Tarjuma ya Quran Tukufu kwa
kiswahili

KWA JINA LA MWENYEEZI MUNGU
MWINGI WA REHEMA MWENYE KUREHEMU 0

1. AMETUKUKA ambaye mkononi mwake umo Ufalme wote; na
Yeye ni Mwenye uweza juu ya kila kitu. 1

2. Ambaye ameumba mauti na uhai ili kukujaribuni ni
nani miongoni mwenu mwenye vitendo vizuri zaidi. Na Yeye ni Mwenye nguvu na
Mwenye msamaha. 2

3. Aliye umba mbingu saba kwa matabaka. Huoni tafauti
yoyote katika uumbaji wa Mwingi wa Rehema. Hebu rudisha nadhari! Unaona kosa
lolote? 3

4. Tena rudisha nadhari mara mbili, nadhari yako
itakurejea mwenyewe hali ya kuwa imehizika nayo imechoka. 4

5. Na kwa hakika tumeipamba mbingu ya karibu kwa mataa,
na tumeyafanya ili kuwapigia mashetani, na tumewaandalia adhabu ya Moto uwakao
kwa nguvu. 5

6. Na kwa walio mkufuru Mola wao Mlezi ipo adhabu ya
Jahannamu. Na ni marejeo maovu yalioje hayo! 6

7. Watakapo tupwa humo watausikia mngurumo wake na huku
inafoka. 7

8. Inakaribia kupasuka kwa hasira. Kila mara likitupwa
kundi humo walinzi wake huwauliza: Kwani hakukujieni mwonyaji? 8

9. Watasema: Kwani! Ametujia mwonyaji, lakini
tulimkadhibisha, na tukasema: Mwenyezi Mungu hakuteremsha chochote. Nyinyi
hamumo ila katika upotovu mkubwa! 9

10. Na watasema: Lau kuwa tungeli sikia, au tungeli
kuwa na akili, tusingeli kuwa katika watu wa Motoni! 10

11. Wakakiri dhambi zao. Basi kuangamia ni kwa watu wa
Motoni! 11

12. Hakika wanao mwogopa Mola wao Mlezi kwa ghaibu,
watapata maghfira na ujira mkubwa. 12

13. Na ficheni kauli zenu, au zitangazeni; hakika Yeye
ni Mjuzi wa yaliyomo vifuani. 13

14. Asijue aliye umba, naye ndiye Mjua siri, Mwenye
khabari? 14

15. Yeye ndiye aliye idhalilisha ardhi kwa faida yenu,
basi tembeeni katika pande zake, na kuleni katika riziki zake. Na kwake Yeye
ndio kufufuliwa. 15

16. Mnadhani mko salama kwa alioko juu kuwa
hatakudidimizeni kwenye ardhi, na tahamaki hiyo inatikisika! 16

17. Au mnadhani mko salama kwa alioko juu ya kuwa Yeye
hakupelekeeni kimbunga chenye changarawe? Mtajua vipi maonyo yangu? 17

18. Na bila ya shaka walikwisha kanusha walio kuwa
kabla yao; basi kulikuwaje kukasirika kwangu? 18

19. Kwani hawawaoni ndege walioko juu yao namna wanavyo
zikunjua mbawa zao, na kuzikunja? Hawawashikilii ila Mwingi wa rehema. Hakika
Yeye ni Mwenye kuona kila kitu. 19

20. Au ni lipi hilo jeshi lenu la kukunusuruni badala
ya Mwingi wa Rehema? Hakika makafiri hawamo ila katika udanganyifu. 20

21. Au ni nani huyo ambaye atakupeni riziki kama Yeye
akizuia riziki yake? Bali wao wanakakamia tu katika jeuri na chuki. 21

22. Je! Anaye kwenda akisinukia juu ya uso wake ni
mwongofu zaidi, au yule anaye kwenda sawasawa katika Njia Iliyo Nyooka?
22

23. Sema: Yeye ndiye aliye kuumbeni tangu mwanzo, na
akakupeni masikio na macho, na nyoyo. Ni kidogo kabisa shukrani zenu. 23

24. Sema: Yeye ndiye aliye kutawanyeni katika ardhi, na
kwake mtakusanywa. 24

25. Na wanasema: Lini ahadi hii, ikiwa mnasema kweli?
25

26. Sema: Hakika ujuzi wake uko kwa Mwenyezi Mungu; na
hakika mimi ni mwonyaji tu mwenye kubainisha. 26

27. Lakini watakapo iona karibu, nyuso za walio kufuru
zitahuzunishwa, na itasemwa: Hayo ndiyo mliyo kuwa mkiyaomba. 27

28. Sema: Mwaonaje, ikiwa Mwenyezi Mungu atanihiliki
mimi na walio pamoja nami, au akiturehemu, ni nani atakaye walinda makafiri na
adhabu chungu? 28

29. Sema: Yeye ndiye Mwingi wa Rehema; tunamuamini
Yeye, na juu yake tunategemea. Mtakuja jua ni nani aliye katika upotovu ulio
dhaahiri. 29

30. Sema: Mwaonaje, yakiwa maji yenu yamedidimia chini,
nani atakueleteeni maji yanayo miminika? 30
Imetarjumiwa na Sheikh Ali Muhsin
Al-Barwani
Ikiwa
una ushauri au maoni juu ya tarjuma hii, andika kwa anwani hii qurani-tukufu@geocities.com
Copyright � 22 August 1997, Sheikh
Ali Muhsin Al Barwani