2. Enyi Waumini! Msivunje hishima ya alama ya Dini
ya Mwenyezi Mungu, yaani ibada alizo amrisha Mwenyezi Mungu, kama ibada za Hija
wakati wa Ihram (1), na sharia na hukumu nyenginezo. Wala msivunje hishima ya
miezi mitakatifu kwa kuzua vita katika miezi hiyo. Wala msipinge wanyama wanao
pelekwa Makka, kwa kupokonya au kuzuia wasifike huko, wala msiwavue vigwe
walivyo fungwa shingoni mwao kuwa ni alama kuwa wamekusudiwa kupelekwa Nyumba
Takatifu, na kuwa watakuwa dhabihu wa Hija. Wala msiwapinge wanao kusudia kwenda
Hija nao wakitafuta fadhila na radhi za Mwenyezi Mungu. Na mkisha vua Ihram na
mkatoka kwenye eneo la Alharam, basi mnaweza kuwinda mtakavyo. Wala msipelekewe
na chuki yenu kubwa kwa wale walio kuzuieni kufika kwenye Msikiti wa Makka
mkawafanyia uadui. Enyi Waumini! Saidianeni katika kutenda kheri na mambo yote
ya ut'iifu, wala msisaidiane katika maasi, na kupindukia mipaka aliyo
iweka Mwenyezi Mungu. Na ogopeni adhabu ya Mwenyezi Mungu na nguvu zake. Hakika
Mwenyezi Mungu ni Mkali wa kuwaadhibu wale wanao mkosa.
(1) Mwenye kuhiji
akisha "harimiya" (yaani kunuia kuhiji) huwa haramu kwake baadhi ya mambo, kama
kuvaa nguo iliyo shonwa, kukata nywele, kuwinda, n.k. mpaka amalize
"Ihram" nako ndio kwisha ibada ya Hija.
3. Enyi Waumini! Mwenyezi Mungu amekuharimisheni
kula nyamafu, yaani aliye kufa bila ya kuchinjwa kisharia.(1) Na damu inayo
tiririka, na nyama ya nguruwe, na yule ambaye wakati wa kuchinjwa ametajiwa jina
lisilo kuwa la Mwenyezi Mungu, na aliye kufa kwa kunyongwa, au aliye pigwa mpaka
akafa, au aliye kufa kwa kuanguka, au kwa kupigwa pembe, au kwa kuliwa na mnyama
mwingine. Ama yule mnaye mdiriki angali yu hai naye ni mnyama wa halali kuliwa,
mkamchinja, basi huyo ni halali kwenu. Mwenyezi Mungu ameharimisha kula wanyama
walio tolewa sadaka au mhanga kwa masanamu. Na pia ameharimisha kuagua yaliyo
ghaibu kwa uganga wa kupiga ramli, na mfano wa hayo. Kula chochote katika
vilivyo tajwa kuwa ni haramu ni dhambi kubwa, na ni kutoka kwenye ut'iifu wa
Mwenyezi Mungu. Tangu sasa tamaa ya makafiri kuiviza Dini yenu imekwisha potea.
Basi msiwaogope kuwa watakushindeni, bali ogopeni kutofuata amri zangu. Leo
nimekukamilishieni hukumu za Dini yenu, na nimekutimizieni neema yangu kwa
kukupeni nguvu na kukuimarisheni, na nimekukhitarieni UISLAMU uwe ndiyo Dini.
Lakini mwenye kulazimika kwa njaa akala kidogo katika hivyo vilivyo harimishwa,
akala ili asife, bila ya kukusudia uasi, basi Mwenyezi Mungu humsamehe mtu huyo
kwa kulazimika kula cha haramu asije akafa. Mwenyezi Mungu ni Mwenye huruma na
rehema kwa alivyo halalisha.
(1) Hafi mnyama wenyewe ila kwa maradhi, na hayo maradhi
humdhuru mwanaadamu akila nyama yake, na huenda maradhi mengine yakawa ya
kuambukiza. Katika damu vimo vijidudu vya maradhi. Ama katika nyama ya nguruwe
mna vitu kadhaa wa kadhaa vya kumdhuru mtu. Na vilivyo chinjwa kwa jina la asiye
kuwa Mwenyezi Mungu, na walio chinjiwa masanamu au mashetani, hayo ni mambo ya
ibada potovu. Na vilivyo nyongeka, na vilivyo anguka, na kupigwa pembe ni sawa
na mfu, au mzoga, kwa kuwa vimekufa kwa vifo vibaya, na khasa kwa kuwa damu yake
haikutoka imevilia humo humo.
4. Ewe Mtume! Waumini wanakuuliza nini
walicho halalishiwa katika vyakula na vyenginevyo? Waambie: Mwenyezi Mungu
amekuhalalishieni kila chema kipendacho nafsi njema. Na pia amekuhalalishieni
kula kinacho windwa na wanyama wenu mlio wafunza kuwinda, kwa kutokana na alivyo
kufunzeni Mwenyezi Mungu. Basi kuleni wanacho winda wanyama hao mlio watuma, na
mtaje jina la Mwenyezi Mungu pale mnapo watomeza. Na mcheni Mwenyezi Mungu kwa
kuzishika sharia zake, wala msikiuke mipaka yake. Tahadharini kumkhalifu
Mwenyezi Mungu katika hayo, kwani Yeye ni Mwepesi wa kuhisabu.
6. Enyi Waumini! Mkitaka kusali nanyi
hamna udhu, tawadhini kwa kukosha nyuso zenu, na mikono yenu mpaka vifundoni, na
mpake maji kichwa kizima au baadhi yake. Na mkoshe miguu yenu mpaka vifundoni.
Mnapo taka kusali nanyi mna janaba kwa kuingiliana na wake zenu, basi kogeni
mwili mzima. Ikiwa mna maradhi ambayo hayakufaliini kutumia maji, au mpo
safarini na ipo taabu ya maji, au mmetoka chooni kukidhi haja, au mmeingiliana
(kwa lugha ya Qur'ani "kugusana") na wanawake na msipate maji, basi inakupaseni
kutayamamu, yaani kujipaka vumbi lilio safi. Na hayo ni kwa kupangusa kwa hilo
vumbi nyuso zenu na mikono yenu. Na Mwenyezi Mungu hataki kukudhikini katika
hayo anayo kuamrisheni, bali anakupeni sharia za kukusafisheni ndani na nje, ili
atimize neema zake juu yenu kwa uwongofu, na kubainisha na kusahilisha, mpate
kumshukuru kwa uwongofu wake na kutimilia neema yake kwa kudumisha ut'iifu
kwake.
T'ahara
(Usafi) wa Kiislamu una maana mbili: Moja ni kumwelekea
Mwenyezi Mungu Mtukufu moyoni kwa kujiweka tayari kwa hayo, na
kufunga azimio kusimama mbele yake na hali ni mwenye nafsi iliyo
t'aahiri, na moyo ulio safi kabisa kwake Yeye tu. Pili ni
unadhifu wa dhaahiri kwa udhu. Na katika hayo ni kuvikosha
viungo vyote vinavyo weza kuchafuka. Na udhu ni jambo la
kufanywa mara kwa mara, na huweza kufika hata kutwa mara tano. Pia kuna kukoga
unapo ingiliana na mke, na wakati wa damu ya mwezi na uzazi. Udhu na kukoga ni
kuondoa takataka zenye vijidudu vya maradhi, na pia huleta uchangamfu kwa
kusisimua damu ya kwenye ngozi, na kupoza mishipa. Na kwa hivyo Mtume s.a.w.
aliusia: "Ukihamaki tawadha".
7. Kumbukeni, enyi Waumini, neema za
Mwenyezi Mungu alizo kuneemesheni kwa kukuongoeni kwenye Uislamu. Jitahidini
kutimiza ahadi yake aliyo itaka kwenu wakati mlipo muunga mkono Mtume wake,
Muhammad, kuwa mtamsikia na mtamt'ii. Na mcheni Mwenyezi Mungu kwa kuzihifadhi
ahadi hizi. Yeye, Subhanahu, ni Mjuzi sana wa yote yaliyo fichikana
nyoyoni mwenu, naye atakulipeni kwayo.
8. Enyi Waumini! Jitahidini kutimiza
haki za Mwenyezi Mungu, na shuhudieni kwa haki baina ya watu. Chuki zenu kubwa
kwa watu fulani zisikupelekeeni mkaacha kuwafanyia uadilifu. Bali jilazimisheni
uadilifu, kwani hiyo ndiyo njia ya kupelekea kumcha Mwenyezi Mungu, na kuepukana
(1) na ghadhabu yake. Na mcheni Mwenyezi Mungu katika mambo yenu yote; kwani
Yeye, Sub hanahu, anayajua vilivyo yote mnayo yafanya, naye atakulipeni kwayo.
(1) Uislamu unalingania
uadilifu moja kwa moja, sawa kwa rafiki na adui.Haifai chuki ikakupelekea
kudhulumu. Na hayo unapo amiliana na watu, na kuamiliana baina ya dola ya
Kiislamu na dola nyenginezo. Na kumfanyia uadilifu adui kunaambiwa na
Qur'ani kuwa ni karibu zaidi na uchamngu na usafi wa kidini. Lau
kuwa wasia huu ungeli tumiwa katika sharia za baina ya madola basi pasingeli
kuwapo vita. Kama kila dini ina kitambulisho chake na alama, basi kitambulisho
cha Uislamu ni Dini ya Mungu Mmoja na Uadilifu.
9. Mwenyezi Mungu kwa fadhila yake
amewaahidi walio isadiki Dini yake na wakatenda mema kuwa atawasamehe dhambi
zao, na atawalipa badala yake thawabu.
10. Na wale wanayo ipinga Dini ya
Mwenyezi Mungu, na wakakanusha Ishara zinazo onyesha Umoja wa Mwenyezi Mungu
Mtukufu, na ukweli wa Ujumbe wake, hao ni watu wa kudumu katika Jahannamu.
11. Enyi Waumini! Kumbukeni neema za
Mwenyezi Mungu juu yenu katika wakati wa shida, pale baadhi ya Washirikina
walipo kusudia kukuuweni nyinyi na Mtume wenu, Mwenyezi Mungu akazuia balaa yao
isikufikieni, na akakuokoeni. Shikamaneni na kumcha Mwenyezi Mungu, na
mumtegemee Yeye peke yake, katika mambo yenu. Kwani Yeye anakutosheni. Inavyo
muelekea Muumini ni kumtegemea Mwenyezi Mungu peke yake daima milele.
12. Mwenyezi Mungu alichukua ahadi
kutokana na Wana wa Israili kuwa watamsikia na watamt'ii. Akawateulia marais
thinaashara kutokana miongoni mwao ili itimie hiyo ahadi. Na Yeye Mwenyezi Mungu
akawaahidi ahadi ya nguvu kuwa atakuwa pamoja nao, atawasaidia na atawanusuru
ikiwa watashika Sala kama ipasavyo, na watatoa Zaka walizo faridhiwa, na
watawasadiki Mitume wake wote, na watawanusuru, na watatoa mali kwa ajili ya
mambo ya kheri. Na kwamba pindi wakifanya hayo basi Mwenyezi Mungu
atawafutia dhambi zao, na atawatia katika Bustani zake zipitazo mito kati yake.
Na mwenye kukufuru, na akavunja ahadi baada ya hayo, basi huyo amepotoka na
hakufuata njia iliyo kaa sawa iliyo nyooka.
13. Basi kwa sababu ya Wana wa Israili
kuvunja agano lao ndio wakastahiki kufukuzwa kutokana na rehema ya Mwenyezi
Mungu. Nyoyo zao zikawa ngumu, si laini za kupokea Haki; na wakaingia kupotoa
maneno ya Mwenyezi Mungu yaliyomo katika Taurati kutokana na maana yake ya asli,
na yafuate yanayo wafikiana na wapendavyo wao. Wakaachilia mbali pande
kubwa ya mambo waliyo amrishwa katika Taurati !! Na wewe, Mtume, huachi kuona
kila namna ya khadaa na uvunjaji wa ahadi kwa hawa Wana wa Israili, isipo kuwa
kwa wachache tu miongoni mwao ambao wanakuamini wewe. Hao hawakhuni wala
hawadanganyi. Basi, ewe Mtume! Yasamehe yaliyo pita kutokana na watu hawa, na
wachilia mbali, bali wafanyie wema. Kwani Mwenyezi Mungu huwapenda wafanyao
wema.
14. Hali kadhaalika Mwenyezi Mungu
alichukua ahadi kwa Wakristo, ambao wamesema: Sisi ni Manasara, kwa kuwa
wataiamini Injili, na watamuamini Mwenyezi Mungu Mmoja. Nao wakaacha mengi walio
amrishwa katika Injili. Mwenyezi Mungu akawaadhibu kwa hayo, kwa kutia uadui na
khasama baina ya wao kwa wao, wakawa makundi mbali mbali yenye uadui mpaka Siku
ya Kiyama. Na hapo Mwenyezi Mungu atawaambia waliyo kuwa wakiyafanya, na
atawalipa kwayo.
15. Enyi Watu wa Kitabu! Amekujilieni
Mtume wetu, Muhammad, akiita watu wafuate Haki. Anakufichulieni mengi mliyo kuwa
mkiyaficha katika Taurati na Injili. Na anayaacha mengi katika mliyo yaficha
ambayo hayana haja kuyadhihirisha. Amekuleteeni kutoka kwa Mwenyezi Mungu Sharia
kaamili, ambayo Sharia hiyo peke yake ni nuru, na inabainishwa na Kitabu kilicho
wazi.
16. Mwenyezi Mungu kwa Kitabu hichi
anawaongoa kwenye njia ya uwokofu wanao elekea kutaka radhi zake, na anawatoa
kwenye giza la ukafiri kuendea mwangaza wa Imani kwa tawfiki yake, na
anawaongoza kwenye njia ya Haki.
17. Hakika wamekufuru wale wanao dai ati
Mwenyezi Mungu ndiye Masihi mwana wa Maryamu!! Ewe Mtume! Waambie hao wanao
thubutu kuchezea cheo cha Ungu: Hapana ye yote anaye weza kuzuia matakwa ya
Mwenyezi Mungu akitaka kumteketeza Isa na mama yake, na kuwahiliki wote waliomo
katika ardhi. Kwani ufalme wa mbingu na ardhi na vilivyo baina yao ni wa
Mwenyezi Mungu peke yake. Yeye huumba mfano autakao. Na Mwenyezi Mungu ana uweza
mkubwa kabisa. Hashindwi na kitu.
18. Na Mayahudi na Wakristo husema: Sisi
ndio tulio fadhiliwa, kwani sisi ndio wana wa Mwenyezi Mungu na vipenzi vyake
atupendao. Waambie ewe Mtume! Basi kwa nini anakuadhibuni kwa dhambi zenu, na
anakutieni katika moto wa Jahannamu? Waongo nyinyi! Nyinyi, kama wanaadamu
wengineo, ni viumbe, na mtahisabiwa kwa vitendo vyenu. Na maghfira yamo mikononi
mwa Mwenyezi Mungu peke yake, humsamehe amtakaye. Na adhabu yake ni kwa amtakaye
kumuadhibu. Kwani ufalme wa mbingu na ardhi na viliomo baina yao ni wa
Mwenyezi Mungu tu, na kwake Yeye ndio
marejeo ya mwisho.
19. Enyi Watu wa Kitabu! Umekujieni
ujumbe wa Mtume wetu ambaye anakudhihirishieni Haki, baada ya kusita ujumbe kwa
muda wa zama, ili msitafute udhuru wa ukafiri wenu, kwa kudai ati kuwa Mwenyezi
Mungu hakukuleteeni mbashiri wa kukupeni khabari njema, wala mwonyaji wa
kukuhadharisheni. Sasa, basi, huyo amekujilieni mbashiri na mwonyaji. Na
Mwenyezi Mungu ni muweza wa kila jambo - na katika hayo mambo ni kutuma Mitume,
na kukuhisabuni kwa mliyo nayo.
20. Na taja, ewe Mtume! pale Musa alipo
waambia watu wake: Enyi watu wangu! Zikumbukeni neema za Mwenyezi Mungu kwa
kushukuru na kut'ii, kwa kuwa amewateua Manabii wengi miongoni mwenu, na
akakufanyeni watukufu kama wafalme baada ya kuwa mlikuwa wanyonge chini ya
utawala wa Firauni, na akakupeni neema nyingi nyenginezo ambazo hawajapewa
wowote wengineo.
21. Enyi watu wangu! T'iini amri
ya Mwenyezi Mungu. Ingieni ardhi takatifu aliyo kujaalieni Mwenyezi Mungu
muingie, wala msirejee nyuma kuwaogopa hao watu wake majabari, mkaja
kukosa nusura ya Mwenyezi Mungu na radhi zake.
22. Wana wa Israili wakaikhalifu amri ya
Mwenyezi Mungu na wakasema: Ewe Musa! Katika nchi hii wamo watu majabari. Sisi
hatuna nguvu za kupambana nao. Basi hatutoingia humo maadamu wao wamo. Wakitoka
basi tena hapo sisi tutaingia.
23. Wawili kati ya wakubwa wao walio
kuwa wanamwogopa Mwenyezi Mungu, na ambao Mwenyezi Mungu amewapa neema ya imani
na ut'iifu, walisema: Enyi watu! Waingilieni hao majabari wa mjini kwa
kupitia mlangoni kwa ghafla. Mkifanya hivyo nyinyi mtawashinda. Na mtegemeeni
Mwenyezi Mungu peke yake katika mambo yenu yote, ikiwa nyiny ni wenye Imani ya
kweli.
24. Lakini wakakakamia katika ukhalifu
wao. Wakasema: Ewe Musa! Sisi bila ya shaka yoyote tumekwisha azimia kuwa
hatutaingia nchi hii kabisa, maadamu wamo hao majabari. Basi tuache na yetu;
kwani wewe huna madaraka yoyote juu yetu. Nenda wewe na Mola wako Mlezi
mkapigane nao hao majabari. Sisi tutakaa hapa hapa hatubanduki.
25. Hapo tena Musa akamrejea Mola wake
Mlezi akisema: Mola wangu Mlezi! Sina madaraka ila juu ya nafsi yangu na ndugu
yangu. Basi tuhukumie baina yetu na hawa watu wakaidi.
26. Mwenyezi Mungu akamuitikia Musa,
akawapigia marfuku hao wakhalifu wasiingie nchi hiyo kwa muda wa miaka arubaini,
wakipotea ovyo majangwani hawajui wendako wala watokako. Mwenyezi Mungu
akamwambia Musa kama kumuasa: Usisikitike kwa masaibu yaliyo wasibu, kwani hawa
ni wapotovu, wameiasi amri ya Mwenyezi Mungu.
27. Hakika kupenda kutenda uadui ni
tabia ya baadhi ya watu. Basi ewe Nabii! Wasomee Mayahudi - na wewe ni msema
kweli - khabari za Haabila na Qaabila, wana wawili wa Adam. Kila mmoja alichinja
dhabihu kama ni mhanga kwa kutaka kuruba kwa Mwenyezi Mungu. Mwenyezi Mungu
alimkubalia mmoja kwa ajili ya usafi wa niya yake, na akamkatalia wa pili kwa
kuwa niya yake haikuwa safi. Basi yule aliye kataliwa akamhusudu mwenzie na
akamuahidi kuwa atamuuwa. Yule nduguye akamrudi kwa kumbainishia kuwa Mwenyezi
Mungu hapokei a'mali ila kwa wachamngu walio safisha niya zao katika kule
kutafuta kuruba.
28. Akamwambia: Shetani akikuzuga hata
ukaninyooshea mkono ili kuniuwa, mimi sitofanya kama hivyo, wala
sitanyoosha mkono wangu kwa ajili ya kukuuwa. Hakika mimi naogopa adhabu
ya Mola wangu Mlezi, naye ndiye Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa viumbe vyote.
29. Mimi sitakuzuia utapo taka kuniuwa
ili upate kubeba dhambi za kuniuwa mimi pamoja na dhambi zako za tangu hapo za
kutomsafia niya Mwenyezi Mungu. Kwa hivyo wewe unastahiki huko Akhera kuwa
katika watu wa Motoni. Na hayo ni malipo ya haki ya Mwenyezi Mungu kumlipa kila
mwenye kudhulumu.
30. Basi nafsi yake ilimsahilishia
kukhalifiana na maumbile, kumuuwa nduguye, akamuuwa. Kwa hivyo akawa kwa mujibu
wa hukumu ya Mwenyezi Mungu miongoni mwa walio khasiri, kwa kuwa ameipoteza
imani yake na amempoteza nduguye.
31. Baada ya kumuuwa yakamjia majuto na
kubabaika. Akawa hajui amfanyeje maiti! Mwenyezi Mungu akampeleka kunguru
akafukua udongo amzike kunguru mwengine aliye kufa, ili amfunze muuwaji vipi
kumsitiri mwenzake aliye kwisha kufa. Alipo hisi uovu wa aliyo yatenda, alijuta
kwa ukhalifu wake, akasema: Nimeshindwa hata kuwa kama kunguru huyu nikamsitiri
ndugu yangu? Akawa basi miongoni wa walio juta kwa makosa yake, na kwenda
kinyume na yanavyo takikana na maumbile.
32. Kwa sababu ya uasi huo na kupenda
kwa baadhi ya watu kuwafanyia uadui wenginewe, ndio tukawajibisha kumuuwa
muuwaji, kwani mwenye kumuuwa mtu bila ya sababu zinazo pasa kisasi (1), au bila
ya kufanya uharibifu katika nchi, ni kama amewauwa watu wote. Yeye huyo amemwaga
damu za watu, na amewashajiisha wengine wafanye kama hayo. Kwa hivyo kumuuwa
mmoja ni kama kuwauwa watu wote kwa kujiletea maudhiko ya Mwenyezi Mungu
na adhabu yake. Na mwenye kumhuisha mtu kwa kumlipia kisasi, basi ni kama
amewahuisha watu wote kwa kuhifadhi damu ya wanaadamu isimwagwe ovyo. Huyo
anastahiki thawabu nyingi kutokana na Mola wake Mlezi. Sisi tumewatumia Mitume
wetu kutilia mkazo hukumu yetu kwa dalili na hoja. Kisha baadaye wengi
miongoni mwa Wana wa Israili walipindukia mipaka katika uharibifu wao katika
nchi.
(1) Maneno haya yanaonyesha
kuwa kumfanyia uadui mtu mmoja ni kuwafanyia jamii ya watu, na kulipa kisasi
ndio kuhuisha jamii. Katika Sharia ya Kiislamu kisasi ni haki ya waliy-amri,
yaani aliye mkhusu maiti. Akipenda atasamehe achukue fidiya, na akipenda atataka
kisasi na akitimize. Naye anapo samehe anayo haki ya kumfedhehesha mkosefu akiwa
amekithiri uwovu wake na uharibifu.
33. Hakika adhabu ya wale wanao mpiga
vita Mwenyezi Mungu na Mtume wake kwa kuacha hukumu za Sharia, na wakafanya
uharibifu katika nchi kwa uharamia na kunyan'ganya mali, ni kuuliwa pindi
wakiuwa, na kutundikwa msalabani, pindi wakiuwa na wakapokonya mali ya watu, na
kukatwa mikono yao na miguu kwa mabadilisho (yaani mkono wa kulia na mguu wa
kushoto, au kinyume cha hayo), pindi ikiwa watavamia watu njiani na kuwapokonya
mali bila ya kuwauwa. Na ikiwa watawatisha watu tu, basi adabu yao ni kuhamishwa
nchi au wafungwe. Adhabu hizo ni hizaya ya hapa duniani tu, na Akhera watapata
adhabu kuu, nayo ni adhabu ya Motoni.
34. Ila wale walio tubu, miongoni mwa
hawa wanao piga vita nidhamu na wakavamia watu majiani, kabla hamjawatia mkononi
mkawakamata. Basi adhabu ya Mwenyezi Mungu itaondoka, itabaki juu yao haki za
waja wa Mwenyezi Mungu wazirejeshe. Na jueni kuwa Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa
maghfira na rehema.
Katika hukumu
hii inabainishwa kuwa Sharia inaangalia ukhalifu unao athiri jamii, na kwa hivyo
adhabu yake ni kali kwa kuwafikiana na kitisho chake kwa wapendao amani.
Mazingatio hapa si kwa mujibu wa kile kitendo cha ukhalifu, bali kwa mujibu wa
kiasi ya kitisho na fazaa inayo letwa na hicho kitendo.
35. Enyi mlio amini! Mcheni Mwenyezi
Mungu kwa kujitenga na anayo yakataza , na kut'ii amri zake. Na takeni kuyafanya
yatakayo kukurubisheni kupata thawabu zake, nayo ni kutenda mambo ya ut'iifu na
mambo ya kheri. Na wanieni kwa jihadi katika Njia yake kwa kuitukuza Dini yake
na kuwapiga vita maadui zake. Huenda kwa hivyo mkafuzu mkapata karama zake na
thawabu zake.
36. Hakika walio kufuru hata lau kuwa
wana kila namna ya mali yote yaliyomo duniani na mambo mengine yanayo onekana
yenye maana katika uhai, na wakawa nayo mfano wa yaliyomo duniani juu ya hayo
yaliomo humo, na wakataka yawe ni fidiya wajiokoe na adhabu ya Mwenyezi Mungu
Siku ya Kiyama kwa ukafiri wao, basi fidiya hiyo yote haitofaa kitu. Wala
Mwenyezi Mungu hawakubalii hayo. Hapana njia yo yote ya wao kuepukana na malipo
ya ukafiri wao; nao watapata adhabu kali.
37. Hawa makafiri wanatamani kutoka
Motoni, na wala hawatatoka humo. Watapata adhabu ya daima dawamu.
38. Na mwanamume aliye iba, na mwanamke
aliye iba, ikateni mikono yao kuwa ni malipo ya madhambi waliyo yatenda, na njia
ya kuwaonya wenginewe wasitende jambo hilo. Hiyo ni hukumu ya Mwenyezi Mungu, na
amri ya Mwenyezi Mungu ndiyo yenye kushinda, naye ndiye Mwenye hikima katika
kutunga Sharia. Kila ukhalifu ameuwekea malipo yake, yenye kumzuia mtu asitende
tena na wengine watahadhari wasifanye kama hayo. (Ajabu iliopo ni kuwepo wajinga
wakashtushwa na amri hii ya Mwenyezi Mungu aliye tuumba, na wasiseme lolote kuwa
katika China wakati wa vita na Taiwan ilikuwapo sharia ya kuwa mwizi auwawe, na
katika baadhi ya wilaya za Amerika mpaka hii leo ipo sharia ya kuwa mwizi wa
farasi auwawe, na katika Kenya adabu ya wizi wa kutumia nguvu ni kunyongwa, na
katika sharia za Kiingereza na nchi zote za magharibi mtu ana haki ya kuuwa kwa
ajili ya kulinda mali na roho. Ikiwa ni haki ya mtu kumuuwa atakaye kuja kwiba,
jee ni kuu hilo kwa serikali kumkata mkono aliye kwisha iba?) Kwa kuwepo sharia
kama hii ndiyo ikawa wizi umetoweka katika nchi kama Saudi Arabia, na ukawa
vururu kwengineko.
39. Lakini mwenye kutubu baada ya
kutenda kosa lake hilo, na akatengeneza vitendo vyake, na akanyoosha mwendo
wake, basi Mwenyezi Mungu hakika humkubalia toba yake. Hakika Mwenyezi Mungu ni
mwingi mno wa kusamehe na kurehemu.
40. Jua, ewe mwenye fahamu, kwa ujuzi wa
yakini, ya kwamba ni Mwenyezi Mungu peke yake ndiye Mwenye kumiliki kila kitu
kiliomo katika mbingu na ardhi. Yeye humpa adhabu yake amtakaye, kwa hikima yake
na uwezo wake. Na humsamehe amtakaye, kwa hikima yake na rehema yake. Na
Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu.
41. Ewe Mtume! Visikuhuzunishe vitendo
vya makafiri wanao wania ukafiri wa kila aina, hawa wadanganyifu wenye khadaa
wasemao kwa ndimi zao: Tumeamini, ilhali nyoyo zao hazifuati haki. Na miongoni
mwa Mayahudi wapo wanao kithiri kusikiliza uzushi wa makohani wao na
wanayakubali, na wanakisikiliza na kukikubali kikundi maalumu miongoni mwao, na
hawaji barazani kwako kwa sababu ya kiburi na chuki! Na hawa huyageuza
maneno ya Taurati kutokana pahala pake, baada ya Mwenyezi Mungu kwisha
yasimamisha na kuyahukumia! Nao huwaambia wafwasi wao: Mkipewa maneno haya
yaliyo potoshwa na kubadilishwa yakubalini na muyafuate. Na kama mkipewa mengine
tahadharini nayo msiyakubali. Basi, ewe Mtume! Usihuzunike Mwenyezi Mungu
akimhukumia mtu kupotea kwa kumziba moyo wake, wewe hutoweza
kumwongoa, au kumnafiisha kwa chochote asicho mtakia Mwenyezi Mungu.
Na hao ndio walio pita mipaka katika upotovu na inda. Mwenyezi Mungu Mwenyewe
hakutaka kuzisafisha nyoyo zao na uchafu wa chuki, na inadi, na ukafiri. Duniani
watapata madhila, kwa kufedheheka na kushindwa, na Akhera watapata adhabu kuu.
42. Hao hukithiri kusikiliza ili wapate
kuzua, na hukithiri kula mali ya haramu ambayo hayana baraka yoyote, kama
vile rushwa na riba na mengineyo. Basi wakikujia kukutaka uwahukumu, wewe
wahukumu pindi ukiona hayo yana maslaha, au jipuuze nao. Na ukijipuuza nao
hawatokudhuru kwa lolote, kwa kuwa Mwenyezi Mungu ndiye wa kukulinda na watu. Na
ukihukumu baina yao basi hukumu kwa uadilifu alio kuamrisha Mwenyezi Mungu.
Hakika Mwenyezi Mungu huwapenda waadilifu, naye huwahifadhi na huwalipa thawabu.
43. Ama ajabu ya watu hawa Mayahudi!
Vipi wanataka hukumu yako na hali wao wanayo hukumu ya Mwenyezi Mungu imeandikwa
katika Taurati? Na kinacho staajabisha ni kuwa wao huikataa hukumu yako inapo
kuwa haikubaliani na mapendeleo yao, ijapo kuwa imewafikiana na ilivyo katika
kitabu chao! Watu hawa sio miongoni mwa Waumini wanaoit'ii Haki.
44. Hakika Sisi tumemteremshia Musa
Taurati. Ndani yake mna uwongofu unao endea Haki, na mna bayana yenye kutoa
mwangaza unao nawirisha hukumu wanazo zihukumia Manabii, na wale walio safisha
nafsi zao kwa ajili ya Mola wao Mlezi, na wanazuoni wenye kufwata njia ya
Manabii, na wale walio chukua ahadi kukihifadhi Kitabu cha Mwenyezi Mungu
kisibadilishwe, kwa kukilinda na kushuhudia kuwa hicho ndiyo Haki. Basi
msiwakhofu watu mnapo hukumu, na nikhofuni Mimi tu, Mimi Mola wenu Mlezi, Mola
Mlezi wa walimwengu wote. Wala msizibadilishe Aya zangu nilizo ziteremsha kwa
thamani duni ya kutaka starehe ya dunia, kama vile mrungura au kutaka cheo! Na
wote wasio hukumu kwa mujibu alivyo teremsha Mwenyezi Mungu ni miongoni mwa
makafiri.
45. Tumewalizimisha Mayahudi katika
Taurati wafuate sharia ya kisasi kwa ajili ya kuhifadhi maisha ya watu. Basi
tukahukumu mwenye kuuwa auwawe. Mwenye kutofoa jicho la mtu atofolewe.
Kadhaalika pua kwa pua, sikio kwa sikio, jino kwa jino, na jaraha hivyo hivyo
lilipiziwe kisasi ikimkinika. (Hiyo ni hukumu ya Mayahudi kama ilivyo katika
Kutoka 21.23-25; Mambo ya Walawi 24.18-21; Kumbukumbu la Torati 19.21. Katika
Uislamu ipo fursa ya msamaha.)
Mwenye kusamehe akatolea
sadaka ile haki ya kulipiza kisasi kwa mkhalifu, basi hiyo sadaka huwa ni kafara
kwake. Mwenyezi Mungu naye atamfutia sehemu ya madhambi yake. Na watu wasio
hukumu kwa mujibu wa alivyo teremsha Mwenyezi Mungu basi hao ndio wenye
kudhulumu.
46. Na baada ya hawa Manabii tulimtuma
Isa mwana wa Maryamu, naye ni mwenye kufuata njia yao, na kuithibitisha Taurati
iliyo mtangulia. Naye tulimteremshia Injili yenye uwongofu kuelekea Haki,
na yenye kubainisha hukumu, na tuliiteremsha ili isadikishe Taurati iliyo
tangulia, na ndani yake pana uwongofu wa kupelekea Haki, na ni mawaidha kwa
wachamngu. (Tazama Injili ya Mathayo 5.17 maneno ya Nabii Isa: "Msidhani ya kuwa
nalikuja kuitangua torati au manabii; la, sikuja kutangua, bali kutimiliza.")
47. Na Sisi tuliwaamrisha wafuasi wa
Isa, yaani Watu wa Injili, Wakristo, wahukumu kwa hukumu alizo teremsha Mwenyezi
Mungu. Na wasio hukumu kwa mujibu wa alivyo teremsha Mwenyezi Mungu basi hao
wameiacha Sharia ya Mwenyezi Mungu, ni waasi.
48. Na wewe, ewe Nabii, tumekuteremshia
Kitabu kikamilifu, nacho ni Qur'ani, chenye kushikamana na haki katika hukumu
zake zote na khabari zake, chenye kuwafikiana na kuthibitisha Vitabu vyetu
vilivyo tangulia, na kinavishuhudia kuwa ni Vitabu vya Mwenyezi Mungu, na
kinalinda yaliyo sahihi, kwa sababu hii Qur'ani haibadiliki. Basi hukumu baina
ya Watu wa Kitabu, Mayahudi na Wakristo, wakikutaka uwahukumu kwa mujibu alivyo
kuteremshia Mwenyezi Mungu. Wala katika hukumu yako usifuate matamanio yao na
matakwa yao, usije ukapotoka ukaacha Haki iliyo kujia. Kila umma katika
nyinyi watu, tumeujaalia kuwa na njia yake ya kuitambua Haki, na njia iliyo wazi
ya Dini ya kuifuata. Na lau kuwa Mwenyezi Mungu angeli taka angeli kufanyeni
nyote kundi moja lililo wafikiana, lenye mwendo mmoja, hazikhitalifiani njia
zake za kupita kwa zama zote. Lakini Yeye amekujaalieni hivi ili iwe kama
mtihani kwenu katika hizo Sharia alizo kupeni, atambulikane mwenye kut'ii na
mwenye kuasi. Basi tumieni fursa hii, na mfanye haraka kuwania kutenda vitendo
vya kheri. Kwani marejeo yenu nyote yatakuwa kwa Mwenyezi Mungu peke yake. Hapo
atakwambieni hakika ya hayo mliyo kuwa mkikhitalifiana, na kila mmoja wenu
atalipwa kwa a'mali yake.
49. Na wewe ewe Mtume! Tumekuamrisha
uhukumu baina ya watu kwa alivyo teremsha Mwenyezi Mungu, wala usifuate matakwa
yao katika kuhukumu. Na wahadharishe wasije kukugeuza ukaacha baadhi ya aliyo
kuteremshia Mwenyezi Mungu. Pindi wakiipuuza hukumu ya Mwenyezi Mungu na
wakataka nyengineyo, basi jua kuwa Mwenyezi Mungu anataka kuwapatiliza kwa
kuwafisidia mambo yao, kwa vile zilivyo kwisha fisidika nafsi zao kwa sababu ya
madhambi yao waliyo yatenda kwa kukhalifu hukumu zake na Sharia yake.
Kisha atawalipa vitendo vyao vyote huko Akhera (1). Na hakika watu wengi
ni wenye kuziasi hukumu za Sharia.
(1) Maneno haya yanatukuza Sharia ya Kiislamu katika
kuwahukumu watu. Kwanza inatukuka kwa kuwa ni hukumu ya uadilifu na
haifuati mipango ya watu ijapo kuwa ni mipotovu, bali inahukumu juu ya hiyo
mipango ya watu kwa kheri na shari. Pili Kanuni huwa katika dola ni moja tu kwa
watu wote na mat'abaka yote.
50. Je, hao wanao kataa amri na makatazo
ya Mwenyezi Mungu wanataka wahukumiwe kwa hukumu ya Kijahiliya, ya
kijinga, ya kabla ya kufika Uislamu, kulipo kuwa hapana uadilifu, bali
matamanio ya nafsi tu ndiyo yliyo kuwa yakihukumu, na mapendeleo na
udanganyifu ndio msingi wa hukumu? Huo ndio mwendo wa watu wa zama za
Kijahiliya! Yuko aliye bora kuliko Mwenyezi Mungu kuhukumu watu wenye kuyakinika
na Sharia na wenye kunyenyekea Haki? Kwa hakika hao ndio wanao tambua ubora wa
hukumu za Mwenyezi Mungu.
51. Enyi mlio amini! Si halali kwenu
kuwachukua Mayahudi na Wakristo mkawafanya ndio marafiki zenu. Wao hao ni sawa
sawa katika kukufanyieni uadui. Na mwenye kufanya urafiki nao, basi ni kundi
moja nao. Na hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi wanao jidhulumu nafsi zao kwa
kufanya urafiki na makafiri.
52. Ilivyo kuwa kuwafanya hao marafiki
hawafanyi ila walio dhulumu, basi utaona kuwa wanao wafanya makafiri ndio rafiki
zao wana maradhi katika nyoyo zao, maradhi ya udhoofu na unaafiki. Wao husema:
Tunaogopa usije kutupata msiba kwa kugeuka mambo na wao wasitusaidie!
A'saa, huenda, Mwenyezi Mungu akamletea Mtume wake kufunguka mambo, na Waislamu
wakawashinda maadui zao, au ukadhihiri unaafiki wa hao wanaafiki, wakaamkia
majuto, wakijuta kwa zile kufuru na shaka shaka walizo kuwa wakizificha katika
nafsi zao.
53. Na hapo tena Waumini wa kweli
watasema kuwastaajabia wanaafiki: Ndio hawa walio kula yamini kwa viapo vya
kupita kiasi kwa jina la Mwenyezi Mungu, ya kwamba wao ni wenzenu katika Dini,
wenye kuamini kama nyinyi? Wamesema uwongo! Na vitendo vyao vimefisidika, wakawa
wamekosa Imani na nusura kutokana na Waumini.
54. Enyi mlio amini! Mwenye kurejea
ukafirini katika nyinyi, baada ya kuamini, hamdhuru kitu Mwenyezi Mungu. Yeye
ametukuka na hayo. Badala yao ataleta kaumu iliyo bora kuliko hao, na wao hao
Mwenyezi Mungu atawapenda, na atawafikisha kwenye uwongofu, na ut'iifu. Na wao
watampenda Mwenyezi Mungu, kwa hivyo watamt'ii. Nao watakuwa na unyenyekevu na
huruma kwa ndugu zao Waumini, na watakuwa wakali na wenye nguvu mbele ya maadui
zao makafiri. Watapigana jihadi kwa njia ya Mwenyezi Mungu, wala hawaogopi
lawama yoyote ya mwenye kulaumu! Hiyo ni fadhila ya Mwenyezi Mungu humpa
amtakaye anaye muwafikia kheri. Na Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa fadhila kwa anaye
stahiki.
55. Enyi Waumini! Urafiki wenu
nyinyi uwe na Mwenyezi Mungu na Mtume wake, na nyinyi kwa nyinyi katika wanao
shika Sala, na wanatoa Zaka, nao wananyenyekea.
56. Na mwenye kufanya urafiki na
Mwenyezi Mungu, na Mtume wake, na Waumini na wakawa hao ndio wa kuwategemea kwa
msaada na nusura, basi huyo atakuwa katika Hizbu (yaani kundi) ya Mwenyezi
Mungu, na Hizbu ya Mwenyezi Mungu ndio yenye kushinda na kufuzu.
57. Enyi mlio amini! Msiwafanye maadui
wa Uislamu walio ifanyia maskhara Dini yenu wakaichezea - nao ni Mayahudi na
Wakristo na washirikina, kuwa ndio wasaidizi, wala msifanye urafiki nao. Na
mkhofuni Mwenyezi Mungu ikiwa nyinyi ni wakweli katika Imani yenu.
58. Na katika kejeli zao kukufanyieni ni
vile pale mnapo ita kwenda kusali katika adhana, wao huifanyia maskhara Sala
yenu, na hukuchekeni, wakafanya ni mchezo. Na hayo ni kwa sababu kuwa wao ni
kaumu wasio na akili, wala hawatambui farka iliopo baina ya upotofu na uwongofu.
59. Sema ewe Mtume! Enyi Watu wa Kitbu!
Hivyo mnatuchukia kwa kuwa tunamuamini Mwenyezi Mungu na tunaamini tuliyo
teremshiwa sisi, nayo ni Qur'ani, na Vitabu vilio sahihi vilio teremshiwa
Manabii wa zamani, na kwa kuwa tunaamini kuwa wengi wenu mmeitupa Sharia ya
Mwenyezi Mungu?
60. Waambie: Nikwambieni malipo maovu
kabisa kutokana na Mwenyezi Mungu? Ni hivyo vitendo vyenu nyinyi mlio tengwa
mbali na Mwenyezi Mungu na rehema yake, na mkakasirikiwa kwa sababu ya ukafiri
wenu na uasi wenu, na mkazibwa nyoyo zenu, mkawa kama manyani na nguruwe, na
mkamuabudu Shetani, na mkafuata upotovu. Nyinyi ndio mko katika daraja ya mwisho
katika shari, kwa sababu nyinyi ni watu walio potea kabisa, mkaiwacha Njia ya
Haki.
61. Wanaafiki wakikujia husema uwongo,
na hukwambia: Tumeamini. Nao wamekuingilia na hali ni makafiri, na wametoka
kwenu nao ni makafiri vile vile! Na Mwenyezi Mungu anaujua vyema unaafiki
wanao uficha. Na Yeye ndiye atakaye waadhibu.
62. Na utawaona wengi wao hawa
wanakimbilia kufanya maasi na kuwatendea uadui wengineo, na pia katika kula mali
ya haramu kama rushwa (mrungura) na riba! Uwovu gani huu wautendao!
63. Si ingelikuwa vyema lau kuwa
wanazuoni wao na makohani wangeli wakataza kusema uwongo, na kula haramu? Uwovu
mkubwa huo wanao ufanya kwa kuacha kusemezana na kukatazana maasi.
64. Mayahudi walisema: Mkono wa Mwenyezi
Mungu umefumba, haukukunjuka ukatoa! Mwenyezi Mungu ameifumba mikono yao wao, na
amewatenga mbali na rehema yake! Mwenyezi Mungu ni Mkwasi, anajitosha. Yeye
hutoa apendavyo. Na hakika wengi wa watu kwa kupita kiasi katika upotovu wao,
haya yalio teremka kwako huwazidisha udhalimu na ukafiri, kwa sababu ya chuki na
husda yao. Na Sisi tumetia baina yao kwa wao uadui na bughdha mpaka Siku ya
Kiyama. Kila wanapo washa moto kumpiga vita Mtume na Waumini, Mwenyezi Mungu
huuzima kwa kumpa ushindi Nabii wake na wafuasi wake. Na wao wanajitahidi
kueneza fisadi katika nchi, na kufanya vitimbi, na kutia fitina, na kuchochea
vita. Na Mwenyezi Mungu hawapendi mafisadi.
65. Na lau kuwa Watu wa Kitabu, yaani
Mayahudi na Wakristo, wangeli uamini Uislamu na Nabii wake, na wakaacha madhambi
tuliyo yataja, tungeli wafutia makosa yao, na tungeli watia katika Bustani
(Pepo) za neema, wakastarehe humo.
66. Na lau kuwa wao wamezihifadhi
Taurati na Injili kama zilivyo teremshwa, na wakazitenda, na wakaamini yote
waliyo teremshiwa kutokana na Mola wao Mlezi, nayo ni Qur'ani, Mwenyezi Mungu
angeli wakunjulia riziki ikiwajia kutoka kila upande. Na wao si wote sawa katika
upotovu. Miongoni mwao, wapo jamaa walio waadilifu, wana akili zao timamu. Hao
ndio wale walio muamini Muhammad na wakaiamini Qur'ani. Lakini wengi wao
wanatenda vitendo viovu, na wanasema mabaya, na wanajitenga na haki.
67. Ewe uliye tumwa na Mwenyezi Mungu!
Waeleze watu yote uliyo funuliwa na Mola wako Mlezi, na waite wafuate huo
ujumbe, wala usiogope maudhi ya yeyote. Na ukitofanya hivyo basi imekuwa
hukufikisha ujumbe wa Mwenyezi Mungu. Kwani wewe umekalifishwa ufikishe ujumbe
kwa watu wote. Na Mwenyezi Mungu atakulinda na maudhi ya makafiri. Ni mtindo
wake Mwenyezi Mungu kuwa hamnusuru aliye potea akaiacha Haki. Hakika
Mwenyezi Mungu hawaongoi makafiri kwenye Njia iliyo kaa sawa.
68. Ewe Mtume! Waambie Watu wa Kitabu
(yaani Biblia): Hakika nyinyi hamtakuwa mnafuata Dini sahihi ila mtapo zitangaza
hukumu zote za Taurati na Injili na mkazitenda. Na mkaiamini Qur'ani iliyo
teremshwa na Mwenyezi Mungu kwa Mtume wake kwa ajili ya kuwaongoa watu. Na
yakinika, ewe Mtume, kwamba wengi wa Watu wa Kitabu watazidi udhalimu, na
ukafiri, na inadi, juu ya Qur'ani kwa uhasidi wao na chuki. Basi usiwahuzunikie
watu ambao wametiwa muhuri wa upinzani.
69. Hakika walio muamini Mwenyezi Mungu
(yaani Waislamu), na wafwasi wa Musa katika Mayahudi, na walio toka kwenye dini
nyenginezo, na wafwasi wa Isa katika Manasara - wote hao wakisafisha imani yao
kwa Mwenyezi Mungu, na wakaamini kufufuliwa na malipo na wakatenda mema kama
ilivyo funzwa na Uislamu, hao wote watasalimika na adhabu na watakuwa katika
furaha ya Peponi Siku ya Kiyama.
70. Sisi tuliagana na Mayahudi, Wana wa
Israili, kwa agano madhubuti katika Taurati kuwa wafuate hukumu zake. Na
tukawapelekea Manabii wengi wawabainishie, na wawatilie mkazo ahadi yetu. Lakini
walivunja ahadi.Wakawa kila akiwajia Mtume ambaye hakuwafikiana na matamanio
yao, ama walimkanusha au walimuuwa.
71. Na hao Wana wa Israili walidhani
hawatapata majaribio, yaani shida za kuwafafanua baina ya walio simama imara na
wasio simama imara. Kwa hivyo hawakuweza kustahamili, bali wengi wao walipotea
wakawa kama vipofu na viziwi. Wakaiacha Haki, na Mwenyezi Mungu akawapatiliza
kwa madhila. Baadae walipo rejea kwa Mwenyezi Mungu na wakatubu, alikubali toba
zao, na akawarejeshea utukufu wao. Lakini baadae tena wakaingia katika upotofu,
na wakawa kama vipofu na viziwi! Na Mwenyezi Mungu anawajua vyema, na
atashuhudia vitendo vyao, na atawalipa kwavyo.
72. Wenye kudai kuwa Mwenyezi Mungu yu
katika Isa bin Maryam hata akawa yeye Mungu, kama wasemavyo Wakristo hii leo,
hakika wamekufuru! Yeye Isa hana dhambi ya haya, kwani hakupata kudai hivyo hata
mara moja. Bali yeye aliwaamrisha Wana wa Israili wamsafie imani Mwenyezi Mungu
peke yake kwa kusema: Hakika Mwenyezi Mungu ndiye aliye niumba mimi na nyinyi,
na ndiye anaye niendeshea mambo yangu yote, na kwamba kila mwenye kumshirikisha
Mwenyezi Mungu malipo yake ni kuwa hatoingia Peponi kabisa, bali ataingia
Motoni, kwa kuwa amekiuka mipaka ya Mwenyezi Mungu. Na mwenye kuvunja mipaka
yake hataepuka na adhabu.(Yesu kasema: "Sikia, Israeli, Bwana Mungu wetu ni
Bwana mmoja." Marko 12.28. "Mimi siwezi kufanya neno mwenyewe".Yohana 5.30
"Ninapaa kwenda kwa...Mungu wangu naye ni Mungu wenu." Yohana 20.17 )
73. Haiwi mwenye kudai kuwa Mwenyezi
Mungu ni mmoja katika Utatu, kama wadaivyo Wakristo sasa, awe anamuamini
Mwenyezi Mungu.!! Na hakika iliyo thibiti ni kuwa hapana mungu ila Mwenyezi
Mungu mmoja pekee. Na ikiwa hawa walio potoka hawatoacha itikadi zao potovu,
wakarejea kwenye ut'iifu wa Mwenyezi Mungu, hapana budi ila itawasibu adhabu
kali. (Biblia inasema kuwa ya kwanza katika Amri Kumi alizo pewa Musa ni: "Usiwe
na miungu mingine ila mimi." - Kutoka 20.3. "Wewe umeonyeshwa haya, ili upate
kujua ya kuwa Bwana ndiye Mungu, hapana ila yeye." - Kumbukumbu la Torati 4.35.
Katika Injili ya Yohana 17.3 Yesu anamsemeza Mwenyezi Mungu: "Na uzima wa milele
ndio huu, Wakujue wewe, Mungu wa pekee wa kweli na Yesu Kristo uliyemtuma.")
74. Je! Watu hawa hawaziachilii mbali
hizo itikadi za uzushi na uwongo, wakarejea kwenye Imani ya Mwenyezi Mungu, na
wakaomba wafutiwe dhambi zao walizo zitenda? Hakika Mwenyezi Mungu ni Mkunjufu
wa maghfira, Mwingi wa rehema.
75. Isa bin Maryamu si chochote ila ni
mwanaadamu aliye pata neema ya Mwenyezi Mungu kwa kuteuliwa kuwa ni Mtume kama
walivyo mtangulia wengi kabla yake. Na Mama yake Isa ni mmoja katika wanawake,
aliye jaaliwa kuwa ni mkweli katika kauli yake na mwenye kumuamini Mola wake
Mlezi. Na yeye na mwanawe, Isa, walikuwa wana mahitajio yanayo hitajiwa na kila
mwanaadamu, kama kula na kunywa, na kwenda haja. Na hizo ni dalili za ubinaadamu
wao. Basi hebu zingatia, ewe mwenye kusikia, hali ya hao walio ingia upofu hata
hawaoni dalili za Ishara zilizo wazi ambazo amewabainishia Mwenyezi Mungu. Tena
zingatia vipi wanaiacha Haki juu ya kuwa ni iwazi kabisa.
76. Ewe Mtume! Waambie hawa wapotovu:
Vipi mnamuabudu mungu asiye weza kukudhuruni kwa lolote mkiacha kumuabudu, wala
hawezi kukufaeni kwa lolote mkimuabudu!! Vipi mnaacha kumuabudu Mwenyezi Mungu
ambaye Yeye ndiye Mungu Mwenye uweza wa kila kitu, naye ni Mwenye kusikia, na
Mwenye ujuzi.
77. Ewe Mtume! Waambie Watu wa Kitabu,
yaani Mayahudi na Wakristo: Mwenyezi Mungu anakukatazeni msivuke mipaka katika
itikadi zenu hata mkaingia katika upotovu, mkawafanya baadhi ya viumbe vyake
kuwa ni miungu; au mkakanusha ujumbe wa baadhi ya Mitume. Na anakukatazeni
kufuata matamanio ya watu walio kutangulieni, walio acha njia ya uwongofu, na
wakawazuia watu wengi kuifuata njia hiyo, na wakaendelea katika kuiepuka Njia ya
Haki.
78. Mwenyezi Mungu amewatenga mbali na
rehema yake wale makafiri miongoni mwa Wana wa Israili, na haya yameteremka
katika Zaburi juu ya Nabii wake Daud, na katika Injili juu ya Nabii wake Isa
mwana wa Maryam. Na hayo ni kwa sababu ya uasi wao, kutokana na ut'iifu wa
Mwenyezi Mungu na kuzama kwao katika udhalimu na ufisadi.(Katika Zaburi Daud
anawaapiza Mayahudi:"Wewe, Mungu, uwapatilize. Na waanguke kwa mashauri yao,
Uwatoe nje kwa ajili ya wingi wa makosa yao, kwa maana wamekuasi Wewe." - Zaburi
5.10. Katika Injili Yesu anawalaani: "Enyi nyoka, wana wa majoka, mtaikimbiaje
hukumu ya jehannum?" - Mathayo 23.33.)
79. Mtindo wao ulikuwa kutoambizana.
Hapana amkatazaye mwenzie kufanya uovu. Kufanya kwao uovu na kuacha kukatazana
ni katika vitendo vinavyo chusha mno!
80. Utawaona wengi miongoni mwa Wana wa
Israili hufanya urafiki na washirikina, mapagani, na wanawafanya hao ndio wenzi
wao wakishirikiana katika kuupiga vita Uislamu! Kitendo hichi kiovu
wanajirimbikizia wenyewe nafsi zao, waje kupata malipo yake kwa kupata ghadhabu
ya Mwenyezi Mungu, na wapate kudumu milele katika adhabu ya Jahannamu.(Hayo
yalikuwa zama za Mtume s.a.w. na mpaka hii leo. Mayahudi wanatafuta kila rafiki
ambaye atauvunja Uislamu, ilhali yafaa wawaone Waislamu ndio wa karibu mno nao,
kwa kuwa wanaamini Mungu Mmoja na wanaamini Manabii wao wote.)
81. Na lau kuwa itikadi yao ni sawa kama
inavyo faa iwe kwa kumuamini Mwenyezi Mungu, na Mtume wake Muhammad s.a.w., na
Qur'ani aliyo teremshiwa, basi wasingeli wafanya makafiri kuwa ni wenzao
kuwapinga Waumini. Lakini wengi miongoni mwa Wana wa Israili ni maasi, wameacha
dini.
82. Ewe Nabii! Tunakuhakikishia ya
kwamba utaona hapana watu wanao kuchukia na kukubughudhi wewe na wanao kuamini
kama Mayahudi na hawa wanao mshirikisha Mwenyezi Mungu katika ibada. Na
utawakuta walio karibu mno nawe kwa mapenzi ni wafwasi wa Isa, walio jiita
wenyewe "Manasara". Kwa sababu wamo miongoni mwao makasisi wanao ijua dini yao,
na marahibu (mamonaki) wat'awa, wanao mcha Mola Mlezi, na kuwa wao hawana kiburi
cha kuwazuia wasisikie Haki. (Na haya yameonakana kuwa Waislamu wengi duniani
asili yao walikuwa Manasara, Wakristo. Wao wakisha pata fursa ya kuufahamu
Uislamu huufuata, lakini ni wachache miongoni mwa Mayahudi walio silimu. Kinacho
wazuia ni kiburi. Lakini walio silimu basi wamekuwa Waislamu wakubwa.)
83. Na pia miongoni mwa Manasara
wakiisikia Qur'ani aliyo teremshiwa Mtume huathirika nayo, macho huwatiririka
machozi, kwa kuwa wanajua kuwa wanayo yasikia ni kweli tupu, basi nyoyo zao
humili kwayo, na ndimi zao huomba dua kumwomba Mwenyezi Mungu kwa kusema: Mola
wetu Mlezi! Tumekuamini Wewe na Mitume wako, na Haki ulio wateremshia. Basi
ipokee Imani yetu, na utufanye miongoni mwa Umma wa Muhammad ulio wafanya
mashahidi na hoja kwa watu wote Siku ya Kiyama.
84. Na nini cha
kutuzuia tusimsadiki Mwenyezi Mungu peke yake, na Haki iliyo teremka kwa
Muhammad? Na hali sisi tunamtaraji Mwenyezi Mungu atuingize Peponi pamoja na
watu wenye Imani njema na vitendo vyema.
85. Kwa hivyo Mwenyezi Mungu
amewaandikia malipo kwa vile kuungama kwao, nayo ni Bustani yenye kupita mito
chini ya miti yake, na majumba ya fakhari ya kukaa humo daima, pamoja na watu
ambao ni njema itikadi zao na vitendo vyao.
86. Na walio
mpinga Mwenyezi Mungu na Mitume wake, na
wakazikanya dalili alizo wateremshia
kuwa ni uwongofu wa kufikia Haki, ni wao peke yao wanao
stahiki adhabu kali katika Jahannamu.
87. Enyi mlio amini! Msijiharimishie
nafsi zenu vitu vizuri alivyo kuhalalishieni Mwenyezi Mungu, wala msipite mipaka
aliyo kuwekeeni Mwenyezi Mungu ya kufuata mambo ya wastani. Hakika Mwenyezi
Mungu hawapendi watu wanao pindukia mipaka.
88. Na kuleni vitu alivyo kupeni
Mwenyezi Mungu na akavifanya vyepesi kwenu, na akavifanya ni halali na ni vizuri
kwa nafsi zenu. Na daima mwogopeni Mwenyezi Mungu, na mt'iini Yeye maadamu
nyinyi mnamuamini Yeye.
89. Mwenyezi Mungu hakutiini adabu kwa
sababu ya kuapa kiapo msicho kusudia. Bali hakika Yeye hukutieni adabu kwa
sababu ya kuvunja viapo mlivyo vikusudia na yamini mliyo jifunga nayo. Basi
ikiwa mmevunja kiapo itakupaseni mfanye jambo la kukughufirieni dhambi zake.
Na mambo yenyewe ni: kuwalisha mafakiri kumi kwa siku moja, kwa chakula
cha kawaida mnacho kila nyinyi na jamaa zenu mnao waangalia, yaani watu wenu wa
nyumbani bila ya israfu wala ubakhili. Au kuwavika mafakiri kumi kwa kivazi
kilicho zowewa. Au kumkomboa mtu kutoka utumwani. (Na mfano wa mtumwa ni mtu
alioko kifungoni kwa dhulma, au chini ya utawala wa dhulma.) Ikiwa mwenye
kuapa hawezi kutenda lolote katika hayo, basi itampasa afunge siku tatu. Na kila
moja katika mambo haya hufuta dhambi za mwenye kuapa kiapo cha kutilia niya na
akakivunja. Nanyi zilindeni yamini zenu, msiape katika mambo yasiyo kuwa laiki
yake, na wala msiache kutenda kitendo cha kughufiria dhambi pindi mkivunja
kiapo. Kwa mpango huu Mwenyezi Mungu anakufafanulieni hukumu zake ili mpate
kushukuru neema zake kwa kuzijua na kuzifuata vilivyo.
Katika hukumu ya yamini pana mawili
yafaa tuyazingatie. Kwanza: Uislamu umeraghibisha sana kukomboa watumwa.
Sababu nyingi zinazo wajibisha hayo. Kafara nyingi za dhambi zinahitaji
kukomboa. Kafara ya kula mchana Ramadhani yahitaji ukombozi, n.k. Na katika hayo
yanaonyesha Uislamu unachukia utumwa. Uislamu uliukiri utumwa kwa kuwa maadui
wao walikuwa wakiwatia utumwani Waislamu, basi na Uislamu ukaruhusu kuwatendea
wao vivyo hivyo. Pili: Uislamu unakazania kulisha masikini kila
ikipatikana fursa.
90. Enyi wenye kumsadiki Mwenyezi Mungu
na Vitabu vyake na Mitume wake, wenye kuifuata Haki! Kunywa au kuvuta chochote
kinacho lewesha, kucheza kamari, na kusimamisha mawe ya kutolea mihanga kwa
ajili ya masanamu mnayo yaabudu, na kuagua kwa mishale (1), na mawe, na karatasi
za kuagulia kudra iliyo ghaibu...yote hayo si chochote ila ni uchafu wa kiroho,
na upotovu. Na hayo ni kupambiwa na Shetani tu. Basi yaachilieni mbali ili mpate
kufuzu duniani kwa maisha bora, na Akhera mpate Janna yenye neema.
(1) Kuagua kwa mishale: ilikuwa
ikiandikwa juu ya vijiti, kimoja kiliandikwa: "Mola wangu Mlezi kaniamuru", na
kingine:"Mola wangu Mlezi kanikataza", na kingine hakikuandikwa kitu. Hutiwa
vijiti hivyo katika mfuko kisha huchanganywa, na kohani hutia mkono wake
akachomoa kimojapo, na akamjuvya mwenye kuuliza lilio aguliwa.
91. Bila ya shaka Shetani hana atakalo
kwa kukushawishini kunywa ulevi na kucheza kamari ila kuleta khitilafu na ugomvi
na kuchukiana baina yenu ili mdhoofike kwa kuondoka masikizano, na uvunjike
umoja wenu, kwa sababu anavyo kukupendeleeni mnywe ulevi na mcheze kamari. Na
hayo ili mpate kuacha kumuabudu Mwenyezi Mungu, na muache Sala, ili Akhera yenu
iwe ovu kama ilivyo dunia yenu. Basi jee! Baada ya nyinyi kujua maovu haya
hamyatupilii mbali ninayo kukutazeni, mkamkosesha Iblisi makusudio yake?
Mwenyezi Mungu Mtukufu Aliye takasika
ametaja mambo mane yaliyo pelekea kuharimishwa ulevi na kamari:
* La Kwanza - Kuwa nafsi yake ni
uchafu na uovu, kwani hayumkiniki kusifika kuwa ni mambo mazuri, kwa kuwa
madhara yake yanaonekana wazi. Katika ulevi kuna uharibifu wa akili, na katika
kamari ni kupoteza mali, na kwa yote mawili hayo upo uharibifu wa moyo. Na
Shetani ndiye mwenye kuyapamba hayo.
* La pili - Hayo hueneza uadui na chuki. Kamari humalizikia
ugomvi, na kama haifikii hayo basi huleta chuki na bughdha. Na ulevi ndio
Mama wa Maasi. Utamwona mtu mwenye adabu zake mpole, akisha kunywa hugeuka nyama
mwitu, akatenda mambo ya ukhalifu, kwani ulevi huidhoofisha sauti ya utu inayo
mkataza mwanaadamu kutenda maovu. Utamwona mtu anajizuia kufanya kitendo kiovu,
lakini akisha kunywa ulevi, au akavuta bangi, japo kidogo, huiendea shari bila
ya kujali. Basi si kama ulevi unaharibu akili tu, bali unalaza dhamiri ya mtu.
Anakuwa hana junaha.
* La
tatu: Ni kuwa kamari na ulevi huuwa moyo. Mtu huwa hamkumbuki Mwenyezi Mungu, na
kumkumbuka Mwenyezi Mungu ndiko kunako huisha nyoyo.
* Lane: Maasi hayo yanamzuilia mtu na
Sala. Kamari na ulevi humsahaulisha Muumini na Sala zake, na akiwa anasali
hatimizi nguzo zake kama zitakikanavyo. Basi inakuwa Sala zake ni kuinama na
kuinuka bila ya kufuatana na moyo. Kwa hivyo basi imethibiti kuwa
kuharimishwa mvinyo, pombe, tembo, bangi n.k. si kwa sababu ya kulevya kwake tu,
bali ni kwa kumziba mtu fahamu zake, kumgubika asitambue atendalo. Na kwa hivyo
ndio imepokewa kuwa kinacho levya kwa wingi wake, basi hata kidogo chake ni
haramu, kwani hicho kidogo nacho kinapumbaza akili. Na juu ya haya pana madhara
ya mwili kama madaktari walivyo thibitisha.
Kwa hivyo ulevi hata kidogo ni haramu. Mwenyezi Mungu
Subhanahu ametaja sababu mbili za kuharimisha ulevi, na udaktari
umezidisha kuwa ulevi kidogo haupotezi akili, lakini huzidisha uchangamfu au
husabibisha hali ya huzuni na kuona dhiki ya moyo. Na katika hali zote mbili
anakuwa mtu amepungukiwa na ukamilifu wa akili yake kubeba jukumu, na kwa hivyo
hutenda vitendo ambavyo kwa dhahiri ni sawa kumbe ni madhara. Ama kuuzoea ulevi
hudhuru maini, matumbo, na mishipa ya akili na hisiya, na hurithisha madhara
mpaka kwa vizazi.
92. Na fuateni amri ya Mwenyezi Mungu na
amri ya Mtume wake kwa yale anayo kuleteeni kutoka kwa Mola wake Mlezi. Na
yaepukeni mbali yatakayo kuleteeni adhabu mnapo kwenda kinyume. Mkitofuata anayo
kuamrisheni Mwenyezi Mungu kuweni na yakini kuwa Yeye atakupeni adabu. Wala
nyinyi hamna udhuru wowote baada ya kuwa Mtume amekwisha wabainishieni adabu ya
kupewa wakhalifu. Na hakika haimpasi Mtume wetu ila kukujuvyeni hukumu zetu tu,
na kukubainishieni kwa ukamilifu wa uwazi.
93. Walio mkubali Mwenyezi Mungu na
Mtume wake, na wakatenda mema, hawana dhambi kwa vyakula vya halali na vizuri
wanavyo kula, wala vya haramu walivyo wahi kula zamani kabla hawajajua kuwa ni
haramu, ikiwa wanamkhofu Mwenyezi Mungu na wakajitenga navyo vyakula hivyo baada
ya kujua kuwa vinakatazwa. Kisha ikawa wao wakaendelea kumkhofu Mwenyezi Mungu
na kuzikubali sharia zake, na kisha wakadumu katika khofu yao ya kumwogopa
Mwenyezi Mungu katika kila hali, na wakawa wanafanya a'mali zao kwa usafi wa
niya, na kwa njia ya ukamilifu. Kwani hakika Mwenyezi Mungu huwalipa wenye
ikhlasi katika vitendo vyao kwa kadri ya ikhlasi yao na a'mali yao.
94. Enyi mlio amini! Hakika Mwenyezi
Mungu anakufanyieni mtihani wakati wa Hija kwa kukuharimishieni baadhi ya
wanyama na ndege ambao mnaweza kuwawinda kwa wepesi kwa mikono yenu na mikuki
yenu. Makusudio ni kutaka wajuulikane ambao wanamt'ii Mwenyezi Mungu ijapo kuwa
hawaonekani na watu. Na wanao pindukia mipaka aliyo iweka Mwenyezi Mungu baada
ya kuibainisha watakuja pata adhabu kali.
95. Enyi ambao mmeamini! Msiuwe nyama wa
kuwinda nanyi mmenuia Hija na Umra na mmo kuzitimiliza. Na mwenye kumuuwa
mnyama kama huyo kwa kukusudia basi itampasa atoe fidiya mfano wa mnyama aliye
muuwa, ikiwa katika ngamia, ng'ombe au kondoo. Na hujuulikana huyo mfano wake
kwa kukadiriwa na watu wawili waadilifu kati yenu, wahukumu na wawape mafakiri
kwenye Al Kaaba, au atoe badala yake awape, au atoe chakula kadiri ya yule
mnyama kuwapa mafakiri. Kila fakiri apewe chakula cha kumtosha kutwa yake. Hayo
ndio kuondoa dhambi za kuwinda kuliko katazwa. Au badala ya hayo yote, afunge
idadi ya siku za kadri ya wale masikini iliyo mbidi kuwalisha lau angewalisha.
Na Mwenyezi Mungu amelazimisha hayo ili huyo mwenye kufanya lile kosa apate
kuhisi matokeo ya kosa lake na uwovu wa malipo yake. Mwenyezi Mungu, lakini,
amesamehe ukhalifu ulio tendekea kabla ya jambo hilo halijaharimishwa. Na mwenye
kurejea tena kufanya uovu baada ya kujua kuwa ni haramu, basi hakika Mwenyezi
Mungu atampa adabu kwa kitendo chake, naye Mwenyezi Mungu ni Mwenye kushinda
hashindiki, Mkali wa kumuadhibu anaye kakamia kutenda dhambi. (Tunaona kuwa
Uislamu ulianzisha kulinda mazingara, na utajiri wa asili tangu hapo kale.
Kutokana na kuhifadhiwa wanyama na ndege wa porini huko Makka, ndio hii leo
tunaona zipo nyanda na mapori yanayo hifadhiwa wanyama wake, kwa mujibu wa
utaalamu wa kisasa.)
96. Mwenyezi Mungu amekuhalalishieni
kuvua wanyama wa baharini, na muwale, na wanufaike kwao wakaazi wenyeji na
wasafiri. Na amekuharimishieni kuwinda wanyama wa bara wasio fugwa kwa kawaida
majumbani, katika muda ule unapo kuwa katika Hija au Umra, kwenye eneo takatifu
linalo itwa Alharam. Na mzingatieni Mwenyezi Mungu, na iogopeni adhabu yake.
Basi msende kinyume naye, kwani nyinyi mtarejea kwake Siku ya Kiyama, na hapo
atakulipeni kwa yote mliyo yatenda. (Huu ni mfano katika mifano mingi ya Uislamu
tangu hapo kale unavyo pendelea kulinda tabia ya mazingara kwa kuhifadhi wanyama
wasiuliwe ovyo, na miti isikatwe ovyo, na hata maji ya mito na maziwa yasitumiwe
kwa fujo, kwani Mwenyezi Mungu hawapendi wafujaji!)
97. Mwenyezi Mungu ameijaalia Al Kaaba,
nayo ni hiyo nyumba aliyo itukuza na akaharimisha watu na wanyama kufanyiwa
uadui ndani yake na karibu yake, ameijaalia kuwa yenye kusimama na yenye
kutukuzwa, na yenye kuwapa amani watu, na iwe ndiyo Kibla cha kuelekea watu
katika Sala zao, na watu waiendee kwa Hija wawe ni wageni wa Mwenyezi Mungu, na
ili watende yale ya kuupa nguvu umoja wao. Hali kadhaalika ameufanya mwezi wa
Hija na wanyama wanao tolewa dhabihu, na khasa wale wanao vishwa vigwe ili
watambuliwe na wanao waona kuwa hao wametolewa hidaya kwenye hiyo Nyumba. Na
natija ya kuweka yote hayo ni kuwa mpate kuyakinika kuwa ujuzi wake Mwenyezi
Mungu umeenea kila kitu kilioko mbinguni kunakotoka wahyi (ufunuo) wa sharia, na
umeenea duniani, anako weka sharia ya kuwaletea watu maslaha yao. Na hakika
ujuzi wa Mwenyezi Mungu umeenea juu ya kila kitu.
98. Enyi watu! Jueni kuwa adhabu ya
Mwenyezi Mungu ni kali, humteremkia anaye halalisha vya haramu, naye pia ni
Mwingi wa kusamehe dhambi za mwenye kutubu na akaingia kumt'ii. Naye ni Mwenye
rehema sana, na kwa hivyo hamchukulii mtu papo kwa papo kwa kila alitendalo.
99. Haimlazimikii Mtume ila kuwafikishia
watu anayo funuliwa yeye, ili isimame hoja juu yao na wasiwe na kisingizio
chochote cha kuwa ati hawakuonywa wala hawakufunzwa. Basi yajueni anayo
kuleteeni Mtume, kwani Mwenyezi Mungu anayajua mnayo dhihirisha na mnayo
yaficha.
100. Ewe Nabii! Waambie watu: Si sawa
sawa vile vizuri anavyo kuhalalishieni Mwenyezi Mungu na vibaya anavyo
kuharimishieni. Kwani farka iliyo baina ya viwili hivyo kwa Mwenyezi Mungu ni
kubwa, na hata hivyo vibaya vingawa ni vingi na vinawapendeza watu wengi. Basi
enyi wenye akili! Ufanyeni ut'iifu kwa Mwenyezi Mungu uwe ni kinga yenu
isikupateni adhabu yake kwa kukhiari vilivyo vyema, na kujiepusha na viovu, ili
mpate kuwa miongoni walio fuzu duniani na Akhera.
101. Enyi mlio amini! Msimuulize Nabii
mambo ambayo Mwenyezi Mungu amekuficheni mkataka yafichuliwe, na mkamuuliza
Nabii katika uhai wake, kwani Qur'ani inamteremkia bado. Na Mwenyezi Mungu
atakubainishieni itapo hitajika. Mwenyezi Mungu amekusameheni kwa yasiyo tajwa,
hatokuadhibuni kwayo. Na Mwenyezi Mungu ni Mwingi wa maghfira, na Mwenye wasaa
katika upole. Basi hana papara katika kuadhibu.
102. Katika jamaa walio kutangulieni
walikuwapo walio uliza mfano wa haya, mambo mazito mazito; na Manabii wao
walipo wakalifisha ya kufanya wakaona mazito kuyatenda, wakayaacha, na wakawa ni
wenye kuyakanya. Kwani Mwenyezi Mungu hupendelea wepesi, wala hapendelei uzito;
na huwakalifisha watu kwa wanayo yaweza.
103. Mwenyezi Mungu hakukupeni
ruhusa kuharimisha kitu alicho kuhalalishieni, na kwa hivyo mkenda
mkawapasua ngamia masikio yao, na mkajizuia kuwatumia mkawaita
"Bahira" mkawawacha kwa kuwekea nadhiri, na mkawaita "Saiba"; na mkaharimisha
kula kondoo dume, na mkawatoa kuwa tunza kwa masanamu; na hata kondoo akizaa
dume na jike mkamwita "Wasila", na mkakataa kumchinja dume lake. Wala Mwenyezi
Mungu hakukufanyieni sharia ya kukuharimishieni msimtumie ngamia dume baada
wakisha zalikana kutokana naye matumbo kumi, naye mkamwita "Hami"! Mwenyezi
Mungu hakukutungieni sharia yoyote ya namna hiyo. Lakini walio kufuru wanazua
uwongo na wanamsingizia Mwenyezi Mungu. Na wengi wao hawatumii akili.
Wakati wa Jahiliya, kabla ya Uislamu,
Waarabu wakijiharimshia wenyewe asiyo yaharimisha Mwenyezi Mungu. Katika hizo ni
kuwa:-
1. Ngamia akizaa mara
tano na mtoto wa mwisho akawa dume, basi wakimpasua sikio lake na wakaharimisha
kumpanda, na akawa haijuzu kumfukuza kwenye kunywa maji au kula machunga. Na
wakimwita: "Bahira", yaani aliyepasuliwa sikio.
2. Ilikuwa mtu husema: Nikirejea safarini, au nikipona
maradhi yangu, basi ngamia wangu ni "Saiba", yaani aliye achwa, na anakuwa
kama "Bahira".
3. Na walikuwa
kondoo akizaa jike humfanya huyo mtoto ni wao, na akizaa dume humfanya ni wa
miungu yao; na akizaa dume na jike basi hawamtoi mhanga huyo dume tena kwa
miungu yao, na humwita huyo kondoo jike: "Wa'sila", yaani amemuwasilia nduguye
dume.
4. Na pia walikuwa
akitokana na fahali mizao kumi basi husema mgongo wake umehamika,yaani
umehifadhika, na wakamwita "Hami". Huwa basi hapandwi, wala hatwikiwi
mizigo.
104. Na hawa makafiri wakiambiwa: Njooni
kwenye yale aliyo yateremsha Mwenyezi Mungu katika Qur'ani, na aliyo yaeleza
Mtume, ili mpate kuongoka kwa kuyafuata, wao husema: Yanatutosha tuliyo wakuta
nayo baba zetu. Yawafalia hawa kusema hayo? Ijapo kuwa hao baba zao ni kama
nyama hoa, hawajui lolote la haki, wala hawaijui njia ya kuendea yaliyo sahihi.
105. Enyi mlio amini! Fanyeni pupa ya
kwendea kwenye matengenezo ya nafsi zenu kwa kumt'ii Mwenyezi Mungu. Upotovu wa
mwengineo hautakudhuruni ikiwa nyinyi mmo kwenye uwongofu na mnalingania Haki.
Na nyote nyinyi marejeo yenu ni Mwenyezi Mungu peke yake Siku ya Kiyama. Hapo
atakupeni khabari ya vitendo vyenu, na kila mmoja wenu atamlipa kwa aliyo
yatanguliza, na wala hapana hata mmoja atae shikwa kwa dhambi za mwenginewe.
106. Enyi mlio amini! Mmoja wenu
anapoona alama za kukaribia mauti na akataka kuusia lolote basi kushuhudia wasia
huo iwe: kushuhudia watu wawili waadilifu katika
jamaa zenu, au watu wawili wengineo ikiwa mmo safarini na ishara za mauti
zikatokea. Wazuieni wawili hao baada ya Sala wanapo kusanyika watu, na waape kwa
jina la Mwenyezi Mungu wakisema: Hatubadilishi kwa kiapo chake kwa chochote,
hata ikiwa ni kutufaa sisi au yeyote katika jamaa zetu. Wala hatutaficha
ushahidi alio tuamrisha Mwenyezi Mungu kuutimiza baraabara. Kwani tukificha
ushahidi au tukasema lisio la kweli, tutakuwa miongoni mwa wenye kudhulumu na
kustahiki adhabu ya Mwenyezi Mungu.
107. Na ikionekana kuwa mashahidi wawili
hao wamesema uwongo katika ushahidi wao, au wameficha kitu, basi walio na haki
zaidi kushika mahala pao ni wawili wengine walio karibu zaidi kukhusika na
warithi wa maiti. Hao washike pahala pao baada ya Sala, wadhihirishe uwongo wa
walio tangulia, na waape kwa Mwenyezi Mungu kuwa wale mashahidi wa mwanzo
walisema uwongo, na: Yamini yetu inafaa zaidi kuliko yamini ya wale, na wala
hatuitupi haki katika yamini zetu, wala hatuwatuhumu mashahidi wale kwa uzushi.
Kwani tukifanya hivyo tutakuwa katika walio dhulumu, wenye kustahiki adhabu ya
mwenye kumdhulumu mwenginewe.
108. Hukumu hii ndiyo njia ya karibu mno
ya kuwezesha mashahidi watoe ushahidi ulio sawa kwa kuhifadhi kiapo chao kwa
Mwenyezi Mungu, au kwa kuogopa kufedheheka kwa kudhihiri uwongo wao, pindi ikiwa
warithi watakula yamini kupinga kiapo chao. Nanyi mumuangalie sana Mwenyezi
Mungu katika viapo vyenu na amana zenu, na zit'iini hukumu zake, na muwe radhi
nazo. Kwani katika hayo ndiyo yanapatikana maslaha yenu. Na msikhalifu hukumu za
Mwenyezi Mungu, msije kutoka kwenye ut'iifu wake, kwani Yeye hamnafiishi
kwa uwongzi wake mwenye kutoka katika ut'iifu wake.
109. Nanyi ikumbukeni Siku ya Kiyama
pale Mwenyezi Mungu atapo wakusanya mbele yake Mitume wote akawauliza: Hao
kaumu zenu niliyo kutumeni kwao wamekujibuni nini? Waliamini au walikanya?
Na hao kaumu wakati huo watakuwa wamehudhuria ili hoja iwe juu yao kwa ushahidi
wa Mitume wao wakisema: Hakika sisi hatujui yaliyo tokea baada yetu kwa
hao ulio tupeleka kwao. Ni Wewe peke yako ndiye unaye jua hayo, kwa kuwa Wewe
ndiye uliye kusanya ujuzi wa vilivyo fichikana kama unavyo jua viliyo dhaahiri.
110. Na wakati huo, Mwenyezi Mungu
atamwambia Isa mwana wa Maryamu miongoni mwa Mitume: Kumbuka neema niliyo
kuneemesha wewe na mama yako katika dunia, nilipo kutia nguvu kwa
Wahyi,(Ufunuo), na nikakutamkisha nawe ni mtoto mchanga ili kumuondolea tuhuma
aliyo tuhumiwa mama yako, kama nilivyo kutamkisha nawe ni mtu mzima kwa ufunuo
niliyo kufunulia; na nilipo kuneemesha kwa kukufunza kuandika, na nikakuwezesha
kusema na kutenda yaliyo sawa, na nikakufunza Kitabu cha Musa na Injili niliyo
kuteremshia wewe, na nikakuwezesha kutenda miujiza asiyo weza mtu mwingine
kuitenda, ulipo tengeneza ndege kwa udongo kwa idhini ya Mwenyezi Mungu,
ukapuliza akawa ndege aliye hai kwa uweza wa Mwenyezi Mungu, si kwa uweza wako,
na ukamponesha mtoto kipofu, na ukamponesha mkoma kwa idhini na uweza wa
Mwenyezi Mungu, na yakawa kwa kupitia mikononi mwako makadara ya kufufuka maiti
kwa idhini ya Mwenyezi Mungu na kudra yake, na pale nilipo wazuia Mayahudi
wasikuuwe na kukusalibu nilipo waletea miujiza wapate kuamini, nao baadhi yao
walikanya na wakadai kuwa hiyo miujiza si lolote ila ni dhaahiri uchawi tu.
(Katika Injili ya Luka inasemwa "Malaika kutoka mbinguni akamtokea akamtia
nguvu." Luka 22.43. Na katika Injili ya Yohana 5.30 Yesu anakiri: "Mimi siwezi
kufanya neno mwenyewe.")
111. Ewe Mtume! Watajie umma wako yaliyo
tokea tulipo watia hima kikundi cha alio wataka Isa wamuamini Mwenyezi Mungu na
Mtume wake Isa, na wakamuitikia wakawa ndio Wanafunzi wake makhsusi, na
wakasema: Tumeamini. Na shuhudia ewe Mola wetu Mlezi, kuwa sisi tumesafi niya
zetu, na tunafuata amri zako, yaani Waislamu.
112. Ewe Nabii! Taja pia yaliyo tokea
pale wafuasi wa Isa wenye ikhlasi walipo sema: Ewe Isa bin Maryamu! Hivyo Mola
wako Mlezi atakuitikia ukimtaka akuteremshie chakula kutoka mbinguni? Isa
akawaambia kuwajibu: Kama nyinyi ni kweli mnamuamini Mwenyezi Mungu, basi
mkhofuni Yeye, na fuateni amri zake na makatazo yake. Wala msitafute hoja ila
nilizo kuleteeni.
113. Wakasema: Hakika sisi tunataka kula
katika chakula hicho, ili nyoyo zetu zitue kwa kudra ya Mwenyezi Mungu tunayo
iamini, na tujue kwa kuona kwa macho ya kuwa hakika ni kweli hayo unayo twambia
yanatoka kwake Subhanahu, Aliye takasika, na tupate kutoa ushahidi kwa muujiza
huu kwa hao ambao hawakuuona.
114. Isa akawaitikia, na akasema: Ewe
Mola wetu Mlezi, uliye miliki mambo yetu yote! Tuteremshie chakula kutoka
mbinguni, kiwe ni siku-kuu kwetu kitapo teremka kwa walio amini miongoni mwetu,
kwa walio tangulia na walio taakhari, na kiwe ni muujiza wa kutilia nguvu wito
wako, na uturuzuku riziki njema, na Wewe ndiye Mbora wa kuruzuku.
115. Mwenyezi Mungu akamwambia: Mimi
nitakuteremshieni chakula kutoka mbinguni. Lakini mtu yeyote atakaye pinga neema
hii baada ya kuteremka, basi Mimi nitampa adabu ambayo sijapata kumpa mtu
yeyote. Kwani huyo atakuwa anakanya baada ya kwisha shuhudia dalili ya Imani
aliyo itaka mwenyewe.
116. Ewe Nabii! Taja yatakayo tokea Siku
ya Kiyama, Mwenyezi Mungu atapo mwambia Isa bin Maryamu kauli ya kutangaza haki:
Ati wewe ndiye uliye waambia: Nifanyeni mimi na mama yangu kuwa ni miungu, na
muache kumuabudu Mwenyezi Mungu wa pekee? Isa atasema: Mimi ninakutakasa mtakaso
wa ukamilifu ya kuwa Wewe huna mshirika. Wala hainifalii mimi nitake jambo
ambalo sina haki nalo hata chembe. Lau kuwa nimesema
hayo, basi Wewe ungeli jua. Kwani Wewe unayajua yaliyo
fichikana ndani ya nafsi yangu, licha yanayo dhihiri kwa kuyasema. Wala mimi
siyajui unayo nificha. Hakika Wewe ndiye Mwenye ujuzi ulio enea kila kilicho
fichikana na kilicho ghibu. (Wakristo wote wanamuabudu Yesu, na Wakatoliki
wanamwomba Maryamu pia, na wanamwita: "Mama wa Mungu")
117. Mimi sikuwaambia ila uliyo
niamrisha niwafikishie. Nimewaambia: Muabuduni Mwenyezi Mungu peke yake. Kwani
Yeye ndiye Mwenye kumiliki mambo yangu na yenu. Na mimi nilikuwa naijua hali yao
nilipo kuwa nao. Na ulipo malizika muda uliyo nikadiria nikae nao ulikuwa Wewe
peke yako ndiye unaye wajua. Na Wewe ni Mwenye kujua kila kitu.
118. Ukiwaadhibu kwa waliyo yatenda basi
hao ni waja wako, unawafanya upendavyo. Na ukiwasamehe, basi hakika Wewe peke
yako ndiye Mtenda nguvu usiye shindwa, Mwenye hikima yenye kufikilia kila linalo
toka kwako.
119. Mwenyezi Mungu atasema: Hii
ndiyo siku ambayo wasemao kweli utawafaa ukweli wao. Watapata mabustani yanayo
pitiwa na mito chini ya miti yake. Na humo watakaa, wala hawatatoka milele,
wakistarehe humo kwa radhi ya Mwenyezi Mungu anavyo waridhia wao, na wao watavyo
kuwa radhi kwa malipo alio walipa. Na Neema hiyo ndio kufuzu kukubwa.
120. Ufalme wa mbinguni na katika ardhi
na vyote viliomo humo ni wa Mwenyezi Mungu peke yake. Yeye peke yake ndiye
Mwenye kustahiki kuabudiwa, na Yeye tu ndiye Mwenye uweza ulio timia kutekeleza
kila alitakalo.