Tarjuma ya Quran Tukufu kwa kiswahili

28.Surat Al-Qasas


image
KWA JINA LA MWENYEEZI MUNGU MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU 0

image
1. T'A SIN MIM 1

image
2. Hizi ni Aya za Kitabu kinacho bainisha. 2

image
3. Tunakusomea khabari za Musa na Firauni kwa Haki kwa ajili ya watu wanao amini. 3

image
4. Hakika Firauni alitakabari katika nchi, na akawagawa wananchi makundi mbali mbali. Akalidhoofisha taifa moja miongoni mwao, akiwachinja watoto wao wanaume na akiwaacha watoto wao wanawake. Hakika yeye alikuwa katika mafisadi. 4

image
5. Na tukataka kuwafadhili walio dhoofishwa katika nchi hiyo na kuwafanya wawe waongozi na kuwafanya ni warithi. 5

image
6. . Na kuwapa nguvu katika nchi, na kutokana na wao kuwaonyesha kina Firauni na Hamana na majeshi yao mambo yale waliyo kuwa wakiyaogopa. 6

image
7. Tulimfunulia mama yake Musa kwa kumwambia: Mnyonyeshe. Na utakapo mkhofia basi mtie mtoni, na usikhofu wala usihuzunike. Hakika Sisi tutamrudisha kwako na tutamfanya miongoni mwa Mitume. 7

image
8. Basi wakamwokota watu wa Firauni, aje kuwa adui kwao na huzuni. Hakika Firauni na Hamana na majeshi yao walikuwa wenye makosa. 8

image
9. Na mkewe Firauni alisema: Atakuwa kiburudisho cha macho kwangu na kwako. Msimuuwe! Huenda akatufaa, au tumpange kuwa mwenetu. Wala wao hawakutambua. 9

image
10. . Na moyo wa mama yake Musa ukawa mtupu. Alikuwa karibu kumdhihirisha, ingeli kuwa hatukumtia nguvu moyo wake ili awe miongoni mwa Waumini. 10

image
11. . Naye akamwambia dada yake Musa: Mfuatie. Basi naye akawa anamuangalia kwa mbali bila ya wao kujua. 11

image
12. Na tukamjaalia awakatae wanyonyeshaji wote tangu mwanzo, mpaka dada yake akasema: Je! Nikuonyesheni watu wa nyumba watakao mlea kwa ajili yenu, nao pia watakuwa wema kwake? 12

image
13. Basi tukamrudisha kwa mama yake ili macho yake yaburudike, wala asihuzunike. Na ajue ya kwamba ahadi ya Mwenyezi Mungu ni ya kweli, lakini wengi wao hawajui. 13

image
14. Na Musa alipo fika utu-uzima baraabara, tulimpa akili na ilimu. Na hivi ndivyo tunavyo walipa walio wema. 14

image
15. Na akaingia mjini wakati wa kughafilika wenyeji wake, na akakuta humo watu wawili wanapigana - mmoja ni katika wenzake, na mwengine katika maadui zake. Yule mwenzake alimtaka msaada kumpiga adui yake. Musa akampiga ngumi, akamuuwa. Akasema: Hiki ni kitendo cha Shet'ani; hakika yeye ni adui, mpotezaji dhaahiri. 16

image
16. Akasema: Mola wangu Mlezi! Hakika mimi nimejidhulumu nafsi yangu; basi nisamehe. Akamsamehe; hakika Yeye ni Mwenye kusamehe Mwenye kurehemu. 16

image
17. Akasema: Mola wangu Mlezi! Kwa ulivyo nineemesha, basi mimi sitakuwa kabisa msaidizi wa wakosefu. 18

image
18. Akapambazukiwa mjini asubuhi naye ana khofu, akiangalia huku na huku. Mara yule yule aliye mtaka msaada jana akawa anampigia kelele amsaidie. Musa akamwambia: Hakika wewe ni mgomvi kweli kweli. 18

image
19. Basi alipo taka kumshika kwa nguvu yule aliye adui wao wote wawili, akasema: Ewe Musa! Unataka kuniuwa kama ulivyo muuwa mtu jana? Wewe hutaki ila kuwa jabari katika nchi, wala hutaki kuwa miongoni mwa wenye maslaha.. 19

image
20. Na akaja mtu kutoka mwisho wa mji akipiga mbio, akasema: Ewe Musa! Wakubwa wanashauriana kukuuwa. Basi toka! Hakika mimi ni katika wanao kupa nasaha. 20

image
21. . Basi akatoka, naye ana khofu, akiangalia huku na huku. Akasema: Mola wangu Mlezi! Niokoe na watu madhaalimu. 21

image
22. Na alipo elekea upande wa Madyana alisema: Asaa Mola wangu Mlezi akaniongoa njia iliyo sawa. 22

image
23. Na alipo yafikia maji ya Madyana alikuta umati wa watu wananywesha (wanyama wao), na akakuta karibu yao wanawake wawili wanawazuia wanyama wao. Akasema: Mna nini? Wakasema: Hatunyweshi sisi mpaka wamalize hao wachunga. Na baba yetu ni mzee sana. 23

image
24. Basi Musa akawanyweshea; kisha akarudi kivulini, na akasema: Mola wangu Mlezi! Hakika mimi ni mhitaji wa kheri utakayo niteremshia. 24

image
25. Basi mmoja katika wale wanawake wawili akamjia, naye anaona haya. Akasema: Baba yangu anakwita akulipe ujira wa kutunyweshea. Basi alipo mjia na akamsimulia visa vyake, alisema: Usiogope; umekwisha okoka kwenye watu madhaalimu. 25

image
26. Akasema mmoja katika wale wanawake: Ewe baba yetu! Muajiri huyu. Hakika mbora wa kumuajiri ni mwenye nguvu na muaminifu. 26

image
27. Akasema: Mimi nataka kukuoza mmojawapo katika binti zangu hawa wawili kwa kunitumikia miaka minane. Ukitimiza kumi, khiari yako; lakini mimi sitaki kukutaabisha. Inshallah utanikuta miongoni mwa watu wema. 27

image
28. Musa akasema: Hayo yamekwisha kuwa baina yangu na wewe. Muda mmojapo nikiumaliza sitiwi ubayani. Na Mwenyezi Mungu ni Mlinzi juu ya haya tunayo yasema. 28

image
29. Basi alipo timiza muda wake na akasafiri na ahali zake, aliona moto upande wa Mlima T'uri. Akawaambia ahali zake: Ngojeni! Mimi nimeona moto, labda nitakuleteeni kutoka huko khabari au kijinga cha moto ili mpate kuota moto. 29

image
30. Basi alipo ufikia aliitwa kutoka ng'ambo ya bonde la kuliani katika eneo lilio barikiwa kutoka kwenye mti: Ewe Musa! Hakika Mimi ni Mwenyezi Mungu, Mola Mlezi wa walimwengu wote. 30

image
31. Na tupa chini fimbo yako. Basi alipo iona ikitikisika kama nyoka, akarudi nyuma wala hakutazama. (Akaambiwa): Ewe Musa! Njoo mbele wala usiogope. Hakika wewe ni miongoni mwa walio salimika. image
32. Ingiza mkono wako kwenye mfuko wako, utatoka mweupe pasipo na ubaya. Na jiambatishe mkono wako ukihisi khofu. Basi hizi ni dalili mbili zitokazo kwa Mola wako Mlezi kumpelekea Firauni na wakuu wa umma wake. Hakika hao walikuwa watu mafaasiki. image
33. Akasema: Mola wangu Mlezi! Hakika mimi nilimuuwa mtu katika wao, kwa hivyo naogopa wataniuwa. image
34. Na ndugu yangu Harun ni fasihi zaidi ulimi wake kuliko mimi. Basi mtume ende nami kunisaidia, ili anisadikishe. Hakika mimi nina khofu watanikadhibisha. image
35. (Mwenyezi Mungu) akasema: Tutautia nguvu mkono wako kwa nduguyo, na tutakupeni madaraka, hata wasikufikilieni. Kwa sababu ya Ishara zetu nyinyi na watakao kufuateni mtashinda. image
36. Basi alipo wafikia Musa na Ishara zetu, walisema: Haya si chochote ila ni uchawi ulio zuliwa. Na hatukuyasikia haya kwa baba zetu wa zamani. image
37. Na Musa akasema: Mola wangu Mlezi ni Mwenye kujua kabisa nani anaye kuja na uwongofu unao toka kwake, na nani atakaye kuwa na mwisho mwema wa makaazi. Hakika wenye kudhulumu hawatafanikiwa. image
38. Na Firauni akasema: Enyi waheshimiwa! Sijui kama mnaye mungu asiye kuwa mimi. Ewe Haman! Niwashie moto unichomee udongo, unijengee mnara nipate kumchungulia mungu wa Musa. Na hakika mimi namwona yeye ni katika waongo. image
39. Na alipanda kiburi yeye na majeshi yake katika nchi bila ya haki, na wakadhania kuwa hawatarudishwa kwetu. image
40. Basi tukamshika yeye na majeshi yake, na tukawatupa baharini. Basi hebu angalia ulikuwaje mwisho wa wenye kudhulumu? image
41. . Na tuliwafanya ni waongozi waitao kwenye Moto. Na Siku ya Kiyama hawatanusuriwa. 41

image
42. Na tukawafuatishia laana katika dunia hii, na Siku ya Kiyama watakuwa miongoni mwa wanao chusha. 42

image
43. Na hakika bila ya shaka tulimpa Musa Kitabu baada ya kwisha ziangamiza kaumu za mwanzo, ili kiwafumbue macho watu, na kiwe uwongofu, na rehema, ili wapate kukumbuka. 43

image
44. . Wala wewe hukuwa upande wa magharibi tulipo mpa Musa amri, wala hukuwa katika walio hudhuria. 44

image
45. Lakini Sisi tuliziumba kaumu, na ukawa mrefu umri juu yao. Wala hukuwa mkaazi na watu wa Madyana ukiwasomea Aya zetu. Lakini ni Sisi tulio kuwa tukiwatuma Mitume. 45

image
46. Wala hukuwa kando ya mlima tulipo nadi. Lakini ni rehema itokayo kwa Mola wako Mlezi ili uwaonye watu wasio pata kufikiwa na mwonyaji kabla yako, huenda wakakumbuka. 46

image
47. Na usije kuwasibu msiba kwa iliyo yatanguliza mikono yao, wakasema: Ewe Mola wetu Mlezi! Mbona hukututumia Mtume nasi, tukafuata Ishara zako, na tukawa miongoni mwa Waumini? 47

image
48. Ilipo wajia Haki kutoka kwetu walisema: Mbona hakupewa kama aliyo pewa Musa? Je! Kwani wao hawakuyakataa aliyo pewa Musa zamani? Walisema: Ni wachawi wawili wanasaidiana. Na wakasema: Hakika sisi tunawakataa wote. 48

image
49. Sema: Basi leteni Kitabu kinacho toka kwa Mwenyezi Mungu chenye kuongoka zaidi kuliko hivi viwili tukifuate, kama nyinyi mnasema kweli. 49

image
50. Na ikiwa hawakuitikii, basi jua kuwa wanafuata pumbao lao tu. Na nani aliye potea zaidi kumshinda anaye fuata pumbao lake bila ya uwongofu utokao kwa Mwenyezi Mungu. Hakika Mwenyezi Mungu hawaongoi watu wenye kudhulumu. 50

image
51. Na sasa kwa yakini tumewafikishia Neno ili wapate kukumbuka. 51

image
52. Wale tulio wapa Kitabu kabla yake wanakiamini hiki. 52

image
53. Na wanapo somewa wanasema: Tunaiamini. Hakika hii ni Haki inayo toka kwa Mola wetu Mlezi. Hakika sisi kabla yake tulikuwa ni Waislamu, tulio nyenyekea. 53

image
54. . Basi hao watapewa ujira wao mara mbili kwa walivyo vumilia, na wakaondoa ubaya kwa wema, na wakatoa katika tuliyo waruzuku. 54

image
55. Na wanapo sikia upuuzi hujitenga nao na husema: Sisi tuna vitendo vyetu, na nyinyi mna vitendo vyenu. Salamun Alaikum, Amani juu yenu! Sisi hatutaki kujibizana na wajinga. 55

image
56. Kwa hakika wewe humwongoi umpendaye, lakini Mwenyezi Mungu humwongoa amtakaye. Na Yeye ndiye anawajua zaidi waongokao. 56

image
57. Na wakasema: Tukiufuata uwongofu huu pamoja nawe tutanyakuliwa kutoka nchi yetu. Je! Kwani Sisi hatukuwaweka imara katika pahala patakatifu, penye amani, ambapo huletewa matunda ya kila aina kuwa ni riziki itokayo kwetu? Lakini wengi wao hawajui. 57

image
58. Na miji mingapi iliyo jifakharisha tumeiangamiza! Na hayo maskani yao hayakukaliwa tena baada yao, ila kwa uchache tu. Na Sisi ndio tumekuwa warithi wao. 58

image
59. . Na Mola wako Mlezi haangamizi miji mpaka ampeleke Mtume katika miji yake mikuu awasomee Ishara zetu. Wala hatuiangamizi miji mpaka watu wake wawe madhaalimu. 59

image
60. .. Na chochote mlicho pewa ni matumizi ya maisha ya dunia na pambo lake. Na yaliyoko kwa Mwenyezi Mungu ndio bora na yatakayo baki zaidi. Basi je, hamfahamu? 60

image
61. Je! Yule tuliye muahidi ahadi nzuri, tena naye akayapata, ni kama tuliye mstarehesha kwa starehe za maisha ya duniani, na kisha Siku ya Kiyama akawa miongoni mwa wanao hudhurishwa? image
62. Na siku atakapo waita na akasema: Wako wapi mlio kuwa mkidai kuwa ni washirika wangu? image
63. Watasema wale iliyo thibiti juu yao kauli: Mola wetu Mlezi! Hawa ndio tulio wapoteza. Tuliwapoteza kama tulivyo potea sisi. Tunajitenga nao mbele yako. Hawakuwa wakituabudu sisi. image
64. . Na itasemwa: Waiteni hao miungu wa kishirikina wenu! Basi watawaita, lakini hawatawaitikia, na wataiona adhabu; laiti wangeli kuwa wameongoka! image
65. Na siku atapo waita na akasema: Mliwajibu nini Mitume? image
66. Basi zitawapotea khabari siku hiyo, nao hawataulizana. image
67. Ama mwenye kutubu na akaamini na akatenda mema, huyo atakuwa miongoni mwa wenye kufanikiwa. image
68. Na Mola wako Mlezi huumba na huteuwa atakavyo. Viumbe hawana khiari. Mwenyezi Mungu ametukuka na ametakasika na hao wanao washirikisha naye. image
69. Na Mola wako Mlezi anayajua yaliyo ficha vifua vyao, na wanayo yatangaza. image
70. . Naye ni Mwenyezi Mungu ambaye hapana mungu isipo kuwa Yeye. Sifa zote njema ni zake Yeye, mwanzo na mwisho. Na hukumu ni yake Yeye. Na kwake Yeye mtarejeshwa. image
71. Sema: Mwaonaje, Mwenyezi Mungu angeli ufanya usiku umekukalieni moja kwa moja mpaka Siku ya Kiyama, mungu gani asiye kuwa Mwenyezi Mungu atakaye kuleteeni mwangaza? Basi je, hamsikii? 71

image
72. Sema: Mwaonaje, Mwenyezi Mungu angeli ufanya mchana umekukalieni moja kwa moja mpaka Siku ya Kiyama, mungu gani asiye kuwa Mwenyezi Mungu ataye kuleteeni usiku mkapumzika humo? Basi je, hamwoni? 72

image
73. Na ni katika rehema zake amekufanyieni usiku na mchana mpate kupumzika humo na mtafute fadhila zake, na ili mpate kushukuru. 73

image
74. Na siku atakapo waita na akasema: Wako wapi hao mlio kuwa mkidai kuwa ni washirika wangu? 74

image
75. Na tutatoa shahidi katika kila umma, na tutasema: Leteni hoja zenu! Hapo watajua kwamba hakika kweli ni ya Mwenyezi Mungu, na yatawapotea yale waliyo kuwa wakiyazua. 75

image
76. Hakika Qaruni alikuwa katika watu wa Musa, lakini aliwafanyia dhulma. Na tulimpa khazina ambazo funguo zake zinawatopeza watu wenye nguvu kuzichukua. Walipo mwambia watu wake: Usijigambe! Hakika Mwenyezi Mungu hawapendi wanao jigamba. 76

image
77. Na utafute, kwa aliyo kupa Mwenyezi Mungu, makaazi ya Akhera. Wala usisahau fungu lako la dunia. Nawe fanya wema kama Mwenyezi Mungu alivyo kufanyia wema wewe. Wala usitafute kufanya ufisadi katika ardhi. Hakika Mwenyezi Mungu hawapendi mafisadi. 77

image
78. . Akasema: Kwa hakika nimepewa haya kwa sababu ya ilimu niliyo nayo. Je! Hakujua kwamba Mwenyezi Mungu kesha waangamiza, katika vizazi vya walio kabla yake, watu walio kuwa wenye ngubvu zaidi kuliko yeye, na wenye makundi makubwa zaidi kuliko yake. Na wakosefu hawataulizwa khabari ya dhambi zao. 78

image
79. Basi akawatokea watu wake katika pambo lake. Wakasema wale walio kuwa wanataka maisha ya duniani: Laiti tungeli kuwa tunayo kama aliyo pewa Qaruni! Hakika yeye ni mwenye bahati kubwa. 79

image
80. Na wakasema wale walio pewa ilimu: Ole wenu! Malipo ya Mwenyezi Mungu ni bora kwa mwenye kuamini na akatenda mema. Wala hawatapewa hayo isipo kuwa wenye subira. 80

image
81. Basi tukamdidimiza yeye na nyumba yake katika ardhi; wala halikuwepo kundi lolote la kumnusuru kwa Mwenyezi Mungu, wala hakuwa miongoni mwa wanao jitetea. 81

image
82. Na wale walio tamani kuwa pahala pake jana, wakawa wanasema: Kumbe Mwenyezi Mungu humkunjulia riziki amtakaye katika waja wake, na humdhikisha amtakaye. Ingeli kuwa Mwenyezi Mungu hakutufanyia hisani angeli tudidimiza. Kumbe makafiri hawafanikiwi! 82

image
83. Hayo ndiyo makaazi ya Akhera, tumewafanyia wale wasio taka kujitukuza duniani wala ufisadi. Na mwisho mwema ni wa wachamngu. 83

image
84. Atakaye tenda wema atapata malipo bora kuliko huo wema alio utenda. Na atakaye tenda uovu, hawalipwi watendao uovu ila waliyo kuwa wakiyatenda. 84

image
85. Hakika aliye kulazimisha kuifuata Qur'ani hapana shaka atakurudisha pahala pa marejeo. Sema: Mola wangu Mlezi ndiye anaye mjua zaidi mwenye kuja na uwongofu, na nani aliyomo katika upotofu ulio dhaahiri. 85

image
86. Nawe hukuwa unataraji kuletewa Kitabu; lakini ni rehema tu ya Mola wako Mlezi. Basi usiwe msaidizi wa makafiri. 86

image
87. Wala wasikuzuie kuzifuata Aya za Mwenyezi Mungu baada ya kuteremshiwa wewe. Na lingania kwa Mola wako Mlezi, wala usiwe miongoni mwa washirikina. 87

image
88. Wala usimwombe pamoja na Mwenyezi Mungu mungu mwenginewe. Hapana mungu ila Yeye. Kila kitu kitaangamia isipo kuwa Yeye. Hukumu iko kwake, na kwake mtarejezwa.  88


Imetarjumiwa na Sheikh Ali Muhsin Al-Barwani
Ikiwa una ushauri au maoni juu ya tarjuma hii, andika kwa anwani hii qurani-tukufu@geocities.com 
Copyright � 22 August 1997, Sheikh Ali Muhsin Al Barwani