14. Kujiepusha na Dharau


Kudharau wengine ni tabia mbaya na ni kitendo kiovu mbele ya Allah (s.w). Katazo la kuwadharau watu liko bayana katika Qur-an:

“Enyi mlioamini! Wanaume wasiw adharau wanaume wenzao, huwenda wakawa bora kuliko wao; wala wanawake wasiwadharau wanawake wenzao; huwenda wakawa bora kuliko wao...” (49:11)
Mwenye kuwadharau wengine hujihisi kuwa yeye ni bora kuliko hao anaowadharau. Hili ni kosa kubwa kwani anaye mjua aliye mbora ni Allah (s.w) Pekee kama tunavyojifunza katika Qur-an:

“Enyi Watu! Kwa hakika tumekuumbeni(nyote) kutoka kwa (yule) mwanaume(mmoja; Adamu) na (yule yule) mwanamke (mmoja; Hawwa). Na tumekufanyeni mataifa na makabila (mbalimbali) ili mjuane. Hakika ahishimiwaye sana miongoni mwenu mbele ya Mwenyezi Mungu ni yule amchaye Mungu zaidi katika ninyi. Kw a yakini Mw enyezi Mungu ni Mjuzi, Mwenye habari (49:13).
Aya hii kwa ujumla inatuwekea msingi wa usawa. Inatukumbusha kuwa watu wote asili yao ni moja; ni watoto wa Adam ambaye ameumbwa kutokana na udongo.

“Na tulimuumba mtu kwa udongo mkavu unaotoa sauti, wenye kutokana na matope meusi yaliyovunda. ” (15:26).
Tofauti za rangi, kabila, taifa n.k. ziko pale kwa ajili ya anuani tu na kamwe zisiwe msingi wa kubaguana na kudharauliana. Pia tofauti za vipawa zilizopo kati ya watu kama vile elimu, utajiri, ufalme, n.k. isiwe sababu ya kubaguana. Vipawa hivyo ametunukiwa mwanaadamu kama mtihani kwake.Ama atamshukuru Mola wake kwa kutumia vipawa hivyo kwa ajili yake kama inavyostahiki awe mwenye kufaulu au atatakabari kwa kutumia vipawa hivyo apendavyo kinyume na maagizo ya Mola wake awe ni mwenye kufeli.