Tarjuma ya Quran Tukufu kwa kiswahili

16.Surat An-Nahl


image
0. KWA JINA LA MWENYEEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU. 0

image
1. Amri ya Mwenyezi Mungu itafika tu. Basi msiihimize. Ametakasika na Ametukuka na wanayo mshirikisha nayo. 1

image
2. Huwateremsha Malaika na Roho kwa amri yake juu ya amtakaye katika waja wake ili nyinyi muonye kwamba hapana mungu ila Mimi, basi nicheni Mimi. 2

image
3. Ameziumba mbingu na ardhi kwa Haki. Ametukuka na wanayo shirikisha. 3

image
4. Amemuumba mtu kwa tone la manii. Naye mara amekuwa mshindani dhaahiri. 4

image
5. Na nyama hoa amekuumbieni. Katika hao mna vifaa vya kutia joto,na manufaa mengineyo, na baadhi yao mnawala. 5

image
6. Na wanakupeni furaha pale mnapo warudisha jioni na mnapo wapeleka malishoni asubuhi.6

image
7. Na hubeba mizigo yenu kupeleka kwenye miji msiyo weza kuifikia ila kwa mashaka ya nafsi. Hakika Mola wenu Mlezi ni Mpole na Mwenye kurehemu. 7

image
8. Na farasi, na nyumbu, na punda ili muwapande, na kuwa ni pambo.Na ataumba msivyo vijua. 8

image
9. Na ni juu ya Mwenyezi Mungu kuelekeza Njia. Na zipo njia za upotovu.Na angeli penda angeli kuongoeni nyote. 9

image
.10 Yeye ndiye anaye kuteremshieni maji kutoka mbinguni. Katika hayo nyinyi mnapata ya kunywa, na miti ya kulishia. 10

image
11. Kwa hayo Yeye anaizalisha kwa ajili yenu mimea, na mizaituni,na mitende, na mizabibu, na kila namna ya matunda. Hakika katika haya zipo ishara kwa watu wanao fikiri. 11

image
12. Na amefanya ukutumikieni usiku na mchana, na jua na mwezi,na nyota zikutumikieni kwa amri yake. Hakika katika hayo zipo ishara kwa watu wenye akili. 12

image
13. Na hivi alivyo vieneza katika ardhi vya rangi mbali mbali. Hakika katika hayo ipo ishara kwa watu wanao waidhika. 13

image
14. Yeye ndiye aliye ifanya bahari ikutumikieni, ili kutokana na humo mpate kula nyama laini, na mtoe humo mapambo mnayo yavaa. Na unaona marikebu zikikata maji humo, ili mtafute fadhila yake, na mpate kushukuru. 14

15 image
15. Na kaweka katika ardhi milima ili ardhi isiyumbe yumbe nanyi.Na mito, na njia ili mpate kuongoka. 15

image
16. Na alama nyengine. Na kwa nyota wao wanajiongoza. 16

image
17. Ati anaye umba ni kama asiye umba? Basi hebu, hamkumbuki? 17

image
18. Na mkizihisabu neema za Mwenyezi Mungu, hamwezi kuzidhibiti.Hakika Mwenyezi Mungu ni Mwenye maghfira, Mwenye kurehemu. 18

image
19. Na Mwenyezi Mungu anayajua mnayo yaficha na mnayo yatangaza. 19

image
20. Na wale wanao waomba wasio kuwa Mwenyezi Mungu hawaumbi kitu,bali wao wameumbwa. 20

image
21. Ni wafu si wahai, na wala hawajui watafufuliwa lini. 21

image
22. Mungu wenu ni Mungu Mmoja. Lakini wasio iamini Akhera nyoyo zao zinakataa, nao wanajivuna. 22

image
23. Hapana shaka kuwa hakika Mwenyezi Mungu anayajua wanayo yaficha na wanayo yatangaza. Kwa hakika Yeye hawapendi wanao jivuna. 23

image
24. Na wanapo ambiwa: Kateremsha nini Mola wenu Mlezi? Husema: Hadithi za kubuni za watu wa kale! 24

image
25. Ili wabebe mizigo yao kwa ukamilifu Siku ya Kiyama, na sehemu ya mizigo ya wale wanao wapoteza bila ya kujua. Angalia, ni maovu mno hayo wanayo yabeba! 25

image
26. Walipanga vitimbi walio kuwa kabla yao, Mwenyezi Mungu akayasukua majengo yao kwenye misingi, dari zikawaporomokea juu yao, na adhabu ikawajia kutoka wasipo kujua. 26

image
27. Kisha Siku ya Kiyama atawahizi na atasema: Wako wapi hao washirika wangu ambao kwao mkiwakutisha (Manabii) mashaka? Watasema walio pewa ilimu:Hakika leo ndiyo hizaya na adhabu itawashukia makafiri, 27

image
28. Ambao Malaika waliwafisha nao wamejidhulumu nafsi zao! Basi watasalimu amri, waseme: Hatukuwa tukifanya uovu wowote. (Wataambiwa): Kwani! Hakika Mwenyezi Mungu anajua sana mliyo kuwa mkiyatenda. 28

image
29. Basi ingieni milango ya Jahannamu, humo mdumu. Ni maovu mno makaazi ya wafanyao kiburi! 29

image
30. Na wataambiwa walio mcha Mungu: Mola wenu Mlezi kateremsha nini? Watasema: Kheri. Walio fanya wema katika dunia hii watapata wema. Na nyumba ya Akhera ni bora zaidi, na njema mno nyumba ya wachamngu. 30

image
31. Bustani za milele wataziingia; iwe inapita kati yake mito. Humo watapata watakacho. Hivi ndivyo Mwenyezi Mungu awalipavyo wenye kumcha. 31

image
32. Wale ambao Malaika huwafisha katika hali njema, wanawaambia:Amani iwe juu yenu! Ingieni Peponi kwa sababu ya yale mliyo kuwa mkiyatenda. 32

image
33. Wanangojea jengine hawa ila Malaika wawafikie, au iwafikie amri ya Mola wako Mlezi? Kama hivyo walitenda walio kuwa kabla yao. Na MwenyeziMungu hakuwadhulumu, lakini walijidhulumu wenyewe. 33

image
34. Basi ukawafikia uovu wa waliyo yatenda, na waliyo kuwa wakiyakejeli yakawazunguka. 34

image
35. Na washirikina wanasema: Mwenyezi Mungu angeli taka tusingeliabudu chochote badala yake, sisi wala baba zetu, wala tusingeli harimisha chochote bila ya Yeye. Kama hivyo walifanya walio kuwa kabla yao. Basi lipo lolote juu ya Mitume isipo kuwa kubalighisha kwa uwazi? 35

image
36. Na kwa hakika kwa kila umma tuliutumia Mtume kwamba: Muabuduni Mwenyezi Mungu, na muepukeni Shetani. Basi kati yao wapo alio waongoa MwenyeziMungu. Na kati yao wapo ambao ulio wathibitikia upotovu. Basi tembeeni katika ardhi, muangalie ulikuwaje mwisho wa wanao kanusha. 36

image
37. Hata ukiwa na pupa ya kutaka kuwaongoa, lakini Mwenyezi Mungu hamwongoi yule anaye shikilia kupotea. Wala hawatapata wa kuwanusuru. 37

image
38. Na wanaapa kwa Mwenyezi Mungu ukomo wa viapo vyao kwamba MwenyeziMungu hatomfufua aliye kufa. Kwani! Ni ahadi iliyo juu yake kikweli; lakini watu wengi hawajui. 38

image
39. Ili kuwabainishia yale waliyo khitalifiana, na ili wajue waliokufuru kwamba wao walikuwa ni waongo. 39

image
40. Kauli yetu kwa kitu tunacho kitaka kiwe, ni kukiambia: Kuwa!Basi kinakuwa. 40

image
41. Na wale walio hama kwa ajili ya Mwenyezi Mungu baada ya kudhulumiwa,bila ya shaka tutawaweka duniani kwa wema; na ujira wa Akhera ni mkubwa zaidi; laiti kuwa wanajua! 41

image
42. Wale wanao subiri na wakamtegemea Mola wao Mlezi. 42

image
43. Nasi hatukuwatuma kabla yako ila watu wanaume tulio wapa Wahyi(Ufunuo). Basi waulizeni wenye ukumbusho kama nyinyi hamjui. 43

image
44. Kwa Ishara wazi na Vitabu. Nasi tumekuteremshia wewe Ukumbusho ili uwabainishie watu yaliyo teremshwa kwao, wapate kufikiri. 44

image
45. Je! Wameaminisha wanao fanya vitimbi vya uovu kwamba MwenyeziMungu hatawadidimiza katika ardhi, na haitawafika adhabu kutoka wasipopajua? 45

image
46. Au hatawashika katika nyendo zao, na wala hawataponyoka? 46

image
47. Au hatawashika kwa kitisho na kuwapunguza kidogo kidogo? Hakika Mola wenu Mlezi ni Mwenye huruma, Mwenye kurehemu.47

image
48. Je! Hawavioni vitu alivyo viumba Mwenyezi Mungu - vivuli vyao vinaelekea kushotoni na kuliani, kumsujudia Mwenyezi Mungu na vikinyenyekea? 48

image
49. Na vyote viliomo katika mbingu na katika ardhi, tangu wanyama mpaka Malaika, vinamsujuidia Mwenyezi Mungu, na wala havitakabari. 49

image
50. Vinamkhofu Mola wao Mlezi aliye juu yao, na vinafanya vinavyoamrishwa. image
51. Na Mwenyezi Mungu amesema: Msiwe na miungu wawili! Hakika Yeye ni Mungu Mmoja. Basi niogopeni Mimi tu! 51

image
52. Na ni vyake Yeye viliomo katika mbingu na ardhi. Na Dini ni yake Yeye daima. Je! Mtamcha mwengine asiye kuwa Mwenyezi Mungu? 52

image
53. Na neema yoyote mliyo nayo inatoka kwa Mwenyezi Mungu. Kisha yakikuguseni madhara mnamyayatikia Yeye. 53

image
54. Na anapo kuondosheeni madhara mara kundi moja miongoni mwenu linamshirikisha Mola wao Mlezi, 54

image
55. Wakizikataa neema tulizo wapa. Basi stareheni. Mtakuja jua! 55

image
56. Na hao ambao hata hawawajui wanawawekea sehemu ya tunavyo waruzuku.Wallahi! Bila ya shaka mtasailiwa kwa hayo mliyo kuwa mnayazua! 56

image
57. Na wanamfanyia Mwenyezi Mungu ati ana mabinti, Subhanahu, Aliyetakasika! Na wao wenyewe, ati ndio wawe na hayo wanayo yatamani! 57

image
58. Na mmoja wao akibashiriwa kwa msichana, uso wake unasawijika,naye kajaa chuki. 58

image
59. Anajificha asionekane na watu kwa ubaya wa aliyo bashiriwa! Je,akae naye juu ya fedheha hiyo au amfukie udongoni? Tazama uovu wa wanavyohukumu! 59

image
60. Hali ya wasio iamini Akhera ni ovu; na Mwenyezi Mungu ndiye Mwenye sifa tukufu. Naye ni Mwenye nguvu na Mwenye hikima. 60

image
61. Na lau kuwa Mwenyezi Mungu angeli wachukulia watu kwa mujibu wa dhulma zao, basi asingeli mwacha hapa hata mnyama mmoja. Lakini anawaakhirisha mpaka muda ulio wekwa. Na unapo fika muda wao hawatakawilia hata saa moja wala hawatatangulia. 61

image
62. Na wanampa Mwenyezi Mungu wanavyo vichukia wao, na ndimi zao zinasema uwongo kwamba wao watapata mema. Hapana shaka hakika wamewekewa Moto, nao wataachwa humo. 62

image
63. Wallahi! Sisi tulituma Mitume kwa umati zilizo kuwa kabla yako,lakini Shetani aliwapambia vitendo vyao. Kwa hivyo leo yeye ndiye rafiki yao; nao watapata adhabu chungu. 63

image
64. Na hatukukuteremshia Kitabu isipo kuwa uwabainishie yale ambayo wanakhitalifiana, na kiwe Uwongofu na Rehema kwa watu wanao amini. 64

image
65. Na Mwenyezi Mungu ameteremsha maji kutoka mbinguni na kwa hayo akaihuisha ardhi baada ya kufa kwake. Kwa hakika katika hayo imo Ishara kwa watu wanao sikia. 65

image
66. Na hakika katika nyama hoa nyinyi mna mazingatio. Tunakunywesheni katika vile viliomo matumboni mwao, vikatoka baina ya mavi na damu, maziwa safi mazuri kwa wanywao. 66

image
67. Na kutokana na matunda ya mitende na mizabibu mnatengeneza ulevi na riziki nzuri. Hakika katika hayo ipo Ishara kwa wanao tumia akili. 67

image
68. Na Mola wako Mlezi amemfunulia nyuki: Jitengenezee majumba yako katika milima,na katika miti, na katika wanayo jenga watu. 68

image
69. Kisha kula katika kila matunda, na upite katika njia za Mola wako Mlezi zilizo fanywa nyepesi kuzipita. Na kutoka matumbo yao kinatoka kinywaji chenye rangi mbali mbali; ndani yake kina matibabu kwa wanaadamu.Hakika katika haya ipo Ishara kwa watu wanao fikiri. 69

image
70. Na Mwenyezi Mungu amekuumbeni; kisha anakufisheni. Na miongoni mwenu wapo wanao rudishwa kwenye umri mbaya kabisa, hata akawa asijue kitu baada ya ujuzi alio kuwa nao. Hakika Mwenyezi Mungu ndiye Mjuzi na Mweza. 70

image
71. Na Mwenyezi Mungu amewafadhilisha baadhi yenu kuliko wengine katika riziki. Na wale walio fadhilishwa hawarudishi riziki zao kwa wale ilio wamiliki mikono yao ya kulia ili wawe sawa katika riziki hiyo. Basi je, wanazikataa neema za Mwenyezi Mungu? 71

image
72. Na Mwenyezi Mungu amekuumbieni wake katika jinsi yenu, na akakujaalieni kutoka kwa wake zenu wana na wajukuu, na akakuruzukuni vitu vizuri vizuri.Basi je, wanaamini upotovu na wanazikataa neema za Mwenyezi Mungu? 72

image
73. Na badala ya Mwenyezi Mungu wanawaabudu wasio wamilikia riziki kutoka mbinguni wala kwenye ardhi, wala hawawezi kitu. 73

image
74. Basi msimpigie Mwenyezi Mungu mifano. Hakika Mwenyezi Mungu anajua,na nyinyi hamjui. 74

image
75. Mwenyezi Mungu anapiga mfano wa mtumwa aliye milikiwa, asiyeweza kitu, na mwingine tuliye mruzuku riziki njema inayo toka kwetu,naye akawa anatoa katika riziki hiyo kwa siri na dhaahiri. Je, hao watakuwa sawa? Alhamdu Lillahi! Kuhimidiwa kote ni kwa Mwenyezi Mungu.Lakini wengi wao hawajui. 75

image
76. Na Mwenyezi Mungu anapiga mfano wa watu wawili. Mmoja wao ni bubu, hawezi chochote, naye ni mzigo kwa bwana wake. Popote anapo muelekeza haleti kheri. Je! Huyo anaweza kuwa sawa na yule anaye amrisha uadilifu,naye yuko juu ya Njia Iliyo Nyooka. 76

image
77. Na siri zote za katika mbingu na ardhi ziko kwa Mwenyezi Mungu.Wala halikuwa jambo la Saa (ya Kiyama) ila kama kupepesa kwa jicho, au akali ya hivyo. Hakika Mwenyezi Mungu ni Muweza wa kila kitu. 77

image
78. Na Mwenyezi Mungu amekutoeni matumboni mwa mama zenu, hali ya kuwa hamjui kitu, na amekujaalieni masikio na macho na nyoyo ili mpate kushukuru. 78

image
79. Je! Hawawaoni ndege walivyo wat'iifu katika anga la mbingu? Hapana mwenye kuwashika isipo kuwa Mwenyezi Mungu. Hakika katika haya zipo ishara kwa watu wanao amini. 79

image
80. Na Mwenyezi Mungu amekujaalieni majumba yenu yawe ni maskani yenu, na amekujaalieni kutokana na ngozi za wanyama nyumba mnazo ziona nyepesi wakati wa safari zenu na wakati wa kutua kwenu. Na kutokana na sufi zao na manyoya yao na nywele zao mnafanya matandiko na mapambo ya kutumia kwa muda. 80

image
81. Na Mwenyezi Mungu amekufanyieni vivuli katika vitu alivyo viumba,na amekufanyieni maskani milimani, na amekufanyieni nguo za kukingeni na joto, na nguo za kukingeni katika vita vyenu. Ndio hivyo anakutimizieni neema zake ili mpate kut'ii. 81

image
82. Basi wakikengeuka lilio juu yako wewe ni kufikisha ujumbe waziwazi. 82

image
83. Wanazijua neema za Mwenyezi Mungu, kisha wanazikanusha; na wengi wao ni makafiri. 83

image
84. Na siku tutakapo wainua kutokana na kila umma shahidi, kisha hawataruhusiwa walio kufuru wala hawataachiliwa kutaka radhi. 84

image
85. Na walio dhulumu watakapo iona adhabu hawatapunguziwa hiyo adhabu,wala hawatapewa muhula. 85

image
86. Na walio shirikisha watakapo waona hao walio washirikisha na Mwenyezi Mungu, watasema: Mola wetu Mlezi! Hawa ndio washirikishwa wetu ambao tulikuwa tukiwaabudu badala yako. Ndipo wale watakapo watupia kauli:Hakika nyinyi ni waongo! 86

image
87. Na siku hiyo watasalimu amri mbele ya Mwenyezi Mungu, na yatapotea waliyo kuwa wakiyazua. 87

image
88. Wale walio kufuru na kuzuilia Njia ya Mwenyezi Mungu tutawazidishia adhabu juu ya adhabu, kwa walivyo kuwa wakifisidi. 88

image
89. Na (waonye) siku tutakapo wainua mashahidi katika kila umma wakiwashuhudia kwa yanayo tokana na wao, na tutakuleta wewe uwe shahidi juu ya hao. Na tumekuteremshia Kitabu hiki kinacho bainisha kila kitu, na ni uwongofu,na rehema, na bishara kwa Waislamu. 89

image
90. Hakika Mwenyezi Mungu anaamrisha kufanya uadilifu, na hisani,na kuwapa jamaa; na anakataza uchafu, na uovu, na dhulma. Anakuwaidhini ili mpate kukumbuka. 90

image
91. Na timizeni ahadi ya Mwenyezi Mungu mnapo ahidi, wala msivunje viapo baada ya kuvithibitisha, ilihali mmekwisha mfanya Mwenyezi Mungu ndiye mdhamini wenu. Hakika Mwenyezi Mungu anayajua myatendayo. 91

image
92. Wala msiwe kama mwanamke anaye uzongoa uzi wake baada ya kwisha usokota ukawa mgumu. Mnavifanya viapo vyenu kuwa ni njia ya kudanganyana baina yenu kwa kuwa ati taifa moja lina nguvu zaidi kuliko jengine? Hakika Mwenyezi Mungu anakujaribuni kwa njia hiyo. Na bila ya shaka atakubainishieni Siku ya Kiyama mliyo kuwa mkikhitalifiana. 92

image
93. Na Mwenyezi Mungu angeli taka, kwa yakini angeli kufanyeni umma mmoja. Lakini anamwachia kupotea anaye mtaka, na anamwongoa amtakaye. Na hakika mtaulizwa kwa yale mliyo kuwa mkiyafanya. 93

image
94. Wala msifanye viapo vyenu ni njia ya kudanganyana baina yenu.Usije mguu ukateleza badala ya kuthibiti, na mkaonja maovu kwa sababu ya kule kuzuilia Njia ya Mwenyezi Mungu, na mkapata adhabu kubwa. 94

image
95. Wala msinunue ahadi ya Mwenyezi Mungu kwa thamani ndogo. Hakika kilichoko kwa Mwenyezi Mungu ndicho bora kwenu, ikiwa mnajua. 95

image
96. Mlivyo navyo vitakwisha na vilivyoko kwa Mwenyezi Mungu ndivyo vitakavyo bakia. Na kwa yakini Sisi tutawapa walio subiri ujira wao kwa bora ya waliyo kuwa wakiyatenda. 96

image
97. Mwenye kutenda mema, mwanamume au mwanamke, naye akawa ni Muumini,tutamhuisha maisha mema; na tutawapa ujira wao kwa bora ya waliyo kuwa wakiyatenda. 97

image
98. Na ukisoma Qur'ani mwombe Mwenyezi Mungu akulinde na Shetani maluuni. 98

image
99. Hakika yeye hana madaraka juu ya walio amini na wakamtegemea Mola wao Mlezi. 99

image
100. Hakika madaraka yake ni juu ya wanao mfanya rafiki yao, na wale wanao fanya ushirika naye. 100

image
101. Na tunapo badilisha Ishara pahala pa Ishara nyengine, na MwenyeziMungu anajua anayo teremsha, wao husema: Wewe ni mzushi. Bali wengi wao hawajui kitu. 101

image
102. Sema: Ameiteremsha hii Roho takatifu kutokana na Mola wako Mlezi kwa haki, ili awathibitishe wale walio amini, na kuwa ni uwongofu, na ni bishara kwa Waislamu. 102

image
103. Na Sisi hakika tunajua kwamba wanasema: Yuko mtu anaye mfundisha.Lugha ya huyo wanaye muelekezea ni ya kigeni, na hii ni lugha ya Kiarabu mbayana. 103

image
104. Hakika wasio ziamini Ishara za Mwenyezi Mungu, Mwenyezi Mungu hawaongoi, nao watapata adhabu chungu. 104

image
105. Wanao zua uwongo ni wale tu wasio ziamini Ishara za MwenyeziMungu. Na hao ndio waongo. 105

image
106. Anaye mkataa Mwenyezi Mungu baada ya kuamini kwake - isipo kuwa aliye lazimishwa na hali ya kuwa moyo wake umetua juu ya Imani, lakini aliye kifungulia kifua chake kukataa - basi hao ghadhabu ya Mwenyezi Mungu ipo juu yao, na wao watapata adhabu kubwa. 106

image
107. Hayo ni kwa sababu wameyapenda zaidi maisha ya duniani kuliko ya Akhera, na kwa sababu Mwenyezi Mungu hawaongoi watu makafiri. 107

image
108. Hao ndio Mwenyezi Mungu ameziziba nyoyo zao na masikio yao na macho yao. Na hao ndio walio ghafilika. 108

image
109. Hapana shaka ya kwamba hao ndio wenye kukhasiri Akhera. 109

image
110. Kisha hakika Mola wako Mlezi, kwa wale walio hama makwao baada ya kuteswa, kisha wakapigania Dini na wakasubiri, bila ya shaka Mola wako Mlezi baada ya hayo ni Mwenye kusamehe Mwenye kurehemu. 110

image
111. Siku ambayo kila nafsi itakuja jitetea, na kila nafsi italipwa sawa sawa na a'mali ilizo zifanya, nao hawatadhulumiwa. 111

image
112. Na Mwenyezi Mungu amepiga mfano wa mji ulio kuwa na amani na utulivu, riziki yake ikiufikia kwa nafasi kutoka kila mahali. Lakini ukazikufuru neema za Mwenyezi Mungu; kwa hivyo Mwenyezi Mungu akauvika vazi la njaa na khofu kwa sababu ya yale waliyo kuwa wakiyafanya. 112

image
113. Na alikwisha wajia Mjumbe wa miongoni mwao wenyewe. Lakini wakamkanusha;basi iliwafika adhabu hali ya kuwa wamedhulumu. 113

image
114. Basi kuleni katika vile alivyo kupeni Mwenyezi Mungu, vilivyo halali na vizuri. Na shukuruni neema za Mwenyezi Mungu, ikiwa kweli mnamuabudu Yeye. 114

image
115. Amekuharimishieni nyamafu tu, na damu, na nyama ya nguruwe,na mnyama aliye chinjwa kwa ajili isiyo kuwa ya Mwenyezi Mungu. Lakini anaye lazimishwa bila ya kuasi, wala kuruka mipaka, basi hakika MwenyeziMungu ni Mwenye kusamehe na Mwenye kurehemu. 115

image
116. Wala msiseme uwongo, kwa kuropokwa na ndimi zenu: Hichi halali,na hichi haramu - mkimzulia uwongo Mwenyezi Mungu. Hakika wanao mzulia uwongo Mwenyezi Mungu hawatafanikiwa. 116

image
117. Ni starehe ndogo, nao watapata adhabu chungu. 117

image
118. Na Mayahudi tuliwaharimishia yale tuliyo kuhadithia zamani.Na Sisi hatukuwadhulumu, bali walikuwa wakijudhulumu wenyewe. 118

image
119. Kisha hakika Mola wako Mlezi kwa walio tenda uovu kwa ujinga,kisha wakatubia baada ya hayo na wakatenda mema; bila ya shaka Mola wako Mlezi baada ya hayo ni Mwenye kusamehe na Mwenye kurehemu. 119

image
120. Hakika Ibrahim alikuwa mfano mwema, mnyenyekevu kwa MwenyeziMungu, mwongofu, wala hakuwa miongoni mwa washirikina. 120

image
121. Mwenye kuzishukuru neema zake, Mwenyezi Mungu. Yeye kamteuwa,na akamwongoa kwenye Njia Iliyo Nyooka. 121

image
122. Na tukampa wema duniani, na hakika Akhera atakuwa miongoni mwa watu wema. 122

image
123. Kisha tukakufunulia ya kwamba ufuate mila ya Ibrahim, mwongofu,wala hakuwa miongoni mwa washirikina. 123

image
124. Hakika siku ya Sabato (Jumaamosi) waliwekewa wale walio khitalifiana kwa ajili yake. Na hakika Mola wako Mlezi bila ya shaka atahukumu baina yao Siku ya Kiyama katika yale waliyo kuwa wakikhitalifiana. 124

image
125. Waite waelekee kwenye Njia ya Mola wako Mlezi kwa hikima na mawaidha mema, na ujadiliane nao kwa namna iliyo bora. Hakika Mola wako Mlezi ndiye anaye mjua zaidi aliye ipotea Njia yake, na Yeye ndiye anaye wajua zaidi walio ongoka. 125

image
126. Na mkilipiza basi lipizeni sawa na vile mlivyo adhibiwa. Na ikiwa mtasubiri, basi hakika hivyo ni bora zaidi kwa wanao subiri. 126

image
127. Na subiri. Na kusubiri kwako kusiwe ila kwa sababu ya MwenyeziMungu tu. Wala usiwahuzunikie; wala usiwe katika dhiki kwa hila wanazozifanya. 127

image
128. Hakika Mwenyezi Mungu yu pamoja na wenye kumcha, na watendao mema. . 128


Imetarjumiwa na Sheikh Ali Muhsin Al-Barwani
Ikiwa una ushauri au maoni juu ya tarjuma hii, andika kwa anwani hii qurani-tukufu@geocities.com 
Copyright � 22 August 1997, Sheikh Ali Muhsin Al Barwani