, na akakuiteni mwende kuufuata uwongofu, na kutengeza
nyoyo, na kujiepusha na ghadhabu ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, kwa kutaraji muwe
katika rehema ya Mwenyezi Mungu Mtukufu duniani na Akhera? Haifai kuwa
mnastaajabu na mnakanusha juu ya kuwepo hoja zenye kuthibitisha Utume huu.
64. Lakini wao juu ya hoja
hizo zilizo wazi wengi wao hawakuamini, bali walimkanusha. Kwa hivyo
tukawateremshia adhabu ya kuwazamisha katika maji, na tukawaokoa wale walio
amini katika jahazi alilo liunda kwa kuongozwa nasi. Na wakazama wale walio
kanusha juu ya kuwapo hoja zilizo wazi, nao wakafanya inda wakawa hawaioni Haki
kwa kuwa walipofuka wasiione.
65. Kama tulivyo mtuma
Nuhu kwa kaumu yake kuwalingania Tawhidi, kadhaalika tuliwatumia kina 'Aad Nabii
Hud,(1) naye ni mmoja wao, makhusiano yake nao ni kama ndugu kwa ndugu.
Akawaambia: Enyi watu wangu! Muabuduni Mwenyezi Mungu peke yake, nanyi hamna
Mungu asiye kuwa Yeye. Na hii ndiyo njia ya kujikinga na shari na adhabu. Nayo
ndiyo Njia Iliyo Nyooka. Basi je, mtaifuata njia mjikinge na shari na upotovu?
(1) 'Aad ni katika kabila yenye
nguvu katika matumbo ya taifa la Sam, na ni katika mat'abaka ya kwanza katika
Waarabu wa jangwani. Ama makaazi yao yalikuwa katika Al-ah'qaaf iliyo tajwa
katika Kitabu kitukufu katika Sura ya Al-ah'qaaf Aya 21.
Wamewafikiana wanachuoni wa Kiislamu
wa kutegemewa kuwa hiyo Ah'qaaf ipo katika nchi ya Yaman, ijapo kuwa
wamekhitalifiana kidogo wapi khasa pahala penyewe. Kwa mujibu wa Yaaqut
Al-h'amawy ni bonde baina ya Oman na nchi ya Mahara. Na kwa mujibu wa Is-haaq
akimnukulu Ibn Abbas na Ibn Khaldun ni sehemu ya mchanga baina ya Oman na
Hadhramaut. Kwa mujibu wa Qutaada ni sehemu ya mchanga karibu na bahari katika
Shajar katika nchi ya Yaman. Na yafaa kutaja kuwa nchi ya 'Aad kwa mujibu wa
baadhi ya Wamagharibi wa zamani ipo pande za juu za Hijaz katika jimbo la
Husmaa, na karibu na makaazi ya Thamud. Vyo vyote ilivyo si mbali kuwa hao kaumu
ya 'Aad walisafiri wakahamia jimbo hili wakati mmoja wapo.
66. Wakasema wenye
uwongozi na umbele mbele katika kaumu yake: Sisi tunakuona umepungukiwa na
akili, kwa kutuitia wito huu; na tunaitakidi kuwa wewe ni mwongo.
67. Akasema: Enyi watu
wangu! Katika wito huu sina upungufu wa akili hata chembe, wala mimi si mwongo.
Lakini mimi nimekuja na uwongofu, na mimi ni Mtume wa Mwenyezi Mungu kwenu, naye
Yeye ndiye Mola Mlezi wa viumbe vyote.
68. Katika haya ninayo
kwambieni mimi nafikisha amri na makatazo ya Mola Mlezi wangu, na hayo ndio
Ujumbe wake kwenu. Na mimi nakupeni nasaha ya dhati, kwa niya safi kabisa. Na
mimi ni muaminifu katika ninayo kwambieni, wala mimi si miongoni ya watu waongo.
69. Tena Hud akawaambia:
Hivyo mmestaajabu mno, na mkaona mageni kukujieni ukumbusho wa Haki kwa ulimi wa
mtu aliye mmoja wenu, kukuonyeni? Mkiendelea na haya mliyo nayo matokeo yake
yatakuwa ni mabaya mno. Na hakika jambo hilo si la kustaajabiwa. Kisha Hud
akawatajia yaliyo wasibu walio kanusha katika watu walio watangulia, na
akawakumbusha neema za Mwenyezi Mngu juu yao. Akasema: Kumbukeni Mwenyezi Mungu
alivyo kufanyeni ndio warithi wa nchi baada ya kaumu ya Nuhu alio waangamiza kwa
kumkadhibisha Nuhu, na Mwenyezi Mungu akakuzidishieni nyinyi nguvu za mwili na
nguvu za utawala. Na neema hizo zinatakikana zilete Imani. Basi zikumbukeni
neema zake ili mpate kufuzu.
70. Lakini wao juu ya wito
mzuri huu walisema kwa kuona mageni: Hivyo wewe umetujia kututaka tumuabudu
Mwenyezi Mungu mmoja peke yake, na tuache masanamu waliyo kuwa wakiyaabudu baba
zetu? Na hapana shaka sisi hatutofanya hayo, nawe tuletee hiyo adhabu unayo
tutishia, kama wewe kweli ni katika wasema kweli!
71. Hakika kwa hii inadi
yenu mmestahiki adhabu ya Mwenyezi Mungu ikuteremkieni, na ghadhabu yake
ikufikieni! Nyinyi mnabisha kwa ajili ya masanamu ambayo mliyo yaita kuwa ni
miungu nyinyi na baba zenu, na wala si chochote ila ni majina tu walio pewa, na
wala Mwenyezi Mungu hakuleta hoja ya kuonyesha ungu wao. Hayo hayana nguvu za
muumbaji inayo kuruhusuni kuyaabudu! Na ikiwa mtashikilia ukaidi huu basi
ingojeeni adhabu ya Mwenyezi Mungu, nami pamoja nanyi, sote tungoje nini
kitakushukieni.
72. Basi Sisi tukamwokoa
A'ad na walio amini pamoja naye kwa rehema yetu, na tukawateremshia makafiri cha
kuwateketeza, na hapana chao kilicho bakia wala hapana athari yao, na wala
hawakuingia katika kundi la Waumini.
73. Na tuliwapelekea kina
Thamud (1) ndugu yao Saleh, ambaye ni mwenzi wao kwa nasaba na uwananchi. Na
wito wake ulikuwa kama wito wa Mitume walio kuwa kabla yake na baada yake.
Akawaambia: Msafishieni ibada Mwenyezi Mungu peke yake, na wala hapana Mungu
isipo kuwa Yeye. Na hoja ya Utume wangu imekwisha kukujilieni kutoka kwa Mola
wenu Mlezi. Nayo ni huyo ngamia mwenye sifa za pekee. Katika huyo ngamia pana
hoja. Yeye ni ngamia wa Mwenyezi Mungu, muacheni ale atakapo katika ardhi ya
Mwenyezi Mungu, wala msimdhuru isije kukupateni adhabu chungu.
(1) Thamud ni kabila ya Kiarabu iliyo
kuwa Al Hijr, baina ya Hijaz na Sham karibu na Wadi Alquraa
74. Na kumbukeni kuwa
Mwenyezi Mungu amekujaalieni ndio wa kurithi nchi ya A'ad, na akakupeni katika
hiyo nchi makaazi mema, mkijenga majumba ya fakhari katika nyanda zake. Na
mkichonga milima mkifanya majumba. Basi kumbukeni neema za Mwenyezi Mungu
Mtukufu, alivyo kuwekeni kwa makini katika nchi, wala msifanye maovu katika
nchi, mkawa wenye kufisidi na kuharibu baada ya kukaa kwa makini kama huku.
75. Wale wenye kiburi
katika watu wa mbele-mbele na uwongozi waliwasemeza wanyonge kwa kuwalaumu na
kuwadhalilisha: Hivyo nyinyi mnaitakidi kuwa kweli Saleh ametumwa na Mola Mlezi
wake? Watu wa Haki wakawajibu: Sisi tunaitakidi na tunakubali aliyo tumwa kwetu.
76. Wakasema wenye kiburi:
Sisi tunapinga na tunayakataa hayo mnayo yaamini nyinyi, na hayo anayo itia
Saleh ya kuwa Mungu ni mmoja.
77. Inda ya wenye kiburi
ikakakamia, na wakampinga Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na wakamchinja Ngamia.
Walivuka mpaka katika kiburi chao, wakaitupilia mbali amri ya Mola wao Mlezi, na
wakasema kwa upinzani: Ewe Saleh! Tuletee hiyo adhabu uliyo tuahidi ikiwa kweli
wewe ni miongoni ya alio watuma Mwenyezi Mungu.
78. Tetemeko la
nguvu lilikuja kuwanyakua, na kulipo pambazuka wakawa wote
wamekwisha jifia majumbani mwao wamejifudikiza kifudifudi.
79. Na kabla ya
kuwateremkia adhabu hiyo ndugu yao Saleh aliwaachilia mbali (kwa kukata tamaa
nao), akawaambia: Enyi watu wangu! Mimi nimekufikishieni amri na makatazo ya
Mola Mlezi wangu. Na nimekusafieni nasaha yangu, lakini nyinyi kwa ushindani
wenu na ushupavu wenu, mmekuwa hamumpendi anaye kunasihini!
80. Na hakika tulimtuma
Nabii wa Mwenyezi Mungu, Lut', kwa kaumu yake; awaite wafuate Tawhidi, yaani
ibada ya Mwenyezi Mungu mmoja. Na awazindue juu ya waajibu wa kuachana na makosa
maovu kabisa waliyo kuwa wakiyafanya. Aliwaambia: Nyinyi mnakwenda kufanya jambo
lilio pita mpaka kwa ubaya wake, kinyume na maumbile? Mmezua uchafu huo ambao
unapingana na khulka, na ambao hapana watu walio kutangulieni walio fanya hayo!
81. Na jambo hilo ni kuwa
mnawaendea wanaume kwa kuwatamani, na mnawawacha wanawake! Nyinyi kwa jambo hili
inakuwa mnafanya fujo, na mmetoka nje ya maumbile, na mmefanya kitendo asicho
fanya hata mnyama.
82. Na haikuwa jawabu ya
watu wake kwa kukatazwa hichi kitendo kiovu kisicho kuwa na mfano, ila ni
kusema: Watoeni Lut' na jamaa zake na wafuasi wake katika mji wenu! Nayo ni kwa
kuwa wao wanajitahirisha na wanajitenga na hichi kitendo ambacho akili na
maumbile yanakiona ni kibaya, na wao hao watu wanakioni kizuri!
83. Amri ya kuadhibiwa
ilikwisha thibiti. Basi Sisi tukamwokoa Lut' na watu wake, isipo kuwa mkewe,
kwani yeye alikuwa katika hao walio potea.
84. Basi tuliwateremshia
mvua ya mawe ya kuteketeza, na ardhi ikatandazwa kwa mitetemeko ya chini yao!
Basi ewe Nabii! Angalia vipi ulikuwa mwisho wa wakosefu.
85. Na kwa watu wa Madyana
tulimtuma ndugu yao, Shua'ib. Akasema: Enyi watu wangu! Muabuduni Mwenyezi Mungu
peke yake. Kwani nyinyi hamna mungu isipo kuwa Yeye. Hoja zilizo wazi za
kuthibitisha Haki inayo toka kwa Mola Mlezi wenu juu ya Utume wangu kwenu
zimekwisha kujieni. Na umekujieni Ujumbe wa Mola wenu Mlezi kwamba mtengeneze
kwa uadilifu maingiliano yenu nyinyi kwa nyinyi. Basi timizeni vipimo na mizani
mnapo uziana, wala msipunguze haki za watu, wala msiiharibu nchi nzuri, kwa
kufisidi mapando na kadhaalika, na kuwatenga jamaa na kuondoa mapenzi. Kwani
hayo ni bora kwenu mkiwa mnamuamini Mwenyezi Mungu Mtukufu, na mnaamini Haki
iliyo wazi.
86. Wala msikae katika
kupinga kila njia za Haki na uwongofu na a'mali njema, mkiwatishia wapitao, na
kwa hivyo mkawazuia watafutao kheri wasiifikie. Nao hao ndio watu wa Imani wanao
muamini Mwenyezi Mungu, nanyi mnaitaka njia iliyo potoka! Na kumbukeni mlivyo
kuwa ni watu wachache, Mwenyezi Mungu akakufanyeni mkawa wengi kwa kwenda sawa
kutaka uzazi na mali. Na zingatieni nini ulikuwa mwisho wa waharibifu walio kuwa
kabla yenu.
87. Ikiwa kipo kikundi
kati yenu kilicho amini Haki niliyo kuja nayo, na kikundi kingine hakikuamini,
basi ngojeni mpaka Mwenyezi Mungu alete hukumu yake baina ya pande mbili hizo.
Naye ndiye Mbora wa mahakimu.
88. Hii ni khabari ya
Shua'ib katika wito wake kuwalingania kaumu yake. Ama hao kaumu yake walikuwa
wamemili juu ya upotovu. Na wale wakubwa wao walio takabari waliukataa wito, na
wakaona ni uvunjifu kuifuata Haki. Wakamkabili Shua'ib kumwambia dhamiri yao kwa
kusema: Hakika hapana vingine ila tukutoe wewe na hao walio amini pamoja nawe
katika mji wetu. Na tutakufukuzeni, wala hamtasalimika na adhabu hii ila
mkirejea katika hii dini yetu mliyo iacha. Shua'ib a.s. akawajibu kwa kusema:
Turejee katika mila yenu na hali sisi tunaichukia kwa uharibifu wake? Hayawi
hayo abadan!
89. Akaendelea zaidi
kuwavunja tamaa yao ya kuwarejeza kwenye mila yao kama walivyo taka. Akasema:
Tutakuwa tunamzulia uwongo Mwenyezi Mungu tukiwa katika mila yenu baada ya
Mwenyezi Mungu kesha tuhidi kwenye Njia Iliyo Nyooka. Na haifai sisi kuwa katika
mila yenu kwa khiari yetu na kutaka kwetu, ila akipenda Mwenyezi Mungu turejee
katika mila yenu. Na hayo hayawi! Kwa sababu Mola Mlezi wetu anatujua vyema, na
Yeye hataki turejee kwenye upotovu wenu. Yeye aliye tukuka shani yake amekienea
kila kitu kwa ujuzi wake. Anatuongoa kwa upole wake na hikima yake kwenye jambo
litalo tuhifadhia Imani yetu. Kwa Yeye peke yake ndio tumesalimisha mambo yetu,
na huku tunashikilia yale aliyo tuwajibisha tuyashike. Ewe Mola Mlezi wetu!
Tutenge sisi na hao kaumu yetu kwa Haki, kama ilivyo kuwa mwendo wako unavyo
amua baina ya wenye kufuata Haki na wakatenda mema, na wale wapotovu waharibifu.
Na Wewe kwa kuwa ujuzi wako na uwezo ulivyo enea ndiye Muadilifu na Muweza
kuliko mahakimu wote.
90. Hapo basi wale watu
walikata tamaa ya kuwafanya Shua'ib na walio kuwa naye wawafuate wao. Na wakajua
kuwa hakika hao walikuwa wamethibiti katika Dini yao. Kadhaalika waliogopa
wasizidi kuwa wengi wale walio hidika pamoja na Shua'ib kwa kudhihiri nguvu zake
na kuthibiti kwake juu ya wito wake. Kwa hivyo wale waheshimiwa wa kikafiri
wakawaelekea wafwasi wao wakiwatisha kwa kusema: Wallahi! Mkimfuata Shua'ib
mkakubali wito wake, basi hapana shaka nyinyi utakutokeni utukufu wenu na
utajiri wenu kwa kufuata dini potovu wasio kuwa wakiifuata wazee wenu.
91. Basi hapo kauli ya
kuteremka adhabu ikawa imethibiti. Wakasibiwa kwa tetemeko lilio tikisa nyoyo
zao, wakawa katika majumba yao wamesinukia kifudifudi hawana tena uhai.
92. Hii ndio shani ya
Mwenyezi Mungu na hao walio mkanusha Shua'ib, na wakamtishia, na wakamwonya kuwa
watamfukuza katika mji wao, na wakafanya kila kitu kuupinga wito wake.
Wamehiliki wao na ukahiliki mji wao, ikawa kama kwamba humo hawakuwahi kuishi
wale walio mkadhibisha Shua'ib na wakadai kuwa ati atakaye mfuata atakuwa
amekhasiri, na wakatilia nguvu madai hayo. Na lililo kuwa ni kuwa wao ndio walio
poteza neema yao ya dunia na Akhera.
93. Shua'ib alipo ona
hilaki ya kuvuruga iliyo wateremkia wale watu, basi aliwaachilia mbali, na
akasema kujivua nafsi yake asiwe mkosa pamoja nao: Mimi nimekufikishieni ujumbe
wa Mola wenu Mlezi unao pelekea mpate wema nyinyi, lau kuwa mngeli ufuata. Na
mimi nimefanya ukomo wa uwezo wangu katika kukunasihini, na kukuwaidhini kwa
mambo ya kukuokoeni na adhabu ya Mwenyezi Mungu. Basi vipi tena niwasikitikie
mno watu makafiri? Hayawi hayo baada ya kuwa mimi nimekwisha jiudhuru kwao, na
nikatumia juhudi yangu kwa ajili ya kutaka kuwahidi na kuwaokoa, na wao
wakakhiari kufuata yale yale ya kuwahiliki.
94. Na Sisi hatukumpeleka
Nabii yeyote kwenye mji akawalingania watu wake wafuate Dini ya Mwenyezi Mungu
iliyo sawa, na wao wakakataa kuukubali huo wito, ila tuliwapatiliza kwa ufakiri
na maradhi, ili wapate kuwa wanyonge na wamwombe Mwenyezi Mungu kwa unyenyekevu,
na kumsafia niya wapate kuondokewa na balaa na wamuitikie Mtume wake.
95. Basi tena ilivyo kuwa
hawakufanya hayo, bali wakaendelea na ukafiri wao na inadi yao, tukawapa mtihani
wa kuwapa neema badala ya dhiki ili kuwapururia tu. Tukawapa kutononoka, na
nafasi nzuri, na siha na afya, mpaka wakawa wengi, na mali yao yakazidi,
wakasema kwa ujinga wao: Hayo yaliyo wapata baba zetu ya mahna, na balaa, na
starehe na neema - hayo yote ndio shani ya ulimwengu. Shida na neema huwajia
watu kwa zamu. Hawakuzindukana wakajua kuwa haya ni malipo ya kufru zao
wakajizuia! Na kwa hivyo wakawa hawaujui mwendo wa Mwenyezi Mungu, iliyo tukuka
shani yake, katika sababu za matengenezo na uharibifu wa binaadamu, na nini
linalo leta neema na nini linalo leta dhiki! Matokeo ya hayo ni kuwa Mwenyezi
Mungu aliwapatiliza kwa kuwaletea adhabu ya kuteketeza kwa ghafla, na wao bila
ya kujua nini litawafika.
96. Na lau kuwa watu wa
hiyo miji wangeliamini walio kuja nayo Mitume, na wakatenda walio wausia, na
wakajitenga na aliyo yaharimisha Mwenyezi Mungu, tungeli wapa baraka nyingi
zitokazo mbinguni na kwenye ardhi, kama mvua, na mimea, na matunda, na wanyama,
na riziki, na amani na kusalimika na misiba. Lakini wao wakapinga na
wakawakadhibisha Mitume. Basi tukawapatiliza kwa adhabu nao wamelala, kwa sababu
ya ukafiri na maasi waliyo yazua. Basi huko kushikwa waliko shikwa kwa adhabu ni
matokeo ya lazima kuwa kwa ajili ya maovu waliyo yachuma, na yawe kuwa ni somo
kwa walio kama wao ikiwa wanayatia akilini!
97. Je, watu wa hii miji
walio letewa wito wa Manabii wao na wasiwaamini, wamejiaminisha kuwa adhabu yetu
haitawafika nao wamezama katika usingizi wao?
98. Je, watu hawa
wameghafilika na wamejiaminisha kuwa adhabu haitawajia mchana kweupe na jua
linawaka, nao wameshughulikia mambo yasiyo na faida nao?
99. Je, hawaujui mwendo wa
Mwenyezi Mungu anavyo kwenda nao wanao kanusha, hata wakajitumainisha kuwa
haitowafikia adhabu usiku au mchana? Naye, huipeleka kwa mpango wake wasio uona
watu. Hakika hawawi wajinga wa mpango na mwendo wa Mwenyezi Mungu katika
kuadhibu ila wale wanao kanusha, wenye kuzikhasiri nafsi zao kwa kutozinduka
katika mambo yaliyo khusu kufanikiwa kwao.
100. Je, hawaujui mwendo
wa Mwenyezi Mungu kwa kaumu zilizo kwisha pita kabla yao, na kuwa shani yetu
kwao ni kama ilivyo kuwa kwa walio watangulia? Na kwamba wao lazima wafuate
tuyatakayo. Tukitaka kuwaadhibu kwa sababu ya madhambi yao tutawapatiliza kama
tulivyo wapatiliza walio kama wao. Nasi tunatia muhuri nyoyo zao kwa kuwa
zimeharibika bila ya kiasi, mpaka ikafika ukomo kuwa hazipokei tena uwongofu.
Kwa muhuri huo imekuwa hawasikii hikima wala nasiha, kwa msikio wa kufahamu na
kuwaidhika.
101. Hiyo ni miji iliyo
dumu karne nyingi, na imepitiwa na muda mrefu katika taarikhi yao. Tunakusimulia
hivi sasa baadhi ya khabari zao zenye somo la kuzingatiwa. Na watu wa miji hiyo
walifikiwa na Mitume wao kwa Ishara zilizo wazi zenye kuonyesha ukweli wa wito
wao. Lakini haikuwa shani yao kuamini baada ya kuja hizo Ishara zilizo wazi, kwa
sababu ya mtindo wao wa kuwakanusha wasemao kweli. Basi wakawakadhibisha Mitume
wao, wala hawakuongoka! Basi ni hivyo Mwenyezi Mungu huweka kizuizi juu ya nyoyo
na akili za makafiri, ikafichika kwao Njia ya Haki, na wakajitenga nayo.
102. Wala hatukuwakuta
wengi wa watu hao kuwa ni wenye kutimiza ahadi kwa Imani tulio wausia kwa ndimi
za Mitume, na yanayo tambuliwa na akili na nadhari nzuri. Na mwendo ulio thibiti
kwao ni vile kuselelea katika upotofu na kwenda kinyume na kila ahadi.
103. Tena baada ya Mitume
hao tulimtuma Musa a.s. Naye akaja na dalili zenye kuonyesha ukweli wa anayo
yafikisha kutokana nasi kumpelekea Firauni na kaumu yake. Musa akaufikisha
wito wa Mola wake Mlezi, na akawaonyesha Ishara ya Mwenyezi Mungu. Nao
wakadhulumu nafsi zao na watu wao kwa kuzikataa kwa kiburi na upinzani tu! Basi
wakastahiki adhabu kali kutokana na Mwenyezi Mungu, na hivyo ukawa mwisho wa
mambo yao! Basi ewe Nabii! Angalia vyema mwisho wa mafisadi katika ardhi.
104. Musa akasema: Ewe
Firauni! Hakika mimi nimetumwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe
vyote, Mwenye mamlaka juu ya mambo yao yote, ili nikufikishieni wito wake, na
nikuiteni muifuate Sharia yake.
105. Na mimi pupa yangu
ni kumsemea kweli Mwenyezi Mungu Mtukufu. Na nimekujieni na Ishara yenye shani
kubwa, yenye hoja iliyo dhaahiri katika kubainisha Haki niliyo kuja nayo. Basi
waachilie waje nami Wana wa Israili, na uwatoe kwenye utumwa wa kahari
yako, wende nami kwenye nchi nyengine isiyo kuwa yako, na huko wapate kumuabudu
Mola Mlezi wao na wako.
106. Firauni akamwambia
Musa: Ikiwa umekuja na Ishara (muujiza) kutokana na huyo aliye kutuma, basi
nionyeshe kama wewe ni katika watu wakweli wanalo lishika neno la haki.
107. Kiasi ya Musa
kuitupa fimbo aliyo kuwa nayo mkononi mwake wa kulia mbele ya Firauni, mara hiyo
fimbo ikawa nyoka khasa dhaahiri, anakwenda mbio huku na huku, kwa nguvu zinazo
onyesha kuwa ana uhai timamu.
108. Akautoa
mkono wake kutoka mfukoni mwake, na hapo hapo ukawa mweupe safi
kabisa ukimeremeta katika macho ya wanao angalia!
109. Musa alipo ionyesha
Ishara ya Mwenyezi Mungu Mtukufu, zilitibuka roho za wapambe wa Firauni na
waheshimiwa wa kaumu yake, wakasema katika kujipendekeza kwa Firauni na
kumtetea: Hakika huyu ni bingwa katika ilimu ya uchawi, wala hii si Ishara
itokayo kwa Mwenyezi Mungu!!
110. Na yeye
ameelekeza lengo lake akupokonyeni ufalme wenu, na akutoeni katika nchi yenu kwa
uchawi wake na yatayo tokea hapo kwa kuwavutia watu wamili na wamfuate. Basi
tazameni, mnaamrisha njia gani ya kutokana naye huyu?
111. Wakasema: Akhirisha
kukata shauri juu yake na nduguye huyu anaye msaidia katika wito wake, na watume
watu katika askari wako wende katika miji ya ufalme wako wawakusanye walio
mafundi katika ilimu ya uchawi.
112.
Wakuletee kila mwanachuoni wa ilimu za uchawi. Na wao watakufichulia
nini khasa hakika ya aliyo kuja nayo Musa, asije akafitinika yeyote.
113. Basi wakaja kwa
Firauni wachawi walio kusanywa na askari wake. Nao wakasema: Hapana shaka nasi
tutapata malipo makubwa yanayo lingana na hili linalo takikana kwetu, ikiwa sisi
tutamshinda Musa.
114. Haraka haraka
Firauni akawajibu kwa walitakalo: Naam! Hapana shaka mtapata malipo makubwa. Na
hapana shaka juu ya hayo nyinyi mtakuwa watu wenye cheo kwangu.
115. Kisha wachawi
wakamgeukia Musa, baada ya Firauni kuwaahidi alivyo waahidi, na wao wakaonyesha
wana imani na nafsi zao na kujitayarisha kwao kwa uchawi wao katika uwanja wa
mapambano. Wakamwabia: Ama utupe ulicho nacho kwanza, au sisi tuwe wenye kutupa
tulicho nacho.
116. Musa akwajibu
jawabu ya mwenye imani ya kushinda, akionyesha kutowabali: Tupeni nyinyi kwanza
hicho mnacho tupa. Walipo tupa kila mmoja wao, navyo ni kamba na fimbo, macho ya
watu yalizugwa, na ikawapitikia kuwa walicho kifanya kile ni hakika kweli. Na
hali haikuwa ila ni kiini macho tu. Mambo yale yaliwatisha watu, na nyoyo zao
zikaingia khofu na kitisho. Kwani wachawi wale waliwaletea watu uchawi unao
onekana ni mkubwa, na athari yake katika macho yao ni kubwa!
117. Mwenyezi Mungu
akaitoa amri yake kumpelekea Musa: Tupa fimbo yako. Sasa umekwisha fika wakati
wake. Akaitupa kama alivyo amrishwa. Mara hiyo fimbo ikaingia kuvimeza vile
vizushi vyao walivyo zua na kubuni!
118. Basi Haki
ikathibiti na kudhihiri upande wa Musa a.s. na ukabwatika
udanganyifu wa wachawi.
119. Firauni na
waheshimiwa wake wakashindwa katika ule mkutano mkubwa, na wakawa madhalili
mbele ya watu wote kwa masaibu yaliyo wapata, nayo ni kuvunjika moyo na
kukata tamaa.
120. Haya ni mambo
yaliyo wafika Firauni na waheshimiwa wake. Ama wale wachawi Haki iliangaza kwao,
na wakaanguka kwa kumsujudia Mwenyezi Mungu nao wanainyenyekea Haki.
121. Huku wakisema hao
wachawi walio tubia: Tumemuamini Muumba wa viumbe vyote, Mwenye kumiliki
na kuendesha mambo yao yote.
122. Hakika
huyo ndiye Mungu anaye itakidiwa na kuaminiwa na Musa na
Haarun.
123. Jambo hili
lilimtisha Firauni na ikafoka ghadhabu yake, akasema: Hivyo nyinyi mmemuamini na
kumsadiki Mola Mlezi wa Musa na Haarun kabla sijakupeni ruhusa mimi?
Hakika hapa pana kijambo mmekizua nyinyi na Musa na Haarun kwa kuwafikiana. Na
haya si chochote ila ni vitimbi mlivyo vipanga katika mji wa Misri mpate kuwatoa
wenyewe kwa hila yenu. Basi ngojeni, mtaiona adhabu itayo kushukieni kuwa ndio
jaza yenu kwa kumfuata Musa na Haarun, na ndio adabu yenu kwa hivi vitimbi
vyenu na khadaa!
124. Na ninakuapieni
kuwa nitakuteseni vikali, na nitakukateni mikono yenu na miguu yenu mbali mbali,
nitakata mkono wa upande mmoja na mguu wa upande wa pili, kisha nitakutundikeni
misalabani, kila mmoja wenu, nanyi mmo katika hali hiyo, ili muwe ni
zingatio kwa anaye jifikiria kutufanyia vitimbi, au kutaka kuufanyia uasi
utawala wetu!
125. Nao hawakuibali
kauli yake wala vitisho vyake, kwa kuwa Imani ilikwisha saki ndani ya nyoyo zao.
Wakamwambia: Hakika sisi ni wenye kurejea kwa Mola wetu Mlezi. Kwa hivyo
tunaneemeka katika rehema yake na bora ya malipo yake.
126. Na wewe hutuchukii
na kutuadhibu ila kwa kuwa tumemsadiki Musa, na tumezikubali zilipo tujia Ishara
za Mola wetu Mlezi zilio wazi, zenye kuonyesha Haki! Kisha wakamuelekea Mwenyezi
Mungu kwa unyenyekevu, wakisema: Ewe Mola Mlezi wetu! Tumiminie subira kubwa,
itupe nguvu kuhimili shida zote; na utufishe katika Uislamu bila ya kuteseka kwa
anayo tuahidi Firauni.
127. Baada ya Firauni na
watu wake kuona waliyo yaona, katika vile kudhihiri mambo ya Musa na nguvu za
ushindi wake, na wachawi wakamuamini, walisema wakuu wa kaumu yake: Unamuacha
Musa na watu wake wawe huru katika amani, ili mwisho wao wawafisidi kaumu yako
dhidi yako katika nchi ya Misri kwa kuwatia katika dini yao, na wakuache wewe na
miungu yako bila ya wao kujali? Hapo watu wa Misri watakuona wewe na hiyo miungu
kuwa mmeshindwa. Firauni akasema kuwajibu: Tutawawauwa watoto wao wa kiume wa
watu hawa, kila anaye zaliwa; na tutawabakisha wa kike wawe hai, ili wasiwe na
nguvu, kama tulivyo fanya zamani. Na sisi tuko juu yao kwa kuwashinda na
kwa utawala, na kuwafanyia kahari.
128. Na hapo Musa aliona
kama dalili za huzuni katika watu wake, basi akawatia nguvu katika azma yao.
Akawambia: Mtakeni Mwenyezi Mungu msaada na kukuungeni mkono. Na kuweni imara,
wala msifazaike. Kwani ardhi yote imo katika nguvu za uwezo wa Mwenyezi
Mungu na ufalme wake. Humrithisha amtakaye katika waja wake, wala si ya Firauni.
Na mwisho mwema wataupata wale wanao mcha Mwenyezi Mungu kwa kushikamana naye na
kuzikamata hukumu zake.
129.
Wakasema wale watu kwa huzuni na unyonge: Sisi tulipata maudhi zamani
kutoka kwa Firauni kabla hujatujia, na hivi sasa tena baada ya kuja kwako. Musa
akawafungulia mlango wa matarajio mema kwa kuwaambia: Hakika linalo tarajiwa kwa
fadhila za Mola wenu Mlezi ni kumteketeza adui yenu, aliye kufanyeni watumwa na
akakuteseni kwa dhulma yake, na akujaalieni nyinyi ndio wa kuimiliki ardhi aliyo
kuahidini. Yeye Subhanahu, Aliye takasika, anayajua mnayo yatenda baada ya
kukuwekeni huku. Je, mtaishukuru neema au mtaikufuru? Na mtatenda mema katika
nchi au mtafanya fisadi? Hayo ili apate kukulipeni duniani na Akhera kwa mujibu
wa mtendayo.
130. Na hakika Sisi
tuliwaadhibu Firauni na watu wake kwa ukame, na dhiki ya maisha, na upungufu wa
matunda na mazao na miti, kwa kutaraji kuwa watazindukana wautambue unyonge wao,
na kushindwa ufalme wao wa jeuri mbele ya nguvu za Mwenyezi Mungu, wapate
kuwaidhika na waache kuwadhulumu Wana wa Israili, na wauitikie wito wa Musa a.s.
Kwani mtindo wa shida ni kuzuia kujidanganya, na kutengeza tabia, na kuzielekeza
nafsi ziikubali Haki, na kumridhi Mola Mlezi wa viumbe vyote, na
kumnyenyekea Yeye tu, si mwenginewe.
131. Lakini tabia ya
Firauni na wasaidizi wake ni kuto thibiti juu ya Haki. Wepesi kurejea kwenye
khiana na uasi. Hao ni watu wa kigeugeu! Ikiwajia kutononoka na neema - na mara
nyingi huwa hivyo - wao wakisema: Sisi tunastahiki haya tuliyo nayo kuwapita
watu wengineo! Na likiwasibu la kuwaudhi, kama ukame, au tauni, au msiba wa
miili au riziki, wakiona yamewapata hayo kwa ukorofi wa Musa na walio pamoja
naye. Na wanaghafilika kuwa dhulma zao, na fisadi zao ndizo zilizo pelekea kuja
hayo yanayo wapata! Basi na watanabahi, na wajue kuwa ujuzi wa ukorofi wao uko
kwa Mwenyezi Mungu. Yeye ndiye anaye wapatiliza kwa sababu ya vitendo vyao
viovu. Yeye ndiye anaye wapelekea hayo yanao waudhi, wala si Musa na alio nao.
Lakini wengi wao hawaijui Hakika ambayo haina shaka.
132. Na kwa hii fikra
mbovu waliyo nayo wakaendelea na upinzani. Walisema walipo ona miujiza ya Musa:
Wewe hata ukituletea kila namna ya Ishara zinazo onyesha ukweli wa wito wako,
ili kutuachisha dini yetu, na tusiwafanye watumwa watu wako, sisi hatukusadiki
wala hatukufuati.
133. Basi Mwenyezi Mungu
aliwateremshia masaibu na balaa zaidi, kama tufani lilio funika mwahala
mwao, na nzige walio kula kila mmea na mti ulio bakia, na chawa, yaani vijidudu
vinavyo haribu matunda na kuteketeza wanyama na mimea. na vyura vilivyo enea
vikafanya maisha yao dhiki, na vikachafua kila pahala, na damu iliyo sabibisha
maradhi mengi, kama kupasuka mishipa ya damu katika mwili, na damu inayo
najisisha kila pahala ikasabibisha presha, au kupasuka ikaleta kiharusi na
kupooza, na kutokwa na mkojo wa damu kwa sababu ya kichocho na mfano wake, au
ikawa inachanganyika na maji yao wanayo hitajia kunywa au kupikia. Mwenyezi
Mungu aliwapatiliza na Ishara hizi zote zilio wazi! Nao wasiathirike, nyoyo zao
zikabaki kuwa ngumu, na wenye kutakabari hawataki Imani wala kurejea kwenye
Haki. Walikuwa watu walio bobea kwenye madhambi na ukosefu, kama ilivyo ada yao.
134. Katika kuzidi
kigeugeu chao kama zinavyo badilika sababu, walikuwa kila ikiwashukia namna
yoyote ya adhabu wakisema kwa shida na machungu yanayo wapata: Ewe Musa! Tuombee
kwa Mola Mlezi wako, kwa vile alivyo kuahidi kuwa ukimwomba atakupa
miujiza na atakuitikia dua, atuondolee adhabu hii. Na sisi tunakuapia kuwa
ukituondolea basi bila ya shaka tutakuitikia na tutawaachilia wende nawe Wana wa
Israili kama ulivyo taka!
135. Tulipo waondolea
adhabu kila mara kwa muda wao mpaka mwisho wake ukisha huivunja ahadi yao, na
huenda kinyume na kiapo chao, na hurejea yale yale waliyo kuwa nayo. Kwao wao
hayo majaribio ya kuwaachisha maovu hayakuleta faida!
136. Tuliwateremshia
nakama yetu. Tukawazamisha baharini kwa sababu ya kushikilia kwao kukanusha
Ishara zetu, na hadi ya kutoyabali mafunzo ya Imani na ut'iifu yaliyomo katika
hizo Ishara.
137. Tukawapa watu ambao
walikuwa wakidharauliwa katika Misri, nao ni Wana wa Israili, ardhi alio ipa
baraka Mwenyezi Mungu kwa kuifanya ina rutba na kheri nyingi, tangu mashariki
mpaka magharibi yake. Neno jema la Mwenyezi Mungu likatekelezwa kwa ukamilifu,
na pia ahadi yake ya ushindi kwa Wana wa Israili, kwa sababu ya kuvumilia kwao
dhiki. Na tukayateketeza majumba ya fakhari, na kila majenzi, na chanja za mimea
ya kutambaa, na bustani, na pandio za mizabibu, waliyo kuwa wakisimamisha na
kujenga akina Firauni na watu wake! Hiyo ndiyo shani ya Mwenyezi Mungu, na
ametimiza kweli ahadi yake kwa Wana wa Israili.
138. Wana wa
Israili wakaivuka bahari kwa uangalizi wetu, na kuwaunga mkono na kuwafanyia
mepesi mambo yao. Baada ya kwisha vuka waliwakuta kaumu wameshika ibada ya
masanamu. Walipoona hivi yale waliyo kuwa wameyazoea kuwaona Wamisri wakiabudu
masanamu yaliwaghilibu, wakamtaka Musa awafanyie nao masanamu wayaabudu, kama
ilivyo kuwa wale kaumu wana masanamu yao wanayo yaabudu! Hapo hapo Musa a.s.
aliwatahayarisha na kuwakanya, akasema: Hakika nyinyi ni watu wapumbavu, msio na
akili! Hamjui ibada ya Haki, wala hamumjui Mungu anaye stahiki kuabudiwa!
139. Hawa mnao waona
wanaabudu masanamu, hapana shaka haya walio nayo ni yenye kuangamia, na hii dini
waliyo nayo ni potovu , bure bilashi. Na a'mali zao ni zenye kupotea, wala
hazibaki.
140. Je, nikutafutieni
wa kuabudiwa asiye kuwa Mwenyezi Mungu Mola Mlezi wa viumbe vyote, na Yeye ndiye
aliye kupeni fadhila, na akakupeni neema asio pata kupewa mwengine asiye kuwa
nyinyi katika zama zenu?
141. Kumbukeni alipo
kuvueni Mwenyezi Mungu Mtukufu kwa uangalizi wake na watu wa Firauni, walio kuwa
wakikuadhibuni ukomo wa adhabu, wakikudhalilisheni muwatumikie katika kazi
ngumu, wala hawakukuoneeni huruma kama wanyama, wakiuwa wavulana wenu na
wakiwabakisha wasichana ili mzidi kudhoofika kwa wingi wa wanawake! Na katika
adhabu za Firauni zilizo kushukieni, na kukuvueni nazo, pana mtihani mkubwa wa
Mola wenu Mlezi, wala hapana mfano wake.
142. Tulimuahidi Musa
tutazungumza naye na tutampa Taurati baada ya kutimia masiku (wingi wa "usiku")
thalathini ya yeye kuabudu. Na tukauongeza muda huo kwa masiku kumi, kutimiza
ibada. Yakawa masiku arubaini. Musa akamwambia nduguye Haarun alipo kuwa
anakwenda kuzungumza na Mwenyezi Mungu: Kuwa badala yangu kwa hawa watu wangu.
Na watengenezee mambo yao yanayo hitajia kutengenezwa. Na tahadhari na kufuata
njia ya mafisadi. (Angalia: Kwa Kiswahili safi, "Masiku" ni wingi wa
"Usiku". Ama wingi wa "Siku" ni "Siku" vile vile kama ilivyo katika aghlabu ya
maneno mengine yanayo anzia "S", kama Saa, Sanda, Sahani, Sabuni, Safari,
Sufuria n.k.)
143. Na alipo kuja Musa
kuzungumza nasi, na Mola Mlezi wake akanena naye kwa maneno ambayo siyo kama
kusema kwetu, Musa alisema: Ewe Mola Mlezi wangu! Nionyeshe dhati yako na
unidhihirikie, nipate kukutazama nizidi utukufu. Mwenyezi Mungu akasema: Huwezi
kuniona. Kisha Subhanahu, Aliye takasika alitaka kumkinaisha kuwa hawezi
kumwona, akamwambia: Walakini utazame huo mlima ambao una nguvu kuliko wewe.
Ukithibiti pahala ulipo wakati wa kudhihiri kwangu, basi utaniona
nikijidhihirisha kwako. Basi Mola wake Mlezi alipo jionyesha kwa huo mlima kwa
njia inayo wafikiana naye Mtukufu, mlima ulivurugika ukawa sawa sawa na ardhi.
Musa akaanguka, kazimia kwa kitisho alicho kiona. Alipo zindukana kutokana na
kuzimia kwake alisema: Nakutakasa mtakaso mkuu na kuonekana kwako duniani!
Hakika mimi ninatubu kwako kuja kukutaka kitu bila ya ruhusa yako. Na mimi ni wa
mwanzo katika zama zangu wa wanao amini utukufu wako na ubora wako.
144. Mwenyezi Mungu
alipo mzuilia Musa asimwone, akaingia kumhisabia neema zake ili amliwaze kwa
vile kumkatalia, akamwambia: Ewe Musa! Mimi nimekufadhilisha, na nimekuteua
kuliko watu wote wa zama zako, ili ufikishe vitabu vya Taurati, na kwa kusema
nawe bila ya kuwapo mtu kati. Basi yashike hayo niliyo kukufadhili, na
unishukuru kama wafanyavyo wenye kushukuru, wanao kadiri neema.
145. Na tulimbainishia
Musa katika zile mbao za Taurati kila kitu kilicho khusu mawaidha na hukumu
zilizo elezwa mbali mbali, wanazo hitajia watu duniani na Akhera. Na
tukamwambia: Zishike hizi mbao baraabara na kwa kuazimia. Na waamrishe
watu wako washike yaliyo bora humo, kama kusamehe badala ya kulipiza kisasi, na
kuachilia badala ya kungojea, na kulegeza badala ya kukaza. Enyi kaumu ya Musa!
Nitakuonyesheni katika vitabu vyenu makaazi ya wale wanao asi amri za Mwenyezi
Mungu, na watavyo angamia, ili mpate kuzingatia. Basi msende kinyume
yakakusibuni yalio wasibu hao waasi.
146. Hao walio majeuri
na wakapanda kiburi katika ardhi wakakataa kukubali yaliyo sawa bila ya haki,
nitawazuia wasiweze kuzizingatia dalili za uwezo wangu ziliomo katika nafsi za
watu na jiha zote. Watu hawa hata wakiona kila Ishara inayo thibitisha
ukweli wa Mitume wetu hawaisadiki. Na wakiiona njia ya uwongofu hawaipiti, na
wakiiona njia ya upotofu ndio wanaipita! Hayo yanatokea kwao kwa sababu
wamezikanusha Ishara zetu zilio teremshwa, na wameghafilika na kuongoka kwazo.
147. Na walio zikanusha
Ishara zetu zilio teremshwa juu ya Mitume wetu kwa ajili ya uwongofu, na
wakakanusha kukutana nasi Siku ya Kiyama, wakakataa kufufuliwa na kulipwa,
vitendo vyao walivyo kuwa wakitarajia viwafae vitapotelea mbali. Hawatokuta ila
malipo ya kufru na maasi waliyo endelea nayo kuyatenda.
148. Na baada ya Musa
kwenda kwenye mlima kusema na Mola Mlezi wake, kaumu yake walichukua vyombo vyao
vya kujipamba wakatengeneza Sura ya ndama, asiye na akili wala hatambui kitu.
Lakini akitoa sauti mfano wa sauti ya ng'ombe, kwa namna walivyo muunda na
ukipita upepo ndani yake. Na aliye waundia ni Saamiriyu (Msamaria). Naye
akawaamrisha wamuabudu! Upumbavu gani huu wa akili zao! Hivyo wao walipo mfanya
ndiye mungu wakamuabudu, hawakuona kuwa hawasemezi, wala hawezi kuwaongoa
wafuate njia iliyo sawa? Hakika hawa wamejidhulumu nafsi zao kwa kitendo hichi
kiovu.
149. Walipo tambua
kuteleza kwao, na makaso yao, wakababaika, na wakajuta majuto makubwa kwa
kumfanya ndama ndiye mungu. Makosa yao yakabainika wazi, wakasema: Wallahi!
Ikiwa Mola wetu Mlezi hakutusamehe hakika tutakuwa miongoni walio khasiri
khasara iliyo dhaahiri; kwa vile kuabudu kisicho faa kuabudiwa.
150. Na Musa alipo rejea
kutoka kuzungumza na Mola Mlezi wake kuja kwa watu wake, naye kakasirika nao kwa
vile walivyo muabudu ndama, na amehuzunika kwa kuwa Mwenyezi Mungu amewatia
mtihanini - kwani Mwenyezi Mungu alikwisha mpa khabari ya yale kabla hajarejea -
aliwaambia: Kitendo gani kiovu hichi mlicho kitenda baada ya kuondoka kwangu!
Mmetangulia kwa kumuabudu ndama msifuate amri ya Mola wenu Mlezi kuwa mningojee,
na mkawa hamkuishika ahadi yangu mpaka nikakuleteeni Taurati? Akaziweka zile
mbao, na akamuelekea nduguye kwa huzuni kubwa kwa yale aliyo yaona kwa kaumu
yake. Akaingia kumvuta ndugu yake kwa kichwa akimbururia kwake kwa wingi wa
ghadhabu. Haya ni kuwa alidhani kuwa amefanya taksiri hakuwazuia kufanya walio
yafanya! Haarun akasema: Ewe mwana wa mama yangu! (1) Hakika hawa watu walipo
fanya waliyo yafanya walinidharau na wakanishinda nguvu. Na wakakaribia kuniuwa
kwa kuwa niliwakataza wasimuabudu ndama. Basi usiwafurahishe maadui kwa kunitesa
mimi, wala usiitakidi kuwa mimi ni mmoja wa wenye kudhulumu, kwani mimi ni mbali
nao na dhulma yao.
(1) Haarun
amemwita Musa kwa kumnasibisha na mama yao, ijapo kuwa hao walikuwa ndugu
khalisa, wa baba na mama, kwa sababu huyo mama alikuwa Muumini. Kumtaja yeye ni
kuzidi kukumbusha mapenzi.
151. Musa alisema: Ewe
Mola wangu Mlezi! Nisamehe kwa haya niliyo mfanyia ndugu yangu kabla sijayajua
mambo. Na msamehe ndugu yangu ikiwa kakosea katika kushika pahala pangu kwa
vizuri. Na tuingize katika eneo la rehema yako, kwani Wewe ndiwe Mwenye rehema
nyingi kushinda wote wenye kurehemu.
152. Hakika wale walio
endelea kumfanya ndama kuwa mungu, kama Msamaria na wenziwe, itawafika ghadhabu
kubwa kutoka kwa Mola wao Mlezi huko Akhera, na uvunjifu mkubwa katika maisha ya
duniani. Na mfano wa malipo hayo ndio tunamlipa kila mwenye kumzulia Mwenyezi
Mungu uwongo, na akaabudu kinginecho.
153. Na wale walio tenda
vitendo vibaya vya ukafiri na kuabudu ndama na maasi mengineyo, kisha wakarejea
kwa Mwenyezi Mungu baada ya kutenda hayo, na wakamsadiki, basi hakika Mola wako
Mlezi baada ya toba yao, ni Mwenye kuwasitiri, na kuwasamehe kwa hayo waliyo
kuwa nayo.
154. Na Musa zilipo
muondoka ghadhabu kwa kutoa udhuru nduguye, akazirejea zile mbao alizo ziweka
chini akazichukua. Na kwenye hizo mbao umeandikwa uwongofu, na uwongozi, na njia
za kupata rehema, kwa wale wanao iogopa ghadhabu ya Mola wao Mlezi.
155. Kisha Mwenyezi
Mungu alimuamrisha awalete baadhi ya jamaa katika kaumu yake wawatakie radhi
walio muabudu ndama, na akawapa miadi. Musa akawateuwa katika kaumu yake watu
sabiini katika wasio muabudu ndama, nao wakawa wanawawakilisha kaumu yao. Akenda
nao mpaka kwenye mlima. Na huko wakamwomba Mwenyezi Mungu awaondolee balaa, na
akubali toba ya walio muabudu ndama kati yao. Ikawachukua zilzala (tetemeko)
kubwa pahala hapo, wakazimia kwa sababu yake. Na hayo kwa kuwa hawakuwaacha
kaumu yao walipo abudu ndama, wala hawakuamrisha mema, wala hawakuwakanya maovu!
Musa alipoona yale alisema: Ewe Mola wangu Mlezi! Lau ungeli penda kuwaangamiza
ungeli waangamiza kabla hawajaja hapa kwenye miadi, na ukaniangamiza na mimi
pia, ili waone hayo Wana wa Israili wasinituhumu kuwa mimi nimewauwa. Basi ewe
Mola Mlezi wangu! Usituhiliki kwa walio yafanya wajinga kati yetu. Kwani hii
balaa ya kuabudu ndama haikuwa ila ni majaribio yaliyo toka kwako. Wewe
unampoteza unaye taka apotee katika hao wanao ishika njia ya shari, na unawahidi
unaye taka ahidike. Wewe ndiye mwenye kusema: Nitawaandikia wenye kujikinga na
ukafiri na maasi katika kaumu yako, na akatoa Zaka iliyo faridhiwa, na Mwenye
kusamehe madhambi.
156. Na tukadirie hapa
duniani maisha mema, na tupate tawfiqi tuweze kut'ii, na Akhera tupate malipo
mazuri, na maghfira, na rehema, kwa kuwa sisi hakika tumekwisha rejea kwako na
tunatubu kwako. Mola Mlezi wao akawaambia: Adhabu yangu namfikishia nimtakaye
katika wasio tubu, na rehema yangu imeenea juu ya kila kitu, na
nitawaandikia khasa wale wanao jikinga na ukafiri na maasi katika kaumu
yako, na wanao toa Zaka zilio lazimishwa, na wanao sadiki Vitabu vyote vilivyo
teremka.
157. Na nawakusudia
khasa wanao mfuata Mtume Muhammad, ambaye haandiki wala hasomi, na ambaye
wanakuta sifa zake zimeandikwa katika vitabu vyao vya Taurati na Injili. Yeye
anawaamrisha kila kheri na anawakataza kila shari. Na anawahalalishia vitu
ambavyo tabia inaviona ni vizuri, na anawaharimishia vitu ambavyo tabia
inavichukia kwa kuwa vina madhara, kama damu na mzoga. Na anawaondolea mizigo
mizito na mikazo iliyo kuwa ikiwabana. Basi wanao usadiki Utume wake, na
wakamsaidia, na wakamuunga mkono, na wakamnusuru na maadui zake, na wakaifuata
Qur'ani aliyo teremshiwa pamoja naye kama nuru ya uwongofu, hao basi ndio wenye
kufuzu, sio wenginewe ambao hawakumuamini.
158. Ewe Nabii! Waambie
watu: Hakika mimi nimetumwa kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwenu nyinyi nyote, bila
ya farka baina ya Mwaarabu na asiye kuwa Mwaarabu, baina ya mweusi na mweupe. Na
Mwenyezi Mungu aliye nituma ni Yeye peke yake ndiye Mwenye ufalme wa mbingu na
ardhi. Huipitisha amri yake kwa mujibu wa hikima yake. Na hufanya mbinguni na
duniani kama anavyo penda. Wala hapana wa kuabudiwa kwa haki ila Yeye. Na Yeye
ndiye Mwenye uwezo wa kuhuisha na kufisha, wala hapana mwenginewe. Basi
muaminini Yeye na Mtume wake, huyu Nabii asiye soma wala kuandika. Naye huyu
anamuamini Mwenyezi Mungu ambaye anaye kuiteni mumuamini. Na anaamini Vitabu
vyake vilivyo teremshwa. Basi mfuateni katika kila afanyalo na asemalo mpate
kuongoka na kuongozeka.
159. Na katika kaumu ya
Musa wako jamaa walio bakia na Dini iliyo sawa. Wakiwahidi watu kwa Haki aliyo
kuja nayo Musa kutoka kwa Mola wake Mlezi, na wakifanya uadilifu pale wanapo
pitisha hukumu.
160. Mwenyezi Mungu
amezitaja neema zake juu ya kaumu ya Musa. Akafahamisha kuwa aliwafanya makundi
thinaashara, na akawafanya mataifa, na kila taifa likawa na mpango wao, ili
kuzuia uhasidi na kukhitalifiana. Na walipo taka watu wake maji jangwani,
alimfunulia Musa alipige jiwe kwa fimbo yake. Akalipiga, zikatibuka kutoka
kwenye hilo jiwe chemchem kumi na mbili kwa idadi ya kabila zao. Kila kabila
kati yao ilijua pahala pake makhsusi pa kunywa. Basi haikuwa huyu
kumuingilia huyu. Na akajaalia kiwingu chende kuwapa kivuli chake katika
jangwa, kuwakinga na mwako wa jua. Akawateremshia Manna, nacho ni chakula kwa
Sura kinafanana na mvua ya barafu, na tamu kama asali. Na akateremsha Salwa,
naye ni ndege aliye nona. Na akawaambia: Kuleni hivi vinono tulivyo kuruzukuni
katika tulivyo kuteremshieni. Lakini walijudhulumu nafsi zao, na wakazikufuru
neema hizo, kwa kuzikataa na kutaka nyenginezo. Na Sisi hatukupata madhara kwa
udhalimu wao, lakini upungufu wamepata wao.
161. Ewe Nabii!
Wakumbushe hao waliopo miongoni mwao katika zama zako - ili iwe ni onyo kwa vile
walivyo tenda walio watangulia - wakumbushe kauli yetu tulio waambia hao
walio watangulia kwa ulimi wa Musa: Kaeni katika mji wa Baitul Muqaddas
(Yerusalemu) baada ya kutoka jangwani. Na kuleni kheri zake kokote humo mtakako,
na semeni: Tunakuomba ewe Mola Mlezi wetu, utufutie makosa yetu. Na muingie
kwenye lango la mji kwa kuinamisha vichwa kama kurukuu kwa kumnyenyekea Mwenyezi
Mungu. Mkifanya hivyo tutakufutieni dhambi zenu, na tutazidisha thawabu za
watendao mema.
162. Lakini waliikhalifu
amri ya Mola wao Mlezi, wakasema kwa udhalimu maneno sio walio ambiwa, kwa
kusudi ya kumkejeli Musa. Basi tukawateremshia adhabu kutoka mbinguni kwa
sababu ya kuendelea kwao na udhalimu na kukiuka mpaka.
163. Na waulize
Mayahudi, kwa kuyachukia walio yafanya wenzao walio watangulia, khabari ya
kijiji, nacho ni Elat, kilicho kuwa karibu na bahari. Wakaazi wake walivunja
amri ya Mwenyezi Mungu ya kupiga marfuku kuvua samaki siku ya Jumaamosi, kuwa
hiyo ni siku ya ibada tu kwao. Na siku hiyo samaki walikuwa wakiwajia vururu juu
ya maji. Na siku isiyo kuwa Jumaamosi samaki walikuwa hawaji. Huo ni
mtihani wa Mwenyezi Mungu! Na kwa mfano wa mtihani huo, au majaribio hayo yaliyo
tajwa, ndio tunawajaribu kwa majaribio mengine kwa sababu ya upotovu wao unao
endelea, ili adhihiri mwema na mbaya.
164. Na wakumbushe pia
hao Mayahudi pale kikundi cha watu wema katika wenzao walio tangulia, ambao
hawakutenda mabaya waliyo yatenda wengineo, walipo waambia wanao wapa mawaidha
wale waovu: Kwa sababu gani mnawapa nasaha watu ambao Mwenyezi Mungu
atawahiliki, au atawaadhibu adhabu kali Akhera, kwa sababu ya madhambi wanayo
yatenda? Wakasema: Tunawapa mawaidha ili tupate udhuru kwa Mola wako Mlezi,
tusiwe tumefanya taksiri, na kutaraji huenda wakamchamngu.
165. Walipo yaacha
mawaidha waliyo pewa, tukawaokoa na adhabu wale ambao walikuwa wakikataza
vitendo viovu, na tukwashika walio dhulumu na wakavuka mipaka na wakakhalifu kwa
kuwapa adhabu kali, nayo ni udhalili na shakawa, kwa sababu ya kuendelea kwao
kutokana na ut'iifu wa Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wao.
166. Walipo zidi kuwa
wagumu, na wakaendelea kutobali waliyo katazwa, wala adhabu kali isiwaachishe
uovu, tukawafanya kama manyani kwa kuzigeuza nyoyo zao, na kuwaondolea uwezo wa
kuifahamu Haki, wakawa mbali na kila kheri.
167. Na wakumbushe pia
hao Mayahudi pale alipo wajuvya Mola Mlezi wako wenzao walio watangulia kwa
ndimi za Manabii wao: Mwenyezi Mungu atawasalitisha Mayahudi mpaka Siku ya
Kiyama adhabu mbaya kabisa kwa sababu ya dhulma yao na upotovu wao. Kwani Mola
wako Mlezi ni Mwepesi wa kuwaadhibu watu makafiri, kwani adhabu yake itakuja tu
bila ya shaka yoyote. Na kila kijacho kipo karibu, (chambilecho Waarabu). Na
Yeye Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusamehe na Mwenye kurehemu kwa anaye rejea kwake
akatubu.
168. Na Sisi tumewagawa
makundi makundi duniani. Wamo kati yao walio wema. Na hao ndio walio amini
wakenda mwendo ulio sawa. Na wapo miongoni mwao watu wasio sifika kwa wema. Na
wote tumewafanyia mitihani kwa kuwapa neema na kuwapa nakama, ili watubu, waache
waliyo katazwa.
169. Baada ya hao tulio
kwisha wataja na tukawagawa sehemu mbili, walifuatia waovu wakairithi Taurati
kutokana na walio watangulia. Lakini hao hawakufanya yalio amrishwa humo. Kwani
wao walishika starehe ya dunia badala ya Neno la Haki. Wakijiambia nafsi zao:
Mwenyezi Mungu atatusamehe kwa tunayo yatenda! Wakitaraji maghfira, na ilhali
kuwa yakiwajia kama yale waliyo yashika watayashika vile vile. Basi wao wamekuwa
wameshikilia kuendelea na madhambi pamoja na kutaka kwao msamaha. Tena basi
Mwenyezi Mungu anawatahayarisha kwa vile kutaka maghfira na huku wanaendelea na
yao, akasema: Sisi tulichukua kwao ahadi katika Taurati - nao wameyasoma yaliomo
humo - kuwa waseme kweli; nao wakasema uwongo! Na hakika neema za nyumba ya
Akhera za wanao jikinga na maasi ni bora kuliko starehe za duniani! Basi je,
mtaendelea na uasi wenu, wala hayaingii akilini mwenu kuwa neema hizo ni bora
kwenu? Na mnakhiari badala yake hizo starehe za dunia?
170. Na
wanao ikamata baraabara Taurati, na wakashika Sala zilizo faridhiwa
kwao, hakika Sisi hatutaupoteza ujira wao kwa sababu ya kutengeneza kwao na
kutenda kwao mema.
171. Mwenyezi Mungu
ameijibu kauli ya Mayahudi walipo sema kwamba Wana wa Israili hawakupata kwenda
kinyume na Haki. Alisema: Ewe Nabii! Wakumbushe pale tulipo unyanyua mlima juu
ya Wana wa Israili ukawa kama kiwingu, na wakafazaika kwa kuwa walidhani
utawaangukia. Nasi tukawaambia wakati ule ulipo nyanyuliwa na wao wamo katika
khofu: Yashikeni ya uwongofu tuliyo kupeni katika Taurati kwa nguvu na kuazimia
ut'iifu. Na kumbukeni yaliyomo ndani yake ili mpate kuzingatia na zitengenee
nafsi zenu kwa kuchamngu.
172. Hapa Mwenyezi Mungu
amebainisha hidaya ya wanaadamu kwa kusimamisha dalili katika viumbe, baada ya
kwisha bainisha kwa njia za Mitume na Vitabu. Alisema: Ewe Nabii! Waambie watu
pale Mola wako Mlezi alipo watoa kutoka migongo ya wanaadamu na watoto wao na
wanao zaliwa karne baada ya karne, kisha akwasimamishia dalili za Ungu
wake, na akawapa akili na nadhari ya kuwawezesha kuzijua, na kwa hizo akili na
nadhari waweze kutambua Tawhidi na Rubuubiya, yaani kuwa Mwenyezi Mungu ni
Mmoja Pekee na ni Mola Mlezi wa viumbe vyote, hata wakawa hao wanaadamu kama
walio ulizwa: Je, Mimi siye Mola wenu Mlezi? Nao wakajibu: Kwani, Wewe ndiye
Mola Mlezi wetu. Tunajishuhudia hayo juu ya nafsi zetu...Haya ni kwa kuwa
kumkini kwao kupata kujua hizo hoja na dalili, na kutamakani kwao katika hayo
imekuwa kama kwamba ni kukiri na kuungama. Na Sisi tumefanya haya ili msije
kusema Siku ya Kiyama: Hakika sisi tulikuwa tumeghafilika na hiyo Tawhidi, na
tulikuwa hatuijui.
Katika Aya
hii inaonyesha kuwa watoto asili yake wanatoka kwenye uti wa mgongo. Na ilimu ya
kisasa imethibitisha kuwa kokwa za khaswa zinakuwa katika sehemu ya mgongo chini
ya mafigo. Na zinakaa hapa mpaka katika miezi ya mwisho ya mimba ndio huteremka
pale pahali pake pa kawaida panapo onekana. Na pengine hata hivyo huchelewa
kuteremka hata baada ya mtoto kuzaliwa. Kadhaalika mayai ya mwanamke yanafanyika
chini ya figo khasa, kisha ndio huteremka pahala pake karibu na tumbo la
uzazi.
173. Au mtasema:
Walishiriki baba zetu kabla yetu, na sisi ni dhuriya zao tumewafuata tu. Basi
ewe Mola Mlezi wetu! Unatushika utuhiliki kwa walio yafanya wapotovu miongoni
mwa baba zetu, kwa kujenga misingi ya ushirikina tulio endelea nao? Basi hamna
hoja.
174. Kwa mfano wa
maelezo wazi yenye hikima tunawabainishia wanaadamu dalili za kuwepo Mwenyezi
Mungu, ili warejee waache ukhalifu wao na kuwafuata wapotovu.
175. Mwenyezi Mungu
amepiga mfano wa wanao kadhibisha kwa Aya zake alizomteremshia Mtume wake.
Akasema: Ewe Nabii! Wasomee kaumu yako khabari za mtu mmoja katika Wana wa
Israili. Tulimpa ilimu ya kuzijua Ishara tulizo wateremshia Mitume wetu. Yeye
huyo akazipuuza, wala asizishughulikie. Basi Shetani akamfuata kwa khatua zake,
na akamtawala kwa upotovu wake, akawa katika kundi la walio potea.
176. Na lau tungeli taka
kumnyanyua afike daraja za watu wema, tungeli mnyanyua kwa kumwezesha kuyatenda
maamrisho ya hizo Aya.. Lakini yeye alishikamana na dunia, na hakuweza
kunyanyuka kwendea uwingu wa uwongofu. Akafuata matamanio yake. Akawa hali yake
daima yumo katika dhiki, na kushughulika kwake ni kwa dunia, na tafakuri zake
duniani ni kutaka kuipata hiyo dunia basi. Hali yake ni kama hali ya mbwa anapo
kuwa katika hali ovu kabisa, anavyo kuwa daima anapumua na kutoa limi lake nje,
ukimkemea au ukimwacha. Hudorora ulimi wake kwa kuvuta pumzi kwa shida!
Kadhaalika mwenye kuipenda dunia hudumu daima katika kuwania starehe zake na
matamanio yake! Hakika hizo ndizo sifa zinazo mueleza huyo mwenye kuziacha Aya
zetu, na ndio sifa ya wote wanao zikadhibisha Aya zetu zilio
teremka. Basi wasimulie kisa chake hichi, huenda wakafikiri na wakaamini.
177.
Ni mbaya kweli hali ya hao wanao zipinga Ishara zetu, na kwa huku
kukengeuka kwao na kuacha Haki hakumdhulumu mtu ila nafsi zao tu.
178. Na yule ambaye
Mwenyezi Mungu amemwezesha kufuata njia ya haki huyo basi ndie aliye ongoka
kweli, mwenye kupata furaha ya kote kuwili duniani na Akhera. Na mwenye kukosa
uwezesho huo kwa sababu ya kumilikiwa na pumbao lake basi watu hao ndio walio
khasiri.
179. Na tumewaumbia
wengi katika majini na watu marejeo yao ni Motoni Siku ya Kiyama. Kwani hao wana
nyoyo zisio funguka ikaingia Haki ndani yake. Wana macho yasiyo angalia dalili
za kudra. Wana masikio yasiyo sikia Aya na mawaidha kwa sikio la kuzingatia na
kuwaidhika! Hao ni kama wanyama kwa kutonafiika kwa neema ya akili za kuzingatia
walizo neemeshwa na Mwenyezi Mungu. Bali hao ni wapotovu zaidi kuliko wanyama,
kwani wanyama hutaka cha kuwafaa na hukimbia cha kuwadhuru. Lakini hawa watu
hata hawatambui hayo. Hao ndio walio fikia ukomo wa kughafilika.
180. Na Mwenyezi Mungu
peke yake ndiye Mwenye Majina yenye kuonyesha sifa za ukamilifu. Basi mtumilieni
hayo mnapo muomba, au mnapo mwita au kumtaja. Na waepukeni hao wanao mili katika
hayo yasiyo elekeana na dhati ya utukufu wake. Hao watakuja lipwa malipo
ya vitendo vyao.
181. Na katika tulio
wajaalia waingie Peponi wapo wanao waita wengineo kwenye Haki kwa kuipenda Haki,
na kwa Haki tu wanafanya uadilifu katika hukumu zao.
182. Na wale walio
zikanusha Ishara (Aya) zetu zilio teremshwa tutawapururia pole pole, na
tutawawacha mpaka wafike ukomo watapo fika. Na hayo ni kwa kuwapururia neema juu
yao, juu ya kushughulika kwao katika maasi, mpaka maangamizo yawazukie nao
wameghafilika wakitaladhadhi na starehe zao.
183. Nitawakunjulia
maisha, bila ya kuyapuuza maovu yao. Na mipango yangu niliyo wapangia ni ya
nguvu na mikali juu yao, inalingana na madhambi yao yaliyo zidi kwa kupita
kiasi.
184. Wao wameanza kwa
kukadhibisha, wala hawakuzingatia yale anayo waitia kwayo Mtume, na hoja anazo
zitoa. Bali wakamsingizia kuwa ni mwendaazimu, na hali hana wazimu chochote.
Yeye huyu ni mwenye kuwaonya wasifikiwe na adhabu ya ushirikina wao. Na onyo
lake liwazi, la dhaahiri.
185. Wamemwambia
Muhammad mwongo kwa Tawhidi anayo waitia, wala hawakutazama kwa kuzingatia na
kutafuta dalili za ufalme mtukufu wa Mwenyezi Mungu ulioko katika mbingu na
ardhi na viliomo ndani yao, zinazo onyesha ukamilifu wa uwezo wa huyu Mwenye
kuunda, na zinazo onyesha Umoja wake wa pekee. Wala hawakufikiri kuwa ajali yao
imekwisha karibia, au huenda ikawa imekaribia, wapate kufanya haraka kutupia
nadhari na kuitafuta Haki kabla ya kuzuka ajali. Ikiwa basi watu hawa hawaamini
maneno ya Qur'ani watakuja amini maneno gani baada yake
186. Aliye andikiwa na
Mwenyezi Mungu kupotea kwa uwovu wa uchaguzi wake mwenyewe, basi hapana mtu wa
kumhidi. Na Yeye Subhana, Aliye takasika, anawaacha watu kama hao wakihangaika
wala hawaitambui njia.
187. Ewe Muhammad!
Mayahudi wanakuuliza khabari ya Saa itakayo malizikia dunia. Itakuwa wakati
gani, kujuulikana khasa? Waambie: Ujuzi wa wakati wake uko kwa Mwenyewe Mola
wangu Mlezi peke yake. Haujui wakati wake mtu yeyote isipo kuwa Yeye. Itapo
tokea kitisho chake kitakuwa kikuu kwa walioko mbinguni na ardhini! Wao
wanakuuliza suala hili kama kwamba wewe una pupa ya kuijua! Basi wakaririe
jawabu, na uwambie kwa kutia mkazo: Hakika kuijua hiyo Saa kuko kwa Mwenyezi
Mungu, lakini aghlabu ya watu hawatambui hakika ya wasiyo yaona au wanayo yaona!
188. Waambie: Mimi
siimilikii nafsi yangu kujiletea nafuu, wala kujikinga na madhara, ila Mwenyezi
Mungu akipenda hayo. Hapo ndio hunipa mamlaka. Na lau kuwa mimi najua yale
yaliyo fichikana kwangu, kama mnavyo dhani, basi ningeli kithirisha kila kheri,
kwa kuwa ninajua sababu zake. Na ninge ilinda nafsi yangu na kila ovu, kwa
kuyaepuka yanayo leta madhara. Mimi si chochote ila ni mwonyaji wa adhabu, na
mbashiri wa thawabu, kwa kaumu wanayo iamini Haki na wanait'ii.
189. Yeye ndiye Allah,
Mwenyezi Mungu, aliye kuumbeni hapo mwanzo kwa nafsi moja. Na akajaalia katika
nafsi ile ile mwenzie, na vizazi vyao vikaendelea kuwepo. Nanyi mlikuwa mume na
mke. Basi alipo muingilia akachukua mzigo mwepesi, nayo ndio mimba changa, inapo
kuwa kama pande la damu na pande la nyama. Mimba ikiwa nzito katika tumbo lake
huyo mke, mume na mke humwomba Mola wao Mlezi wakisema: Wallahi, ukitupa mwana
mzima asiye na ila katika umbo lake, tutakushukuru kwa neema yako.
190. Akisha wapa
wakitakacho, huwafanya masanamu ndio washirika wa Mwenyezi Mungu Mtukufu katika
ile zawadi yake ya ukarimu, kwa kuyatambikia kama kwamba ndio wanayashukuru. Na
Mwenyezi Mungu pekee ndiye anaye stahiki kushukuriwa. Yeye ametukuka, hawezi
kuwa kama hiyo miungu yao ya kishirikina.
191. Jee, inawafalia
kumshirikisha Mwenyezi Mungu na masanamu yasio weza kuumba kitu, bali hayo
yameumbwa na Mwenyezi Mungu?
192. Wala hayawezi
kuwasaidia hao wanayo yaabudu, wala hayajisaidii wenyewe akitokea mtu
kuyashambulia.
193. Na nyinyi mnao
yaabudu masanamu! Mkiyaomba hayo masanamu yakuongozeni mpate mnacho kipenda
hayakuitikieni hayo myatakayo! Ni sawa sawa kwenu kuwa hapana faida ya kuwaomba
au mkinyamaza. Hali yao haibadiliki vyo vyote vile.
194. Hakika hao mnao
waomba badala ya Mwenyezi Mungu, na mkataraji nafuu kwao, wao wenyewe
wanamnyenyekea Mwenyezi Mungu kwa hukumu ya maumbile yao. Kwani Yeye Mwenyezi
Mungu amewafanya wafuate amri yake mfano wenu nyinyi. Kama nyinyi mnasema kweli
katika madai yenu kuwa hao wanaweza lolote, basi watakeni, na wao
wakutimilizieni.
195. Bali haya masanamu
ni duni kuliko nyinyi kwa kuumbwa na kuwa! Kwani wao wana miguu ya kuendea? Au
wana mikono ya kukinga madhara yasikupateni au yasiwapate wenyewe? Au wana macho
ya kuonea? Au masikio ya kusikia hayo mnayo yataka wakakupeni? Hawana chochote
katika hayo! Vipi basi mnawashirikisha hao na Mwenyezi Mungu? Na ikiwa nyinyi
mnadhani kuwa hio miungu ya uwongo inaweza kunidhuru mimi au mtu yeyote,
basi iiteni, na mfanye njama zenu pamoja nao kama mtakavyo, bila ya kunipa
muhula wala kungoja. Hao hakika hawawezi kitu! Basi msiningojee, na wala mimi
siwabali.
196. Hakika msaidizi
wangu wa kuninusuru nanyi ni Yeye Mwenyezi Mungu. Ulinzi wangu uko kwake. Naye
ndiye aliye niteremshia Qur'ani. Na Yeye peke yake ndiye anaye wanusuru waja
wake walio wema.
197. Na hayo masanamu
mnayo taka kwao msaada, badala ya Mwenyezi Mungu, hayawezi kukusaidieni nyinyi,
wala kujisaidia wenyewe.
198. Na ukiwataka
uwongofu katika yaliyo na kheri nanyi hawalisikii ombi lenu, licha ya
kukuongozeni! Unawaona wanavyo kukabili kama kwamba wanakutazama, na kumbe wao
kwa hakika hawaoni kitu!
199. Ewe Nabii!
Waachilie mbali hao majaahili, na endelea katika njia ya Da'wa (Wito). Na
wachukulie watu kwa lilio wepesi kwao. Na waamrishe kila jambo linalo pendeza na
kuingia akilini.
200. Na Shetani
akikuchochea kwa wasiwasi ili apate kukuachisha ulio amrishwa, kama vile
kukasirika kwa kukushikilia kwao mambo ya shari, basi omba ulinzi wa Mwenyezi
Mungu akuepushe naye huyo Shetani. Kwani Mwenyezi Mungu ni Mwenye kusikia na
kujua kila linalo tokea.
201. Hakika wale wamchao
Mola wao Mlezi, na wakaweka baina yao na maasi kinga cha kuzuia uchochezi wa
Shetani unao wapitia kuwaachisha yaliyo waajibu wao, hukumbuka uadui wa Shetani
na vitimbi vyake. Kwa hivyo hao wanaiona Haki, basi ndio wanarejea.
202. Na ndugu zao
mashetani, nao ni hao makafiri, mashetani huwazidisha upotovu kwa kuwajaza
wasiwasi. Tena hawa makafiri hawaachi upotovu wao wakazingatia.
203. Na usipo waletea
makafiri Ishara wanayo itaka kwa inadi na ukafiri, husema: Kwa nini hukuitaka?
(au hukuizua? Makusudio yao ni kuwa Mtume s.a.w. akizibuni Aya zote.) Waambie:
Mimi sifuati ila Qur'ani ninayo funuliwa kwa wahyi kutoka kwa Mola wangu Mlezi.
Na waambie: Hii Qur'ani ni hoja zinazo toka kwa Mola Mlezi wenu kukuonyesheni
njia za Haki. Nayo ina uwongofu, na rehema, kwa Waumini, kwa sababu wao
wanaifuata kwa vitendo.
204. Enyi Waumini!
Mkisomewa Qur'ani isikilizeni kwa masikio yenu, mpate kuzingatia mawaidha yake,
na msikilize vizuri mpate kuipata rehema.
205. Na mtaje Mola wako
Mlezi ndani ya nafsi yako, upate kuhisi kuwa upo karibu na Mwenyezi Mungu, kwa
kumnyenyekea na kumkhofu, bila ya kupiga makelele, bali juu kidogo kuliko kwa
siri, na chini ya kudhihirisha kwa maneno. Na umtaje na umkumbuke asubuhi na
jioni, ili uanzie mchana wako kwa kumkumbuka Mola wako Mlezi, na ukhitimishie
kwayo vile vile. Na wakati wako wote usighafilike na kumtaja na kumkumbuka
Mwenyezi Mungu.
206. Hao walio karibu na
Mola wako Mlezi kwa utukufu na takrimu hawatakabari wakaacha kumuabudu. Na
wanamtakasa Mwenyezi Mungu na kila lisio faa kwake. Na wanamnyenyekea Yeye.